Kazi Ambayo “Haiwezi Kushindwa Kutokeza Staha”
MTUME Petro alionya kwa upole Wakristo wenzake hivi: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, katika jambo ambalo katika hilo wao wanasema dhidi yenu kuwa watenda-maovu, likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu.” (1 Petro 2:12) Kwa miaka mingi Mashahidi wa Yehova katika Italia wameonyesha hadharani mwenendo mzuri kama huo. Wakiwa na roho ya agizo la Yesu la ‘kuhubiri kutoka paa za nyumba,’ wanafanya utendaji wao wa Kikristo waziwazi, wakionekana na watu wote. (Mathayo 10:27; Yohana 18:20) Kwa sababu hiyo, mwanasheria mmoja Mwitalia na kasisi walipochapisha mashtaka kwamba Mashahidi wa Yehova ni “madhehebu ya dini bandia” na kuwatia katika “sosaiti za siri ambazo hunasa watu,” Mashahidi waliamua kuchukua hatua ya kisheria kwa sababu ya maneno hayo yenye kukashifu.
Katika kesi ya kwanza, korti iliamua kwamba mwanasheria na kasisi huyo hawakuwa wamevunja sheria. Hata hivyo, katika Julai 17, 1997, Mahakama ya Rufani ya Venice ilitangua uamuzi wa kwanza wa mahakama, ikiwapata washtakiwa wote wawili kuwa na hatia. Mahakama hiyo ya Rufani ilisema: “Makala zote mbili zilizochapishwa ambazo zinazungumziwa zina maelezo na vifungu vya maneno ambavyo kwa hakika vina uwezo wa kuwaharibia sifa wafuasi hao wa dini ya ‘Mashahidi wa Yehova.’ Yaonekana dhahiri kwamba nia ya makala hizo ni kutweza hao wafuasi hadharani.” Mahakama ilisema kwamba makala hizo “hazina haki ya kuripoti na kuchambua.” Mahakama ilitoza faini wakashifu hao wawili na pia kuwaamuru walipie gharama zote za mahakama, kutia ndani gharama za Mashahidi za kisheria za kesi zote mbili.
Katika hukumu yake iliyoandikwa, Mahakama ya Rufani ya Venice ilisema hivi: “Ni kwa kusawazisha na kulinda tu haki zote zilizotolewa uhakikisho kamili na Katiba ya [Italia] ndipo inapowezekana kuzuia aina za kutovumilia na ushupavu wa kidini.” Uamuzi wakiri kwamba utendaji wa Mashahidi wa Yehova si wa siri wala si wa bandia. “Kuwaweka Mashahidi miongoni mwa sosaiti za siri,” ikasema mahakama, “hata hakustahi kanuni ya kuamulia kweli ya kihistoria, kwa kuwa dini hiyo inayodaiwa imo katika majiji mengi na utendaji mkubwa wa washiriki wake wa kugeuza imani ya wengine, hasa Jumapili na siku nyinginezo za likizo, unajulikana sana na hauwezi kushindwa kutokeza staha kwa jitihada zilizofanywa, hata mtu afikirije kuhusu mafundisho yanayohubiriwa.” Hivyo, rekodi ya kuhubiri kwa bidii na mwenendo unaofaa wa Mashahidi wa Yehova katika Italia umesaidia kuondoa ubaguzi dhidi yao.—Mathayo 5:14-16; 1 Petro 2:15.