Hazini Uhai Ulio Kweli-Kweli
JE, UHAI ndio uu huu tu? Kwa kututia moyo ‘kushika imara uhai ulio kweli-kweli,’ Biblia huonyesha kwamba kuna mengi zaidi. (1 Timotheo 6:17-19, New World Translation) Ikiwa uhai wetu wa sasa si uhai ulio kweli-kweli, huo ni nini?
Muktadha wa andiko lililotajwa waonyesha kwamba ni “uhai udumuo milele” ambao mtu anayemhofu Mungu anapaswa kushika kweli-kweli. (1 Timotheo 6:12, NW) Kwa walio wengi mno, hili lamaanisha uhai udumuo milele duniani. Adamu, yule mtu wa kwanza, alikuwa na taraja la kuishi milele katika paradiso duniani. (Mwanzo 1:26, 27) Angekufa ikiwa tu angekula kutoka kwa “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwanzo 2:17) Lakini kwa sababu Adamu na mkeye, Hawa, kwa kutotii walikula kutoka kwa mti huo, Mungu alitangaza hukumu ya kifo. Katika ‘siku walipokula kutoka kwa mti huo,’ machoni pa Mungu walikufa na wakaanza kutumbukia katika kifo halisi. Uhai wao haukuwa tena wenye ubora waliokuwa wamefurahia mara ya kwanza.
Njia Inayoongoza Kwenye “Uhai Ulio Kweli-Kweli”
Ili kufanya “uhai ulio kweli-kweli” uwezekane, Yehova Mungu alifanya mpango wa kukomboa wanadamu. Ili kutusaidia kuelewa mpango huu, acha tufikirie kiwanda kidogo. Mashine zote ndani yacho zina kasoro na zafanyiza matatizo kwa wenye kuzitumia kwa sababu mfanya-kazi wa kwanza miaka mingi iliyopita alipuuza kitabu cha maagizo na kuharibu mashine zote. Watumiaji wa sasa waweza tu kufanya yote wawezayo kufanya kazi kwa kile walicho nacho. Mwenye kiwanda hicho ataka kuzitengeneza mashine hizo ili kusaidia wafanya-kazi wake, naye anaweka kando pesa zinazotakiwa kwa kusudi hilo.
‘Mtumiaji wa kwanza wa mashine,’ Adamu, hakuhazini uhai aliokuwa amepewa. Kwa hiyo, alipitishia wazao wake uhai usio mkamilifu, sawa na mashine isiyofanya kazi vizuri. (Warumi 5:12) Kama vile wale watumiaji wa baadaye katika kile kiwanda, ambao hawangeweza kusuluhisha hali hiyo, wazao wa Adamu wameshindwa kufikia uhai ulio kweli-kweli wao wenyewe. (Zaburi 49:7) Ili kusuluhisha hali hii ionekanayo kuwa isiyo na matumaini, Yehova alimtuma Mwana wake wa pekee duniani kununulia wanadamu uhai udumuo milele. (Luka 1:35; 1 Petro 1:18, 19) Kwa kufa kifo cha kidhabihu kwa ajili ya wanadamu, Mwana wa pekee wa Mungu, Yesu Kristo, alitoa gharama—uhai unaolingana na aliopoteza Adamu. (Mathayo 20:28; 1 Petro 2:22) Kwa dhabihu hii yenye thamani, sasa Yehova ana msingi wa kutoa uhai ulio kweli-kweli.
Kwa wanadamu watiifu, dhabihu ya fidia ya Yesu itamaanisha uhai udumuo milele katika paradiso duniani. (Zaburi 37:29) Tumaini hili linatolewa kwa waokokaji wote wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,” irejezewayo kama Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14-16) Itaondolea mbali uovu wote duniani. (Zaburi 37:9-11) Wale walio katika kumbukumbu la Mungu wafao kabla ya wakati huo watafufuliwa katika Paradiso itakayorudishwa duniani na watakuwa na taraja la kufurahia uhai ulio kweli-kweli ulio akibani kwa wote wanaomtii Mungu.—Yohana 5:28, 29.
Uhitaji wa Kutunza Uhai Wetu wa Sasa
Hili halimaanishi kwamba twaweza kwa kufaa kupuuza utakato wa uhai wetu wa sasa. Je, mwenye kiwanda atatumia wakati na pesa kutengeneza upya mashine kwa ajili ya mfanya-kazi asiyeitunza? Badala ya hivyo, je, mwajiri huyo hangempa mashine iliyotengenezwa upya mtu aliyefanya awezayo kudumisha ile nzee?
Uhai ni zawadi yenye thamani kubwa kutoka kwa Yehova. Akiwa mwanzilishi mkarimu wa zawadi hiyo, anatutaka tuitunze. (Zaburi 36:9; Yakobo 1:17) Akizungumza juu ya ufikirio wa Yehova kwa wanadamu duniani, Yesu alisema: “Hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote.” (Luka 12:7) Yehova aliwaamuru Waisraeli wasiue kimakusudi, jambo ambalo kihalisi lilitia ndani kutojiua kimakusudi. (Kutoka 20:13) Hili hutusaidia kutoona ujiuaji kimakusudi kama chaguo.
Wakijua upendezi wenye upendo wa Yehova kwa hali yetu bora, watu wenye kumhofu Mungu hutumia kanuni za Biblia katika mazoea ya kisasa. Kwa kielelezo, kwa kuwa Wakristo wa kweli wanapaswa ‘kujitakasa nafsi zao na uchafu wote wa mwili na roho, huku wakitimiza utakatifu katika kumcha Mungu,’ huepuka tumbako na dawa za kulevya zibadilizo akili.—2 Wakorintho 7:1.
Upendezi wa Mungu kwa uhai wa wanadamu unaonyeshwa zaidi katika shauri lake la kudumisha ‘moyo mtulivu’ na kuepuka mwenendo usio wa adili. (Mithali 14:30, NW; Wagalatia 5:19-21) Kwa kushikamana na hivi viwango vya hali ya juu, sisi tunalindwa kutoka kwa mambo kama hasira yenye kudhuru afya na maradhi yenye kupitishwa kingono.
Ufikirio wa Yehova kwa uhai wa watu wake pia waonekana wazi katika himizo lake la kujizuia kutokana na ulafi na unywaji wa kileo kupita kiasi. (Kumbukumbu la Torati 21:18-21; Mithali 23:20, 21) Wakristo wanaonywa kwamba watu wenye pupa na walevi hawataurithi Ufalme wa Mungu, yaani, hawataona uhai ulio kweli-kweli. (1 Wakorintho 6:9, 10; 1 Petro 4:3) Kwa kutia moyo kuwa na kiasi, Yehova hutufundisha ili tujifaidi wenyewe.—Isaya 48:17.
Tunaposhika viwango vya Mungu, twaonyesha kwamba twahazini uhai wetu wa sasa. Bila shaka, ulio wa maana hata zaidi ni uhai ulio kweli-kweli. Kwa kuwa ni wenye kudumu milele, Wakristo wa kweli huona ukiwa wa maana zaidi kuliko uhai wao wa sasa. Wakati Yesu Kristo alidhabihu uhai wake, alijitiisha chini ya mapenzi ya Yehova. Utii kwa Baba yake ulimaanisha mengi zaidi kwake kuliko maisha yake hapa duniani. Mwendo wa Yesu ulitokeza ufufuo wake na kupokea kwake uhai usioweza kufa katika mbingu. (Warumi 6:9) Kifo chake kinamaanisha pia uhai udumuo milele kwa wanadamu watiifu wanaozoea imani katika dhabihu yake ya fidia.—Waebrania 5:8, 9; 12:2.
