Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 5/15 kur. 4-31
  • Je, Wewe Hutumia Wakati Ukiwa Pamoja na Familia Yako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Wewe Hutumia Wakati Ukiwa Pamoja na Familia Yako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukosefu wa Mawasiliano
  • Jitihada ya Kudhamiria Inahitajika
  • Msaada Kutoka kwa Neno la Mungu
  • Wazazi Na Watoto—wasilianeni Kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Kuwasiliana Ndani Ya Familia Na Katika Kundi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Kuzuia Mtengano Kati Yako na Watoto Nyumbani Mwako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Fanya Bidii ili Kuihifadhi Familia Yako Iingie Ndani ya Ulimwengu Mpya wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 5/15 kur. 4-31

Je, Wewe Hutumia Wakati Ukiwa Pamoja na Familia Yako?

“AKINA Baba Wajapani Wanapendwa—Ingawa Wana Shughuli Nyingi Nao Hawachezi na Watoto Wao.” Kichwa hicho kilikuwa katika gazeti Mainichi Shimbun miaka kadhaa iliyopita. Makala hiyo iliripoti kuwa asilimia 87.8 ya watoto Wajapani walioshiriki katika uchunguzi uliofanywa na serikali walionyesha tamaa ya kuwatunza baba zao wakati wa uzee. Hata hivyo, katika chapa ya Kiingereza ya gazeti hilo, makala hiyo iliandikwa chini ya kichwa tofauti. Kichwa hicho kilisema hivi: “Akina Baba na Wana: Hali ya Kutojali.” Kinyume cha ile chapa ya Kijapani, makala hiyo ilikazia jambo jingine katika uchunguzi huohuo: Kila siku ya kazi, akina baba Wajapani walitumia dakika 36 tu wakiwa pamoja na watoto wao. Kwa kulinganisha, akina baba wa Ujerumani Magharibi walitumia dakika 44 wakiwa pamoja na watoto wao katika siku ya juma, na huko Marekani, walitumia dakika 56.

Sio akina baba pekee wanaotumia wakati mchache wakiwa pamoja na watoto wao. Idadi inayozidi kuongezeka ya akina mama wanafanya kazi ya kuajiriwa. Kwa mfano, akina mama wasio na wenzi wa ndoa wanalazimika kufanya kazi ya kuajiriwa ili kuisaidia familia. Matokeo ni kuwa, kiasi cha wakati ambacho wazazi—akina baba kwa akina mama—hutumia wakiwa pamoja na watoto wao kimepungua.

Uchunguzi uliofanyiwa matineja 12,000 Wamarekani mwaka wa 1997 ulionyesha kwamba vijana walio na uhusiano wa karibu na wazazi wao hawaelekei kupatwa na matatizo kama vile mkazo wa kihisia-moyo, mawazo ya kujiua, kutenda jeuri, au kutumia vibaya alkoholi au dawa za kulevya. Naye mmoja wa watafiti walioshiriki katika uchunguzi huo mkubwa alisema: “Huwezi kuwa na uhusiano wa karibu na watoto isipokuwa uwepo wanapokuhitaji.” Kutumia wakati ukiwa pamoja na watoto wako na kuwasiliana nao ni jambo muhimu.

Ukosefu wa Mawasiliano

Familia ambazo hasa zaweza kudhuriwa na ukosefu wa mawasiliano ni zile zilizo na mzazi anayefanya kazi mbali na nyumbani. Lakini ukosefu wa mawasiliano hauathiri familia za mzazi anayeishi mbali na nyumbani pekee. Wazazi fulani, hata ingawa wanaishi nyumbani, huenda kazini huku watoto wakiwa wamelala bado na kurudi nyumbani watoto wakiwa tayari wamelala. Ili kulipia ukosefu wa mawasiliano unaotokea kwa sababu hiyo, wazazi fulani hutumia wakati wakiwa pamoja na familia siku za mwisho-juma na sikukuu. Wao husema juu ya kutumia ule uitwao wakati “bora” wakiwa pamoja na watoto wao.

Lakini je, kukosa kutumia wakati mwingi pamoja na watoto hulipiwa na ule wakati bora pamoja nao? Mtafiti Laurence Steinberg anajibu hivi: “Kwa ujumla, watoto wanaotumia wakati mwingi wakiwa pamoja na wazazi wao huwa bora kuliko watoto wanaotumia wakati mchache pamoja na wazazi wao. Yaonekana ni vigumu sana kulipia ukosefu huo wa wakati. Lile wazo la wakati bora limekaziwa isivyofaa.” Hivyo hasa ndivyo mwanamke wa Burma anavyohisi. Mume wake—mwanamume Mjapani anayefuata mtindo wa Kijapani—huja nyumbani kutoka kazini saa saba au saa nane kila usiku. Ingawa yeye hutumia wakati akiwa pamoja na familia yake siku za mwisho-juma, mke wake asema hivi: “Kuwa nyumbani siku za Jumamosi na Jumapili hakuwezi kulipia kule kukosa kuwa pamoja na familia kwa juma zima. . . . Je, unaweza kukosa milo yote katikati ya juma na ule milo yote ya juma hilo siku za Jumamosi na Jumapili?”

Jitihada ya Kudhamiria Inahitajika

Ni rahisi kusema juu ya kudumisha mawasiliano mazuri katika familia kuliko kufanya hivyo. Mkazo wa kutafuta riziki na kuiandalia familia mahitaji hufanya iwe vigumu kwa baba au mama aliyeajiriwa kutumia wakati akiwa pamoja na familia. Wengi ambao hali zao huwalazimu kuwa mbali na nyumbani huwasiliana kikawaida kwa simu au kwa barua. Lakini hata wawe pamoja nyumbani au la, jitihada ya kudhamiria inahitajika ili kudumisha mawasiliano mazuri katika familia.

Wazazi wanaopuuza kuwasiliana na familia zao hulazimika kulipia kupuuza kwao. Baba mmoja aliyetumia wakati mchache na familia yake, bila hata kula nao, alikabiliwa na matokeo mabaya sana. Mwana wake wa kiume aligeuka akawa mjeuri, binti yake naye akakamatwa akiiba dukani. Baba huyo alipokuwa akijitayarisha kwenda kwenye uwanja wa gofu Jumapili moja asubuhi, mwana wake alifoka kwa hasira. “Je, mama ndiye mzazi pekee katika nyumba hii?” akapiga kelele. “Mama huamua kila jambo katika familia hii. Baba, wewe kamwe . . . ,” kijana huyo akalia.

Maneno hayo yalimfanya baba afikiri. Hatimaye akaamua kuwa anapaswa kula kifungua-kinywa pamoja na familia, hiyo ikiwa hatua ya kwanza. Mwanzoni, alikula na mke wake pekee. Baadaye, watoto wakaungana nao, ndipo meza ya kifungua-kinywa ikawa eneo la mawasiliano. Hatua hiyo ilifanya waanze kula milo ya jioni pamoja. Hivyo, mwanamume huyo akawa ameanza kuchukua hatua ya kuokoa familia yake isivunjike kabisa.

Msaada Kutoka kwa Neno la Mungu

Biblia inawatia moyo wazazi wawe na wakati wa kuwasiliana na watoto wao. Waisraeli waliagizwa hivi kupitia nabii Musa: “Sikiza, Ee Israeli; BWANA, Mungu wetu, BWANA ndiye mmoja. Nawe mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii [“uyakaze kikiki katika mwana wako,” NW], na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” (Kumbukumbu la Torati 6:4-7) Ndiyo, sisi tulio wazazi tunahitaji kuchukua hatua ya kwanza ya kutumia wakati tukiwa na familia yetu ikiwa tutakazia kikiki maneno ya Mungu katika akili na mioyo ya watoto.

Kwa kupendeza, uchunguzi uliokwisha tajwa wa mwaka wa 1997, kuhusu vijana Wamarekani zaidi ya 12,000 ulifunua kuwa “kati ya watu asilimia 88 hivi . . . waliosema kwamba ni wanadini, ule unaodhaniwa kuwa umuhimu wa dini na sala ulikuwa ulinzi kwao.” Wakristo wa kweli hutambua kuwa maagizo mazuri ya kidini nyumbani huwalinda vijana dhidi ya utumizi mbaya wa alkoholi na dawa za kulevya, mkazo wa kihisia-moyo, kujiua, jeuri, na kadhalika.

Wazazi fulani huona ni vigumu kupata wakati wa kuwa pamoja na familia yao. Jambo hili ni kweli hasa kwa akina mama wasio na wenzi wa ndoa, ambao wangependa kutumia wakati wakiwa pamoja na watoto wao lakini hulazimika kufanya kazi ya kuajiriwa. Wanaweza kutafutaje kwa bidii wakati wenye thamani ili wawe na familia yao? “Zingatia hekima safi na busara,” Biblia yasihi. (Mithali 3:21, Biblia Habari Njema) Wazazi wanaweza kutumia “busara” ili kupata wakati kwa ajili ya familia. Jinsi gani?

Ikiwa wewe ni mama anayefanya kazi ya kuajiriwa nawe hujisikia umechoka sana baada ya kazi ya siku, mbona usiwaombe watoto wako wapike mlo pamoja nawe? Wakati kama huo unaotumiwa mkiwa pamoja ungeandaa fursa kwenu kukaribiana zaidi. Huenda kuhusisha watoto kukachukua wakati zaidi mara ya kwanza. Hata hivyo, baada ya muda mfupi utaona inafurahisha na hata kuokoa wakati.

Huenda wewe ni baba aliye na mambo mengi sana ya kufanya siku za mwisho-juma. Kwa nini usifanye baadhi ya kazi hizo ukiwa pamoja na watoto wako? Unaweza kuwasiliana nao mnapofanya kazi pamoja na wakati huohuo uwape mazoezi yafaayo. Shauri la Biblia la kukazia kikiki maneno ya Mungu katika watoto wako hukutia moyo useme nao ‘uketipo nyumbani mwako, utembeapo njiani’—naam, kila wakati. Unaonyesha “hekima safi” unapowasiliana na watoto wako wakati mnapofanya kazi pamoja.

Kutumia wakati ukiwa pamoja na familia yako huleta thawabu za kudumu. “Hekima hukaa nao wanaoshauriana,” mithali moja ya Biblia yasema. (Mithali 13:10) Ukitumia wakati kuwasiliana na familia yako, utakuwa katika hali bora ya kuwapa mwelekezo wenye hekima wa kupambana na matatizo ya maisha kila siku. Mwelekezo huo unaotolewa sasa unaweza kuokoa wakati mwingi na kuzuia masikitiko wakati ujao. Na zaidi, huo unaweza kukufurahisha wewe na wao pia. Ili utoe mwelekezo huo, unahitaji kutumia birika lenye hazina nyingi ya hekima inayopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Itumie kufundisha watoto wako na kuongoza hatua za familia yako.—Zaburi 119:105.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Vijana walio na uhusiano wa karibu na wazazi wao hawaelekei sana kuwa na matatizo ya mkazo wa kihisia-moyo

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mawasiliano mazuri huleta thawabu nyingi katika maisha ya familia

[Picha katika ukurasa wa 6]

Unapofanya kazi ukiwa pamoja na mtoto wako, unaweza kuwasiliana naye na kumpa mazoezi yafaayo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki