Uhai Ni Wenye Thamani Kadiri Gani Kwako?
MVULANA mmoja tineja alikufa kwa kuruka kutoka orofa ya nane ya jengo la makao. Yeye alikuwa amesoma kitabu kilichofafanua kifo cha kuruka kuwa “hakina uchungu au masumbufu au woga; badala ya hivyo, mtu huhisi vizuri.” Mwandikaji wa kitabu hiki, kilichochapishwa Japani, alidai kwamba yeye alikuwa tu akitoa “ujiuaji kama moja ya chaguo la maisha.”
Watu ambao hujiua kimakusudi si ndio pekee hudhihirisha kutojali uhai leo. Madereva wasio waangalifu pia huonyesha heshima ndogo sana kwa uhai. Wengine hata hunywa pombe na kuendesha gari, wengi wakiendesha kwa mwendo uwezao kutokeza aksidenti.
Wengine huonyesha jinsi wasivyoheshimu uhai wao kwa kutilia mkazo raha. Wavuta sigareti hukataa kuacha uvutaji sigareti, ijapokuwa uvutaji sigareti waweza kusababisha kifo na umejulikana kuwa ujiuaji wa polepole. Badala ya kudumisha usafi wa maadili katika ulimwengu huu wenye kichaa cha ngono, wengi hufuatia mwendo wa ngono za ovyo-ovyo ambao mara nyingi huongoza kwenye kifo.
Wengine bila hata wao kujua, hufupisha maisha zao kwa ulafi, unywaji wa kileo kupita kiasi, mazoezi yasiyotosha, na utafutaji wa raha. Mwandikaji Mjapani Shinya Nishimaru alionya hivi: “Mazoea ya kula yasiyodhibitiwa hutatanisha miendo ya mwili, na utafutaji wa starehe na raha huondolea watu nguvu polepole.” Wengine hushiriki maoni ya wale wa nyakati za kale waliosema: ‘Na . . . tule, tunywe, kwa maana kesho tutakufa.’—Isaya 22:13; 1 Wakorintho 15:32.
Ndio, kutojali uhai kumeenea sana leo. Hivyo, huenda swali hili vilevile likaulizwa, Uhai ni wenye thamani kadiri gani kwako? Je uhai wapaswa kulindwa kwa njia zozote? Na je, kuna kitu kingine chenye thamani zaidi kuliko uhai wetu wa sasa?