Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ti kur. 7-12
  • Fundisho la Utatu Lilisitawi Jinsi Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Fundisho la Utatu Lilisitawi Jinsi Gani?
  • Je, Uamini Utatu?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sehemu Aliyoshiriki Konstantino Kule Nisea
  • Usitawi Zaidi
  • Imani ya Athanasio
  • Uasi-Imani Watabiriwa
  • Uvutano Uliolitokeza
  • Uplato
  • Kwa Nini Manabii wa Mungu Hawakuufundisha?
  • Sehemu ya 4-Fundisho la Utatu Lilisitawi Wakati Gani na Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Je, Uamini Utatu?
    Amkeni!—2013
  • Sehemu ya 1—Je! Yesu na Wanafunzi Wake Walifundisha Fundisho la Utatu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Je! Kwa Wazi Hilo Ni Fundisho la Biblia?
    Je, Uamini Utatu?
Pata Habari Zaidi
Je, Uamini Utatu?
ti kur. 7-12

Fundisho la Utatu Lilisitawi Jinsi Gani?

KUFIKIA hapo wewe ungeweza kuuliza: ‘Ikiwa Utatu si fundisho la Kibiblia, lilikujaje kuwa fundisho la Jumuiya ya Wakristo?’ Wengi hufikiri kwamba lilifanyizwa rasmi kwenye Baraza la Nisea katika 325 W.K.

Hata hivyo, hiyo si sahihi kabisa. Baraza la Nisea lilikazania kwamba Kristo alikuwa wa asili moja na Mungu, na hiyo ikaweka msingi wa theolojia ya Utatu baadaye. Lakini halikuthibitisha Utatu kuwa wa kweli, kwa maana kwenye baraza hilo hakukuwa na mtajo wowote wa roho takatifu kuwa ni mtu (nafsi) wa tatu wa Uungu wa muungano wa watatu.

Sehemu Aliyoshiriki Konstantino Kule Nisea

KWA miaka mingi, kwa kutegemea sababu za Kibiblia upinzani mwingi ulikuwa umekuwako kwenye wazo lililokuwa likisitawi kwamba Yesu ni Mungu. Ili kujaribu kutatua ubishi huo, maliki Mroma Konstantino aliita maaskofu wote waende Nisea. Karibu 300, kisehemu tu cha jumla yenyewe, ndio waliohudhuria hasa.

Konstantino hakuwa Mkristo. Yadhaniwa kwamba aliongoka baadaye maishani, lakini hakubatizwa mpaka alipokuwa amelala akifa. Kuhusu yeye, Henry Chadwick husema hivi katika The Early Church: “Konstantino, kama baba yake, aliabudu Jua Lisiloweza Kushindwa; . . . uongofu wake haupasi kufasiriwa kuwa alikuwa na neema ya kindani . . . Hilo lilikuwa jambo la kijeshi. Ufahamivu wake juu ya fundisho la Kikristo haukuwa wazi sana kamwe, lakini yeye alikuwa na uhakika kwamba ushindi katika pigano ulitegemea karama ya Mungu wa Wakristo.”

Maliki huyu asiyebatizwa alishiriki sehemu gani kwenye Baraza la Nisea? Encyclopædia Britannica husimulia hivi: “Konstantino mwenyewe ndiye aliyesimamia, akiongoza mazungumzo kwa utendaji mwingi, na yeye binafsi akapendekeza . . . ile kanuni kuu yenye kuonyesha uhusiano wa Kristo kwa Mungu katika imani iliyotolewa na baraza, ‘wa asili moja na Mungu’ . . . Kwa kumhofu mno maliki, maaskofu hao, isipokuwa wawili tu, walitia sahihi imani hiyo, wengi wao wakifanya hivyo dhidi sana ya mbetuko wao.”

Kwa hiyo, Konstantino alishiriki sehemu ya maana. Baada ya miezi miwili ya mjadala mkali sana wa kidini, mwanasiasa huyu mpagani aliingilia mambo na kuamua kwa kupendelea wale waliosema kwamba Yesu ni Mungu. Lakini kwa nini? Kwa uhakika haikuwa kwa sababu ya usadikisho wowote wa Kibiblia. “Kwa msingi Konstantino hakuwa na uelewevu wowote ule wa maswali yaliyokuwa yakiulizwa katika theolojia ya Kigiriki,” chasema A Short History of Christian Doctrine. Aliloelewa ni kwamba mgawanyiko wa kidini ulikuwa tisho kwa milki yake, naye alitaka kuimarisha eneo la utawala wake.

Hata hivyo, hakuna yeyote wa maaskofu huko Nisea aliyetetea wazo la Utatu. Wao waliamua juu ya asili ya Yesu tu lakini si sehemu ambayo roho takatifu hushiriki. Kama Utatu ungalikuwa ni ukweli ulio wazi wa Biblia, je! wasingalipaswa kuupendekeza wakati huo?

Usitawi Zaidi

BAADA ya Nisea, mijadala juu ya habari hiyo iliendelea kwa miongo mingi. Wale walioamini kwamba Yesu hakuwa sawa na Mungu hata walipendelewa kwa muda. Lakini baadaye Maliki Theodosius alifanya uamuzi dhidi yao. Alithibitisha imani ya Baraza la Nisea kuwa kiwango cha milki yake na akakutanisha Baraza la Konstantinopo katika 381 W.K. ili kuelewesha wazi kanuni hiyo.

Baraza hilo liliafikiana kuweka roho takatifu kwenye usawa mmoja na Mungu na Kristo. Kwa mara ya kwanza, Utatu wa Jumuiya ya Wakristo ukaanza kutokea.

Na bado, hata baada ya lile Baraza la Konstantinopo, Utatu haukuja kuwa imani yenye kukubaliwa mahali pengi. Wengi waliipinga na hivyo wakajiletea mnyanyaso wenye jeuri. Ni katika karne za baadaye tu kwamba Utatu ulifanyizwa katika imani zilizopangwa imara. The Encyclopedia Americana hutaarifu hivi: “Usitawi kamili wa Imani ya Utatu ulitukia Magharibi, katika Mifumo ya Kinadharia ya Wanachuo wa zile Enzi za Katikati, ambapo ufafanuzi ulianza kutolewa kwa namna ya falsafa na saikolojia.”

Imani ya Athanasio

UTATU ulifasiliwa kikamili zaidi katika Imani ya Athanasio. Athanasio alikuwa kasisi aliyemwunga mkono Konstantino huko Nisea. Imani hiyo yenye jina lake hujulisha wazi hivi: “Sisi huabudu Mungu mmoja katika Utatu . . . Baba ni Mungu, Mwana ni Mungu, na Mzuka [Roho] Mtakatifu ni Mungu; na bado wao si miungu watatu, bali Mungu mmoja.”

Hata hivyo, wanachuo wenye maarifa ya kutosha huafikiana kwamba si Athanasio aliyetunga imani hii. The New Encyclopædia Britannica hueleza hivi: “Imani hiyo haikujulikana kwa Kanisa la Mashariki mpaka karne ya 12. Tangu karne ya 17, kwa ujumla wanachuo wameafikiana kwamba Imani ya Athanasio haikuandikwa na Athanasio (alikufa 373) lakini labda ilitungwa kusini mwa Ufaransa wakati wa karne ya 5. . . . Uvutano wa imani hiyo waonekana kuwa ulikuwa kusini mwa Ufaransa hasa na Hispania katika karne za 6 na 7. Ulitumiwa katika liturjia ya kanisa katika Ujeremani katika karne ya 9 na baadaye kidogo katika Roma.”

Kwa hiyo ilichukua karne nyingi kuanzia wakati wa Kristo ili Utatu ukubaliwe na wengi katika Jumuiya ya Wakristo. Na katika yote haya, ni nini kilichoongoza maamuzi hayo? Je! ni Neno la Mungu au ni mafikirio ya kikasisi na ya kisiasa? Katika Origin and Evolution of Religion, E. W. Hopkins hujibu hivi: “Fasili iliyokubaliwa mwishowe juu ya utatu ilihusiana sana-sana na siasa za kanisa.”

Uasi-Imani Watabiriwa

HISTORIA hii yenye sifa mbaya juu ya Utatu yalingana na yale ambayo Yesu na mitume wake walitabiri yangekuja baada ya wakati wao. Walisema kwamba kungekuwa na uasi-imani, mpotoko, mwanguko wa kutoka kwenye ibada ya kweli mpaka kurudi kwa Kristo, wakati ambapo ibada ya kweli ingerudishwa kabla ya siku ya Mungu ya uharibifu wa mfumo huu wa mambo.

Kuhusu “siku” hiyo, mtume Paulo alisema: “Haiji, usipokuja kwanza ule ukengeufu [uasi-imani, NW]; akafunuliwa yule mtu wa kuasi.” (2 Wathesalonike 2:3, 7) Baadaye, alitabiri hivi: “Mimi nikiisha kwenda mbwa-mwitu wakali watawavamia nyinyi na watakuwa hawana rehema juu ya kundi la kondoo. Hata kutoka miongoni mwenu wenyewe watakuwako wanaume wenye kujitokeza wakiwa na mwigo bandia wa ukweli katika midomo yao ili kushawishi wanafunzi wawafuate wao.” (Matendo 20:29, 30, JB) Wanafunzi wengine wa Yesu waliandika pia juu ya uasi-imani huu pamoja na jamii yao ya makasisi ‘waasi.’—Kwa kielelezo, ona 2 Petro 2:1; 1 Yohana 4:1-3; Yuda 3, 4.

Pia Paulo aliandika hivi: “Hakika wakati utakuja ambapo, bila kuridhika hata kidogo na fundisho timamu, watu watataka sana mambo mapya yaliyo ya karibuni zaidi na kujikusanyia mpororo mzima wa walimu kulingana na ladha yao wenyewe; halafu, badala ya kusikiliza ukweli, watageukia hadithi za kutungwa.”—2 Timotheo 4:3, 4, JB.

Yesu mwenyewe alieleza jambo lenye kuchochea mwanguko huu wa kutoka kwenye ibada ya kweli. Alisema kwamba alikuwa amepanda mbegu zilizo njema lakini adui, Shetani, angepanda magugu juu ya ngano katika shamba. Kwa hiyo magugu pia yalitokea pamoja na vijani vya kwanza vya ngano. Hivyo, mpotoko wa kutoka kwenye Ukristo safi ungetarajiwa mpaka mavuno, ambapo Kristo angenyoosha mambo. (Mathayo 13:24-43) The Encyclopedia Americana hueleza hivi: “Uana-Utatu wa karne ya nne haukuonyesha kisahihi fundisho la mapema la Kikristo kuhusu asili ya Mungu; kwa kinyume, ulikuwa ni kupotoka kutoka fundisho hili.” Basi, mpotoko huu ulianzia wapi?—1 Timotheo 1:6.

Uvutano Uliolitokeza

MUDA wote wa ulimwengu wa kale, kurudi nyuma sana hadi Babulonia, ibada ya miungu ya kipagani iliyopangwa ikiwa miungano mitatu-mitatu, au miungano ya utatu, ilikuwa ya kawaida. Uvutano huo ulikuwapo sana katika Misri, Ugiriki, na Roma pia katika karne zilizotangulia, wakati wa Kristo na baadaye. Na baada ya kifo cha mitume, imani hizo za kipagani zilianza kuvamia Ukristo.

Mwanahistoria Will Durant alitoa maoni haya: “Ukristo haukuangamiza upagani; uliukubali. . . . Kutoka Misri yakaja mawazo ya utatu wa kimungu.” Na katika kitabu Egyptian Religion, Siegfried Morenz huarifu hivi: “Utatu ulikuwa wazo kubwa lililoshughulisha akili za wanatheolojia Wamisri . . . Miungu mitatu imeunganishwa na kutendewa kuwa kitu kimoja tu, chenye kutajwa katika umoja. Kwa njia hii kani ya kiroho ya dini ya Kimisri huonyesha ukamatano wa moja kwa moja na thelojia ya Kikristo.”

Hivyo, katika Aleksandria, Misri, wanakanisa wa mwishoni-mwishoni mwa karne ya tatu na wa mapema mwa karne ya nne, kama vile Athanasio, walionyesha uvutano huu huku wakifanyiza mawazo yaliyoongoza kwenye Utatu. Uvutano wao wenyewe ulienea, hivi kwamba Morenz huiona “theolojia ya Kialeksandria kuwa kipatanishi cha urithi wa dini ya Kimisri na Ukristo.”

Katika dibaji ya History of Christianity cha Edward Gibbon, twasoma hivi: “Ikiwa Upagani ulishindwa na Ukristo, kwa hali sawa na hiyo Ukristo ulifisidiwa [ulichafuliwa] na Upagani. Imani safi ya Wakristo wa kwanza katika Mungu . . . ilibadilishwa, na Kanisa la Roma, kuwa kanuni ya imani isiyofahamika ya utatu. Nyingi za itikadi za kipagani, zilizovumbuliwa na Wamisri na zikakamilishwa na Plato, zilidumishwa kuwa zastahiki kuaminiwa.”

A Dictionary of Religious Knowledge huarifu kwamba wengi husema kwamba Utatu “ni ufisadi ulioazimwa kutokana na dini za wasio Wakristo, nao ukapachikwa juu ya imani ya Kikristo.” Na The Paganism in Our Christianity hujulisha wazi hivi: “Asili ya [Utatu] ni ya kipagani kabisa.”

Ndiyo sababu, katika Encyclopædia of Religion and Ethics, James Hastings aliandika hivi: “Kwa kielelezo, katika dini ya Kihindi twakuta kikundi cha utatu wa Brahmā, Siva, na Viṣṇu; na katika dini ya Kimisri twakuta kikundi cha utatu wa Osiris, Isis, na Horus . . . Wala si katika dini za kihistoria tu kwamba twapata Mungu akionwa kuwa Utatu. Mtu hukumbuka hususa maoni ya Uplato-Mamboleo kuhusu Aliye Mkuu Kabisa au Uhakika wa Mwisho Kabisa,” ambaye “huwakilishwa kiutatu.” Mwanafalsafa Mgiriki Plato ana uhusiano gani na Utatu?

Uplato

PLATO afikiriwa kuwa aliishi kuanzia 428 hadi 347 kabla ya Kristo. Ingawa hakufundisha Utatu kwa namna ulivyo sasa, falsafa zake ziliutengenezea njia. Baadaye, harakati za kifalsafa zilizotia ndani imani za utatu zilitokea, nazo zikaathiriwa na uvutano wa mawazo ya Plato juu ya Mungu na asili.

Nouveau Dictionnaire Universel (Kamusi Mpya ya Ulimwengu Wote Mzima) ya Kifaransa husema hivi juu ya uvutano wa Plato: “Utatu wa Kiplato, wenyewe ukiwa ni mpango mpya tu wa utatu-utatu mwingi wa kale zaidi wenye kurudi nyuma kwenye watu wa mapema kabisa, huonekana kuwa ni maelezo ya akili ya kifalsafa ya sifa zilizozalia nyutu tatu, au watu wa kimungu wanaofundishwa na makanisa ya Kikristo. . . . Wazo hili la mwanafalsafa Mgiriki la utatu wa kimungu . . . laweza kupatikana katika dini zote za kale [za kipagani].”

The New Schaff-Herzog Encyclopedia of Religious Knowledge huonyesha uvutano wa falsafa hii ya Kigiriki: “Mafundisho ya Logos na Utatu yaliundwa na Mababa Wagiriki, ambao . . . kwa njia iliyo au isiyo ya moja kwa moja, waliathiriwa na uvutano wa falsafa ya Kiplato . . . Kwamba makosa na mafisadi yalipenya ndani ya Kanisa kutokana na chanzo hiki ni jambo lisiloweza kukanwa.”

The Church of the First Three Centuries husema hivi: “Fundisho la Utatu lilifanyizwa kidato kwa kidato na ni la baadaye kwa kulinganishwa . . . lilipata awali yalo katika chanzo kigeni kabisa kilicho tofauti na kile cha Maandiko ya Kiyahudi na ya Kikristo; . . . lilikua, na likapandikizwa juu ya Ukristo, kupitia mikono ya Mababa wenye kufuata mawazo ya Plato.”

Kufikia mwisho wa karne ya tatu W.K., “Ukristo” na falsafa mpya za Kiplato zikawa zimeungamana bila kutenganika. Kama vile Adolf Harnack ataarifu katika Outlines of the History of Dogma, fundisho la kanisa ‘lilitia mizizi imara katika udongo wa Uheleni [mawazo ya kipagani ya Kigiriki]. Hivyo likawa fumbo kwa Wakristo walio wengi.”

Kanisa lilidai kwamba msingi wa mafundisho yalo mapya ulikuwa Biblia. Lakini Harnack husema hivi: “Kwa kweli lilihalalisha lile kisio la Kiheleni, yale maoni ya kishirikina na desturi za ibada-fumbo ya kipagani kwa kuziingiza katikati yalo.”

Katika kitabu A Statement of Reasons, Andrews Norton husema hivi juu ya Utatu: “Twaweza kufuatilia historia ya fundisho hili, na kugundua kwamba chanzo chalo, si katika ufunuo wa Kikristo, bali katika falsafa ya Kiplato . . . Utatu si fundisho la Kristo na Mitume wake, bali bunilizi tu la shule ya Waplato wa baadaye.”

Hivyo, katika karne ya nne W.K., uasi-imani uliotabiriwa na Yesu na mitume ulichipuka kabisa. Usitawi wa Utatu ulikuwa uthibitisho mmoja tu wa jambo hili. Makanisa ya uasi-imani yalianza pia kuyakubali kwa moyo mawazo mengine ya kipagani, kama vile moto wa mateso, kutokufa kwa nafsi, na ibada ya sanamu. Kwa uneni wa kiroho, Jumuiya ya Wakristo ikawa imeingia katika vipindi vyayo vya giza vilivyotabiriwa, ikitawalwa na jamii yenye kukua ya makasisi walio “mtu wa kuasi.”—2 Wathesalonike 2:3, 7.

Kwa Nini Manabii wa Mungu Hawakuufundisha?

KWA nini, kwa maelfu ya miaka, hakuna yeyote wa manabii wa Mungu aliyefundisha watu wake juu ya Utatu? Na hata mwishowe kabisa, je! Yesu hangetumia uwezo wake akiwa Mfundishaji Mkubwa kufanya Utatu ueleweke wazi kwa wafuasi wake? Je! Mungu angevuvia mamia ya kurasa za Andiko na bado asitumie kadiri yoyote ya mafundisho haya kufundisha Utatu ikiwa huo ungekuwa ndilo “fundisho kuu” la imani?

Je! Wakristo waamini kwamba karne nyingi baada ya Kristo na baada ya Mungu kuwa amevuvia uandikaji wa Biblia, Yeye angeunga mkono kufanyizwa kwa fundisho lisilojulikana kwa watumishi wake kwa maelfu ya miaka, moja lililo “fumbo lisilochunguzika” ambalo “limezidi uwezo wa kufahamu wa akili ya kibinadamu,” moja ambalo hukiriwa kwamba lilikuwa na mwanzo wa kipagani na ‘likahusiana sana-sana na siasa za kanisa’?

Ushuhuda wa historia ni wazi: Fundisho la Utatu ni mpotoko kutoka kwenye ukweli, kuuacha kwa kuasi imani.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

‘Imani ya Utatu ya karne ya nne ilikuwa mpotoko kutoka kwenye fundisho la mapema la Kikristo.’—The Encyclopedia Americana

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

“Utatu wa Miungu Mikubwa”

Karne nyingi kabla ya wakati wa Kristo, kulikuwako utatu, au utatu-utatu, wa miungu katika Babulonia na Asiria ya kale. “Larousse Encyclopedia of Mythology” ya Kifaransa hutaja utatu wa jinsi hiyo katika eneo hilo la Mesopotamia: “Ulimwengu wote mzima uligawanywa katika majimbo matatu ambayo kila moja lilikuwa eneo la utawala wa mungu mmoja. Hisa ya Anu ilikuwa anga. Enlili alipewa dunia. Ea akawa mtawala wa maji. Wote pamoja wakafanyiza utatu wa Miungu Mikubwa.”

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Utatu wa Kihindu

Kitabu “The Symbolism of Hindu Gods and Rituals” husema hivi kuhusu utatu wa Kihindu uliokuwako karne nyingi kabla ya Kristo: “Siva ni mmoja wa miungu ya Utatu. Yeye husemwa kuwa mungu wa uharibifu. Miungu miwili mingine ni Brahma, mungu wa uumbaji na Vishnu, mungu wa udumishaji. . . . Ili kuonyesha kwamba taratibu tatu hizi ni kitu kimoja tena kile kile kimoja, miungu mitatu hiyo imeunganishwa katika namna moja.”—Kimechapishwa na A. Parthasarathy, Bombay.

[Picha katika ukurasa wa 8]

“Kwa msingi Konstantino hakuwa na uelewevu wowote ule juu ya maswali yaliyokuwa yakiulizwa katika theolojia ya Kigiriki.”—A Short History of Christian Doctrine

[Picha katika ukurasa wa 10]

1. Misri. Utatu wa Horusi, Osirisi, Isisi, mileani ya 2 K.W.K.

2. Babuloni. Utatu wa Ishtari, Sini, Shamashi, mileani ya 2 K.W.K.

3. Palmyra. Utatu wa mungu mwezi, Bwana wa Mbingu, mungu jua, karibu karne ya 1 W.K.

4. India. Uungu wa Utatu wa Kihindu, karibu karne ya 7 W.K.

5. Kampuchea. Uungu wa Utatu wa Kibuddha, karibu karne ya 12 W.K.

6. Norowei. Utatu (Baba, Mwana, roho mtakatifu), karibu karne ya 13 W.K.

7. Ufaransa. Utatu, karibu karne ya 14 W.K.

8. Italia. Utatu, karibu karne ya 15 W.K.

9. Ujeremani. Utatu, karibu karne ya 19 W.K.

10. Ujeremani. Utatu, karne ya 20 W.K.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki