Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 7/15 kur. 20-23
  • Okoa Maisha ya Mtoto Wako!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Okoa Maisha ya Mtoto Wako!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uwe Rafiki wa Karibu
  • Kumpenda Mungu
  • Kuhofu Mungu
  • Thawabu Zenye Shangwe
  • Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Wazazi—Wazoezeni Watoto Wenu Kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Je! Wewe Unafundisha Watoto Wako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Wazazi—Wasaidieni Watoto Wenu Wampende Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 7/15 kur. 20-23

Okoa Maisha ya Mtoto Wako!

MICHAEL na Alphina huishi katika bonde la mashambani katikati ya vilima vya kijani kibichi vya KwaZulu-Natal, Afrika Kusini. Walikabili magumu mengi katika kuwalea watoto saba. Kwa utegemezo kamili wa mkewe, Michael alifanya yote aliyoweza katika kutii hii amri ya Biblia kwa akina baba: “Endeleeni kuwalea [watoto wenu] katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Lakini nyakati nyingine matatizo hutokea.

Kwa kielelezo, ni jambo la kawaida kwa wachungaji wavulana Waafrika kuchanganya makundi ya ng’ombe za familia zao na zile za familia nyingine ili wawe na wakati wa kucheza pamoja. Nyakati nyingine wao hufanya utundu na huzungumza juu ya mambo ambayo hawapaswi kuyazungumza. Wana wa Michael walipotoka kwenda kuchunga ng’ombe za familia, aliwatolea maagizo makali wasishirikiane na watoto fulani. (Yakobo 4:4) Hata hivyo, aliporudi nyumbani kutoka kazini, nyakati nyingine aliwapata wakifanya hivyo. Tokeo ni kwamba, alilazimika kuwatia nidhamu.—Mithali 23:13, 14.

Je, wafikiri kwamba Michael alikuwa mkali mno kwa watoto wake? Huenda wengine wakahisi hivyo, lakini Yesu Kristo alisema kwamba “hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kwa kazi zayo.” (Mathayo 11:19) Michael na Alphina walitokeza hali yenye upendo nyumbani mwao, wakitumia wakati pamoja na watoto wao na kuwafundisha masimulizi na kweli za Biblia.

Michael na Alphina wana binti wanne—Thembekile, Siphiwe, Tholakele, na Thembekani. Wote ni wahubiri wa wakati wote wa habari njema ya Ufalme wa Mungu. Wawili wa wanao hutumikia wakiwa waangalizi-wasimamizi katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Mwana wao wa tatu, ambaye mkewe pia ni mweneza-evanjeli wa wakati wote, hutumikia akiwa mtumishi wa huduma.

Wazazi wengi Wakristo walio na familia kubwa wamebarikiwa kwa mafanikio katika kuwalea watoto wao. Hata hivyo, watoto fulani ambao hupokea malezi mazuri kutoka kwa wazazi huiacha kweli. Bila shaka, wazazi wao hukumbuka kielezi cha Yesu cha yule mwana mpotevu na wanatumaini kwamba mwana wao au binti yao atatubu na hatimaye afikie wokovu.—Luka 15:21-24.

Kwa kusikitisha, wazazi fulani Wakristo wanapoteza watoto wao wote kwenye ulimwengu. Hilo hasa ni sababu ya kuwa na hangaiko katika sehemu mbalimbali za Afrika ambako watoto waonekana kufanya vyema hadi wafikiapo miaka yao ya utineja. Ndipo, katika mchanuko wa ujana, wanatongozwa na njia zisizo za adili za ulimwengu wa Shetani. (1 Yohana 5:19) Tokeo ni kwamba, akina baba wengi huwa hawastahili kutumikia wakiwa wazee wa kutaniko. (1 Timotheo 3:1, 4, 5) Kwa wazi, baba Mkristo apaswa kuuona wokovu wa watu wa nyumbani mwake kuwa jambo lenye umaana mkubwa. Hivyo, wazazi waweza kufanya nini ili waokoe uhai wa watoto wao?

Uwe Rafiki wa Karibu

Yesu alikuwa si mkamilifu tu bali pia mkuu sana kuliko mwanadamu mwingine yeyote katika ujuzi na uzoefu. Hata hivyo, aliwatendea wanafunzi wake wasio wakamilifu kuwa marafiki wa karibu. (Yohana 15:15) Hiyo ndiyo sababu walitamani kuwa pamoja naye na kusitawi katika kuwapo kwake. (Yohana 1:14, 16, 39-42; 21:7, 15-17) Wazazi wanaweza kujifunza kutokana na hilo. Kama miti midogo iliyo na majani yenye kutambaa kuelekea mwanga wa jua, watoto husitawi kunapokuwa na hali ya urafiki, yenye upendo nyumbani.

Wazazi, je, watoto wenu hujihisi huru kuwafikia wakiwa na mahangaiko yao yote? Je, nyinyi huwasikiliza? Kabla ya kufikia mikataa, je, nyinyi huwafanya waseme mawazo na hisia zao ili mpate kuwaelewa kikamili? Je, nyinyi huwasaidia kwa subira kupata majibu ya maswali fulani kwa kufanya utafiti pamoja nao katika vichapo vya Biblia?

Mama mmoja kutoka Afrika ya Kusini aeleza hivi: “Tangu ile siku ya kwanza binti yetu alienda shuleni, tulimtia moyo asimulie yaliyotukia katika hiyo siku. Kwa kielelezo, ningemwuliza hivi: ‘Ulitumia mapumziko ya chakula cha mchana ukiwa na nani? Niambie juu ya mwalimu wako mpya. Anaonekanaje? Ni utendaji gani ambao umepangwa kwa ajili ya hili juma?’ Siku moja, binti yetu alikuja nyumbani na kusema kwamba mwalimu wa Kiingereza alikuwa akipanga kupeleka darasa kuona sinema ambayo baadaye wangeandika pitio juu yake. Kichwa cha hiyo sinema kilikuwa chenye kutilika shaka. Tulipofanya uchunguzi, tuligundua kwamba haingefaa kwa Mkristo. Tulizungumza juu yake tukiwa familia. Siku iliyofuata binti yetu alimfikia huyo mwalimu, akimweleza kwamba hakutaka kuiona hiyo sinema, kwa kuwa maadili iliyoyaonyesha hayangepatana na itikadi zake za Kikristo. Huyo mwalimu alilifikiria jambo hilo tena na baadaye akamshukuru binti yetu, akisema kwamba hakutaka kuipeleka hilo darasa kuona kitu ambacho angejutia.” Upendezi ambao hawa wazazi walionyesha bila ugeugeu katika wokovu wa binti yao ulizaa matunda mazuri. Yeye ana asili chanya, yenye furaha na sasa anatumikia akiwa mjitoleaji kwenye ofisi ya tawi ya Afrika Kusini ya Watch Tower Bible and Tract Society.

Yesu alitoa kielelezo bora kabisa katika kushughulika na watoto wa watu wengine. Alifurahia ushirika wao. (Marko 10:13-16) Wazazi wapaswa kuwa wenye furaha kama nini kufanya mambo pamoja na watoto wao! Katika sehemu fulani za Afrika, baba huona aibu kuonekana akicheza mpira au michezo mingine pamoja na wana wake. Lakini baba Mkristo hapaswi kamwe kuhisi kwamba yeye ni wa maana mno kuonekana akifanya mambo pamoja na watoto wake. Wachanga huhitaji wazazi wanaofurahia kutumia wakati pamoja nao. Hilo hulifanya liwe jambo rahisi zaidi kwa watoto kueleza mahangaiko yao. Mahitaji hayo ya kihisia-moyo yanapopuuzwa, huenda watoto wakawa wenye kusumbuka au wakajitenga, hasa ikiwa wanasahihishwa kila wakati.

Alipowaandikia Wakolosai juu ya uhusiano mbalimbali wa familia, Paulo alisema hivi: “Nyinyi akina baba, msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike, ili wasishuke moyo.” (Wakolosai 3:21) Huenda hilo likaonyesha kwamba nyakati nyingine kunakosekana usawaziko kati ya nidhamu nyingi mno na urafiki mdogo sana. Watoto, kutia ndani matineja, wanaopendwa na kuthaminiwa wataelekea zaidi kuitikia nidhamu inayohitajiwa.

Kumpenda Mungu

Urithi ulio wa thamani zaidi ambao wazazi waweza kuwapa watoto wao ni kielelezo chao katika kuonyesha upendo. Watoto wanahitaji kuona na kusikia wazazi wao wakisema na kuonyesha upendo wa kweli wa Mungu. Mwanamume kijana anayetumikia kwenye ofisi ya tawi ya Afrika Kusini ya Watch Tower Bible and Tract Society aeleza hivi: “Nilipokuwa mvulana, nilikuwa nikimsaidia baba yangu kazi za nyumbani. Nilifurahia kumsaidia, kwa sababu tu baba alithamini kikweli yale machache niliyofanya. Alikuwa akitumia huo wakati kuniambia mambo mengi juu ya Yehova. Kwa kielelezo, ninakumbuka Jumamosi moja tulipokuwa tukijitahidi kufyeka nyasi bustanini. Kulikuwa na joto sana. Baba alikuwa akitoa jasho, hivyo nilikimbia na kuleta gilasi mbili za maji na kuyatia barafu. Baba alisema hivi: ‘Mtoto, je, unaona jinsi Yehova alivyo mwenye hekima? Barafu huelea juu ya maji. Ikiwa ingezama, uhai wote ulio chini ya maziwa na vidimbwi ungekufa. Badala ya hivyo, barafu hutumika kama blanketi ya kufunikia! Je, hilo halitusaidii kumjua Yehova vizuri zaidi?’a Baadaye, nilipofungwa kwa ajili ya kudumisha kutokuwamo, nilikuwa na wakati wa kufikiri. Usiku mmoja nikiwa nimeshuka moyo katika seli yangu gerezani, nilikumbuka maneno hayo ya baba. Yalikuwa na maana ilioje! Ningemwabudu Yehova milele ikiwa ningeweza.”

Ndiyo, watoto huhitaji kuona kumpenda Mungu kukidhihirishwa katika kila jambo ambalo wazazi hufanya. Kumpenda Mungu na utii wenye hiari kwake wapaswa hasa uonekane kuwa nguvu inayochochea kuwapo kwenye mikutano ya Kikristo, kushiriki katika huduma ya shambani, na usomaji na funzo la familia la Biblia. (1 Wakorintho 13:3) La maana zaidi, kumpenda Mungu kwapaswa kudhihirishwa katika sala za familia za moyo wote. Umaana wa kuwapa watoto wako urithi kama huo hauwezi kukaziwa kupita kiasi. Hiyo ndiyo sababu Waisraeli waliamriwa hivi: “Nawe mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.”—Kumbukumbu la Torati 6:5-7; linganisha Mathayo 22:37-40.

Kizuizi kikubwa katika kumpenda na kumtii Mungu ni hali yetu ya kiasili yenye dhambi. (Waroma 5:12) Kwa hiyo, Biblia pia huamuru hivi: “Enyi mmpendao BWANA, uchukieni uovu.” (Zaburi 97:10) Mawazo mabaya mara nyingi huongoza kwenye matendo mabaya. Ili kuepukana nayo, lazima mtoto pia akuze tabia nyingine iliyo ya muhimu.

Kuhofu Mungu

Upendo uliochanganywa na hofu yenye staha ya kutompendeza Yehova ni jambo lifaalo sana. Yesu Kristo mwenyewe alituwekea kielelezo kikamilifu cha mmoja ambaye alipata upendezi “katika kumcha BWANA.” (Isaya 11:1-3) Hofu hiyo ni yenye umuhimu mtoto afikiapo mchanuko wa ujana na aanzapo kupata misukumo ya kingono yenye nguvu. Kumhofu Mungu kwaweza kumsaidia kijana kukinza misongo ya kilimwengu ambayo huenda ikaongoza kwenye mwenendo usio wa adili. (Mithali 8:13) Katika jumuiya fulani, wazazi huepuka kuwafundisha watoto wao jinsi ya kushughulika na vishawishi vya kingono. Kwa hakika, wengi huhisi kwamba ni makosa kuzungumza mambo hayo. Lakini tokeo la kuzembea huko kwa wazazi limekuwa nini?

Wataalamu watatu wa kitiba waitwao Buga, Amoko, na Ncayiyana walihoji wasichana 1,702 na wavulana 903 kutoka maeneo ya mashambani ya Transkei, Afrika Kusini. Jarida South African Medical Journal liliripoti kwamba “asilimia 76 ya wasichana na asilimia 90.1 ya wavulana katika uchunguzi huo tayari walikuwa na uzoefu wa kingono.” Umri wa wastani wa wasichana ulikuwa miaka 15, na wengi walikuwa wamelazimishwa kufanya ngono. Zaidi ya wasichana 250 walikuwa wamepata mimba mara moja au zaidi. Tokeo jingine lilikuwa kuathiriwa kwa kadiri kubwa na magonjwa ya kupitishwa kingono.

