Sababu Iliyofanya Atumie Jina Kuu Kupita Yote
“Kulingana na mmoja wa wahakiki wangu, nimetenda dhambi kwa kuingiza neno ‘Yehova’ badala ya ‘Bwana,’ ambalo kwa karne nyingi limekuwa jina la badala kidesturi.”
Hilo lilikuwa elezo la J. J. Stewart Perowne katika utangulizi wa toleo la pili la tafsiri yake ya kitabu cha Zaburi, kilichotangazwa kwa mara ya kwanza katika 1864. Huyo mhakiki, akiandika katika Saturday Review la Julai 2, 1864, alipinga utumizi wa jina la Mungu katika hiyo tafsiri, kwa kuwa halikuwa likitumiwa tena ama katika makanisa ya Kiyahudi au ya Kikristo. Alidai kwamba jina Yehova linahusiana kwa ukaribu sana na Wayahudi na kwamba neno jingine lapaswa kutumiwa, kama vile “Bwana” au “Mungu,” “ambalo halihusiani na jambo lolote la mahali fulani au la kitaifa.”
Perowne hakukubaliana na kusababu huku, kwa kuwa “hakutamani kamwe kuondoa herufi hata moja” ya ufunuo wa Mungu kwa mwanadamu. Yeye alibisha kwa haki kwamba watafsiri wanaotafsiri jina la kimungu la Kiebrania “Bwana” hukosa kutofautisha kati ya maneno mawili ya Kiebrania.
Perowne aliendelea kusisitiza kwamba kulikuwa na wataalamu wenye kustahili ambao waliunga mkono kurudishwa kwa jina la kimungu. Alimnukuu mshairi mashuhuri Mwingereza Samuel Taylor Coleridge:
“Kwa nini kuendeleza tafsiri ya Kiebrania katika Kiingereza kwa njia ya kati, kupitia njia ya Septuagint? Je, hatujakubali rasmi neno la Kiebrania Jehovah? Je, lile Κύριος, au Bwana, ya Septuagint, si kibadala cha Kigiriki katika visa visivyohesabika kwa ajili ya neno la Kiebrania, Jehovah? Basi, kwa nini neno la awali lisirudishwe; na katika Agano la Kale lisitafsiriwe kwa umakini sana Yehova, kwa kutumia neno Yehova; na kila andiko katika Agano Jipya, linalorejezea Agano la Kale, kwa nini lisitumie neno la Kiebrania katika andiko linalorejezewa?”
Perowne alikiri kwamba tamko halisi la Tetragramatoni ya Kiebrania lilikuwa limepotea, lakini akasema: “Ikiwa kwa sababu za kishirikina tu utumizi wa jina hilo ulikomeshwa katika Kanisa la Kiyahudi, na ikiwa kwa sababu ya kunakili Tafsiri za Kigiriki na Kilatini kwa mwigizo Tafsiri yetu wenyewe [ya Kiingereza] ilipoteza jina hilo, hizi si sababu nzito dhidi ya kurudisha utumizi wa awali.” Perowne alipendelea jina “Yehova” kwa sababu lajulikana sana. Tangu wakati huo tafsiri kadhaa za kisasa pia zimetumia jina la kimungu. New World Translation of the Holy Scriptures hutumia jina hilo Yehova zaidi ya mara 7,200 katika Maandiko ya Kiebrania na Kigiriki.
Katika tafsiri yake ya Zaburi, Perowne alijaribu kushikamana “kwa ukaribu na namna ya lugha ya Kiebrania, katika msemo na katika muundo wa kisarufi wa maneno.” Alipokuwa akitafsiri Zaburi 69, mistari 5 na 6, aliona uhitaji wa kutofautisha kati ya maneno ya Kiebrania kwa “Mungu” (ʼElo·himʹ), “Bwana” (ʼAdho·naiʹ), na “Yehova”: “Ee Mungu [ʼElo·himʹ], Unajua upumbavu wangu, na hatia yangu haijafichwa kutoka Wewe. Usiache wale wanaokungoja waaibishwe kupitia mimi, Ee Bwana [ʼAdho·naiʹ], Yehova (Mungu wa) majeshi. Usiache wafedheheshwe, kupitia mimi, wale wanaokutafuta, Ee Mungu wa Israeli.”