Je, Kweli Yesu Alikuwa na Imani Katika Mungu?
Tatizo la Wanautatu
“YESU angekuwaje na imani? Yeye ni Mungu; yeye ajua na kuona kila kitu bila kutegemea mtu mwingine yeyote. Lakini imani yamaanisha hasa kutegemea mwingine na kukiri kile ambacho hakionekani; kwa hiyo, jambo la kwamba yawezekana Yesu-Mungu alikuwa na imani halipo.”
Kulingana na mwanatheolojia Mfaransa Jacques Guillet, hayo ndiyo maoni makubwa ya Ukatoliki. Je, maelezo hayo yakushangaza? Huenda ulifikiri kwamba kwa kuwa Yesu ni kielelezo cha Wakristo katika kila jambo, ni lazima pia awe kiolezo cha kuigwa cha imani. Kama unafikiri hivyo, basi hujafikiria fundisho la Jumuiya ya Wakristo la Utatu.
Suala la imani ya Yesu kwa kweli si wazi kwa wanatheolojia wa Katoliki, wa Protestanti, na wa Orthodoksi wanaoamini kuwa Utatu ni “fumbo kuu la imani na maisha ya Kikristo.”a Hata hivyo si wote wanaokataa imani ya Yesu. Jacques Guillet athibitisha kwamba “haiwezekani kutotambua kwamba Yesu alikuwa na imani,” hata ingawa Guillet akiri kwamba, kwa kufikiria fundisho la Utatu, hilo ni jambo “tata.”
Myesuiti Mfaransa Jean Galot, na kama yeye wengi zaidi wa wanatheolojia, ni wazi sana asemapo kwamba kwa kuwa “Mungu wa kweli na mtu wa kweli, . . . Kristo hawezi kuwa na imani katika yeye mwenyewe.” “Imani yahusu kuamini mtu mwingine, si kujiamini wewe mwenyewe,” lasema jarida La Civiltà Cattolica. Basi kizuizi cha kutambua imani ya Yesu ni fundisho la Utatu, kwa kuwa maoni hayo mawili kwa wazi yapingana.
“Zile Gospeli hazisemi kamwe juu ya imani ya Yesu,” wanatheolojia hao wasema. Basi, maneno yatumiwayo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pi·steuʹo (amini, kuwa na imani) na piʹstis (imani) kwa kawaida hurejezea imani ya wanafunzi kwa Mungu au kwa Kristo, badala ya kumaanisha imani ya Yesu kwa Baba yake wa mbinguni. Je, basi tuamue kwamba Mwana wa Mungu hakuwa na imani? Twaweza kuelewa nini kutokana na yale aliyofanya na kusema? Maandiko yasema nini?
Sala Pasipo Imani?
Yesu alikuwa mtu wa sala. Alisali katika kila pindi—alipobatizwa (Luka 3:21); usiku kucha kabla ya kuchagua mitume wake 12 (Luka 6:12, 13); na kabla ya kugeuka kwake sura kimwujiza mlimani, alipokuwa na mitume Petro, Yohana, na Yakobo. (Luka 9:28, 29) Alikuwa akisali wakati mmoja wa wanafunzi wake alipomwuliza: “Tufundishe sisi kusali,” kwa hiyo akawafundisha Sala ya Bwana (ile ya “Baba Yetu”). (Luka 11:1-4; Mathayo 6:9-13) Alisali akiwa peke yake na kwa muda mrefu mapema asubuhi (Marko 1:35-39); kuelekea jioni, mlimani, baada ya kuwaondosha wanafunzi wake (Marko 6:45, 46); akiwa pamoja na wanafunzi wake na kwa ajili ya wanafunzi wake. (Luka 22:32; Yohana 17:1-26) Ndiyo, sala ilikuwa sehemu muhimu ya maisha ya Yesu.
Alisali kabla ya kufanya miujiza, kwa mfano, kabla ya kumfufua rafiki yake Lazaro: “Baba, nakushukuru kwa kuwa umenisikia. Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia sikuzote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma.” (Yohana 11:41, 42) Uhakika wa kwamba Baba yake angejibu sala hiyo waonyesha nguvu ya imani yake. Uhusiano huo kati ya sala kwa Mungu na imani Kwake waonekana wazi katika maneno ambayo Kristo alieleza wanafunzi wake: “Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea.”—Marko 11:24.
Ikiwa Yesu hakuwa na imani, kwa nini alisali kwa Mungu? Fundisho lisilo la kimaandiko la Jumuiya ya Wakristo la Utatu, kwamba Yesu alikuwa binadamu na Mungu vilevile, lafunika ujumbe wa Biblia. Lazuia watu wasielewe usahili na uwezo wa Biblia. Yesu alimtolea nani sala? Yeye mwenyewe? Je, hakujua kwamba yeye alikuwa Mungu? Na kama alikuwa Mungu na kujua hivyo, kwa nini alisali?
Sala za Yesu katika siku ya mwisho ya maisha yake ya duniani zatupa hata ufahamu wa ndani zaidi wa imani yake thabiti kwa Baba yake wa mbinguni. Akionyesha tazamio lenye tumaini na uhakika, yeye aliomba hivi: “Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.”—Yohana 17:5.
Akijua kwamba majaribu yake magumu zaidi na kifo chake kilikuwa kinakaribia, ule usiku aliokuwa katika bustani ya Gethsemane katika Mlima wa Mizeituni, “akaanza kuhuzunika na kusononeka,” naye akasema: “Roho yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa.” (Mathayo 26:36-38) Kisha akapiga magoti na kusali: “Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” Kisha “malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.” Mungu alisikiliza sala yake. Kwa sababu ya hisia zake nyingi sana na ukali wa jaribu hilo, “hari yake ikawa kama matone ya damu yakidondoka nchi.”—Luka 22:42-44.
Mateseko ya Yesu, uhitaji wake wa kuimarishwa, na dua zake zaonyesha nini? “Kuna uhakika mmoja,” aandika Jacques Guillet, “Yesu alisali, na sala ni sehemu muhimu ya maisha yake na matendo yake. Yeye alisali kama vile wanadamu wasalivyo, naye alisali kwa niaba ya wanadamu. Sasa, haiwezekani wanadamu wasali bila imani. Je, sala za Yesu zingetolewa bila imani?”
Akining’inia katika mti wa mateso muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alilia kwa sauti kubwa, akinukuu zaburi moja ya Daudi. Kisha kwa imani, kwa sauti kubwa, akatoa ombi lake la mwisho: “Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu.” (Luka 23:46; Mathayo 27:46) Tafsiri moja ya Kiitalia yenye kushirikisha dini nyingi, Parola del Signore, yasema kwamba Yesu ‘alimpa Baba uhai wake.’
Jacques Guillet aeleza hivi: “Wakituonyesha Kristo aliyesulubiwa, akimlilia Baba yake kwa kunukuu zaburi ya Israeli, waandikaji wa Gospeli wanatuhakikishia kwamba huo mlio, mlio wa Mwana-mzaliwa wa pekee, mlio wa kihoro kikuu, mlio wa uhakika kamili, ni mlio wa imani, mlio wa kifo katika imani.”
Wakikabiliwa na uthibitisho huo wa wazi na wenye kutazamisha wa imani, wanatheolojia fulani hujaribu kutofautisha imani na “uhakika.” Hata hivyo, kutofautisha huko hakutegemei Maandiko.
Lakini majaribu makali aliyovumilia yaonyesha nini hasa kuhusu imani ya Yesu?
“Mkamilishaji wa Imani Yetu” Akamilishwa
Katika sura ya 11 ya barua yake kwa Waebrania, mtume Paulo ataja wingu kubwa la wanaume na wanawake waaminifu kabla ya nyakati za Ukristo. Yeye amalizia hivi, akielekeza kwenye kielelezo kikuu zaidi na kilicho kamilifu cha imani: “Tumkaziapo macho Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu. Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu . . . Fikirieni sana yeye ambaye amevumilia maongezi yaliyo kinyume ya namna hiyo yenye kufanywa na watenda-dhambi dhidi ya masilahi yao wenyewe, ili nyinyi msipate kuchoka na kuzimia katika nafsi zenu.”—Waebrania 12:1-3, NW.
Wengi wa wanatheolojia wasema kwamba mstari huu hausemi juu ya “imani ya Yesu binafsi,” bali wasema juu ya daraka lake akiwa “mwanzilishi wa au chanzo cha imani.” Neno la Kigiriki te·lei·o·teś litokealo katika fungu hili larejezea mtu anayekamilisha, anayetimiza au kukamilisha kitu. Akiwa “Mkamilishaji,” Yesu alimaliza imani kwa maana ya kwamba kuja kwake duniani kulitimiza unabii mbalimbali wa Biblia na hivyo kuweka msingi mzuri zaidi kwa imani. Lakini je, hilo lamaanisha kwamba yeye hakuwa na imani?
Mafungu yatokayo katika barua kwa Waebrania uwezayo kuona katika sanduku katika ukurasa 15 yaondoa shaka lolote. Yesu alikamilishwa kwa mateseko yake na utii wake. Ingawa tayari alikuwa mtu mkamilifu, maono yake yalimfanya mkamilifu na kamili katika mambo yote, hata katika imani, ili awe Kuhani Mkuu aliyestahili kabisa kwa ajili ya wokovu wa Wakristo wa kweli. Yeye aliomba dua kwa Baba yake kwa “vilio vyenye kupaazwa kwa nguvu na machozi,” alikuwa “mwaminifu” kwa Mungu, naye alikuwa na ‘hofu ya kimungu.’ (Waebrania 3:1, 2; 5:7-9; NW) ‘Alijaribiwa katika mambo yote’ “sawasawa na sisi,” yasema Waebrania 4:15, yaani, kama Mkristo mwingine yeyote ambaye imani yake inapitia “majaribu mbalimbali.” (Yakobo 1:2, 3) Je, ni kufikiri kuzuri kuamini kwamba Yesu angejaribiwa “sawasawa” na wafuasi wake bila kujaribiwa imani kama wao?
Dua, utii, mateseko, majaribu, uaminifu, na hofu ya kimungu zathibitisha imani kamili ya Yesu. Zaonyesha kwamba alikuja kuwa “Mkamilishaji wa imani yetu” baada tu ya yeye kufanywa kuwa mkamilifu katika imani yake mwenyewe. Kwa wazi, yeye hakuwa Mungu Mwana, kama vile fundisho la Utatu likaziavyo.—1 Yohana 5:5.
Je, Si Kweli Kwamba Aliamini Neno la Mungu?
Fundisho la Utatu lafinyanga kufikiri kwa wanatheolojia hivi kwamba wao hufikia maoni yapitayo kiasi wakisisitiza kwamba Yesu “hawezi kuamini Neno la Mungu na ujumbe walo” kwa sababu “akiwa Neno lenyewe la Mungu, yeye aweza tu kulitangaza neno hilo.”—Angelo Amato, Gesù il Signore, chenye mambo rasmi ya kanisa.
Lakini, marejezo ya daima ya Yesu kwenye Maandiko kwa kweli yaonyesha nini? Alipojaribiwa, yeye alinukuu kutoka kwenye Maandiko mara tatu. Jibu lake la tatu lilimwambia Shetani kwamba Yesu alimwabudu Mungu peke yake. (Mathayo 4:4, 7, 10) Katika pindi nyinginezo Yesu alitaja unabii mbalimbali uliomhusu, akionyesha imani katika kutimizwa kwao. (Marko 14:21, 27; Luka 18:31-33; 22:37; linganisha Luka 9:22; 24:44-46.) Kutokana na uchunguzi huu ni lazima tukate kauli kwamba Yesu alijua Maandiko yalivuviwa na Baba yake, aliyafuata kwa imani, naye alikuwa na tumaini kamili katika utimizo wa unabii mbalimbali uliotabiri majaribu, mateseko, kifo, na ufufuo wake.
Yesu, Kiolezo cha Imani cha Kuiga
Ilimbidi Yesu apigane vita ya imani mpaka mwisho ili adumishe uaminifu-mshikamanifu kwa Baba yake na ‘kuushinda ulimwengu.’ (Yohana 16:33) Bila imani, haiwezekani kupata ushindi huo. (Waebrania 11:6; 1 Yohana 5:4) Kwa sababu ya imani hiyo ishindayo, yeye alikuwa kielelezo kwa wafuasi wake waaminifu. Hakika alikuwa na imani katika Mungu wa kweli.
[Maelezo ya Chini]
a Mazungumzo marefu zaidi juu ya ukosefu wa msingi wa Utatu yaweza kupatikana katika broshua Je! Uamini Utatu?, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Sanduku katika ukurasa wa 15]
Yesu, “Mkamilishaji,” Akamilishwa
Waebrania 2:10, NW: “Ilifaa yule ambaye kwa ajili yake vitu vyote vipo na kupitia kwake vitu vyote vipo, katika kuleta wana wengi kwenye utukufu, amfanye Wakili Mkuu wa wokovu wao kuwa mkamilifu kupitia mateso.”
Waebrania 2:17, 18, NW: “Aliwajibika kuwa kama ‘ndugu’ zake katika mambo yote, ili apate kuwa kuhani wa cheo cha juu mwenye rehema na mwaminifu katika mambo yanayohusiana na Mungu, kusudi atoe dhabihu ya kutuliza kwa ajili ya dhambi za watu. Kwa maana yeye mwenyewe ameteseka alipokuwa akiwekwa kwenye mtihani, aweza kuja kusaidia wale wanaotiwa kwenye mtihani.”
Waebrania 3:2, NW: “Yeye alikuwa mwaminifu kwa Yule aliyemfanya kuwa namna hiyo, kama vile Musa alivyokuwa pia katika nyumba yote ya Huyo.”
Waebrania 4:15, NW: “Tuna kuhani wa cheo cha juu, si mmoja asiyeweza kushiriki hisia za udhaifu wetu mbalimbali, bali mmoja ambaye ametahiniwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kufanya dhambi.”
Waebrania 5:7-9, NW: “Siku za mwili wake Kristo alitoa dua na pia maombi ya bidii kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa kutoka katika kifo, pamoja na vilio vyenye kupaazwa kwa nguvu na machozi, naye akasikiwa kwa kupendelewa kwa sababu ya hofu yake ya kimungu. Ijapokuwa yeye alikuwa Mwana, alijifunza utii kutokana na mambo aliyoteseka; naye baada ya kuwa amefanywa kamili akawa ndiye mwenye daraka la wokovu udumuo milele.”