Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 5/15 kur. 7-9
  • Ziara ya Kihistoria Yafanya Kisiwa Kishangilie

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ziara ya Kihistoria Yafanya Kisiwa Kishangilie
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Kukutana Tena kwa Furaha
  • Mambo Makuu ya Mkusanyiko
  • “Mambo Ambayo Hatutayasahau Kamwe”
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 5/15 kur. 7-9

Ziara ya Kihistoria Yafanya Kisiwa Kishangilie

Kuba, kisiwa kizuri cha Karibea, hivi karibuni kilikuwa na wakati wa burudiko la kiroho lisilo na kifani. Mwisho wa mwaka wa 1998 uliletea Mashahidi wa Yehova wanaoishi katika nchi hii ya West Indies baraka waliyongojea kwa muda mrefu. Kwa mara ya kwanza katika miaka zaidi ya 30, washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova walizuru Kuba, nao waliandamana na wajumbe wengine 15. Wageni hao walikuwa raia wa Australia, Austria, Italia, New Zealand, Puerto Riko, Ubelgiji, na Uingereza.

TUKIO hilo lilikuwa la kihistoria kwa wahubiri wa Ufalme 82,258 nchini humo na watu 87,890 waliojiunga nao kusherehekea Mlo wa Jioni wa Bwana katika masika ya 1998!

Kuanzia Desemba 1 hadi 7, 1998, Lloyd Barry, John Barr, na Gerrit Lösch walizuru Makao ya Betheli ya Havana na kuhudhuria baadhi ya Mikusanyiko ya Wilaya ya “Njia ya Mungu ya Maisha” iliyofanywa Kuba. Walifurahi kuweza kukutana na wazee wasafirio na kufahamiana vema zaidi na maofisa wa umma wa Kuba.

“Hilo lilikuwa jambo kuu la kitheokrasi katika maisha yangu na ya mke wangu,” John Barr akasema. “Ndugu na dada zetu wapendwa wa Kuba wana bidii nyingi kwa ajili ya kweli! Niliachwa na maoni kwamba udugu wetu wa ulimwenguni pote ni wenye thamani kwelikweli!” “Juma hilo la maana sana lilinisaidia kuelewa vema zaidi hali ya ndugu zetu huko,” Lloyd Barry akaongeza kusema.

Katika muda wa miaka mitano iliyopita, Mashahidi wa Yehova wamepewa uhuru zaidi wa ibada huko Kuba, na maelezo ya wenye mamlaka wa Kuba yafanya mtu aamini kwamba wangetaka hali hiyo iendelee.

Katika Septemba 1994, kazi ya uchapaji ilianzishwa katika Makao ya Betheli ya Havana. Kwa mara nyingine tena, Mashahidi wa Yehova waliweza kukutana waziwazi na kutoa ushahidi kutoka nyumba hadi nyumba. Baadaye katika mwaka wa 1998, wenye mamlaka waliruhusu ziara hiyo ya ujumbe wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova 18, kutia ndani washiriki watatu wa Baraza Linaloongoza.

Kukutana Tena kwa Furaha

Wajumbe walipowasili kwenye uwanja wa ndege wa José Martí ulioko Havana, walilakiwa kwa ukarimu na kikundi cha maofisa wa umma na kikundi kingine kutoka Makao ya Betheli, miongoni mwao akiwa ndugu ambaye alikumbuka ziara ya mwisho iliyofanywa Kuba na mshiriki wa Baraza Linaloongoza—Milton Henschel—mwaka wa 1961. Ndugu huyo alikuwa na umri wa miaka 12 wakati huo; sasa ni mwangalizi asafiriye.

Wajumbe walipowasili kwenye Makao ya Betheli, walilakiwa kwa kupewa mashada ya maua ya mzambarausime, waridi, yasimini, na kibibi yenye rangi ya kimanjano na nyekundu, yaliyokuzwa na ndugu fulani hasa kwa ajili ya pindi hiyo. Familia ya Betheli ilitokwa machozi ilipokuwa ikiwakaribisha wajumbe hao. Baadaye, walishiriki mlo wa nyama choma ya nguruwe wa Kuba, wali na maharagwe, saladi, yucca pamoja na mojo (mchuzi mzito uliopikwa kwa kitunguu saumu na mafuta ya zeituni), na matunda yaliyokuwa yamechumwa karibuni. Baada ya mlo kila mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba yenye kujenga juu ya thamani kubwa ya utumishi wa Betheli. Maneno ya Ndugu Lösch yaligusa moyo hasa, kwa vile alizungumza na ndugu hao kwa Kihispania. Familia ya Betheli ina wafanyakazi wa kawaida wa kujitolea 48 na wasaidizi 18.

Ingawa vitabu na Biblia za ndugu wa Kuba huchapiwa Italia, chapa za rangi nyeusi na nyeupe za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! huchapishwa Kuba kwenyewe kwa mashine mbili za urudufishaji. Muda mwingi pamoja na kazi ya mikono ya kurudiwa-rudiwa, ambayo hufanyiwa mahali penye kufinyana, huhitajika ili kuchapa magazeti yote yanayohitajiwa. Wajitoleaji huthamini utumishi wao kwa Yehova kwa njia ya pekee sana.—2 Wakorintho 4:7.

Mambo Makuu ya Mkusanyiko

Ujumbe huo wa washiriki 18 uligawanywa katika vikundi vitatu ili kuhudhuria mikusanyiko iliyofanywa kwenye maeneo matatu—Havana, Camagüey, na Holguín. Katika kila mojawapo ya siku hizo tatu, kikundi kikubwa cha ndugu na dada, kutia ndani wazee wengi na mapainia, walialikwa kuhudhuria kwenye maeneo hayo matatu. Mashahidi wenyeji walikuwa wameambiwa kwamba huo ungekuwa wakati wa pekee, lakini hawakujua kwamba washiriki wa Baraza Linaloongoza wangehudhuria. Ebu wazia jinsi walivyoshangaa kuwaona ndugu hawa wapendwa na wake zao Ijumaa asubuhi wakishuka kutoka katika mabasi yaliyokodishwa!

Mikusanyiko hiyo ilifanywa katika majengo yaliyo wazi ambayo yalijengwa na akina ndugu kwa ruhusa ya wenye mamlaka. Kwenye eneo la mkusanyiko la Havana, kulikuwa na andiko “Zaburi 133:1” lililokuwa limechongwa kwenye jiwe moja mahali pa kuingilia. Hilo liliwakumbusha akina ndugu maneno yaliyo katika andiko hilo: “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.” Bila shaka, wakati wa mkusanyiko kulikuwa na ushirika wa Kikristo mzuri na wenye kupendeza katika eneo hilo.

Wageni hao walitoa maoni yao juu ya utoaji bora wa hotuba na mahojiano, nao walivutiwa na namna drama ilivyoonyeshwa, ambayo ilitegemea hadithi ya Biblia iliyo katika kitabu cha Danieli sura ya 3, mandhari yakiwa Babiloni la kale. Dada mmoja alieleza hivi: “Waigizaji wote waliigiza vizuri sana, nako kupatanishwa kwa sauti kulikuwa kuzuri sana hivi kwamba hungetambua kwamba hiyo sauti ilikuwa imerekodiwa awali kwenye kinasa sauti. . . . Yule Mbabiloni mwovu alionekana mwovu kwelikweli, nao wale Waebrania watatu walikuwa imara na wenye kuazimia.”

Waakilishi wa Ofisi ya Mambo ya Kidini na maofisa wengine wa serikali waliokuja kuona mikusanyiko hiyo, waliwapongeza akina ndugu kwa utaratibu wao na mwenendo wao mzuri. Ndugu Barry alitoa shukrani zake za moyo mweupe kwa mapokezi mazuri ambayo wajumbe wenye kuzuru walipewa kutoka kwa wenye mamlaka wa Kuba. Kwa makofi ya shangwe, ambayo mara nyingi yaliendelea kwa dakika kadhaa, ndugu walionyesha uthamini wao kwa hotuba, na pia kwa wenye mamlaka kwa kuruhusu mikusanyiko hiyo ifanywe. “Hii ni zaidi ya vile tulivyotarajia—mkusanyiko mdogo wa kimataifa!” familia moja ya Kikristo ikasema. “Hali imekuwa yenye kupendeza sana, kwa kuwa imetoa uthibitisho wa nguvu kuu za Yehova za kutimiza ahadi zake.”

Mikusanyiko hiyo pia ilitoa fursa kwa wengine kupata kuwajua Mashahidi vema zaidi. Mmoja wa madereva wa basi alihudhuria mkusanyiko Jumamosi na Jumapili tena. Alisema kwamba alikuwa amesikia mambo mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova, lakini sasa alijua kwamba ni watu wazuri, wenye amani.

“Mambo Ambayo Hatutayasahau Kamwe”

Watu wa Kuba waliwavutia wajumbe hao kwa uchangamfu wao na urafiki wao. Wakuba ni wenye bidii ya kazi, wenye maadili, na wenye fadhili. “Mara kadhaa, watu wasiotujua kabisa walijitolea kutusaidia,” akasema mjumbe mmoja.

Wajumbe hao walivutiwa sana na imani, furaha, na upendo ulioonyeshwa na Mashahidi wenzao huko Kuba. Wamemfanya Yehova awe ngome yao licha ya vizuizi vikubwa sana. (Zaburi 91:2) John Barr alisema: “Mambo mengi sana yalinishangaza kwa njia yenye kupendeza wakati wa ziara yangu ya kwanza Kuba—uzuri wa nchi hiyo, tabia ya watu niliokutana nao, na zaidi ya yote, shangwe kuu ya Mashahidi wa Kuba. Maishani mwangu sijawahi kamwe kusikia kuimba kwenye kuhisiwa moyoni kama huko kwa nyimbo za Ufalme, na pia makofi yenye kupigwa kwa muda mrefu jinsi hiyo wakati mambo ya kiroho yalipogusa mioyo yao! Hayo ni mambo ambayo hatutayasahau kamwe. Tutayathamini daima.”

Zaburi 97:1 husema: “Visiwa vingi na vifurahi [“vishangilie,” NW].” Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova kisiwani Kuba wanashangilia uhuru wao uliongezeka wa kumwabudu Mungu, na kwa ziara ya kihistoria ya wajumbe hao wa kimataifa.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Familia nyingi zilihudhuria Mikusanyiko ya pekee ya Wilaya, “Njia ya Mungu ya Maisha,” iliyofanywa Kuba

[Picha katika ukurasa wa 8]

Makao ya Betheli ya Havana yalifunguliwa tena mwaka wa 1994

[Picha katika ukurasa wa 8]

Washiriki wa Baraza Linaloongoza wanatia sahihi Biblia zilizotolewa zawadi kwa maofisa wa umma

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki