Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 7/15 kur. 25-29
  • “Hukumu ya Kuchungua”—Je, Ni Fundisho Lenye Msingi wa Biblia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Hukumu ya Kuchungua”—Je, Ni Fundisho Lenye Msingi wa Biblia?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hiyo Ni Nini?
  • Kukosekana kwa Kiungo Muhimu cha Lugha
  • Muktadha Wafunua Nini?
  • Baadhi ya Majibu ya Maana
  • Je, Kitabu cha Waebrania Chaunga Mkono Fundisho la Wasabato?
  • Matatizo na Kipingamizi
  • Yehova Amwahidi Danieli Thawabu ya Ajabu
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
  • Jinsi Kitabu Cha Danieli Kinavyokuhusu
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
  • Kuwatambua Waabudu wa Kweli Katika Wakati wa Mwisho
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
  • Watiwa Nguvu na Mjumbe Kutoka Kwa Mungu
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 7/15 kur. 25-29

“Hukumu ya Kuchungua”—Je, Ni Fundisho Lenye Msingi wa Biblia?

OKTOBA 22, 1844, ilikuwa siku ya matumaini makubwa kwa zaidi ya watu 50,000 katika Pwani ya Mashariki ya Marekani. Kiongozi wao wa kiroho, William Miller, alikuwa amesema kwamba Yesu Kristo angerudi siku hiyo. Wafuasi wa Miller, kama walivyoitwa, walingojea katika sehemu zao za kukutania hadi usiku. Siku iliyofuata ikapambazuka, lakini Bwana hakuwa amekuja. Wakiwa wamezinduka, walirudi nyumbani na baada ya hapo waliiita siku hiyo kuwa “Mtamauko Mkubwa.”

Bado, baada ya muda mfupi, mtamauko uligeuka kuwa tumaini. Mwanamke kijana aliyeitwa Ellen Harmon alikisadikisha kikundi kidogo cha Wafuasi wa Miller kwamba Mungu amemfunulia katika maono kwamba hesabu yao ya wakati ilikuwa sahihi. Aliamini kwamba jambo la maana sana lilikuwa limetokea siku hiyo—wakati huo Kristo alikuwa ameingia “mahali patakatifu zaidi sana pa kimbingu.”

Zaidi ya mwongo mmoja baadaye, mhubiri Msabato James White (ambaye alikuwa amemwoa Ellen Harmon) alitunga maneno ya kuelezea namna ya kazi ya Kristo tangu Oktoba 1844. Katika Review and Herald la Januari 29, 1857, White alisema kwamba Yesu alikuwa ameanza “hukumu ya kuchungua.” Na hili limebaki kuwa fundisho la msingi miongoni mwa watu karibu milioni saba wanaojiita Wasabato.

Lakini, baadhi ya wasomi wanaoheshimiwa katika Kanisa la Sabato (SDA) wamekuwa wakishangaa ikiwa “hukumu ya kuchungua” ni fundisho lenye msingi wa Biblia. Kwa nini wanafikiria jambo hili tena? Ikiwa ungekuwa Msabato, swali hili lingekuhangaisha. Hata hivyo, kwanza, “hukumu ya kuchungua” ni nini?

Hiyo Ni Nini?

Andiko lililotajwa kuwa msingi wa fundisho hili ni Danieli 8:14. Husomeka hivi: “Akaniambia, Hadi siku elfu mbili na mia tatu; ndipo patakatifu patakaposafishwa.” (King James Version) Kwa sababu ya msemo “ndipo patakatifu patakaposafishwa,” Wasabato wengi huhusisha mstari huu na Mambo ya Walawi sura ya 16. Hilo huzungumzia kusafishwa kwa patakatifu na kuhani wa cheo cha juu wa Wayahudi wakati wa Siku ya Kufunika. Pia wao huhusianisha maneno ya Danieli na Waebrania sura ya 9, ambalo humtaja Yesu akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu Zaidi katika mbingu. Msomi mmoja Msabato asema kwamba kusababu huku kunategemea njia ya “kulinganisha maandiko.” Mtu hupata “neno fulani kama vile patakatifu katika Dan. 8:14, neno hilohilo katika Law. 16, neno hilohilo katika Ebr. 7, 8, 9” na huamua “kwamba yote yanazungumzia jambo moja.”

Wasabato husababu hivi: Makuhani wa Israeli la kale walifanya huduma ya kila siku katika chumba cha hekalu kilichoitwa Patakatifu, ikitokeza msamaha wa dhambi. Katika Siku ya Kufunika, kuhani wa cheo cha juu alifanya huduma ya mara moja kwa mwaka katika Patakatifu Zaidi Sana (chumba cha ndani zaidi cha hekalu) ambayo ilitokeza kufutwa kabisa kwa dhambi. Walifikia mkataa kwamba huduma ya kikuhani ya Kristo katika mbingu yatia ndani awamu mbili. Awamu ya kwanza ilianza kwa kupaa kwake katika karne ya kwanza, ikaisha katika 1844, na ilitokeza msamaha wa dhambi. Ya pili, au “awamu ya hukumu,” ilianza Oktoba 22, 1844, na bado inaendelea, na itatokeza kufutwa kabisa kwa dhambi. Hili linatimizwaje?

Tangu 1844, inasemwa kwamba Yesu anachunguza rekodi za maisha za wote wanaodai kuwa waamini (kwanza za wafu, kisha za walio hai) kuangalia ikiwa wanastahili kupata uhai wa milele. Uchunguzi huu ni “hukumu ya kuchungua.” Baada ya watu kuhukumiwa, dhambi za wale wanaopita jaribu hili zinafutwa kabisa kutoka kwenye kitabu cha kumbukumbu. Lakini, akaeleza Ellen White, wale wasiopita jaribu hili, ‘majina yao yatapasa kufutwa katika kitabu cha uhai.’ Hivyo, “mwisho wa watu wote utakuwa umeamuliwa kwa ajili ya uhai au kifo.” Kufikia hapo, patakatifu pa kimbingu panasafishwa na Danieli 8:14 kutimizwa. Hivyo ndivyo Wasabato wanavyofundisha. Lakini kichapo cha SDA Adventist Review chakiri hivi: “Mtajo hukumu ya kuchungua haupatikani katika Biblia.”

Kukosekana kwa Kiungo Muhimu cha Lugha

Fundisho hili limewasumbua baadhi ya Wasabato. “Historia yaonyesha,” asema mchunguzi mmoja, “viongozi wetu wenye uaminifu-mshikamanifu wamepitia maumivu makali ya kihisia-moyo kadiri wafikiriapo fundisho letu la kidesturi kuhusu hukumu ya kuchungua.” Katika miaka ya karibuni, aongeza, maumivu makali yaligeuka kuwa tashwishi wakati wasomi walipoanza “kutilia shaka mengi ya maelezo yetu makuu kuhusu kusafishwa kwa patakatifu.” Acheni tuchunguze mawili kati ya hayo.

Elezo kuu la kwanza: Danieli sura ya 8 launganishwa na Mambo ya Walawi sura ya 16. Maelezo hayo yanadhoofishwa kwa sababu ya matatizo mawili—lugha na muktadha. Kwanza fikiria lugha. Wasabato waamini kwamba ‘patakatifu paliposafishwa’ katika Danieli sura ya 8 ni kifananishi cha ‘patakatifu halisi paliposafishwa’ katika Mambo ya Walawi sura ya 16. Ufanani huo ulionekana kukubaliwa hadi watafsiri walipogundua kwamba “kusafishwa” katika King James Version ni makosa ya tafsiri ya muundo wa kitenzi cha Kiebrania tsadaq (kinachomaanisha “kuwa -enye uadilifu”) kilichotumiwa kwenye Danieli 8:14. Profesa wa theolojia Anthony A. Hoekema alisema: “Inasikitisha kwamba neno hilo lilikuja kutafsiriwa kusafishwa, kwani kitenzi cha Kiebrania ambacho kwa kawaida hutafsiriwa safishwa [ta·herʹ] hakitumiwi hapa hata kidogo.”a Kilitumiwa katika Mambo ya Walawi sura ya 16 ambapo King James Version hutafsiri miundo ya neno ta·herʹ kuwa “safisha” na “kuwa safi.” (Mambo ya Walawi 16:19, 30, NW) Kwa sababu hiyo, kwa usahihi Dakt. Hoekema afikia mkataa: “Ikiwa Danieli alimaanisha kurejezea aina ya kusafishwa ambayo ilifanywa katika Siku ya Kufunika, angetumia taheer [ta·herʹ] badala ya tsadaq [tsa·dhaqʹ].” Lakini, tsa·dhaqʹ halipatikani katika Mambo ya Walawi, na ta·herʹ halipatikani katika Danieli. Kiungo muhimu cha lugha kinakosekana.

Muktadha Wafunua Nini?

Sasa fikiria muktadha. Wasabato washikilia kwamba Danieli 8:14 ni “muktadha wenye kujitegemea,” na hauna uhusiano kabisa na mistari inayotangulia. Lakini je, wapata wazo kama hilo usomapo Danieli 8:9-14 katika kisanduku kilichoambatanishwa chenye kichwa “Danieli 8:14 Katika Muktadha”? Mstari wa 9 wamtambulisha mshambulizi, pembe ndogo. Mstari wa 10-12 watambulisha kwamba huyu mshambulizi atashambulia patakatifu. Mstari wa 13 wauliza, ‘Hata lini ushambulizi huu utaendelea?’ Na mstari wa 14 wajibu: “Hata nyakati za jioni na asubuhi elfu mbili na mia tatu; ndipo patakatifu patakapotakaswa.” Kwa wazi, mstari wa 13 watokeza swali ambalo linajibiwa katika mstari wa 14. Mwanatheolojia Desmond Ford asema: “Kuondoa Dan. 8:14 kutoka mlio huu [“Hata lini?” mstari wa 13] hakuungwi mkono na maandiko.”b

Kwa nini Wasabato wanaondoa mstari wa 14 kutoka katika muktadha? Kuepuka mwisho wenye kuaibisha. Muktadha waonyesha kwamba kunajisiwa kwa patakatifu, kulikotajwa katika mstari wa 14, ni utendaji wa pembe ndogo. Lakini, fundisho la “hukumu ya kuchungua” lahesabia kuchafuliwa kwa patakatifu na utendaji wa Kristo. Anaelezwa kuwa ahamisha dhambi za waamini kwenda katika patakatifu pa kimbingu. Hivyo, itakuwaje Wasabato wakikubali hilo fundisho na huo muktadha? Dakt. Raymond F. Cottrell, Msabato ambaye pia alikuwa mhariri-mshiriki wa SDA Bible Commentary, aandika: “Kujidanganya kwamba fasiri ya SDA juu ya Daniel 8:14 inategemea muktadha ni kuitambulisha pembe ndogo kuwa Kristo.” Dakt. Cottrell akiri kwa unyoofu: “Hatuwezi kuwa na vyote viwili, muktadha na fasiri ya Kisabato.” Kwa hiyo, kuhusiana na “hukumu ya kuchungua,” Kanisa la Kisabato lililazimika kufanya uteuzi—kukubali fundisho hilo au kukubali muktadha wa Danieli 8:14. Kwa kusikitisha, lilikubali fundisho na kukataa muktadha. Si ajabu, asema Dakt. Cottrell, kwamba wanafunzi wa Biblia wenye ufahamu walaumu Wasabato kwa “kufasiri katika Maandiko” kile ambacho hakiwezi “kupatikana katika Maandiko”!

Katika 1967, Dakt. Cottrell alitayarisha somo la shule ya Jumamosi juu ya kitabu cha Danieli, ambalo lilitumwa kwa makanisa ya SDA ulimwenguni pote. Lilifundisha kwamba Danieli 8:14 lahusiana na muktadha wake na kwamba ‘kusafishwa’ hakurejezei waamini. Jambo la maana, somo hilo halitaji “hukumu ya kuchungua.”

Baadhi ya Majibu ya Maana

Wasabato wanafahamu kwa kadiri gani kwamba elezo hili ni dhaifu sana kuweza kuunga mkono fundisho la “hukumu ya kuchungua?” Dakt. Cottrell aliwauliza viongozi mashuhuri 27 ambao ni wanatheolojia Wasabato, ‘Ni sababu zipi za lugha au muktadha mnazoweza kutoa ili kuunganisha Danieli sura ya 8 na Mambo ya Walawi sura ya 16?’ Walijibuje?

“Wote ishirini na saba walithibitisha kutokuwepo kwa sababu za lugha au muktadha kutumia Dan. 8:14 kwa ufananisho wa siku ya kufunika ya kisasa na hukumu ya kuchungua.” Aliwauliza, ‘Je, mna sababu nyingine za kufanya muunganisho huo?’ Wengi wa wasomi Wasabato walisema kwamba hawakuwa na sababu nyinginezo, watano walijibu kwamba walifanya kiunganishi hiki kwa sababu Ellen White alifanya, na wawili walisema kwamba walitegemeza fundisho hili juu ya “aksidenti nzuri” katika tafsiri. Mwanatheleojia Ford aeleza: “Mikataa kama hiyo itolewayo na watu bora kabisa miongoni mwa wasomi wetu yaonyesha kwa hakika kwamba fundisho letu la kidesturi kuhusu Dan. 8:14 haliwezi kutetewa.”

Je, Kitabu cha Waebrania Chaunga Mkono Fundisho la Wasabato?

Elezo kuu la pili: Danieli 8:14 inaunganishwa na Waebrania sura ya 9. “Kazi yetu yote ya awali hutegemea sana Ebr. 9 katika kuelezea Dan. 8:14,” asema mwanatheolojia Ford. Kuunganishwa huko kulianza baada ya “Mtamauko Mkubwa” katika mwaka wa 1844. Akitafuta mwelekezo, Mfuasi wa Miller Hiram Edson aliangusha Biblia yake juu ya meza ili ianguke ikiwa imefunguka wazi. Matokeo yakawa nini? Biblia ilifunguka wazi kwenye Waebrania sura ya 8 na 9. Asema Ford: “Kuna maelezo gani yenye kufaa zaidi na yenye kuonyesha dai la Wasabato kwamba sura hizi zina suluhisho la maana ya mwaka 1844 na Dan. 8:14!”

“Dai hilo ni muhimu sana kwa Wasabato,” aongeza Dakt. Ford katika kitabu chake Daniel 8:14, the Day of Atonement, and the Investigative Judgment. “Katika Ebr. 9 pekee . . . kunaweza kupatikana maelezo ya kina juu ya umaana wa . . . fundisho la patakatifu ambalo ni muhimu sana kwetu.” Naam, Waebrania sura ya 9 ni ile sura katika “Agano Jipya” inayoeleza umaana wa kiunabii wa Mambo ya Walawi sura ya 16. Lakini Wasabato pia wasema kwamba Danieli 8:14 ni ule mstari katika “Agano la Kale” ambao hufanya hivyo. Ikiwa maelezo yote mawili ni kweli, lazima pia kuwe na uhusiano kati ya Waebrania sura ya 9 na Danieli sura ya 8.

Desmond Ford asema: “Mambo fulani ni dhahiri mtu asomapo Ebr. 9. Hakuna dokezo la wazi kwenye kitabu cha Danieli, na kwa hakika hakuna kwenye Dan. 8:14. . . . Sura hiyo kwa ujumla ni utumizi wa Law. 16.” Aeleza: “Fundisho letu la patakatifu haliwezi kupatikana tu katika kitabu cha Agano Jipya ambacho huzungumzia umuhimu wa utumishi mbalimbali wa patakatifu. Hili limekubaliwa na waandishi Wasabato wenye kujulikana ulimwenguni pote.” Hivyo basi, elezo kuu la pili ni dhaifu sana kuweza kuunga mkono fundisho hili lenye utata.

Hata hivyo, mkataa huu si mpya. Kwa miaka mingi, asema Dakt. Cottrell, “wasomi wa Biblia wa kanisa wamekuwa wakijua matatizo ya ufafanuzi wa fasiri yetu ya kawaida ya Danieli 8:14 na Waebrania 9.” Karibu miaka 80 iliyopita, Msabato mashuhuri E. J. Waggoner aliandika: “Fundisho la Kisabato kuhusu patakatifu, pamoja na ‘Hukumu ya Kuchungua’ . . . , ni kukana tu ufuniko.” (Confession of Faith) Zaidi ya miaka 30 iliyopita, matatizo kama haya yaliwasilishwa kwenye Mkutano Mkuu wa viongozi wa Kanisa la Sabato.

Matatizo na Kipingamizi

Mkutano Mkuu uliteua “Halmashauri juu ya Matatizo Katika Kitabu cha Danieli.” Ilipaswa kutayarisha ripoti juu ya jinsi ya kutatua matatizo yanayohusu Danieli 8:14. Halmashauri ya watu 14 ilichunguza hilo tatizo kwa miaka mitano lakini ilishindwa kupendekeza suluhisho la pamoja. Katika 1980, mshiriki wa halmashauri Cottrell alisema kwamba wengi wa washiriki wa halmashauri walihisi kwamba fasiri ya Kisabato ya Danieli 8:14 yaweza “kuthibitishwa vizuri” kwa mfululizo wa “makisio” na kwamba matatizo “yapasa kusahauliwa.” Aliongeza: “Kumbuka, jina la halmashauri lilikuwa Halmashauri juu ya Matatizo Katika Kitabu cha Danieli, na wengi walikuwa wakishauri kwamba tusahau matatizo na tusiseme kitu chochote kuhusu matatizo hayo.” Hiyo ingekuwa sawa na “kusema kwamba hatuna majibu.” Basi wachache walikataa kuunga mkono maoni ya wengi, na hivyo basi hakukuwa na ripoti rasmi. Matatizo ya kimafundisho yalibaki bila kutatuliwa.

Akitoa maelezo juu ya kipingamizi hiki, Dakt. Cottrell asema: “Tatizo la maana ya Danieli 8:14 bado lipo kwa sababu kufikia sasa hatujaukabili ukweli kwamba lipo tatizo kubwa la fasiri ya andiko. Tatizo hili halitakwisha tukiendelea kujifanya kwamba hakuna tatizo, maadamu tunashikilia tukiwa mmoja-mmoja au wote pamoja maoni yetu ya awali bila kufikiri.”—Spectrum, jarida lichapishwalo na Association of Adventist Forums.

Dakt. Cottrell awasihi sana Wasabato “kuchunguza upya makisio ya msingi na kanuni za fasiri ambazo juu yake tumetegemeza fasiri yetu juu ya fungu hili ambalo—kwa Usabato—ni fungu la Maandiko la kimsingi.” Tungewatia moyo Wasabato kuchunguza hili fundisho la “hukumu ya kuchungua” ili kuona ikiwa maelezo yake makuu yana msingi imara wa Biblia au yana msingi usio imara wa mapokeo.c Mtume Paulo alisihi hivi kwa hekima: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana lililo bora.”—1 Wathesalonike 5:21.

[Maelezo ya Chini]

a Wilson’s Old Testament Word Studies hufafanua tsadaq (au, tsa·dhaqʹ) kuwa “kuwa -enye uadilifu, -a haki,” na taheer (au, ta·herʹ) kuwa “kuwa -angavu, -a kuwa bila doa, safi, iliyotakaswa; kuwa safi bila uchafu au unajisi.”

b Dakt. Ford alikuwa profesa wa dini katika chuo kinachoendeshwa na kanisa cha Pacific Union College katika Marekani. Katika 1980, uongozi wa SDA ulimpa likizo ya miezi sita ili kuchunguza hilo fundisho, lakini waliyakataa matokeo ya uchunguzi wake. Aliyachapisha katika kitabu Daniel 8:14, the Day of Atonement, and the Investigative Judgment.

c Kwa maelezo yenye kusababu juu ya Danieli sura ya 8, ona ukurasa wa 188-219 katika kitabu “Your Will Be Done on Earth,” kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

Danieli 8:14 Katika Muktadha

DANIELI 8:9 “Na katika moja ya pembe hizo ilitokea pembe ndogo, iliyokua sana, upande wa kusini, na upande wa magharibi, na upande wa nchi ya uzuri. 10 Nayo ikakua, kiasi cha kulifikilia jeshi la mbinguni; ikaangusha chini baadhi ya jeshi lile, na ya nyota, ikazikanyaga. 11 Naam, ikajitukuza hata juu yake aliye mkuu wa jeshi hilo, ikamwondolea sadaka ya kuteketezwa ya daima, na mahali pa patakatifu pake pakaangushwa chini. 12 Na jeshi likatolewa kwake pamoja na sadaka ya kuteketezwa ya daima, kwa sababu ya makosa; nayo ikaiangusha kweli hata chini; ikatenda ilivyopenda, na kufanikiwa.

“13 Ndipo nikamsikia mtakatifu mmoja akinena, na mtakatifu mwingine akamwuliza huyo aliyenena, Haya maono katika habari ya sadaka ya kuteketezwa ya daima, na lile kosa lifanyalo ukiwa, yataendelea hata lini, kukanyagisha patakatifu na jeshi? 14 Akamwambia, Hata nyakati za jioni na asubuhi elfu mbili na mia tatu; ndipo patakatifu patakapotakaswa.” (Italiki ni zetu.)—Union Version ya Kiswahili.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki