Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 8/1 kur. 19-24
  • Sehemu ya 4-Fundisho la Utatu Lilisitawi Wakati Gani na Jinsi Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sehemu ya 4-Fundisho la Utatu Lilisitawi Wakati Gani na Jinsi Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Lilithibitisha Fundisho la Utatu?
  • “Maoni ya Wachache”
  • Baraza la Konstantinopo
  • Jinsi Lilivyositawi
  • Ni Nini Kinachowakilishwa
  • “Kwa Matunda Yao”
  • Siku ya Kutoa Hesabu
  • Je, Uamini Utatu?
    Amkeni!—2013
  • Fundisho la Utatu Lilisitawi Jinsi Gani?
    Je, Uamini Utatu?
  • Sehemu ya 1—Je! Yesu na Wanafunzi Wake Walifundisha Fundisho la Utatu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Je! Kwa Wazi Hilo Ni Fundisho la Biblia?
    Je, Uamini Utatu?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 8/1 kur. 19-24

Je! Kanisa la Mapema Lilifundisha Kwamba Mungu ni Utatu?

Sehemu ya 4-Fundisho la Utatu Lilisitawi Wakati Gani na Jinsi Gani?

Makala tatu za kwanza za mfululizo huu zilionyesha kwamba fundisho la Utatu halikufundishwa na Yesu na wanafunzi wake wala na Mababa wa Kanisa wa mapema. (Mnara wa Mlinzi wa Novemba 1, 1991; Februari 1, 1992; na Aprili 1, 1992) Makala hii ya mwisho itazungumzia jinsi fundisho la Utatu lilivyositawi na sehemu ambayo Baraza la Nisea lilishiriki katika 325 W.K.

KATIKA mwaka wa 325 W.K., maliki Mroma Konstantino alikutanisha baraza la maaskofu katika jiji la Nisea katika Esia Ndogo. Kusudi lake lilikuwa kusuluhisha yale mabishano ya kidini yenye kuendelea juu ya uhusiano wa Mwana wa Mungu kwa Mungu Mweza Yote. Kuhusu matokeo ya baraza hilo, Encyclopœdia Britannica husema hivi:

“Konstantino mwenyewe ndiye aliyesimamia, akiongoza mazungumzo kwa utendaji mwingi, na yeye binafsi akapendekeza . . . ile kanuni kuu yenye kuonyesha uhusiano wa Kristo kwa Mungu katika imani iliyotolewa na baraza, ‘wa asili moja [ho·mo·ouʹsi·os] na Mungu.‘ . . . Kwa kumhofu mno maliki, maaskofu hao, isipokuwa wawili tu, walitia sahihi imani hiyo, wengi wao wakifanya hivyo dhidi sana ya mbetuko wao.”1

Je! mtawala huyo mpagani alikutanisha baraza hilo kwa sababu ya masadikisho yake ya Kibiblia? La. A Short History of Christian Doctrine hutaarifu hivi: “Kwa msingi Konstantino hakuwa na uelewevu wowote ule wa maswali yaliyokuwa yakiulizwa katika theolojia ya Kigiriki.”2 Lile aliloelewa lilikuwa kwamba mabishano ya kidini yaliutisha umoja wa milki yake, naye alitaka yasuluhishwe.

Je! Lilithibitisha Fundisho la Utatu?

Je! Baraza la Nisea lilithibitisha, au kuyakinisha, Utatu kuwa fundisho la Jumuiya ya Wakristo? Wengi hudhani kwamba ilikuwa hivyo. Lakini mambo ya hakika huonyesha jambo tofauti.

Ile imani iliyofanyizwa na baraza hilo ilidai mambo fulani kuhusu Mwana wa Mungu ambayo yangeruhusu makasisi mbalimbali wamwone kuwa sawa na Mungu Baba katika njia fulani. Hata hivyo, inatia nuru kuona lile ambalo ile Imani ya Nisea haikusema. Kama ilivyotangazwa kwa chapa awali, imani hiyo yote ilitaarifu hivi:

“Tunaamini katika Mungu mmoja, Baba mweza yote, mfanyi wa vitu vyote vionekanayo na visivyoonekana;

“Na katika Bwana mmoja Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, aliyezaliwa kutoka kwa Baba, mzaliwa wa pekee, yaani, kutoka kwa asili ya Baba, Mungu kutoka kwa Mungu, nuru kutoka kwa nuru, Mungu wa kweli kutoka kwa Mungu wa kweli, aliyezaliwa si kufanywa, wa asili moja na Baba, Ambaye kupitia yeye vitu vyote vikawa, vitu mbinguni na vitu duniani, Ambaye kwa sababu yetu wanadamu na kwa sababu ya wokovu wetu akaja chini akawa na mwili, akiwa mwanadamu, akateseka na kuinuka tena siku ya tatu, akapaa mbinguni, na atakuja kuwahukumu walio hai na wafu;

“Na katika Roho Takatifu.”3

Je! imani hiyo husema kwamba Baba, Mwana, na roho takatifu ni watatu katika Mungu mmoja? Je! inasema kwamba hao watatu wako sawa katika umilele, uweza, cheo, na hekima? La, haisemi hivyo. Hakuna kanuni yoyote hapo ya watatu-katika-mmoja. Imani ya Nisea ya awali haikuthibitisha au kuyakinisha Utatu.

Imani hiyo, kwa vyovyote vile, humsawazisha Mwana na Baba kwa kuwa “wa asili mmoja.” Lakini haisemi jambo lolote kama hilo kuhusu roho takatifu. Jambo lisemalo tu ni kwamba “tunaamini . . . katika Roho Takatifu.” Hilo si fundisho la Utatu la Jumuiya ya Wakristo.

Hata yale maneno makuu “wa asili moja” (ho·mo·ouʹsi·os) hayakumaanisha kwa lazima kwamba baraza hilo liliamini katika usawa wa kihesabu wa Baba na Mwana. The New Catholic Encyclopedia hutaarifu hivi:

“Jambo la kwamba Baraza hilo lilinuia kuthibitisha usawa wa kihesabu wa asili ya Baba na Mwana linatiliwa shaka.”4

Ikiwa baraza hilo lilimaanisha kwamba Mwana na Baba walikuwa na usawa wa cheo, huo bado usingekuwa Utatu. Ungekuwa wawili tu katika Mungu mmoja, sio watatu katika Mungu mmoja kama ilivyotakiwa na fundisho la Utatu.

“Maoni ya Wachache”

Katika Nisea, je, maaskofu kwa ujumla waliamini kwamba Mwana alikuwa sawa na Mungu? La, kulikuwako maoni yenye kupingana. Kwa mfano, moja yao liliwakilishwa na Ario, aliyefundisha kwamba Mwana alikuwa na mwanzo hususa katika wakati na kwa hiyo hakuwa sawa na Mungu lakini alikuwa na cheo kidogo katika mambo yote. Athanasio, kwa upande ule mwingine, aliamini kwamba Mwana alikuwa sawa na Mungu katika njia fulani. Na kulikuwako maoni mengine.

Kuhusu uamuzi wa baraza wa kumwona Mwana kuwa wa asili (namna) moja na Mungu, Martin Marty hutaarifu hivi: “Nisea kwa kweli iliwakilisha maoni ya wachache; uamuzi huo ulikuwa wenye fadhaa na haukukubaliwa na wengi ambao hawakuwa na maoni ya Kiario.”5 Vivyo hivyo, kitabu A Select Library of Nicene and Post-Nicene Fathers of the Christian Church huonyesha kwamba “msimamo wa kimafundisho wenye kufanyizwa waziwazi uliotofautiana na Uario ulichukuliwa na wachache tu, ingawa wachache hao walifanikiwa katika kutimiza kusudi lao.”6 Na A Short History of Christian Doctrine huonyesha hivi:

“Jambo lililoonekana kuwa lilikataliwa hasa na maaskofu na wanatheolojia wengi wa Mashariki lilikuwa lile wazo lililowekwa na Konstantino mwenyewe katika imani, ile ho·mo·usʹsi·os [“wa asili moja”], lililokuwa jambo la kubishania katika yale mabishano yaliyofuata kati ya uorthodoksi na uzushi.”7

Baada ya baraza hilo, mabishano yaliendelea kwa muda wa karne kadhaa. Wale waliopendelea lile wazo la kumsawazisha Mwana na Mungu Mweza Yote hata wakachukiwa na wengi kwa muda fulani. Kwa mfano, Martin Marty husema hivi juu ya Athanasio: “Alipata umaarufu akaupoteza naye alihamishwa-hamishwa mara nyingi sana [katika miaka baada ya baraza hilo] hivi kwamba akawa kwa kweli mwenye kusafiri kila wakati.”8 Athanasio alitumia miaka kadhaa uhamishoni kwa sababu maofisa wa kisiasa na wa kanisa waliyapinga maoni yake yaliyomsawazisha Mwana na Mungu.