Yaonekana kwamba, wazazi wengi hawaoni uhitaji wa kuwafundisha watoto wao jinsi ya kuepuka ngono ya kabla ya ndoa. Badala ya hivyo, jarida linalotajwa hapo juu laeleza hivi: “Uzaaji-watoto, na hali ya kuwa mama ni sifa zinazothaminiwa sana za umwanamke katika jamii ya mashambani ya Transkei, na hilo hutambuliwa haraka na wasichana wanaotoka kubalehe.” Tatizo hilohilo limethibitishwa katika sehemu nyingine za ulimwengu.

Vijana wengi katika Afrika wanachambua wazazi wao kwa kukosa kuwasaidia kuelewa utendaji wa kingono. Wazazi fulani Wakristo wameona aibu mno kutumia kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako.b Katika ukurasa wa 20 hadi wa 23, chaeleza matumizi yenye heshima ya viungo vya uzazi na mabadiliko ambayo hutukia wakati wa kubalehe.

Wazazi Wakristo ambao hujitahidi kuzungumza maoni ya Mungu juu ya ngono pamoja na watoto wao ni wa kupongezwa. Jambo hilo linafanywa vizuri zaidi hatua kwa hatua, kulingana na uwezo wa mtoto wa kushika mambo. Ikitegemea jambo kama umri wa mtoto, huenda wazazi wakahitaji kuwa mahususi katika kutaja sehemu za mwili na kazi zake. La sivyo, kijana asiye na uzoefu huenda akakosa kuelewa yanayosemwa.—1 Wakorintho 14:8, 9.

Baba mmoja kutoka Afrika ya Kusini aliye baba wa binti wawili na mwana mmoja aeleza hivi: “Katika pindi nyingi, nilikuwa na fursa za kuzungumza juu ya mambo nyetivu ya kingono hata pamoja na wasichana. Ingawa hivyo, mke wangu alisikiliza kwa uangalifu sana, akitumia kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako. [Ona ukurasa wa 26-31.] Mwanangu alipokuwa na umri wa miaka 12, niliamua kumchukua kwa ajili ya matembezi marefu milimani. Katika pindi hiyo, tulizungumza kinaganaga na kwa urefu juu ya ukuzi wa mwili wa mvulana na kusudi la pekee huo ungetimiza katika ndoa. Nilizungumza naye pia juu ya uhitaji wa kuepuka zoea lenye kushusha la kupiga punyeto na kuwaona wasichana kwa njia yenye heshima na staha—kama awaonavyo mama na dada zake.”

Thawabu Zenye Shangwe

Baba na mama ambao wametoka tu kutajwa walifanya kazi kwa bidii na ni wenye furaha kwamba walikuwa na matokeo mazuri katika kulea watoto wao watatu. Wote wakiwa watatu sasa ni watu wazima, ambao wameolewa na Wakristo waaminifu. Mwana wao na wakwe zao wote hutumikia wakiwa wazee katika kutaniko la Kikristo, na wanne katika hao mume na mke wamekuwa waeneza-evanjeli wa wakati wote kwa miaka mingi.

Ndiyo, wazazi ambao hujitahidi kwa ajili ya wokovu wa watu wa nyumbani mwao waweza kutarajia thawabu yenye shangwe kutokana na watoto ambao huchagua kuitikia mafundisho hayo ya Biblia, kwa maana kitabu cha Mithali 23:24, 25 husema hivi: “Amzaaye mtoto mwenye hekima atamfurahia. Na wafurahi baba yako na mama yako.” Fikiria kwa uangalifu familia kubwa iliyotajwa mwanzoni mwa makala hii. “Nifikiriapo maendeleo ya kiroho ambayo watoto wangu wamefanya,” asema Alphina, “moyo wangu hububujika kwa shangwe.” Wazazi wote Wakristo na wafanye kazi kufikia thawabu hiyo yenye furaha.

[Maelezo ya Chini]

a Maji yafikiapo kiwango cha kuganda, huwa mepesi zaidi na huinuka juu. Ona ukurasa wa 137 hadi wa 138 wa kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Ona pia kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Baba anaweza kupanga kikao kifaacho ili kueleza mambo hakika ya maisha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki