Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Usijizuie Kutangaza Habari Njema
WAVUMBUZI wa Ulaya walipotembelea kwa mara ya kwanza lile Ghuba la Venezuela na Ziwa Maracaibo, pwani hiyo ilikuwa imejaa vibanda vidogo-vidogo vilivyoezekwa kwa makuti ambavyo vilijengwa juu ya milonjo kwenye maji yasiyo na kina. Mwono huo uliwakumbusha kuhusu Venice, Italia, ambapo watu walijenga nyumba zao kandokando ya maji. Wavumbuzi wasemao Kihispania walipaita mahali hapo Venezuela, jina limaanishalo “Venice Ndogo.”
Leo, katika nchi hii yenye kupendeza, aina nyingine ya programu ya ujenzi inaendelea, programu ya kiroho. Huko Mashahidi wa Yehova wana shughuli nyingi za kupanda mbegu ya Ufalme katika kila pindi ifaayo. Matokeo ya mavuno ya kiroho yanaleta sifa nyingi kwa “Bwana-mkubwa wa mavuno,” Yehova Mungu.—Mathayo 9:37, 38.
Mwangalizi asafiriye alipotembelea kutaniko moja katika jimbo la Zulia kaskazini-magharibi mwa Venezuela, Mashahidi wa mahali hapo walimpangia yeye na mke wake watembelee kisiwa kidogo kilicho karibu kiitwacho Toas. Walipokuwa wakipiga foleni ili wawahi feri ya asubuhi na mapema ya kwenda kisiwani humo, Mery, mke wa mwangalizi asafiriye, alimdokezea mwenzake, dada aliye painia wa wakati wote, kwamba wazungumze na baadhi ya wafanyakazi kwenye mashua. Dada painia alikubali.
Akimkaribia fundisanifu, Mery alimtolea kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Alimwonyesha sura yenye kichwa “Kujenga Familia Inayomheshimu Mungu,” ambayo alionekana kuielewa. Kisha Mery akaeleza kwamba kwa kutumia kichapo hicho, angeweza kuwa na funzo la Biblia nyumbani kwake mwenyewe. Alikubali kitabu hicho, na mipango ikafanywa ili mtu fulani amrudie nyumbani kwake.
Muda mfupi baadaye, kulikuwa na siku ya kusanyiko la pekee mahali hapo. Mery alishangaa kama nini kumwona fundisanifu huyo, Senor Nava huko, pamoja na mke wake na binti zake wawili wachanga! Mery alimwuliza mke vile alifikiria kuhusu funzo lao la Biblia la familia. Jibu lake lilikuwa lenye kushangaza sana.
“Namshukuru Yehova kwamba tumejifunza kweli,” akasema. Kisha akaelezea. “Ulipoongea na mume wangu, alikuwa ametoka tu kuniacha na kuchukua mwanamke mwingine. Pia alikuwa mnywaji wa kupindukia. Nyakati nyingi alipolewa, alikuwa mwenye kutukana, ambako jumuiya ndogo kisiwani haikupenda. Pia alizoea uwasiliani-roho. Hata hivyo, ujuzi wa Biblia ambao alipata kutokana na funzo ulimsaidia afanye mabadiliko makubwa sana maishani mwake. Ameacha mazoea yake yote hayo yasiyo safi. Wazazi wake, ambao ni Wakatoliki, wamevutiwa sana na mabadiliko hayo. Wanafurahi kwamba sasa yeye ni mume na baba mwenye kutumainika.”
Senor Nava alibatizwa 1996 na sasa atumikia akiwa mhudumu wa wakati wote. Mke wake, Jenny, alibatizwa 1997. Meya wa mji alivutiwa sana na mabadiliko ya huyu fundisanifu wa feri hivi kwamba yeye pia akaomba awe na funzo la Biblia. Akina dada hao walifurahi kama nini kwamba hawakujizuia kutangaza habari njema walipokuwa wamepiga foleni wakingoja feri asubuhi hiyo!
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kushiriki habari njema na fundisanifu wa feri kulileta matokeo yenye furahay