Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 6/15 kur. 26-29
  • Kutembelea Shamba Letu la Umishonari la Nyumbani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutembelea Shamba Letu la Umishonari la Nyumbani
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Kushinda Kizuizi cha Lugha
  • Huduma Yetu Iliyo Tofauti-Tofauti
  • Tamaduni Mbalimbali
  • Matazamio Mazuri
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 6/15 kur. 26-29

Kutembelea Shamba Letu la Umishonari la Nyumbani

KIKUNDI cha makutaniko ya Kikristo ambacho mimi huzuru hunisafirisha kutoka Ureno hadi China—au hivyo ndivyo huonekana. Hata hivyo, mke wangu, Olive, nami huwa hatuondoki Uingereza kamwe.

Sisi hutembelea idadi inayokua ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yenye kuongea lugha za kigeni yaliyotawanyika kote nchini. Kutoka mbali kama vile kisiwa cha Jersey, yapata kilometa 20 hivi kutoka Normandy pwani ya Ufaransa, ambapo tuna kikundi cha Kireno, hadi kwenye mji wa Sunderland kaskazini mwa Uingereza, ambapo sisi hutembelea watu wenye kuongea Kichina, sisi hushiriki katika shamba lenye kusitawi, lenye fanaka kiroho, la lugha nyingi. Tulipataje mgawo huu usio wa kawaida? Na ni jambo gani linalotukia katika shamba letu la umishonari la nyumbani? Acheni nieleze.

Olive nami tumetumikia miaka ipatayo 20 katika kazi ya kusafiri, tukizuru kutaniko tofauti kila juma. Safari zetu zimetupeleka kutoka kaskazini hadi kusini, mashariki hadi magharibi, kotekote Uingereza, na hivi majuzi, kwa ndugu zetu Wakristo kwenye kisiwa cha Mediterania cha Malta, ambapo tuliona ukaribishaji-wageni wenye kutokeza wa Kikristo. (Linganisha Matendo 28:1, 2.) Baada ya miaka mitatu katika Malta, tulianza kujiuliza mgawo wetu ambao ungefuata ungekuwa wapi. Tuliwazia kwamba labda tungetembelea eneo la vijijini la Kiingereza, nasi tulianza kurekebisha akili zetu kwa uwezekano huo. Tulishangaa jinsi gani tulipopokea mgawo wetu wa kutumikia mzunguko huu mpya ulio na vikundi na makutaniko yanayosema lugha tofauti-tofauti 23!

Tulijiuliza jinsi tungefaulu. Mbali na mambo tuliyojionea Malta, hatukuwa kamwe tumejiingiza sana na watu wa malezi na utamaduni mbalimbali. Je, kweli tungeweza kuwatia moyo wale ambao hawakuelewa Kiingereza vizuri? Tungeweza kuwasilianaje bila kujua lugha nyingine mbalimbali? Vipi chakula na desturi za namna mbalimbali za wengine? Je, tungeweza kubadilikana vya kutosha? Maswali kama hayo yalizunguka akilini mwetu tulipokuwa tukifikiria kwa njia ya sala kujibu mwito huu wa Makedonia.—Matendo 16:9, 10; 1 Wakorintho 9:19-22.

Kushinda Kizuizi cha Lugha

“Mwanzoni nilihisi kuwa mwenye upungufu kwa sababu sikuwa na ujuzi wowote wa lugha,” aeleza Olive. “Sikuona jinsi ningeweza kusaidia akina dada. Kisha nikakumbuka jinsi wenzi waliooana ambao walijifunza nasi Biblia kwa mara ya kwanza walivyotutia moyo tusikatae mgawo kamwe. Walitufundisha kwamba Yehova hatuombi kamwe tufanye jambo tusiloweza kufanya.” Kwa hiyo sisi sote tulikubali mgawo huo kwa hiari.

Kwa kufikiria hilo, twaona kwamba kukosa kwetu kujua lugha nyingine kumetusaidia kumtendea kila mtu bila ubaguzi. Mathalani, kuhudhuria mikutano iliyoongozwa kwa lugha tofauti kila juma kumetufanya tung’amue jinsi akina ndugu walivyohisi walipolazimika kuhudhuria mikutano ya lugha ya Kiingereza huku wakielewa machache ya yale yaliyosemwa. Kwa kweli twalazimika kutayarisha vizuri kwa ajili ya mikutano ili tuweze kufahamu maana ya yale yanayosemwa. Sikuzote Olive hujibu mojawapo ya maswali mkutanoni. Yeye hutayarisha jibu katika Kiingereza na dada mmoja humtafsiria, akiandika tafsiri hiyo kama itamkwavyo. Yeye akubali kwamba hunyoosha mkono wake kwa kusitasita ili kutoa maelezo. Wakati mwingine jitihada zake husababisha kicheko. Lakini jambo hili halimzuii. “Najua akina ndugu huthamini kujaribu kwangu,” yeye asema. “Kwa hakika, maelezo yangu hutia moyo wale walio wazoefu wa lugha kushiriki katika mikutano.”

Kwangu mimi, kutoa hotuba ni jambo tofauti, pia, kwa sababu lazima niruhusu wakati kwa ajili ya mkalimani baada ya kila sentensi. Ni rahisi sana kupoteza mfuatano wangu wa mawazo. Naona kwamba lazima nikaze fikira zaidi na kupunguza habari yangu kwa kiwango kikubwa. Lakini naifurahia.

Huduma Yetu Iliyo Tofauti-Tofauti

Katika maeneo mengi ya majiji ya Uingereza, watu wanaosema lugha za kigeni wametawanyika huku na huko, labda wawili katika barabara moja, kisha lazima usafiri umbali fulani ili upate wengine. Hata hivyo, unapowasalimu katika lugha yao wenyewe na kuona itikio lao, unahisi kuwa ni jambo lenye kufaa. Ikiwa ndugu ninayeandamana naye anatoa ujumbe wa Ufalme kwa lugha ya mwenye nyumba mwenyewe, mara nyingi itikio huwa lenye upendezi mwingi.

Kwa kweli, huduma katika shamba la lugha ya kigeni ni mojawapo ya zile zenye kusisimua zaidi ambazo tumeona wakati wa miaka yetu 40 ya utumishi wa Ufalme. Uwezekano wa ukuzi ni mkubwa ajabu. Hakuna shaka kwamba watu wengi hujifunza haraka zaidi na kwa uthamini mwingi zaidi wanapofundishwa katika lugha yao wenyewe. (Matendo 2:8, 14, 41) Ni jambo lenye kuvutia sana kihisia-moyo kuona ndugu na dada wakiwa na machozi ya shangwe mwishoni mwa mkutano, katika visa fulani wakiwa wameweza kusikiliza na kuelewa programu yote kwa mara ya kwanza.

Tunapohubiri nyumba hadi nyumba, twajitahidi kutoa angalau utangulizi katika lugha ya mwenye nyumba, hata ingawa wakati mwingine twaona ugumu. Kwa kielelezo, salamu ya kawaida kwa watu wa nyumbani wa Kigujarati ni Kemcho, ambayo humaanisha tu “Habari gani?” Kosa nililofanya wakati mmoja katika matamshi lilisikika kana kwamba nilikuwa nikitangaza aina moja ya kahawa inayojulikana sana. Hata hivyo, kwenye nyumba moja mume na mke walitabasamu nilipowasalimu katika Kigujarati. Walitualika mara moja na wakatupatia kahawa kwa fadhili—si kwa sababu ya matamshi yoyote yenye makosa. Ilitokea kwamba walikuwa na uhusiano wa kijamaa na Mashahidi wa Yehova fulani katika kikundi tulichokuwa tukizuru, nao walionyesha kupendezwa kikweli na ile kweli.

Dada mmoja mwenye kuongea Kiingereza alimwachia bibi mmoja mwenye kuongea Kichina magazeti kwa muda wa kipindi cha miaka kadhaa. Pindi kwa pindi alikuwa amemtolea bibi huyo funzo la Biblia nyumbani bila malipo, lakini halikukubaliwa. Siku moja dada aliyekuwa akijifunza Kichina aliandamana naye na kumtolea kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani katika lugha hiyo, ambacho yule mwenye nyumba mwenye kupendezwa alikikubali.a Sasa akiwa na kitabu katika lugha yake mwenyewe, alikubali funzo la Biblia. Maneno hayo machache yaliyosemwa katika lugha ya huyo bibi mwenyewe yalikuwa na matokeo mazuri.

Tamaduni Mbalimbali

Hatukuwa tumeng’amua kwamba katika tamaduni kadhaa wanaume hawapendi wake zao kutoka nyumbani peke yao usiku. Hili hufanya iwe vigumu kwa dada wengi kuhudhuria mikutano inayofanywa jioni. Baadhi ya jamii za Kiasia huamini kwamba wanawake wachanga wanaochagua kutoolewa na ambao huendelea kuishi nyumbani hufedhehesha familia hiyo. Baba ya dada mmoja mchanga alitaka kujiua kwa sumu dada huyo alipokataa kuolewa na mwanamume ambaye familia yake ilikuwa imemchagulia. Naam, mambo ambayo dada hao lazima wavumilie ni ya kutokeza! Hata hivyo, unapoona matokeo ambayo kweli inakuwa nayo juu ya maisha ya familia hizo na jinsi uaminifu-mshikamanifu wa dada hao kwa Yehova unavyovutia wazazi wao, kwa kweli ni jambo zuri ajabu.

Katika kushiriki mgawo huu, tumelazimika kufanya mabadiliko kadhaa. Kabla ya kuanza kazi ya kusafiri, chakula changu kilipasa kutayarishwa kama vile hutayarishwa Uingereza, lakini sasa chakula kilicho na vikolezo, ni bora zaidi. Twajutia miaka mingi tuliyoacha ipite kabla hatujaanza kufurahia mapishi tofauti-tofauti kama hayo, yaani, kuanzia samaki zisizopikwa hadi mchuzi wenye viungo.

Matazamio Mazuri

Yaonekana wazi kwamba huu ndio wakati wa shamba la lugha za kigeni kukua katika maeneo mengi. Vichapo vingi zaidi sasa vinapatikana katika lugha mbalimbali. Waweza kutambua baraka za Yehova makutaniko mapya yapangwapo kitengenezo. Akina ndugu walio na ujuzi wa lugha nyingine mbalimbali huja kutoka makutaniko ya mbali ili kusaidia.

Kielelezo chenye kutokeza kimekuwa kule kuitikia kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme katika Kifaransa. Wakimbizi wengi wenye kusema Kifaransa kutoka Zaire na nchi nyingine za Afrika wamekuja Uingereza miaka ya majuzi. Kutaniko la kwanza katika lugha ya Kifaransa lilipofanyizwa London, baadhi ya watangazaji 65 wa Ufalme walishirikiana nalo. Mwaka mmoja baadaye hiyo idadi iliruka hadi watu 117, na kati ya hawa, watu 48 walitumikia kwa wakati wote wakiwa mapainia wa kawaida. Punde si punde, kutaniko la pili lilianzishwa ili kutunza wenye kupendezwa waliokuwa wakiongezeka. Sasa uangalifu mwingi zaidi waweza kupewa watu wenye kupendezwa, ambao kati yao watu 345 walihudhuria sherehe ya Ukumbusho ya 1995. Wahitimu wa zamani wa Gileadi ambao walitumikia katika Benin, Côte d’Ivoire, Moroko, na Zaire sasa wanatumia uzoefu wao kutunza shamba hili lenye kukua, nalo itikio ni la kushangaza.

Katika ziara moja kwenye kutaniko la Kifaransa, nilienda kwenye funzo la Biblia la mwanamke mmoja mchanga Mwafrika. Ilipotubidi kuondoka, mwanamke huyo mchanga alisihi: “Tafadhali msiende. Kaeni zaidi.” Yeye alitaka hasa kujua mengi zaidi. Alinikumbusha Lidia wa karne ya kwanza.—Matendo 16:14, 15.

Kazi yetu ya kwanza imekuwa kusaidia vikundi vidogo vya lugha za kigeni kuwa makutaniko. Mahali ambapo akina ndugu walifanya Funzo la Kitabu la Kutaniko la kila juma, tuliwaanzishia Shule ya Huduma ya Kitheokrasi iliyofupishwa ya kufanywa mara moja kwa mwezi. Hiyo huwasaidia wajieleze wenyewe vizuri katika utumishi wa shambani. Kisha wanafanyia kazi hatua kwa hatua kufanya mikutano yote mitano ya kutaniko kila juma. Tayari tuna makutaniko mapya ambayo husema Kichina (Kikantone), Kifaransa, Kigujarati, Kijapani, Kireno, Kipunjabi, Kitamil, na lugha ya Wales.

Pia tumefurahia pendeleo la kuhudhuria mikutano ya akina ndugu walio viziwi. Kutazama akina ndugu wakiimba kwa mikono yao ni jambo la kusisimua sana. Kung’amua kwamba katika huduma yao wao husema kwa ishara, nathamini sana jitihada zao bora kabisa za kushiriki katika kuhubiri Ufalme. Pia kuna wafasiri kwa walio viziwi na vipofu vilevile. Yaonekana kwamba Yehova huhakikisha kwamba hakuna mtu anayeachwa.

Ikiwa tungelazimika kufanya ombi mahususi, lingekuwa kama lile la Yesu: “Ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:38) Wengi wa ndugu zetu wanakubali ugumu wa kujifunza lugha ya vikundi vya kikabila vilivyo katika eneo la kutaniko lao. Ijapokuwa hatuna zawadi ya uwezo wa kusema lugha mbalimbali, bila shaka Yehova anafungua huduma katika shamba hili la umishonari la nyumbani—shamba lililo tayari kwa mavuno. (Yohana 4:35, 36)—Kama ilivyosimuliwa na Colin Seymour.

[Maelezo ya Chini]

a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki