Msingi Sahihi wa Kutazamia Mema Leo
MWANAHISTORIA aliye pia msosholojia H. G. Wells, ambaye alizaliwa mwaka wa 1866, alikuwa na uvutano wenye nguvu juu ya kufikiri kwa karne ya 20. Kupitia maandishi yake mbalimbali, alifafanua usadikisho wake wa kwamba mileani ingekuwa wakati uleule na maendeleo ya kisayansi. Hivyo, kichapo Collier’s Encyclopedia chakumbuka “kutazamia mema kusiko na mipaka” kwa Wells, alipokuwa akifanya kazi bila kukoma ili kuendeleza mradi wake. Lakini pia chasema kwamba kutazamia mema kwake kulivunjwa-vunjwa wakati ambapo Vita ya Ulimwengu ya Pili ililipuka.
Wells alipopata kung’amua kwamba “sayansi ingeweza kuwa na matokeo maovu na vilevile mema, imani yake ikatoweka, naye akaanza kutazamia mabaya,” yataarifu kamusi Chambers’s Biographical Dictionary. Kwa nini hilo lilitokea?
Imani ya Wells na kutazamia mema kwake kulitegemea mafanikio ya kibinadamu tu. Alipong’amua kwamba wanadamu walikuwa hawawezi kufikia Mafikirio yake, hakuwa na kwingine kwa kugeukia. Kukata tumaini kuliongoza upesi kwenye kutazamia mabaya.
Leo, watu wengi wamejionea mambo hayohayo kwa sababu hizohizo. Wamejawa na matazamio mema wakiwa wachanga lakini huangukia kuwa na matazamio mabaya ya utusitusi wapatapo kuwa na umri mkubwa zaidi. Hata kuna wachanga ambao hujiuzulu kutoka katika yenye kuitwa maisha ya kawaida na kujitia katika matumizi mabaya ya dawa, ngono za ovyo-ovyo, na mitindo-maisha mingine yenye kuharibu. Utatuzi ni nini? Fikiria vielelezo vifuatavyo vya nyakati za Biblia na uone msingi uliopo wa kutazamia mema—wakati uliopita, wakati uliopo, na wakati ujao.
Kutazamia Mema kwa Abrahamu Kwathawabishwa
Mwaka wa 1943 K.W.K., Abrahamu alihama kutoka Harani, akavuka Mto Frati, na kuingia nchi ya Kanaani. Abrahamu amefafanuliwa kuwa “baba ya wote wale walio na imani,” naye aliweka kielelezo chema kama nini!—Waroma 4:11.
Abrahamu aliandamana na Loti, mwana yatima wa ndugu ya Abrahamu, na familia ya Loti. Baadaye, njaa kali ilipoikumba hiyo nchi, hizo familia mbili zilihamia Misri, na hatimaye zikarudi pamoja. Kufikia wakati huo Abrahamu na pia Loti walikuwa wamekusanya mali nyingi, na pia kondoo na ng’ombe wengi. Ugomvi ulipozuka kati ya wachungaji wao, Abrahamu alichukua hatua ya kwanza na kusema hivi: “Usiwepo ugomvi, nakusihi, kati ya mimi na wewe, wala kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako; maana sisi tu ndugu. Je! nchi hii yote haiko mbele yako? Basi ujitenge nami, nakusihi; ukienda upande wa kushoto, nitakwenda upande wa kuume; ukienda upande wa kuume, nitakwenda upande wa kushoto.”—Mwanzo 13:8, 9.
Abrahamu, akiwa na umri mkubwa zaidi, angaliweza kuelekeza mambo alivyopendelea, na Loti, kwa kumheshimu mjomba wake, angaliweza kukubaliana na chaguo la Abrahamu. Badala yake, “Lutu akainua macho yake, akaliona Bonde lote la Yordani, ya kwamba lote pia lina maji, kabla BWANA hajaharibu Sodoma na Gomora, lilikuwa kama bustani ya BWANA, kama nchi ya Misri hapo unapokwenda Soari. Basi Lutu akajichagulia Bonde lote la Yordani.” Akiwa na chaguo hilo, Loti alikuwa na kila sababu ya kutazamia mema. Lakini vipi Abrahamu?—Mwanzo 13:10, 11.
Je, Abrahamu alikosa busara, akihatarisha hali njema ya familia yake? La. Mtazamo chanya wa Abrahamu na roho yake ya ukarimu zilileta thawabu kubwa. Yehova alimwambia Abrahamu hivi: “Inua sasa macho yako, ukatazame kutoka hapo ulipo, upande wa kaskazini, na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi; maana nchi hii yote uionayo, nitakupa wewe na uzao wako hata milele.”—Mwanzo 13:14, 15.
Kutazamia mema kwa Abrahamu kulikuwa na msingi sahihi. Kulitegemea ahadi ya Mungu ya kwamba angefanya taifa kubwa kutokana na Abrahamu hivi kwamba “jamaa zote za dunia [zingeweza kujibariki kupitia Abrahamu].” (Mwanzo 12:2-4, 7) Sisi pia tuna sababu za kuwa na uhakika, tukijua kwamba “Mungu hufanya kazi zake zote zishirikiane pamoja kwa ajili ya mema ya wale wampendao Mungu.”—Waroma 8:28.
Wapelelezi Wawili Wenye Kutazamia Mema
Zaidi ya miaka 400 baadaye, taifa la Israeli lilikuwa tayari kuingia Kanaani, “ijaayo maziwa na asali.” (Kutoka 3:8; Kumbukumbu la Torati 6:3) Musa aliwatuma wakuu 12 ili ‘wapeleleze nchi na kuleta habari za njia iwapasayo kuipandia, na za miji watakayoifikia.’ (Kumbukumbu la Torati 1:22; Hesabu 13:2) Wapelelezi wote hao 12 walipatana katika ufafanuzi wa ufanisi wa hiyo nchi, lakini 10 kati yao walitoa ripoti ya kutazamia mabaya iliyotia hofu mioyoni mwa watu.—Hesabu 13:31-33.
Kwa upande mwingine, Yoshua na Kalebu waliwatolea watu ujumbe wa kutazamia mema na kufanya yote ambayo wangeweza ili kuiondolea mbali hofu zao. Mtazamo wao na ripoti yao zilionyesha kuwa kwao na uhakika kamili katika uwezo wa Yehova wa kutimiza neno lake la kuwarudisha katika Bara Lililoahidiwa—lakini hawakufanikiwa. Badala yake, “mkutano wote wakaamuru wapigwe kwa mawe.”—Hesabu 13:30; 14:6-10.
Musa aliwahimiza watu wamtumainie Yehova, lakini walikataa kumsikiliza. Kwa sababu waliendelea katika mtazamo wao wa kutazamia mabaya, taifa zima lililazimika kutanga-tanga nyikani kwa miaka 40. Kati ya wale wapelelezi 12, ni Yoshua na Kalebu tu waliojionea thawabu za kutazamia mema. Tatizo la msingi lilikuwa nini? Ukosefu wa imani, kwa kuwa watu walitegemea hekima yao wenyewe.—Hesabu 14:26-30; Waebrania 3:7-12.
Kuyumba-Yumba kwa Yona
Yona aliishi katika karne ya tisa K.W.K. Biblia yaonyesha kwamba alikuwa nabii mwaminifu wa Yehova kwa ule ufalme wa makabila kumi wa Israeli, wakati fulani katika utawala wa Yeroboamu wa Pili. Hata hivyo alikataa kukubali utume wa kwenda Ninawi ili kutoa onyo kwa watu. Mwanahistoria Yosefo asema kwamba Yona “aliona afadhali akimbie” kwenda Yafa badala yake. Huko alipanda mashua kwenda Tarshishi, yaelekea ni Hispania ya siku ya kisasa. (Yona 1:1-3) Sababu iliyomfanya Yona awe na mtazamo mbaya hivyo juu ya mgawo wake yaelezwa kwenye Yona 4:2.
Hatimaye Yona alikubali kutimiza utume wake, lakini alikasirika watu wa Ninawi walipotubu. Kwa hiyo Yehova akamfundisha somo zuri la huruma kwa kusababisha mtango ambao Yona alijikinga kwa kivuli chake, unyauke na kufa. (Yona 4:1-8) Hisia za Yona za majonzi wakati ambapo huo mmea ulikufa zingalipaswa kuelekezwa kwa kufaa zaidi kwa wale watu 120,000 katika Ninawi ambao hawakuweza “kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto.”—Yona 4:11.
Twaweza kujifunza nini kutokana na mambo aliyojionea Yona? Utumishi mtakatifu hauruhusu kutazamia mabaya hata kidogo. Tuking’amua mwelekezo wa Yehova na kuufuata tukiwa na uhakika kamili, tutaonea shangwe mafanikio.—Mithali 3:5, 6.
Kutazamia Mema Katikati ya Majanga
“Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya,” akatangaza Mfalme Daudi. “Usiwahusudu wafanyao ubatili.” (Zaburi 37:1) Hilo, kwa kweli, ni shauri lenye hekima kwa kuwa leo ukosefu wa haki na upotovu ni mambo yatuzungukayo pande zote.—Mhubiri 8:11.
Hata hivyo, hata ikiwa hatuwahusudu wafanyao ubatili, ni rahisi kuhisi tukiwa tumetamauka tuonapo watu wasio na hatia wakiteseka mikononi mwa waovu au wakati ambapo sisi wenyewe tunatendewa kwa ukosefu wa haki. Mambo hayo yaweza hata kusababisha tusitawishe mtazamo wa kukata tamaa au wa kutazamia mabaya. Tuhisipo hivyo, twapaswa kufanya nini? Kwanza, twaweza kukumbuka kwamba waovu hawawezi kudhania kwa kuridhika kwamba kisasi hakitalipizwa kamwe. Zaburi 37 yaendelea kutuhakikishia hivi katika mstari wa 2: “Maana kama majani [watenda mabaya] watakatika mara, kama miche mibichi watanyauka.”
Kwa kuongezea, twaweza kuendelea kufanya lililo jema, kuendelea kutazamia mema, na kumngojea Yehova. “Jiepue na uovu, utende mema, na kukaa hata milele,” akaendelea mtunga-zaburi. “Kwa kuwa BWANA hupenda haki, wala hawaachi watauwa wake.”—Zaburi 37:27, 28.
Kutazamia Mema kwa Kweli Hudumu!
Basi, vipi wakati ujao wetu? Kitabu cha Biblia cha Ufunuo hutuambia juu ya mambo “ambayo lazima yatukie upesi.” Miongoni mwayo, farasi mwenye rangi-moto, akifananisha vita, afunuliwa ‘ili aondolee mbali amani katika dunia.’—Ufunuo 1:1; 6:4.
Dhana maarufu—na ya kutazamia mema—iliyokuwako Uingereza wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilikuwa kwamba ingekuwa vita kubwa ya mwisho. Mwaka wa 1916, mwanasiasa Mwingereza David Lloyd George aliona mambo kihalisi zaidi. Alisema hivi: “Vita hii, kama vile vita ifuatayo, ni vita ya kumaliza vita.” (Italiki ni zetu.) Hakukosea. Vita ya Ulimwengu ya Pili iliongeza tu utokezaji wa njia za kikatili zaidi za kuangamiza matungamo ya watu. Zaidi ya miaka 50 baadaye, bado mwisho wa vita hauko karibu.
Katika kitabu hichohicho cha Ufunuo, twasoma juu ya wapanda-farasi wengine—wakiwakilisha njaa kali, magonjwa ya kuambukiza, na kifo. (Ufunuo 6:5-8) Hizo ni pande zaidi za ishara ya hizo nyakati.—Mathayo 24:3-8.
Je, hizo ni sababu za kutazamia mabaya? La hasha, kwa kuwa hilo ono lafafanua pia “farasi mweupe; na yeye aketiye juu yake alikuwa na upinde; naye akapewa taji, naye akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.” (Ufunuo 6:2) Hapa twaona Yesu Kristo akiwa Mfalme wa kimbingu akiondoa uovu wote, akipanda farasi ili atokeze amani na upatano ulimwenguni pote.a
Akiwa Mfalme-Mteule, Yesu Kristo alipokuwa duniani alifundisha wanafunzi wake wasali juu ya Ufalme huo. Labda wewe pia umefundishwa kusema “Baba yetu,” au Sala ya Bwana. Katika hiyo twasali Ufalme wa Mungu uje, ili mapenzi yake yatimizwe hapa duniani kama mbinguni.—Mathayo 6:9-13.
Badala ya kujaribu kutia kiraka mfumo wa mambo uliopo, Yehova, akitenda kupitia Mfalme wake wa Kimesiya, Kristo Yesu, atauondoa kabisa. Mahali pake, Yehova asema: “Naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” Chini ya serikali ya Ufalme wa kimbingu, dunia itapata kuwa makao ya mwanadamu yenye amani, yenye furaha, mahali ambapo maisha na kazi zitakuwa shangwe yenye kudumu. “Mkashangilie daima kwa ajili ya hivi niviumbavyo,” asema Yehova. “Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.” (Isaya 65:17-22) Ukitegemeza tumaini lako la wakati ujao juu ya ahadi hiyo ya hakika, utakuwa na kila sababu ya kutazamia mema—sasa na milele!
[Maelezo ya Chini]
a Kwa ajili ya mazungumzo marefu ya ono hilo, tafadhali ona sura ya 16 ya kitabu cha Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 4]
H. G. Wells
[Hisani]
Corbis-Bettmann