Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Kufikia Vijiji vya Mbali vya Greenland
KWA miongo mingi Mashahidi wa Yehova wametumia magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika kuhubiri habari njema. Majarida haya hutukuza hekima ya Yehova kama ionyeshwavyo katika Neno lake, Biblia. Yanatazama matukio ya ulimwengu yanayohusu unabii wa Biblia, nayo hutumia shauri lenye busara la Biblia kwa matatizo yaliyopo.—Yakobo 3:17.
Katika 1994, Mashahidi katika Greenland walifanya jitihada ya pekee ya kutoa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa watu wengi iwezekanavyo. Wakati wa kipupwe, walifanya mipango ya kutembelea vijiji kadhaa vya mbali zaidi vya Greenland. Kikundi cha wapiga-mbiu wa Ufalme kilisafiri kwa mashua zaidi ya kilometa 4,000 huko magharibi ya pwani hadi Qaanaaq (Thule), kikifikia jamii iliyoko kaskazini zaidi mwa dunia. Safari yao ilichukua majuma saba. Upande wa pwani ya mashariki, mume na mke walio Mashahidi walifika kijiji cha Ittoqqortoormiit na kwa mara ya kwanza wakahubiri kote habari njema kwa utaratibu.
Mapema mwaka huo, wakati wa mwezi wa Aprili, nakala 7,513 za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ziliangushiwa watu wa Greenland. Hiyo inamaanisha kwamba, kwa kukadiria, kila mhubiri wa Ufalme kati ya wale 127 aliangusha magazeti 59—gazeti 1 kwa kila wakazi 7. Mwezi huo, Amkeni! lilizungumzia mfululizo wa makala yenye kichwa cha jalada “Kansa ya Matiti—Hofu ya Kila Mwanamke.” Shahidi mmoja, aliyeangusha magazeti 140, alimwangushia ripota wa televisheni nakala za Amkeni! hiyo. Siku kadhaa baadaye, programu ya televisheni ilizungumza juu ya nakala za kansa ya matiti. Ripota huyo alionyesha gazeti hilo kwenye televisheni, akionyesha kurasa kadhaa huku akisifu tafsiri ya hali ya juu ya Kigreenland. Pia alikazia madokezo yenye kutumika ya kutunza afya ili kuzuia kansa ya matiti yaliyotolewa na Amkeni!
Shahidi aliyemwangushia ripota huyo magazeti hayo alihojiwa kwenye programu hiyohiyo ya televisheni. Alijibu maswali kadhaa juu ya Mashahidi wa Yehova na kuzungumza juu ya kugawanywa kwa upana kwa magazeti mwezi huo. Pia alitoa maelezo juu ya hekima yenye kutumika ipatikanayo ndani ya Biblia na kuonyesha kwamba shauri lenye busara kama hilo laweza kutusaidia kukabili matatizo ya siku hizi.
Programu hiyo ilimalizika kwa kuhojiwa kwa msimamizi wa Greenlandic Cancer Society. Alisema kwamba hakuwahi kamwe kuona habari nzuri na yenye kuarifu kama hiyo kuhusu jambo hili katika lugha yake. Kisha akawaomba wale wote wanaopendezwa na habari hiyo ya kansa ya matiti wasome nakala za Amkeni! Alisema kwamba kulikuwa na sababu nzuri ya kushukuru Mashahidi wa Yehova kwa ujianzilishi.
Kama ilivyokuwa katika Greenland, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanaendelea kuhubiri habari njema kwa “viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.” (Wakolosai 1:23; Matendo 1:8) Kwa kutumia fasihi ya Biblia, kutia ndani Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, wanasaidia watu wa aina zote kukabili matatizo ya siku hizi na vilevile kuwapa tumaini la wakati ujao ulio bora.
[Ramani katika ukurasa wa 8]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Qaanaaq (Thule)
Ittoqqortoormiit
Nuuk (Godthåb)