Unataka Watoto Wako Wawe na Wakati Ujao wa Aina Gani?
JE, WEWE huwaona watoto wako kuwa urithi wa thamani kubwa? (Zaburi 127:3) Au je, wewe huona kuwalea kuwa mzigo wa kifedha wenye kulemea ambao hauna uhakikisho kamili wa kufanikiwa? Badala ya kuleta faida za kifedha, kulea watoto hugharimu fedha mpaka pale watakapoweza kujitegemeza. Kama vile ambavyo kusimamia mali iliyorithiwa huhitaji mpango mzuri ndivyo ilivyo na kulea watoto.
Wazazi wanaojali watoto wao hutaka kuwapa mwanzo mzuri maishani. Ijapokuwa mambo mabaya na yenye kusikitisha mno huenda yakatukia katika ulimwengu huu, wazazi wanaweza kufanya mengi kuwalinda watoto wao. Fikiria kisa cha Werner na Eva, kilichotajwa katika makala iliyotangulia.a
Wazazi Wanapojali Kikweli
Werner huripoti kwamba badala ya kuachilia tu mambo, wazazi wake walionyesha upendezi wa kweli katika mambo yaliyokuwa yakiendelea shuleni. “Nilithamini sana madokezo yenye kutumika waliyonitolea, na nilihisi kwamba walinijali na walikuwa wakiniunga mkono. Wakiwa wazazi, walikuwa thabiti sana, lakini nilijua kwamba walikuwa marafiki wangu halisi.” Naye Eva alipovurugika akili sana kuhusiana na kazi ya shule hivi kwamba alishuka moyo na kukosa usingizi, wazazi wake Francisco na Inez, walitumia wakati mwingi pia wakizungumza naye na kumsaidia kupata tena usawaziko wake wa akili na wa kiroho.
Francisco na Inez walijaribuje kuwalinda watoto wao na kuwatayarisha kwa ajili ya maisha wakiwa watu wazima? Tangu watoto hao walipokuwa vitoto vichanga, wazazi hao wenye upendo waliwahusisha sikuzote katika shughuli zao za kila siku. Badala ya kushirikiana tu na marafiki wao ambao ni watu wazima, Inez na Francisco waliandamana na watoto wao popote pale walipoenda. Wakiwa wazazi wenye upendo, walimpa mwana wao na binti yao mwongozo ufaao. Inez asema hivi: “Tuliwafundisha kutunza nyumba, kuwa waangalifu katika matumizi, na kutunza mavazi yao wenyewe. Na tulisaidia kila mmoja wao kuchagua kazi na kusawazisha madaraka yao na masilahi ya kiroho.”
Ni jambo muhimu kama nini kuwajua watoto wako na kuwaandalia mwongozo wa kimzazi! Acheni tuchunguze maeneo matatu ambamo waweza kufanya hivyo: (1) Wasaidie watoto wako wachague aina ya kazi ya kimwili ifaayo; (2) watayarishe kukabiliana na mikazo ya kihisia-moyo shuleni na kazini; (3) waonyeshe jinsi ya kutosheleza mahitaji yao ya kiroho.
Wasaidie Wachague Kazi Ifaayo
Kwa kuwa kazi ya mtu ya kimwili huathiri hali yake ya kifedha na pia huchukua wakati wake mwingi, kulea watoto vizuri hutia ndani kufikiria mapendezi na uwezo mbalimbali wa kila mtoto. Kwa kuwa hakuna mtu mwenye kudhamiria atakaye kuwa mzigo wenye kulemea kwa wengine, wazazi wapaswa kufikiria kwa uzito juu ya jinsi mtoto wao awezavyo kutayarishwa ili aweze kujitegemeza na kutegemeza familia. Je, mwana wako au binti yako angehitaji kujifunza kazi fulani ili aishi maisha yafaayo? Ukiwa mzazi mwenye kujali kikweli, fanya jitihada yenye kuendelea ili kumsaidia mtoto wako atokeze sifa kama vile tamaa ya kufanya kazi kwa bidii, utayari wa kujifunza, na uwezo wa kupatana na wengine.
Fikiria Nicole. Yeye asema hivi: “Wazazi wangu walinishirikisha katika kazi yao ya usafi. Walidokeza nitoe asilimia fulani ya mapato yangu ili kugharimia matumizi fulani ya nyumbani na kuweka fedha kwa ajili ya matumizi au akiba yangu mwenyewe. Jambo hilo lilinifanya nihisi kuwa na madaraka yaliyoongezeka, jambo ambalo lilithibitika kuwa lenye mafaa baadaye maishani.”
Neno la Mungu, Biblia, halisemi kihususa aina ya kazi ya kimwili ambayo mtu apaswa kufanya. Lakini huandaa miongozo ifaayo. Kwa mfano, mtume Paulo alisema hivi: “Ikiwa yeyote hataki kufanya kazi, wala msimwache ale.” Akiwaandikia Wakristo katika Thesalonike, alisema hivi pia: “Twasikia watu fulani wanatembea bila utaratibu miongoni mwenu, wakiwa hawafanyi kazi hata kidogo bali wakijiingiza katika lile lisilowahusu wao. Kwa watu wa namna hiyo twatoa agizo na kutoa himizo lenye bidii katika Bwana Yesu Kristo kwamba kwa kufanya kazi kwa utulivu wale chakula ambacho wao wenyewe wachuma.”—2 Wathesalonike 3:10-12.
Hata hivyo maisha si kupata kazi na kuchuma fedha tu. Hatimaye, yaelekea wale wenye kutaka sana makuu hawataridhika na huenda wakawa ‘wanajilisha upepo.’ (Mhubiri 1:14) Badala ya kuwahimiza watoto wao wafuatie umashuhuri na ufanisi, wazazi hufanya vema kuwasaidia waelewe hekima ya maneno haya ya mtume Yohana yaliyopuliziwa: “Msiwe mkipenda ama ulimwengu ama vitu vilivyo katika ulimwengu. Ikiwa yeyote aupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo katika yeye; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu. Zaidi ya hilo, ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:15-17.
Unawezaje Kutosheleza Mahitaji Yao ya Kihisia-Moyo?
Ukiwa mzazi, kwa nini usiwe kama mtu ambaye huzoeza wanariadha? Yeye hakazii uangalifu wake kule kusitawisha tu uwezo wa kimwili wa wanariadha anaozoeza ili wakimbie kwa kasi zaidi au kuruka umbali mkubwa zaidi. Yaelekea, yeye pia hujitahidi kuwasaidia washinde mtazamo wowote usiofaa, hivyo akiimarisha nguvu zao za kihisia-moyo. Kwa habari yako, waweza kutia moyo, kujenga, na kuchochea watoto wako jinsi gani?
Fikiria Rogério, kijana aliye na umri wa miaka 13. Mbali na msukosuko wa kindani usababishwao na mabadiliko ya kimwili, alipatwa na mkazo wa kihisia-moyo kwa sababu ya mtengano wa wazazi na kutotunzwa. Ni nini kiwezacho kufanywa kwa ajili ya vijana kama yeye? Ingawa ni jambo lisilowezekana kuwalinda watoto wako dhidi ya mahangaiko na uvutano mbaya, usiache kamwe daraka lako ukiwa mzazi. Bila kuwa mwenye kuwalinda kupita kiasi, watie watoto wako nidhamu kwa uelewevu, ukikumbuka sikuzote kwamba kila mtoto ni tofauti. Kwa kumwonyesha fadhili na upendo, waweza kutimiza mengi katika kumfanya kijana ahisi akiwa salama. Hilo litamlinda asikue bila uhakika na kujistahi.
Hata wazazi wako mwenyewe wawe walifanikiwa kadiri gani katika kutosheleza mahitaji yako ya kihisia-moyo, mambo haya matatu yaweza kukusaidia kufanikiwa ukiwa mzazi mwenye kusaidia kikweli: (1) Epuka kujiingiza sana katika matatizo yako mwenyewe hivi kwamba unapuuza matatizo ya watoto wako yaonekanayo kuwa madogo; (2) jitahidi kuwa na mawasiliano yenye kupendeza na yenye maana pamoja nao kila siku: (3) kuza mwelekeo ufaao kwa habari ya kutatua matatizo na kushughulika na watu.
Akikumbuka miaka yake akiwa tineja, Birgit asema hivi: “Nililazimika kujifunza kwamba huwezi kuwabadili watu wawe vile wewe utakavyo. Mama yangu alisababu nami kwamba nikiona sifa za wengine nisizopenda, jambo ambalo ningeweza kufanya lilikuwa tu kuepuka kuwa kama wao. Mama pia alisema kwamba, wakati ambapo nilikuwa bado mchanga ndio ungekuwa wakati bora zaidi wa kubadili mwenendo wangu mwenyewe.”
Hata hivyo, watoto wako wahitaji mengi zaidi ya kupata kazi na usawaziko wa kihisia-moyo. Jiulize, ‘Je, mimi huona kulea watoto kuwa daraka nililopewa na Mungu?’ Ikiwa ndivyo, utataka kutosheleza mahitaji ya kiroho ya watoto wako.
Njia za Kutosheleza Mahitaji Yao ya Kiroho
Katika Mahubiri ya Mlimani yake, Yesu Kristo alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao.” (Mathayo 5:3) Ni nini huhusika katika kutosheleza mahitaji ya kiroho? Watoto hunufaika sana wazazi wawekapo kielelezo chema cha imani katika Yehova Mungu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Bila imani haiwezekani kumpendeza [Mungu] vema, kwa maana amkaribiaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Hata hivyo ili imani iwe na maana halisi, sala inahitajiwa. (Waroma 12:12) Ukitambua uhitaji wako wa kiroho, utatafuta mwongozo wa kimungu, kama vile alivyofanya baba ya mtoto Samsoni, aliyepata kuwa Mwamuzi mashuhuri wa Israeli. (Waamuzi 13:8) Utasali na pia kuiendea Biblia, Neno la Mungu lililopuliziwa ili upate msaada.—2 Timotheo 3:16, 17.b
Licha ya kazi yote ya bidii inayohusika katika kuandaa mwongozo mzuri, utegemezo wa kihisia-moyo, na msaada wa kiroho, kulea watoto kwaweza kuwa jambo lenye kuthawabisha. Baba ya watoto wawili katika Brazili asema hivi: “Siwezi hata kuwazia nikiwa bila watoto wangu. Kuna mambo mengi mazuri tuwezayo kushiriki pamoja nao.” Akieleza kwa nini watoto wanafanya vyema, mama aongeza kusema hivi: “Sisi huwa pamoja sikuzote, na hujaribu kufanya mambo yawe yenye shangwe na furaha. Nalo jambo la maana zaidi ni kwamba, sisi husali kwa ajili ya watoto.”
Priscilla akumbuka upendo na subira ambayo wazazi wake walimwonyesha kila alipokuwa na tatizo. “Walikuwa marafiki wangu wa kweli na walinisaidia katika kila jambo,” yeye asema. “Nikiwa mtoto, kwa kweli nilihisi kwamba nilikuwa nikitendewa kama ‘urithi wa BWANA.’” (Zaburi 127:3) Kama wazazi wengine wengi, kwa nini usiratibu wakati pamoja na watoto wako ili mweze kusoma Biblia na vichapo vya Kikristo pamoja? Kufikiria masimulizi na kanuni za Biblia katika hali ifaayo kwaweza kuwasaidia watoto wako wawe wenye uhakika na kuwa na tumaini halisi la wakati ujao.
Wakati Ambapo Watoto Wote Watakuwa Salama
Ijapokuwa wakati ujao waonekana bila matumaini kwa watoto wengi leo, Neno la Mungu latoa uhakikisho kamili kwamba karibuni dunia itakuwa makao salama kwa ajili ya wanadamu. Ebu wazia ule wakati ambapo katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa, wazazi watakuwa bila wasiwasi juu ya usalama wa watoto wao! (2 Petro 3:13) Ebu jaribu kuwazia utimizo mtukufu wa unabii huu: “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza.” (Isaya 11:6) Hata leo, usalama wa kiroho unaofafanuliwa katika maneno hayo una utimizo wa kitamathali miongoni mwa wale wanaomtumikia Yehova. Katikati yao, utahisi utunzaji wa Mungu wenye upendo. Ukidhihirisha upendo kwa Mungu, waweza kuwa na uhakika kwamba kama vile mzazi, yeye huelewa hisia zako na atakusaidia kukabiliana na mahangaiko na majaribu yawezayo kukupata. Jifunze Neno lake na kuweka tumaini lako katika Ufalme wake.
Saidia watoto wako watembee katika njia iendayo kwenye uhai wa milele kwa kuwawekea kielelezo chema. Ukimkimbilia Yehova Mungu, wakati wako ujao na wa watoto wako waweza kuwa na mengi zaidi kushinda matarajio yako yote. Waweza kuwa na uhakika uleule aliokuwa nao mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Nawe utajifurahisha kwa BWANA, naye atakupa haja za moyo wako.”—Zaburi 37:4.
[Maelezo ya Chini]
a Majina yamebadilishwa katika makala hii.
b Ona sura ya 5 hadi 7 katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.