Sheria Muhimu Kuhusu Damu
Inaeleweka kwamba, wafuasi wa Yesu wanaona mambo kama ayaonavyo. Wanatafuta kumpendeza Mungu katika mambo yote, kama vile Kristo alivyofanya. Kwa njia moja, hili laeleza sababu kwa nini wao hukataa utiaji-damu mishipani, ambayo madaktari fulani huiita yenye kuokoa uhai. Acha tuone jinsi mtu huonyesha kwamba anahazini uhai ulio kweli-kweli kwa kukataa utiaji-damu mishipani.
Kama vile Yesu Kristo, Wakristo wa kweli wanatamani kuwa hai machoni pa Mungu, na hilo huhitaji utii kamili Kwake. Neno la Mungu huamuru wafuasi wa Kristo hivi: “Mjiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa na uasherati.” (Matendo 15:28, 29) Kwa nini sheria hii kuhusu damu ilitiwa miongoni mwa amri zinazohusu Wakristo?
Sheria iliyopewa Waisraeli ilitaka wajiepushe na damu. (Mambo ya Walawi 17:13, 14) Wakristo hawako chini ya ile Sheria ya Kimusa. Lakini wanatambua kwamba amri hiyo ya kutokula damu ilitoka kwenye Sheria; hapo mapema ilikuwa imepewa Noa baada ya Gharika. (Mwanzo 9:3, 4; Wakolosai 2:13, 14) Amri hii ilihusu uzao wote wa Noa, ambao mataifa yote ya dunia yametoka kwao. (Mwanzo 10:32) Zaidi ya hayo, ile Sheria ya Kimusa inatusaidia kuona sababu ya Mungu ya kusisitiza juu ya utakato wa damu. Baada ya kuwakataza Waisraeli kutokula damu ya aina yoyote, Mungu alisema: “Kwa kuwa uhai wa mwili u katika hiyo damu; nami nimewapa ninyi hiyo damu juu ya madhabahu, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu; kwani ni hiyo damu ifanyayo upatanisho kwa sababu ya nafsi.” (Mambo ya Walawi 17:11) Damu ilizuiliwa na Mungu kwa ajili ya matumizi ya kidhabihu juu ya madhabahu. Sheria yake juu ya utakato wa damu hufunua mamlaka yake juu ya uhai wote duniani. (Ezekieli 18:4; Ufunuo 4:11) Tuonapo uhai wetu kwa maoni ya Yehova, tunatambua kwamba huo si mali yetu bali umekabidhiwa kwetu tu na Mungu.
Kama vile mtumiaji wa mashine katika kielezi chetu alivyokuwa na daraka juu ya mashine, tumekabidhiwa uhai wetu wa sasa. Ungefanya nini ikiwa mashine yako ilihitaji kutengenezwa na fundi wa mashine alipendekeza kupachika kiraka kwa kutumia vyuma visivyopendekezwa katika kitabu cha maagizo? Je, hungewaendea mafundi wa mashine wengine kuona kama mashine hiyo ingeweza kutengenezwa kupatana na kitabu cha maagizo? Uhai wa binadamu ni bora zaidi na mgumu kufahamika kuliko mashine. Katika Neno lake lililopuliziwa, kile kitabu cha maagizo cha kuwapa wanadamu uhai, Mfanyi wetu anakataza matumizi ya damu kutegemeza uhai. (Kumbukumbu la Torati 32:46, 47; Wafilipi 2:16) Je, si jambo la akili kushikamana na matakwa ya kitabu hicho cha maagizo?
Kwa kweli, Wakristo walio wagonjwa wanaoomba kutibiwa bila damu hawakatai aina zote za matibabu ya kitiba. Wanaomba tu matibabu ambayo yataonyesha heshima kwa uhai wao—wa sasa na wa wakati ujao. Madaktari wanaokubali kwa moyo mkuu msimamo uliochukuliwa na Wakristo wanatoa ushuhuda wa faida ya kuwatibu kulingana na ombi lao. “Kukutana na Mashahidi wa Yehova kuliniongoza kwenye adili zilizobadilika,” asema daktari mmoja mpasuaji aliyezoea kutumia damu sana. Sasa yeye hujaribu kutibu hata wasio Mashahidi bila damu.
Kuhazini Uhai Ulio Kweli-Kweli
Ni adili zipi mpya ambazo daktari-mpasuaji huyu alipata kwa kuwatibu Mashahidi wa Yehova? Yeye sasa anatambua kwamba kutibu mgonjwa kunatia ndani si sehemu ya mwili inayougua tu bali ni mwili mzima. Je, mgonjwa si anapaswa kuruhusiwa kuuliza utunzaji ulio bora kwa ajili ya hali njema yake ya kimwili, kiroho, na maono ya moyoni?
Kwa maoni ya Kumiko mwenye umri wa miaka 15, utiaji-damu mishipani kutibu leukemia yake yenye kuua ulikuwa uchaguzi mbaya zaidi uwezao kufanywa. Kujaribu kurefusha maisha yake kwa njia hii kwa majuma machache, miezi michache, au hata miaka hakukustahili kile ambacho angepoteza mwishowe. Akiwa ameweka maisha yake ya sasa wakfu kwa Yehova Mungu akiwa mmoja wa Mashahidi wake, aliheshimu utakato wa uhai na damu. Ingawa baba yake na watu wa ukoo wengine walipinga kwa nguvu msimamo wake, Kumiko alisimama imara. Daktari wake wakati mmoja alimuuliza hivi: “Ikiwa Mungu wako husamehe makosa, hangekusamehe hata ikiwa ungekubali kutiwa damu mishipani?” Kumiko alikataa kuridhiana na hivyo kukana imani yake yenye msingi wa Biblia. ‘Akifuliza kushika kwa mkazo neno la uhai,’ alidumisha msimamo wake. (Wafilipi 2:16, NW) Kama nyanya yake asiyeamini alivyosema, “Kumiko hangeacha imani yake.” Baada ya muda mfupi mtazamo wa baba na nyanya yake pamoja na ule wa madaktari wenye kumhudumia ulibadilika.
Imani ya Kumiko yenye nguvu katika Yehova Mungu, ambaye anaweza kumfufua kutoka wafu, ilisukuma mioyo ya wengi. Alipokuwa angali hai, alimsihi baba yake hivi: “Hata ikiwa nitakufa, nitafufuliwa katika Paradiso. Lakini ikiwa utaharibiwa katika Har–Magedoni, sitakuona. Kwa hiyo tafadhali jifunze Biblia.” Baba yake alifuliza tu kusema: “Utakapokuwa mzima, nitajifunza.” Lakini Kumiko alipokufa kwa ugonjwa wake usiomwacha, baba yake akaweka ndani ya kisanduku chake barua iliyosema: “Nitakuona katika Paradiso, Kumiko.” Baada ya hotuba ya maziko, alisema na wale waliohudhuria hotuba hiyo na kusema: “Nilimwahidi Kumiko kwamba ningemuona katika Paradiso. Ingawa bado siwezi kuamini hilo kwa sababu sijajifunza vya kutosha, nimeazimia kuchunguza jambo hilo zaidi. Tafadhali nisaidieni.” Wengine katika familia yake pia wakaanza kujifunza Biblia.
Kumiko alikuwa na staha ya kweli kwa uhai na alitaka kuishi. Alithamini yote ambayo madaktari wake walifanya ili kuokoa uhai wake wa sasa. Hata hivyo, kwa kufuata maagizo katika kitabu cha maagizo cha Muumba, alithibitisha kwamba alithamini uhai ulio kweli-kweli. Kwa mamilioni, huo utakuwa uhai udumuo milele katika dunia paradiso. Je, wewe utakuwa miongoni mwao?