Ni Nini Kilichoupata Uaminifu-Maadili?
MIAKA zaidi ya mia moja iliyopita, Barney Barnato, mtafutaji-almasi kwa kujasiria, alirudi Uingereza kutoka Afrika Kusini. Aliporudi hakuafiki hadithi ya gazeti la habari iliyoandikwa juu yake. Kwa hiyo alimpa mhariri maandishi yaliyoandikwa kwa mkono ili yatumiwe kwa makala ya pili, “kusahihisha mambo tu,” pamoja na hundi ya kiasi kikubwa cha fedha.
Mhariri, J. K. Jerome, aliyatupa maandishi hayo ndani ya kikapu cha kutupia takataka kisha akarudisha hiyo hundi. Kwa kustaajabishwa, mara moja Barnato alitoa kiasi maradufu cha fedha alizokuwa ametoa. Hizo zilikataliwa vilevile. “Wataka kiasi gani?” akauliza. Akikumbuka tukio hilo, Jerome asema hivi: “Nilimweleza kwamba hilo halikuwa desturi—si katika London.” Kwa wazi uaminifu-maadili wake akiwa mhariri haukuweza kuhongwa.
“Uaminifu-maadili” umefasiliwa kuwa “unyoofu wa kiadili; ufuatiaji wa haki.” Mtu mwenye uaminifu-maadili ni mwenye kutumainika. Lakini leo, ukosefu wa unyoofu—ukosefu wa uaminifu-maadili—unadhoofisha watu wa kila namna.
Katika Uingereza vyombo vya habari vimetumia sana neno “-shaufu” kufafanua ukosefu wa uaminifu-maadili wa kiadili. Kama lilivyosema gazeti la habari The Independent, -shaufu latia ndani “mambo yote kutoka mambo ya kimapenzi na udanganyifu wa kiserikali wa mahali fulani hadi kutoa kitu kidogo katika maagizo makubwa ya kuingiza bidhaa nchini.” Hakuna sehemu ya maisha isiyotiwa ndani.
Viwango vya Uaminifu-Maadili Vyenye Kubadilika-Badilika
Bila shaka, uaminifu-maadili haumaanishi ukamilifu, hata hivyo unaonyesha sifa ya msingi katika mtu. Katika ulimwengu wetu wa kujitajirisha upesi, uaminifu-maadili huenda ukaonekana kuwa kizuizi, wala si wema wa adili. Kwa kielelezo, kutumia kwa wanafunzi njia mbalimbali za hali ya juu za kupata majibu kwa udanganyifu katika mitihani kunaongezeka, na mbinu hizo mpya hazionekani kwa urahisi. Profesa mmoja Mwingereza wa chuo kikuu adai kwamba zaidi ya nusu ya wanafunzi wote Waingereza wamepata majibu kwa udanganyifu, na Uingereza si nchi pekee yenye udanganyifu huo.
Jambo lisilopasa kupuuzwa ni jinsi watu wasio na hatia wanavyoathiriwa wakati watu wasio wenye kutumainika wanaposema uwongo na kudanganya. Fikiria kisa cha mji wa India wa Bhopal ambako, katika 1984, gesi yenye sumu iliwaua wanaume, wanawake na watoto zaidi ya 2,500 na kujeruhi mamia ya maelfu wengine. The Sunday Times liliripoti hivi: “Mipango ya kusaidia wale wahasiriwa inazuiwa na ufisadi. . . . Ugumu wa kuchagua-chagua visa vilivyo halali umetatanishwa na maelfu ya madai yasiyo ya kweli, hati zilizoandikwa isivyo halali na ushuhuda bandia.” Tokeo ni kwamba, miaka kumi baadaye ni dola 3,500,000 tu kati ya ile ridhaa ya dola 470,000,000 zilizokuwa zimegawanywa kwa wale wenye uhitaji.
Namna gani dini? Inakadirishwaje katika jambo hili la uaminifu-maadili? Kwa kusikitisha, mara nyingi viwango vyayo ni sawasawa na vile vya kilimwengu. Chukua kwa kielelezo askofu Eamon Casey wa Katoliki ya Kiroma, aliyeungama kuwa baba ya mwana haramu, ambaye ni tineja sasa. Hali ya Casey, kama vile gazeti la habari la Uingereza Guardian lilivyoonyesha, “haikuwa ya kipekee.” Vivyo hivyo, The Times liliripoti hivi: “Ukweli juu ya fedheha ya Askofu Casey si kwamba kosa lake lilikuwa la kipekee, bali kwamba kutokuwa mwaminifu kwa useja si jambo jipya wala nadra.” Likiunga mkono hoja hiyo, The Glasgow Herald, la Scotland, ladai kwamba ni asilimia 2 tu ya makasisi wa Katoliki ya Kiroma katika Marekani ambao wameepuka mahusiano ya ngono ya jinsia tofauti na ugoni-jinsia-moja. Iwe tarakimu hiyo ni ya kweli au la, yaonyesha sifa ya makasisi wa Kikatoliki kwa habari ya adili.
Mtu mmoja-mmoja aonapo vielelezo hivyo, je yawezekana kwake kushika uaminifu-maadili wa kiadili? Je, kufanya hivyo kwastahili? Kungetaka mtu afanye nini, na thawabu za kufanya hivyo ni zipi?