Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Watu wa Mungu Hujitoa kwa Hiari
JINA lake lilikuwa Yusufu, naye alikuwa mkaaji wa kisiwa cha Saiprasi. Alikuwa miongoni mwa Wakristo wa karne ya kwanza waliouza mashamba na nyumba kuchangia kifedha kuendelea kwa Ukristo. Kwa sababu ya kuwa kwake na moyo mchangamfu na ukarimu, alijulikana kuwa Barnaba, maana yake “Mwana wa faraja.”—Matendo 4:34-37.
Kupendezwa huko kwa unyoofu katika wengine sikuzote kumekuwa alama ya waabudu wa kweli wa Yehova. Mashahidi wa Yehova leo hawako tofauti, kama ionyeshwavyo na ono lifuatalo kutoka Visiwa vya Solomon.
Kikundi cha Mashahidi zaidi ya 60 kutoka Australia na New Zealand kilisafiri kuelekea Honiara, jiji kuu la Visiwa vya Solomon kwenye Guadalcanal. Walikuja kusaidia ujenzi wa Jumba la Kusanyiko kwa ajili ya mikusanyiko mikubwa ya Kikristo. Iliwachukua karibu majuma mawili tu kujenga jumba lenye ukubwa wa kukaliwa la kiasi cha watu 1,200!
Karibu wakati huohuo, wenye mamlaka wa mji mdogo wa Munda, kwenye kisiwa cha New Georgia, waliwapa kutaniko la Mashahidi wa Yehova ploti katikati kabisa ya mji. Walitaka kujenga Jumba la Ufalme, mahali pa ibada. Na kwa kweli walilihitaji. Walikuwa wakikutana katika sebule ya nyumba ndogo ya majani, lakini hawakuwa na pesa za kujenga Jumba la Ufalme.a Kutaniko hilo lilikuwa hasa na wazee-wazee na watu wasiojiweza na watoto, na hakukuwa na yeyote mwenye ujuzi wa kazi ya ujenzi.
Karibu umbali wa kilometa 380, kwenye kisiwa cha Guadalcanal, Mashahidi katika jiji la Honiara walijitoa kwa hiari. (Zaburi 110:3) Wao walisababu hivi: “Ikiwa ndugu zetu katika nchi nyingine walitamani kutujengea Jumba la Kusanyiko kwa majuma mawili, basi kwa kweli twaweza kusaidia ndugu zetu katika Munda na kuwajengea Jumba la Ufalme kwa majuma mawili.”
Hivyo ndivyo ilivyotokea. Siku moja mashua ikiwa imebeba Mashahidi wajitoleaji wenye shangwe na wenye hamu ilifika katika Munda. Wanaume kwa wanawake, wazee kwa wachanga, wote walijishughulisha katika kupakua mizigo yao na kujitayarisha kuanza kujenga kwa mbao, saruji, mabati ya paa, na vifaa vingine vilivyokuwa vimefika Munda mbele yao.
Mara tu baada ya kazi kuanza, dhoruba kali la radi likakata ugavi wa maji wa mji huo. Hata hivyo, hili halikuthibitika kuwa tatizo lisiloweza kushindwa. Mashahidi walichimba kisima kilichotoa maji wakati wote wa kazi ya kujenga. Vipi juu ya chakula kwa wafanyakazi wote? Wala hilo halikuwa tatizo. Wajitoleaji kutoka Honiara walikuwa wametumwa wakiwa na chakula kingi kilichoandaliwa makutaniko ya Honiara. Walikuja hata na wapishi wao wenyewe!
Majirani walitazama maendeleo ya kazi hiyo kwa mshangao. Mmoja wao alisema hivi: “Mambo hayafanyiki katika siku kadhaa hapa. Yanachukua miaka.” Jirani mwingine, aliye kiongozi wa kidini, alikubali kwamba kanisa lake limekuwa likijengwa kwa muda wa miaka 20 ambayo imepita na kwamba bado halijamalizika. Kinyume cha hayo, Jumba la Ufalme jipya la Mashahidi wa Yehova katika Munda lilimalizwa kwa siku kumi tu!
[Maelezo ya Chini]
a Nyumba ya majani imejengwa na vifaa vilivyokatwa kutoka kichakani au msituni. Kiunzi kimetengenezwa kwa vijiti na fito, na paa na kuta zimefunikwa kwa paneli zilizotengenezwa kutoka majani ya mnazi yaliyofungwa kwenye vijiti na kushonelewa kwa mianzi.y
[Ramani katika ukurasa wa 24]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Bahari ya Pasifiki Kusini
VISIWA VYA SOLOMON
Munda
GUADALCANAL
Honiara
[Ramani]
AUSTRALIA
NEW ZEALAND