Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Uvumilivu Waongoza Kwenye Baraka ya Mungu Katika Malawi
YOSEFU alikuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova. (Waebrania 11:22) Pia alikuwa mtu mwenye uvumilivu wenye kutokeza. Hata ingawa alisalitiwa na ndugu zake mwenyewe, akauzwa utumwani mara mbili, na baadaye akatupwa gerezani kwa sababu ya mashtaka yasiyo ya kweli, Yosefu hakuvunjika moyo. Badala ya hivyo, alivumilia kwa subira miaka ya dhiki, akingojea baraka ya Yehova kwa unyenyekevu.—Mwanzo 37:23-28, 36; 39:11-20.
Hali kadhalika leo, Mashahidi wa Yehova katika Malawi wamengojea baraka ya Mungu kwa subira. Kwa miaka 26, Mashahidi hao Wakristo walivumilia marufuku za kiserikali, upinzani mkali, na ukatili mwingi. Lakini uvumilivu wao ulikuwa na matokeo mazuri!
Mnyanyaso ulipozuka katika Malawi mwishoni mwa mwaka wa 1967, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme wapatao 18,000. Wazia shangwe ya hao Mashahidi walipopata kujua kwamba mwaka wa utumishi wa 1997 ulianza na kilele kipya cha wahubiri 38,393—zaidi ya maradufu ya idadi ya mwanzoni mwa marufuku! Isitoshe, hudhurio kwenye ile “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya 13 iliyofanywa Malawi, liliongezeka kupita 117,000. Kwa kweli, Yehova amebariki imani yao na uvumilivu wao.
Kielelezo cha baraka hiyo ni jambo lililoonwa la Machaka, mvulana mwenye umri wa miaka 14. Machaka alipokubali toleo la kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, wazazi wake walikasirika sana. Walisema hivi: “Ikiwa wataka kuwa Shahidi, lazima uhame kutoka nyumbani.” Hata hivyo, tisho hilo halikumvunja moyo asiendelee na funzo lake. Tokeo ni kwamba, wazazi wa Machaka walitwaa mavazi yake yote. Akina ndugu waliitikia kwa kumnunulia mavazi mengine zaidi. Wazazi wa Machaka walipopata kujua hilo, walimwambia hivi: “Ikiwa hao Mashahidi watakutegemeza, lazima uondoke na kwenda kuishi nao.” Baada ya kufikiria hilo jambo kwa uangalifu, Machaka aliondoka nyumbani, na familia ya Mashahidi katika kutaniko la mahali hapo ikamchukua.
Wazazi wa Machaka walikasirika sana hivi kwamba waliamua kuhama kutoka eneo hilo ili waepuke kabisa kukutana na hao Mashahidi. Bila shaka, Machaka alisononeshwa na hilo, lakini alipata faraja nyingi wakati ambapo hao ndugu walizungumza naye juu ya andiko la Zaburi 27:10, ambalo lataarifu hivi: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.”
Baada ya muda, wazazi wa Machaka walilegeza msimamo wao, naye akaamua kurudi nyumbani. Yaonekana azimio la mwana wao la kumtumikia Yehova lilikuwa na uvutano wenye nguvu juu yao kwa sababu wao pia walitaka funzo la Biblia na Mashahidi wa Yehova! Pia walihudhuria siku zote tatu za “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya, ambao baada yake walisukumwa kujulisha waziwazi hivi: “Kwa kweli, hili ni tengenezo la Mungu.”
Ndiyo, upinzani waweza kuwa wenye kujaribu, lakini wajumbe waaminifu-washikamanifu wa Mungu hawakati tamaa. Wao husonga mbele kwa ujasiri, wakijua kwamba “dhiki hutokeza uvumilivu; nao uvumilivu, hali yenye kukubaliwa.” (Waroma 5:3, 4) Mashahidi wa Yehova katika Malawi waweza kuthibitisha ifaavyo kwamba uvumilivu huongoza kwenye baraka ya Mungu.