Kwa hiyo si kweli kudai kwamba Baraza la Nisea katika 325 W.K. lilithibitisha au kuyakinisha fundisho la Utatu. Lile lililokuja kuwa fundisho la Utatu halikuwako wakati huo. Wazo la kwamba Baba, Mwana, na roho takatifu walikuwa wote Mungu wa kweli na wenye usawa katika umilele, uweza, cheo, na hekima, lakini Mungu mmoja—watatu katika Mungu mmoja—halikusitawishwa na baraza hilo wala na Mababa wa Kanisa wa mapema. Kama kitabu The Church of the First Three Centuries kinavyotaarifu:

“Fundisho la ki-siku-hizi la Utatu lenye kupendwa na wengi . . . haliungwi mkono na maandishi ya Justin: na maoni hayo yaweza kutumiwa kuhusu Mababa wote waliokuwa kabla ya [baraza la] Nisea; yaani, waandikaji wote Wakristo wa karne ya tatu baada ya kuzaliwa kwa Kristo. Ni kweli, wao husema juu ya Baba, Mwana, na yule wa kiunabii, au Roho takatifu, lakini si wakiwa sawa, si wakiwa kitu kimoja kihesabu si wakiwa Watatu katika Mmoja, katika maana yoyote inayokubaliwa sasa na Wanautatu. Kinyume kabisa ndio uhakika. Fundisho la Utatu, kama lielezwavyo na Mababa hao, kwa msingi lilikuwa tofauti na fundisho la ki-siku-hizi. Twataarifu hivyo ukiwa uhakika ambao utastahimili jaribu kama uhakika wowote katika historia ya maoni ya kibinadamu.”

Tunampa mwito wa ushindani yeyote awezaye kutoa mwandikaji maarufu hata mmoja, wa wakati wa karne tatu za kwanza, aliyeamini fundisho hilo [la Utatu] jinsi linavyoaminiwa sasa.”9

Hata hivyo, Nisea liliwakilisha mwanzo wa badiliko. Lilifungulia mlango ule ukubali wa rasmi wa Mwana kuwa sawa na Baba, na hilo liliwekea njia lile wazo la Utatu la baadaye. Kile kitabu Second Century Orthodoxy, la J. A. Buckley, huonyesha hivi:

“Hadi angalau mwisho wa karne ya pili, Kanisa la ulimwenguni pote lilikaa lenye umoja kwa maana moja ya msingi; wao wote walikubali ukuu wa Baba. Walimwona Mungu Baba Mweza Yote kuwa mkuu zaidi peke yake, asiyebadilika, mwenye sifa zisizoelezeka na asiye na mwanzo. . . .

“Waandikaji na viongozi wa karne ya pili walipoondoka, Kanisa lilijipata lenyewe . . . likielekea polepole lakini bila kuzuilika kufikia hatua ile . . . ambapo kwenye Baraza la Nisea upeo wa mmonyoko huo wa kidogo kidogo wa ile imani ya awali ulifikiwa. Hapo wachache wenye nguvu, waliuleta kwa hila uzushi wao juu ya wengi watiifu, na wakiungwa mkono na wenye mamlaka wa kisiasa, waliwalazimisha, wakawavuta kwa werevu na kuwatisha wale waliojitahidi kuudumisha bila waa, ule usafi wa asili wa imani yao.”10

Baraza la Konstantinopo

Katika 381 W.K., Baraza la Konstantinopo lilithibitisha lile Imani ya Nisea. Nalo liliongeza kitu kingine. Liliita roho takatifu “Bwana” na “mpaji-uhai.” Ile imani ya 381 W.K. iliyopanuliwa (ambayo kwa kweli ndiyo inayotumiwa makanisani leo na ambayo huitwa “Imani ya Nisea”) huonyesha kwamba Jumuiya ya Wakristo ilikuwa karibu sana kufanyiza fundisho la Utatu lililo kamili. Hata hivyo, baraza hilo hata halikukamilisha fundisho hilo. New Catholic Encyclopedia hukiri hivi:

“Ni jambo la kupendeza kwamba miaka 60 baada ya Nisea 1 lile Baraza la Konstantinopo 1 [381 W.K.] liliepuka ho·mo·usʹsi·os katika ufafanuzi walo wa uungu wa Roho Takatifu.”11

“Wanachuo wametatizwa na ule uonekanao kuwa urahisi wa maneno kwa upande wa imani hiyo; kwa mfano, ule ukosefu wayo wa kutumia lile neno homoousios kwa habari ya Roho Takatifu kuwa ya namna moja na Baba na Mwana.”12

Ensaiklopedia iyo hiyo hukiri hivi: “Homoousios halipatikani katika Maandiko.”13 La, Biblia haitumii neno hilo ama kuhusu roho takatifu ama kuhusu Mwana kuwa wa namna moja na Mungu. Hilo lilikuwa neno lisilo la kibiblia lililosaidia kuongoza kwenye lile fundisho la Utatu lisilo la kibiblia, ambalo kwa kweli, hupinga Biblia.

Hata baada ya Konstantinopo, ilichukua muda wa karne kadhaa kabla ya fundisho la Utatu kukubaliwa kotekote katika Jumuiya ya Wakristo. The New Catholic Encyclopedia husema hivi: “Katika Magharibi . . . ukimya kwa ujumla ulionekana kuwa ulienea kwa habari ya Konstantinopo 1 na imani yalo.”14 Chanzo hicho huonyesha kwamba imani ya baraza hilo haikutambuliwa kotekote Magharibi hadi karne ya saba au ya nane.

Wanachuo hukiri pia kwamba Imani ya Athanasio, ambayo mara nyingi hunukuliwa kuwa ufafanuzi na utegemezo rasmi wa Utatu, haikuandikwa na Athanasio lakini ilikuwa wa mtungaji wa baadaye zaidi asiyejulikana. The New Encyclopœdia Britannica hueleza hivi:

“Imani hiyo haikujulikana kwa Kanisa la Mashariki mpaka karne ya 12. Tangu karne ya 17, kwa ujumla wanachuo wameafikiana kwamba Imani ya Atanasio haikuandikwa na Athanasio (alikufa 373) lakini labda ilitungwa kusini mwa Ufaransa wakati wa karne ya 5. . . . Uvutano wa imani hiyo waonekana kuwa ulikuwa kusini mwa Ufaransa hasa na Hispania katika karne za 6 na 7. Ulitumiwa katika liturjia ya kanisa katika Ujeremani katika karne ya 9 na baadaye kidogo katika Roma.”15

Jinsi Lilivyositawi

Fundisho la Utatu lilianza ukuzi walo wa polepole kwa kipindi cha karne kadhaa. Mawazo ya Kiutatu ya wanafalsafa Wagiriki kama vile Plato, aliyeishi karne kadhaa kabla ya Kristo, yaliingia kidato kwa kidato ndani ya mafundisho ya kanisa. Kama The Church of the First Three Centuries kisemavyo:

“Tunathibitisha kwamba fundisho la Utatu lilifanyizwa kidato kwa kidato na ni la baadaye kwa kulinganishwa; kwamba lilipata awali yalo katika chanzo cha kigeni kabisa kilicho tofauti na kile cha Maandiko ya Kiyahudi na ya Kikristo; kwamba lilikua, na likapandikizwa juu ya Ukristo, kupitia mikono ya Mababa wenye kufuata mawazo ya Plato; kwamba katika wakati wa Justin, na muda mrefu baadaye, hali ya Mwana kuwa tofauti na mwenye cheo cha chini yalifundishwa ulimwenguni pote; na kwamba lile umbo la kwanza la Utatu la kivulikivuli tu ndilo lilianza kuonekana wakati huo.”16

Kabla ya Plato, utatu-utatu au utatu wa miungu, ulikuwa wa kawaida katika Babuloni na Misri. Na jitihada za wanakanisa za kuwavutia wasioamini katika ulimwengu wa Roma ziliongoza kwenye kutia ndani kwa baadhi ya mawazo hayo katika Ukristo. Mwisho huo uliongoza kwenye ukubali wa ile imani kwamba Mwana na roho takatifu walikuwa sawa na Baba.a

Hata neno “Utatu” lilikubaliwa polepole tu. Ilikuwa katika nusu ya mwisho ya karne ya pili kwamba Theofilo, askofu wa Antiokia katika Siria, aliandika katika Ugiriki na kutokeza lile neno triʹas, linalomaanisha “utatu-utatu,” au “utatu.” Halafu mwandikaji Mlatini Tertuliani katika Karthage, Afrika Kaskazini, akatokeza katika maandishi yake neno trinitas, linalomaansha “utatu.”b Lakini neno triʹas halipatikani katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyopuliziwa roho, na neno trinitas halipatikani katika tafsiri ya Kilatini ya Biblia iitwayo Vulgate. Hakuna lolote kati ya maneno hayo lililokuwa la Kibi-blia. Lakini neno “Utatu,” lenye msingi wa mawazo ya kipagani, lilinyemelea ndani ya vichapo vya makanisa na baada ya karne ya nne likawa sehemu ya mafundisho yao.

Hivyo, si kwamba wanachuo waliichunguza Biblia kwa ukamili wakaone ikiwa fundisho la jinsi hiyo lilikuwa limefundishwa ndani yayo. Badala ya hivyo, siasa za kilimwengu na za kanisa zilikuwa na sehemu kubwa katika kuamua juu ya fundisho hilo. Katika kitabu The Christian Tradition, mtungaji Jaroslav Pelikan huelekezea fikira “zile sehemu za ubishi huo zisizokuwa za kitheolojia, nyingi zazo zikionekana kuwa tayari tena na tena kuamua matokeo yalo, kisha zikitanguliwa amri tu na mamlaka zenye umaarufu sawa na wazo. Fundisho sikuzote lilionekana kuwa ndilo jambo lililoathiriwa—au ndilo tokeo—la siasa za kanisa au mapigano ya kiutu.”17 Profesa wa chuo kikuu cha Yale E. Washburn Hopkins alieleza jambo hilo hivi: “Ufafanuzi wa mwisho wa utatu wa kiorthodoksi ulikuwa kwa sehemu kubwa jambo la siasa za kanisa.”18

Fundisho la Utatu ni jambo lisilofuata sababu kama nini linapolinganishwa na lile fundisho sahili la Biblia kwamba Mungu ni mkuu zaidi naye hana aliye sawa na yeye! Kama Mungu asemavyo, “mtanifananisha na nani, na kunisawazisha naye, na kunilinganisha naye, ili tuwe sawasawa?”—Isaya 46:5.

Ni Nini Kinachowakilishwa

Usitawi wa kidato kwa kidato wa wazo la Utatu uliwakilisha nini? Ulikuwa sehemu ya mwanguko kutoka kwa Ukristo wa kweli uliotabiriwa na Yesu. (Mathayo 13:24-43) Mtume Paulo alikuwa pia ametabiri kuja kwa uasi imani:

“Hakika wakati utakuja ambapo, bila kuridhika hata kidogo na fundisho timamu, watu watataka sana mambo mapya yaliyo ya karibuni zaidi na kujikusanyia mpororo mzima wa walimu kulingana na ladha yao wenyewe; halafu, badala ya kusikiliza ukweli, watageukia hadithi za kutungwa.—2 Timotheo 4:3, 4, Jerusalem Bible ya Kikatoliki.

Mojawapo ya hadithi hizo za kutungwa ilikuwa lile fundisho la Utatu. Nyinginezo za hadithi hizo za kutungwa zilizokuwa za kigeni kwa Ukristo ambazo pia zilisitawi kidato kwa kidato zilikuwa: hali ya asili ya kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, purgatori, Limbo, na mateso ya milele katika moto wa helo.

Kwa hiyo, fundisho la Utatu ni nini? Kwa kweli ni fundisho la kipagani linalosingizia kuwa la Kikristo. Liliendelezwa na Shetani ili kuwadanganya watu, kumfanya Mungu awe mwenye kutatanika na wa kifumbo kwao. Tokeo ni kuwa kwao pia na nia ya kukubali mawazo bandia ya kidini na mazoea mengine yasiyofaa.

“Kwa Matunda Yao”

Kwenye Mathayo 7:15-19, Yesu alisema kwamba ungeweza kutofautisha kati ya dini bandia na dini ya kweli kwa njia hii:

“Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali. Mtawatambua kwa matunda yao. Je! watu huchuma zabibu katika miiba, na tini katika mibaruti? Vivyo hivyo kila mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri. Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni.”

Ona mfano mmoja. Yesu alisema kwenye Yohana 13:35: “Wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” Pia, kwenye 1 Yohana 4:20 na 21, Neno la Mungu lililopuliziwa roho hutangaza rasmi hivi:

“Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. Na amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake.”

Tumia kanuni hilo la msingi kwamba ni lazima Wakristo wa kweli wapendane wenywe kwa wenyewe kwa lile lililotukia katika vita vya ulimwengu vyote viwili vya karne hii, pamoja na katika mapigano mengineyo. Watu wa dini zile zile za Jumuiya ya Wakristo walikutana kwenye nyanja za vita na kuchinjana mmoja na mwenzake kwa sababu ya tofauti za kitaifa. Kila upande ulidai kuwa wa Kikristo, na kila upande uliungwa mkono na kasisi wake, aliyedai kwamba Mungu alikuwa kwa upande wao. Machinjo hayo ya “Wakristo kwa Wakristo” ni matunda mabaya. Ni kuvunja upendo wa Kikristo, mkano wa sheria za Mungu.—Ona pia 1 Yohana 3:10-12.

Siku ya Kutoa Hesabu

Hivyo, mwanguko huo kutoka Ukristo uliongoza si tu kwenye imani zisizomcha Mungu, kama vile fundisho la Utatu, bali pia kwenye mazoea yasiyomcha Mungu. Hata hivyo, kuna siku ya kutoa hesabu inayokuja, kwani Yesu alisema hivi: “Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni.” Ndiyo sababu Neno la Mungu husihi hivi:

“Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake.”—Ufunuo 18:4, 5.

Hivi karibuni Mungu ‘atatia moyoni mwa’ wenye mamlaka za kisiasa kugeuka dhidi ya dini bandia. “Watamfanya kuwa mkiwa . . . watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto.” (Ufunuo 17:16, 17) Dini bandia pamoja na falsafa zayo za kipagani juu ya Mungu zitakuwa zimeharibiwa milele. Kwa kweli, Mungu atawaambia hivi wale wenye kuizoea dini bandia kama Yesu alivyosema katika siku yake: “Nyumba yenu mmachiwa hali ya ukiwa.”—Mathayo 23:38.

Dini ya kweli itaokoka hukumu za Mungu, hivi kwamba, hatimaye, heshima na utukufu wote utapewa Yule ambaye Yesu alisema ndiye “Mungu wa pekee wa kweli.” Yeye ndiye aliyetambulishwa na mtunga zaburi aliyetangaza rasmi hivi: “Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”—Yohana 17:3; Zaburi 83:18.

Marejezeo:

 1. Encyclopœdia Britannica, 1971, Buku 6, ukurasa 386.

 2. A Short History of Christian Doctrine, cha Bernhard Lohse, 1963, ukurasa 51.

 3. Ibid., kurasa 52-3.

 4. New Catholic Encyclopedia, 1967, Buku 7, ukurasa 115.

 5. A Short History of Christian Doctrine, cha Martin E. Marty, 1959, ukurasa 91.

 6. A Select Library of Nicene and Post-Nicene Fathers of the Christian Church, cha Philip Schaff na Henry Wace, 1892, Buku 4, ukurasa 17.

 7. A Short History of Christian Doctrine, ukurasa 53.

 8. Ibid., ukurasa 91.

 9. The Church of the First Three Centuries, cha Alvan Lamson, 1869, kurasa 75-6, 341.

 10. Second Century Orthodoxy, cha J. A. Buckley, 1978, kurasa 114-15.

 11. New Catholic Encyclopedia, 1967, Buku 7, ukurasa 115.

 12. Ibid., Buku 4, ukurasa 436.

 13. Ibid., ukurasa 251.

 14. Ibid., ukurasa 436.

 15. The New Encyclopœdia Britannica, 1985, Chapa ya 15, Micropædia, Buku 1, ukurasa 665.

 16. The Church of the First Three Centuries, ukurasa 52.

 17. The Christian Tradition, cha Jaroslav Pelikan, 1971, ukurasa 173.

 18. Origin and Evolution of Religion, cha E. Washburn Hopkins, 1923, ukurasa 339.

[Maelezo ya Chini]

a Ili kupata habari zaidi, ona broshua Should You Believe in the Trinity? iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Kama ilivyoonyeshwa katika makala za mfululizo huu zilizotangulia, ingawa Theofilo na Tertuliani walitumia yale maneno, hawakumaanisha ule Utatu unaoaminiwa na Jumuiya ya Wakristo leo.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Mungu atawasababisha wenye mamlaka za kisiasa wageuke dhidi ya dini bandia

[Picha katika ukurasa wa 24]

Dini ya kweli itaokoka hukumu za Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki