Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 1/1 kur. 18-27
  • ‘Wenye Furaha Ni Wale Ambao Wamevumilia’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Wenye Furaha Ni Wale Ambao Wamevumilia’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Yehova Huvumilia
  • Uvumilivu Wathawabishwa
  • Mwaka Wetu Ambao Ndio wa Mambo Makubwa Zaidi
  • Uaminifu Wenye Kuendelea Chini ya Jaribu
  • Kukabiliana na Ubaridi
  • Yaliyomo Katika Wakati Ujao
  • Uvumilivu—Muhimu kwa Wakristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Uvumilivu Unaopata Ushindi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • “Mfikirieni Sana Yeye Ambaye Amevumilia”
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • “Acheni Uvumilivu Ukamilishe Kazi Yake”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 1/1 kur. 18-27

‘Wenye Furaha Ni Wale Ambao Wamevumilia’

1. Tangu 1914, ni hali gani duniani imetimiza Mathayo 24:3-8, na ni madai gani ya Ushirika wa Mataifa na Umoja wa Mataifa yameshindwa?

THE PRESENT AGE (Kizazi cha Sasa), kitabu ambacho kimetungwa na Robert Nisbet, chanena juu ya “ile Vita ya Miaka Sabini na Mitano ambayo imeendelea, ikiwa na mara chache tu za kutulia, tangu 1914.” Ndiyo, “vita na ripoti za vita,” kutia na vita vya ulimwengu​—hayo ndiyo mambo ambayo Yesu Kristo alitabiri kwa wakati huu wa mwisho. (Mathayo 24:3-8, NW) Ushirika wa Mataifa ulitokezwa katika 1920 “kuzuia vita milele.” Nao ukashindwa vibaya we! Umoja wa Mataifa ulipangwa kitengenezo katika 1945 “kuokoa vizazi vitakavyofuatana ili visipatwe na pigo la vita.” Lakini kitabu cha Max Harrelson Fires All Around the Horizon chasimulia hivi: “Tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu 2 ni mara haba sana ambapo imekuwako siku isiyokuwa na pigano mahali fulani.”

2. Watu fulani huuliza nini kuhusu hali za ulimwengu, lakini twapaswa kuwa tunauliza maswali gani?

2 Uvamizi-haramu na jeuri, ufisadi na umaskini, dawa za kulevya na magonjwa ya kipuku​—yote haya yaongezea ile hali ya kusikitisha. Huenda watu fulani wakauliza hivi: ‘Jamii ya kibinadamu yawezaje kuendelea kuvumilia hali hizo zenye kusumbua?’ Ingawa hivyo, jambo la maana zaidi ni kwamba twapaswa kuuliza hivi: ‘Ikawaje Mungu avumilie kuumbuliwa kwa sura ya uumbaji wake wa kidunia? Ni kwa muda gani zaidi yeye ataruhusu wanadamu waovu waharibu dunia na kurundika suto juu ya jina lake lenye thamani kubwa?’

3. (a) Nabii Isaya aliuliza swali gani, na kwa nini? (b) Yehova alitoa jibu gani, nalo laonyesha nini kwa siku yetu?

3 Nabii Isaya alitokeza swali kama hilo. Yeye alipewa mgawo awajulishe wazi wananchi wenzake ujumbe fulani kutoka kwa Yehova. Lakini alitangulia kuonywa kwamba hawangemtii yeye wala Mungu aliyemtuma. Kwa hiyo Isaya akauliza hivi: “Ee Bwana [Yehova, NW] hata lini?” Naam, Isaya angekihubiria hata lini kikundi hiki cha watu washupavu, naye Yehova angechukuliana hata lini na katao lao lenye ufidhuli wa kutotii ujumbe wake? Yehova alijibu hivi: “Hata miji itakapokuwa ukiwa, haina wenyeji, na nyumba zitakapokuwa hazina watu, na nchi hii itakapokuwa ganjo kabisa.” (Isaya 6:8-11) Vilevile leo, Mungu huvumilia masuto hayo mpaka ufike wakati wake uliowekwa wa kufikiliza hukumu juu ya ulimwengu ambamo mkosaji mkuu amekuwa ni Jumuiya ya Wakristo isiyo na imani.

4. Tokeo la uvumilivu wa Ayubu lilikuwa nini, na hiyo yatupa uhakikishio gani leo?

4 Yehova amevumilia kwa muda mrefu dhihaka kali za Shetani. Kama miaka 3,600 iliyopita, Ayubu mwenye imani alivumilia pia, akikanusha dai la Shetani kwamba yeye hangeweza kushika ukamilifu chini ya mtihani. Hiyo ilisababisha moyo wa Yehova ushangilie kama nini! (Ayubu 2:6-10; 27:5; Mithali 27:11) Kama vile Yakobo ndugu-nusu wa Yesu alivyotaarifu baadaye: “Tazama! Sisi twawatamka kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia. Nyinyi mmesikia juu ya uvumilivu wa Ayubu na mmeona tokeo ambalo Yehova alitoa, kwamba Yehova ni mwororo sana katika shauku na rehema.” Vilevile, wale ambao huvumilia pamoja na Yehova leo wahakikishiwa tokeo lenye furaha.​—Yakobo 5:11, NW.

5. Yesu alionyeshaje kwamba uvumilivu ungetakwa kwa watu wa Mungu leo, nao wangehitaji kuvumilia wafanyapo kazi gani?

5 Yesu alionyesha wazi kwamba uvumilivu ungetakwa kwa watu wa Mungu katika siku yetu. Katika kutabiri ishara ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” alisema hivi: “Yeye ambaye amevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” Avumilie akifanya nini? Maneno yale yale yafuatayo ya Yesu yajibu hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia nzima yote inayokaliwa kwa ajili ya ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:3, 13, 14, NW) Hapo tu ndipo ‘mwisho utakuja.’​—Ona pia Marko 13:10, 13; Luka 21:17-19.

Kwa Nini Yehova Huvumilia

6. Kwa nini Yehova ni kielelezo cha kutokeza cha uvumilivu, na ni nini sababu moja ambayo imefanya avumilie?

6 Mtume Paulo alieleza kwamba “Mungu; ingawa ana nia ya kuonyesha hasira kuu yake na kufanya nguvu zake zijulikane, alivumiliana kwa ustahimilivu mwingi na vyombo vya hasira kuu vilivyofanywa vifae kwa uharibifu.” (Warumi 9:22, NW) Kwa nini Yehova amevumilia kuendelea kuwako kwa waovu, vyombo hivi vya hasira kuu? Sababu moja ni hii: kuonyesha kwamba utawala wa kibinadamu usipotegemea Muumba wa mwanadamu ni lazima ukose mafanikio hata iweje. (Yeremia 10:23) Muda si muda, enzi kuu ya Mungu itatetewa wakati yeye athibitishapo kwamba yeye peke yake ndiye awezaye kuiletea jamaa ya kibinadamu amani, upatano, na furaha, kupitia utawala wa Ufalme wa Yesu.​—Zaburi 37:9-11; 45:1, 6, 7.

7. Ni kwa sababu gani nyingine Yehova amevumilia, na hiyo imeleta manufaa gani kwa mamilioni tangu miaka ya 1930?

7 Zaidi ya hilo, Yehova amevumilia “ili audhihirishe wingi wa utukufu wake katika vile vyombo vya rehema.” (Warumi 9:23) Vyombo hivi vya rehema ni wapakwa-mafuta wenye kushika uaminifu wa kimaadili ambao ‘wamenunuliwa kutoka miongoni mwa aina ya binadamu’ wakatawale pamoja na Kristo Yesu katika Ufalme wake wa kimbingu. Kutiwa muhuri kwa wale 144,000 kumeendelea kuanzia nyakati za mitume. Sasa kwakaribia kumalizika. (Ufunuo 7:3; 14:1, 4) Na tazama! Tangu miaka ya 1930 uvumilivu wa Yehova wenye kuendelea umeruhusu mamilioni wengine wakusanywe, “umati mkubwa . . . kutoka mataifa yote,” ambao washangilia tazamio la kuokoka ile dhiki ya mwisho ili warithi uhai wa milele katika dunia-paradiso. (Ufunuo 7:4, 9, 10, 13-17) Je! wewe ni mmoja wa umati mkubwa huo? Ikiwa ndivyo, je! wewe huteremi kwamba Yehova amevumilia kuwapo kwa vyombo vya hasira kuu mpaka sasa? Hata hivyo, ni lazima uendelee kuvumilia, kama vile Yehova amevumilia.

Uvumilivu Wathawabishwa

8. Kwa nini sisi sote twahitaji uvumilivu, na twapaswa kufikiria kielelezo gani cha uvumilivu kwa kukikazia macho?

8 Sisi sote twahitaji uvumilivu ikiwa tutapokea ahadi hizo. Baada ya kutaarifu ukweli huu wa msingi kwenye Waebrania 10:36, mtume Paulo aeleza kwa kirefu imani na uvumilivu kabambe wa “wingu [kubwa] la mashahidi” wa nyakati za kale. Halafu yeye atushauri ‘tupige kwa uvumilivu mbio ambayo imewekwa mbele yetu, huku tukimtazama kwa kumkazia macho Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu. Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake,’ Yesu alivumilia katika utumishi wa moyo mzima, bila kuacha kamwe kuitazama thawabu. Lo, jinsi kielelezo chake chatuimarisha sisi kuvumilia pia!​—Waebrania 12:1, 2, NW.

9. Kumekuwa na tokeo gani kutokana na vielelezo vya ki-siku-hizi vya uvumilivu?

9 Vielelezo vya ki-siku-hizi vya uvumilivu ni tele pia. Huenda ukawa wawajua, au umepata kuwajua, ndugu na dada ambao wamekuwa wa kutokeza katika uvumilivu wao. Lo, uaminifu wao umetuchocheaje! Na kila mwaka, Mashahidi wa Yehova wapelekapo ripoti ya utendaji wao wa ulimwenguni pote kwa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, masimulizi zaidi ya uvumilivu na kushika uaminifu wa kimaadili hupokewa. Chati iliyo katika kurasa nne zifuatazo ni muhtasari wa kazi kubwa iliyofanywa katika 1989 wakati ambapo Mashahidi hawa ‘wameongeza uvumilivu kwenye imani yao.’​—2 Petro 1:5, 6, NW.

Mwaka Wetu Ambao Ndio wa Mambo Makubwa Zaidi

10. (a) Mabara na vikundi vya visiwa vilivyoshiriki kuhubiri habari njema za Ufalme katika 1989 ni vingapi, na ni vingapi vilivyokuwa na sehemu katika kazi hii? (b) Ni mapainia wangapi walioripoti katika ule mwezi wa kilele, na ni jumla ya saa ngapi zilizotumiwa katika utumishi wa shambani?

10 Kama vile ionyeshwavyo na chati iliyotangulia, mabara 212 na vikundi vya visiwa vilishiriki kuhubiri Ufalme wa Yehova unaokuja. Ewe msomaji mpendwa wa Mnara wa Mlinzi, je! ulikuwa na pendeleo la kuwa mmoja wa wale 3,787,188 walioshiriki kazi kubwa hii? Je! ulikuwa mmoja wa wale 808,184 walioripoti kuwa mapainia katika mwezi ule wa kilele cha utumishi huo? Hata kiwe ni kiasi gani ambacho wewe ulichanga kwenye jumla ya saa 835,426,538 zilizotumiwa duniani pote katika utumishi wa shambani wakati wa 1989, una sababu ya kushangilia.​—Zaburi 104:33, 34; Wafilipi 4:4.

11. (a) Ni hudhurio gani kwenye Ukumbusho wa Machi 22 iliyopita lililo kisababishi cha ushangilio, na kwa nini? (b) Ni wangapi waliobatizwa, na ni mabara gani katika chati yaliyokuwa yenye kutokeza kuhusiana na jambo hili?

11 Shangilia, pia, katika jumla ile ya kupendeza sana ya wahudhuriaji 9,479,064, Machi 22 iliyopita, kwenye mwadhimisho wa ulimwenguni pote wa Ukumbusho wa kifo cha Yesu! Hii yaonyesha kwaweza kuwako wapiga mbiu zaidi 5,691,876 wa Ufalme, ikiwa tu watu hawa walio kama kondoo waweza kufanyiwa uchungaji wa upendo waingie katika lile zizi la kondoo, wawe na sehemu ya ukawaida katika kutumikia Yehova. Je! sisi twaweza kuwasaidia katika jambo hili? (Yohana 10:16; Ufunuo 7:9, 15) Tayari wengi wanaitikia, kama ionyeshwavyo na ile jumla kuu ya Mashahidi wapya 263,855 waliobatizwa wakati wa mwaka wa utumishi wa 1989.

12. Ni nini baadhi ya sehemu ambazo ile chati haifunui wazi (a) kuhusu viwanda vya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi? (b) kuhusu maangusho ya magazeti na maandikisho?

12 Kuna sehemu fulani-fulani ambazo chati aifunui wazi. Kiu ya kutaka vichapo​—Biblia, vitabu, broshua, magazeti​—ilishindikana kutoshelezwa. Tokeo ni kwamba, viwanda vya Mnara wa Mlinzi katika New York vilitumia tani 25,999 za karatasi katika kuchapa Biblia, vitabu, na broshua 35,811,000, hilo likiwa ni ongezeko la 101 zaidi ya 1988. Viwanda vingine vikubwa vya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, sana-sana katika Ujeremani, Italia, na Japani, vilifanya kazi za ziada kwa zamu, vikimuunga mkono “mtumwa mwenye imani na busara” katika kutoa chakula [cha kiroho] kwa wakati unaofaa.” (Mathayo 24:45, NW) Wakati wa Aprili na Mei, yaliripotiwa maangusho mazuri sana isivyo kawaida ya magazeti na maandikisho katika mabara kadhaa, mkazo wa pekee ukiwa juu ya kugawanya yale matoleo ya Mnara wa Mlinzi yaliyohusu “Babuloni Mkubwa.” (Ufunuo 17:5, NW) Bila shaka, Aprili huu unaokuja, mapainia-wasaidizi na Mashahidi wengine watamiminika kuingia katika shamba la ulimwengu katika ile itakayothibitika tena kuwa ndiyo kampeni yetu iliyo nzuri zaidi ya kutoa ushahidi mwaka wa utumishi wa 1990.​—Linganisha Isaya 40:31; Warumi 12:11, 12.

13. Ni nchi gani zenye kuorodheshwa katika chati ambazo hazikuorodheshwa mwaka uliopita? Eleza.

13 Itazame tena chati. Je! waona nchi fulani ambazo hazikuorodheshwa kwa jina mwaka uliopita? Oh, ndiyo! . . . Hangari, Polandi, . . . Baadhi yazo ni mahali ambapo ni mbali na sehemu nyinginezo na ndiyo sasa tu mbegu za ukweli wa Ufalme zimeanza kutia mizizi. Lakini katika Hangari na Polandi, kazi yetu imehalalishwa kisheria hivi majuzi. Sisi twawashukuru wenye mamlaka katika mabara haya kwa jambo la kwamba sasa wao wawaonyesha Mashahidi wa Yehova ufikirio. Katika habari hii, sala za udugu wa ulimwenguni pote zimejibiwa, “ili kwamba sisi tupate kuendelea kuendesha maisha ya utulivu na ya unyamavu pamoja na ujitoaji kimungu ulio kamili na uzito.”​—1 Timotheo 2:1, 2, NW.

14. Toa baadhi ya mambo makuu ya “Ujitoaji Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya katika Polandi.

14 “Ujitoaji kimungu”! Naam, “Ujitoaji Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya iliweza kufanywa hata katika Polandi, katika mahali patatu, wakati wa Agosti! Lo, ndugu zetu Wapolandi 91,024 walithibitika kuwa wenyeji wazuri kama nini katika kupokea wageni! (Waebrania 13:1, 2, 16) Kana kwamba kwa muujiza, makumi ya maelfu ya akina ndugu Wacheki, Wajeremani, Warusi, na wengine​—walijipatia hati za kusafiria ili waje kwa basi, gari-moshi, na hata kwa miguu. Maelfu wengine waliingia nchini kwa kuruka kwa ndege kutoka zile kontinenti za Amerika, kutoka Ulaya ya Magharibi, na kutoka mbali kule kwenye visiwa vya Pasifiki na Japani. Zile stediamu kubwa sana, ambazo ndugu zetu walizisafisha zikang’aa kabisa, hazikutosha vizuri kuwapa nafasi watu 65,710 kule Chorzow, 40,442 kule Poznan, na 60,366 kule Warsaw​—jumla kubwa ya hudhurio la 166,518! Kwenye kila kitovu, tamasha ya ubatizo ilifanya machozi ya hisia-moyo za shangwe yatiririshwe. Kule Poznan kijana wa miaka 9 na mzee wa miaka 90 walizamishwa, na jumla ya watu 6,093 waliozamishwa kwenye mikusanyiko mitatu hiyo ilikuwa ni kutia ndani matineja wengi sana, wengi wao wakiwa wametoka mabara ambako ilikuwa imesemwa kwamba dini ingefifilia mbali itokomee pamoja na vizee vya zamani. Sivyo ilivyo kuhusu dini ya kweli ambayo msingi wayo ni Neno la Mungu! (Linganisha Zaburi 148:12, 13; Matendo 2:41; 4:4.) Lo, uvumilivu wa ndugu zetu katika Ulaya ya Mashariki umethawabishwa vizuri ajabu!

Uaminifu Wenye Kuendelea Chini ya Jaribu

15. Mashahidi katika Lebanoni wameonyeshaje uvumilivu na uthibitifu, na matokeo yakawa nini?

15 Kama mtume Paulo, Mashahidi wa Yehova huitiwa wito wa kuonyesha uvumilivu chini ya hali nyingi mbalimbali. (2 Wakorintho 11:24-27) Katika Lebanoni vita ya wenyewe kwa wenyewe yawaka moto. Ndugu zetu waitikiaje? Kwa uthibitifu na kupiga moyo konde. Katika mwaka 1989 vikombora na makombora yalimiminwa kweli kweli, lakini hata katika sehemu yalikomiminwa kwa wingi sana, akina ndugu walipiga moyo konde wasipunguze mwendo. Kundi moja katika Beirut laripoti hivi: “Vikundi vya ukawaida kwa utumishi wa shambani vilipangwa katika jioni zote za juma. Kujapokuwa na hali zenye magumu ya usalama, akina ndugu hawakuvunjika moyo. Sisi tulimaliza maeneo mengi zaidi ya wakati mwinginewo uliotangulia. Katika Aprili tulikuwa na kilele katika hesabu ya mapainia. Mafunzo mapya ya Biblia yalianzishwa, na magazeti na vitabu zaidi vikaangushwa.”

16. Ndugu zetu katika Kolombia wameonyeshaje uvumilivu kwa kuleta habari njema kwenye miji ambako hakukuwa na Mashahidi wowote?

16 Kolombia imekuwa ikivuma katika taarifa za habari kwa sababu ya ulanguzi wa dawa za kulevya na jeuri. Lakini pia habari zavuma kwamba Wakristo huko wavumilia kwa uaminifu. Hivi majuzi, mapainia wa pekee wa muda walitumwa kwenye miji 31 yenye wakaaji kumi elfu au zaidi ambako hakukuwa na Mashahidi wowote. Katika mji mmoja, watu walioanza kupendezwa karibuni walipojua kwamba mapainia wangekuwa huko kwa miezi michache tu, waliwaomba sana mapainia hao wakae huko. Katika mji mwingine, watu 18 wenye kupendezwa walitia sahihi barua ya uthamini kwa msaada wa kiroho waliopewa wakati mapainia walipokaa huko miezi mitatu, na wakaomba msaada wa ziada. “Haya si mambo ya kuchezea,” wakasema. Ni wazi kwamba katika visa vyote viwili mipango ilifanywa ili kuendelea kusitawisha upendezo huo. Kusitawisha eneo la mbali hivyo huhitaji uvumilivu, lakini kazi ngumu ya mapainia wenye kufanya hivyo hubarikiwa kwa wingi.

17, 18. (a) Mashahidi wa Yehova wamevumilia katika Italia wakiwa chini ya hali za jinsi gani? (b) Mashahidi wamekuwa na hali gani ijapokuwa mambo ya uwongo yameenezwa kuwahusu?

17 Katika Italia, Mashahidi wa Yehova hukabili upinzani mkali wa makasisi, lakini wamevumilia kwa imara ya Yehova. Katika mitaa mbalimbali ya kanisa, makasisi waligawanya vibandiko ili vibanwe kwenye milango ya nyumba za wanamitaa wao vikiambia Mashahidi wa Yehova wasipige kengele ya kubisha hodi. Mapadri wengi walikusanya wavulana wachanga waweke vibandiko hivyo kwenye milango yote katika eneo fulani hususa​—hata kwenye nyumba za jamaa Mashahidi! Hata hivyo, Mashahidi hawatishiki kwa urahisi, na mara nyingi wao hutumia vibandiko hivyo kuanzisha maongeo. Zaidi ya hilo, magazeti na televisheni ya kitaifa yalitangaza jambo hilo kwa mapana yakilaani vikali ukosefu ulioonyeshwa wa kutovumilia maoni ya wengine kidini na yakakazia kwamba kwa kweli mbinu za namna hii ni ishara ya udhaifu kwa upande wa kanisa. Profesa mmoja wa chuo kikuu aliudhiwa mara nyingi sana na vibandiko hivyo vyenye kuwapinga Mashahidi mpaka akaandikisha awe akipata Mnara wa Mlinzi na Amkeni!

18 Kanisa Katoliki katika Italia hata hutumia waasi-imani kueneza mambo ya uwongo kuhusu watu wa Yehova, lakini hata jambo hili hukosa mafanikio kwa sababu wale wahubiri 172,382 wajulikana sana na kustahiwa. Mwanamume mmoja aliambia Mashahidi wenye kuzuru kwamba alikuwa amesoma mambo mabaya kuhusu sisi katika fasihi zilizoandikwa na waliokuwa Mashahidi hapo kwanza. Kwa hiyo, yeye alipinga sana wakati ndugu yake alipokuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ingawa hivyo, baada ya muda aliona tokeo jema ambalo lilipata ndugu yake kwa kubadili dini. Alishangaa kwa kujiuliza hivi: ‘Yawezekanaje kitu kibaya sana kitokeze matokeo mema jinsi hiyo?’ Kwa sababu hiyo, aliomba awe na funzo la Biblia pamoja na Mashahidi wenye kuzuru.​—Linganisha Wakolosai 3:8-10.

Kukabiliana na Ubaridi

19, 20. (a) Ni hali gani imetaka uvumilivu kwa upande wa Mashahidi katika Finland, na uchunguzi mmoja uliofanywa na kanisa kuhusu maoni ya watu una jambo gani la umaana mkubwa? (b) Ni ono gani latoa kielezi cha umaana wa uvumilivu katika kuhubiri habari njema?

19 Katika mabara ambako Mashahidi huzuru mara nyingi, watu huwa na ubaridi mwingi kuelekea habari njema. Hakika hivyo ndivyo ilivyo katika Finland. Kanisa katika bara hilo liliendesha uchunguzi wa maoni ya watu na kupata kwamba asilimia 70 ya idadi ya watu hawapendi Mashahidi wazuru nyumba zao. Hata hivyo, asilimia 30 hawakatai kwa uthabiti, na kati ya hawa, asilimia 4 walisema kwamba kwa kweli wao wawapenda Mashahidi wa Yehova. Hii ni tarakimu kubwa. Asilimia nne ya idadi ya watu wa Finland yawakilisha watu 200,000. Ilinganishe na tarakimu ya sasa ya wahubiri 17,303!

20 Uangalifu wa mhubiri mmoja akiwa katika utumishi ulielekezwa kwenye uchunguzi huo wa maoni naye akaulizwa hivi: “Je! wewe hujui kwamba asilimia 70 kati yetu huwaona nyinyi watu kuwa msiotamanika? Mbona nyinyi mnakuja-kuja kwenye milango yetu?” Mhubiri huyo alijibu hivi: “Ndivyo ilivyo, lakini uchunguzi uo huo ulionyesha kwamba asilimia 4 kati yenu mwatupenda. Sisi tunajaribu kutafuta watu hao. Hata kama wangekuwa asilimia 1 tu, bado sisi tungeenda nyumba kwa nyumba tukijaribu kuwatafuta.” Mwenye nyumba alifikiria kidogo na kusema: “Ujumbe wenu ni wa maana kwao kadiri hiyo?” Mhubiri akajibu kwa kuuliza: “Wewe ungependa kuusikia?” Muda si muda mwenye nyumba huyu akadhihirisha kupendezwa na habari njema.

Yaliyomo Katika Wakati Ujao

21. (a) Ni pigano la aina gani ambalo ni lazima tufanye katika mfumo huu, na kwa nini? (b) Huenda tukalazimika kuvumilia nini, na unabii wa Habakuki watuhakikishia nini?

21 Namna gani sisi sote leo? Je! sisi tumepiga moyo konde tuvumilie pamoja na Yehova na Kristo Yesu moja kwa moja hadi mwisho? Huenda usiwe ni muda mrefu mno, lakini ni lazima tuvumilie! Katika mfumo wa Shetani, twalazimika kufanya pigano kali kwa ajili ya ile imani, huku ukosefu wa adili, ufisadi, na chuki za ulimwengu zikiwa zatuzunguka pande zote. (Yuda 3, 20, 21) Huenda tukalazimika kuvumilia mnyanyaso wa aina hii au hii. Hata sasa, maelfu ya ndugu zetu wanateseka katika magereza, na baadhi yao hupigwa kikatili. Wao ni wenye shukrani kwa sala zetu. (2 Wathesalonike 3:1, 2) Karibuni sana, mfumo uliopo utatokomea! Kama vile Habakuki ataarifu: “Njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia [haitachelewa, NW].”​—Habakuki 2:3.

22. Ni tokeo gani ambalo sisi twaweza kutarajia kwa uhakika ikiwa tutajizoeza saburi ya manabii na uvumilivu wa Ayubu?

22 Mwanafunzi Yakobo atuambia hivi kwa upendo: “Akina ndugu, wachukueni manabii kama kigezo cha kupatwa na uovu na kujizoeza saburi, ambao walinena katika jina la Yehova.” Sisi leo ambao twanena katika jina la Yehova twaweza kuwa washikaji wa uaminifu wa kimaadili wakati wa majaribu machungu, kama walivyokuwa Isaya, Yeremia, Danieli, na wengine. Kama Ayubu, sisi twaweza kuvumilia. Lo, yeye alithawabishwa ajabu kama nini kwa uvumilivu wake! Rehema na fadhili-upendo za Yehova zitatuletea thawabu zenye kulinganika na hizo​—ikiwa sisi tutavumilia hadi mwisho. Maneno ya Yakobo na yapate kutimizwa kuelekea kila mmoja wetu: “Tazama! Sisi twawatamka kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia.”​—Yakobo 5:10, 11, NW; Ayubu 42:10-13.

Wewe Ungejibuje?

◻ Yesu alikazia uhitaji gani wa uvumilivu?

◻ Yehova amekuwa na sababu gani za kuvumilia?

◻ Ni nini baadhi ya mambo makuu ya ile kazi kubwa iliyofanywa wakati wa 1989?

◻ Uvumilivu wa ndugu zetu katika Polandi umethawabishwaje?

◻ Mashahidi katika Lebanoni, Kolombia, na Italia wameonyeshaje uaminifu chini ya jaribu?

[Chati katika ukurasa wa 20-23]

RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 1989 WA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE

(Ona buku lililojalidiwa)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki