Je, Makasisi Wote Huamini Wanayofundisha?
MUME wa mwanamke huyo ametoka tu kufa. Kasisi wake amweleza kwamba mume wake hakuwa mtu mzuri vya kutosha kumwezesha kwenda moja kwa moja hadi mbinguni, wala mbaya vya kutosha kusafirishwa hadi kwenye mioto ya helo. Hivyo, kulingana na kasisi huyo, yeye anapata adhabu ya kuteseka mpaka atakapostahili kwenda mbinguni. Mwanamke huyo amlipa kasisi ili asali ili mume wake apate kufunguliwa kutoka kwenye purgatori upesi zaidi. Mjane huyo aridhika na hilo, akihisi kwamba kasisi ashiriki imani zake za moyo mweupe.
Je, wafikiri mjane huyo angezinduka ikiwa angegundua kwamba kasisi wake kwa kweli hakuamini juu ya kupata adhabu baada ya kifo? Watu wengi husumbuka wapatapo kujua kwamba makasisi wengi hawaamini mengi ya yale wao wenyewe hufundisha. Kichapo National Catholic Reporter, kikitaja kile kilichokiita “tatizo la kikasisi lililo kubwa kuliko upotovu wa kingono,” kilitaarifu hivi: “Miongoni mwa makasisi kwa ujumla, kuna wengi walioacha kuamini kuwapo kwa Mungu au fundisho la kuthawabishwa na kuadhibiwa au ufufuo . . . hivi kwamba utamaduni wa kikasisi huchukua kutoamini huko kuwa sehemu ya mazingira yake, kama vile ukungu.”
Makanisa mengine yametatanika vivyo hivyo. Uchunguzi wa makasisi wa Kanisa la Uingereza ulifunua kwamba watu wengi “hawaamini sehemu fulani za msingi wa utamaduni wa imani ya Kikristo kama vile uzawa wa kibikira, miujiza ya Yesu na kuja kwa mara ya pili kwa mesiya,” charipoti kichapo Canberra Times cha Australia.
Mwandikaji wa mambo ya kidini George R. Plagenz aliuliza ingewezekanaje mhudumu, kwa dhamiri safi, kukariri kanuni ya imani asiyoamini yeye mwenyewe. Mhudumu mmoja alisema alibadilisha tu yale maneno ya kwanza ya kanuni ya imani, “Naamini.” Alisema hivi: “Mimi huanza kanuni ya imani kwa kusema hivi, ‘WAO huamini katika Mungu Baba Mweza Yote . . . ’” Plagenz aliuita unafiki wa namna hiyo “ulaghai mkubwa zaidi nchini.”
Kwa kusikitisha, kutoamini kwa namna hiyo kwa kikasisi na ukosefu wa kuwa na unyoofu wa moyo kwa mafundisho ya kidini, kumewazindua watu wengi kwa ujumla juu ya dini. Lakini si hilo tu linalosumbua juu ya dini leo. Waenda-makanisa walio wengi wamefunzwa kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Je, wangeshangaa kujifunza kwamba mafundisho fulani ya kidini yaliyokubaliwa kwa muda mrefu hayafundishwi katika Biblia? Makala inayofuata itachunguza kielelezo kimoja.