Kuwasiliana Ndani Ya Familia Na Katika Kundi
“Maneno yenu yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu.”—WAKOLOSAI 4:6.
1. Adamu alisema nini wakati Mungu alipomjulisha Hawa kwake?
“HAKUNA mtu yeyote aliye kisiwa . . . Kila mtu ni kipande cha bara kuu.” Ndivyo alivyoandika msomi mmoja karne nyingi zilizopita. Kwa kusema hivyo, alikuwa akithibitisha tu yale ambayo Muumba alisema juu ya Adamu: “Si vema huyo mtu awe peke yake.” Adamu alikuwa na kipawa cha usemi na lugha, kwa kuwa alikuwa amewapa wanyama wote majina. Lakini Adamu hakuwa na kiumbe mwingine yeyote wa kibinadamu ambaye angewasiliana naye. Si ajabu kwamba Mungu alipojulisha kwake Hawa mwenye kupendeza ili awe mke wake, mwanamume huyo alipaza sauti hivi: “Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu”! Hivyo, wakati familia ya kwanza ya kibinadamu ilipoanza, Adamu alianza kuwasiliana na mwanadamu mwenzake.—Mwanzo 2:18, 23.
2. Ni madhara gani yaweza kuwa tokeo la utazamaji televisheni usiodhibitiwa?
2 Familia ni mahali bora pa uwasiliano. Kwa kweli, kufanikiwa hasa katika maisha ya familia kunautegemea. Hata hivyo, kuwasiliana kunahitaji wakati na jitihada. Leo, mojawapo kati ya wevi wakubwa zaidi wa wakati ni televisheni. Yaweza kuwa kifaa cha kudhuru katika angalau njia mbili. Kwa upande mmoja, yaweza kuwa yenye kuvutia sana hivi kwamba washiriki wa familia wanaizoelea, ikitokeza upungufu wa uwasiliano. Kwa upande mwingine, televisheni yaweza kutumika kama njia ya kuepea kunapokuwa hali za kutoelewana au za maudhiko. Badala ya kuyatatua matatizo, wenzi wa ndoa wengine wamechagua kufunga mdomo na kutazama televisheni. Kwa hiyo televisheni yaweza kuchangia sana ukosefu wa kuwasiliana, ambao wasemekana kuwa kivunjaji ndoa kikuu. Wale walio na tatizo la kufanya utazamaji televisheni uwe wa kadiri ndogo wangefaa kufikiria kuiondoa kabisa.—Mathayo 5:29; 18:9.
3. Wengine wamenufaikaje kwa kupunguza utazamaji televisheni?
3 Kwa kweli, ripoti zenye kuchangamsha zimepokewa zikisimulia juu ya mibaraka inayotokea wakati utumizi wa televisheni ulipopunguzwa au hata kuondolewa kabisa. Familia moja iliandika hivi: “Tunasemezana zaidi . . . , kufanya uchunguzi zaidi wa Biblia . . . Tunacheza michezo pamoja . . . Sehemu zote za utumishi wetu wa shambani zimeongezeka.” Familia nyingine baada ya kuondolea mbali televisheni yao walisema hivi: “Sisi hatupunguzi gharama tu [walikuwa wameandikisha ili kuona programu za televisheni zenye kupelekwa kwa nyuzi za simu] bali pia tumekaribiana zaidi tukiwa familia na kupata mambo mengine zaidi yenye maana ya kufanya na wakati wetu. Hatukosi kamwe utendaji wenye kupendeza.”
Kutazama, Kuongea, na Kusikiliza
4. Wenzi wa ndoa waweza kuwasilishaje uthamini wao kwa ajili ya mmoja na mwenzake?
4 Kuna namna tofautitofauti za uwasilia-no ndani ya familia. Nyingine si za maneno. Watu wawili wanapoangaliana tu, hiyo ni namna moja ya uwasiliano. Kuwa pamoja kwaweza kuwasilisha hisia ya kujali. Wenzi wa ndoa wapaswa kuepuka kuwa mbali kutoka mmoja na mwenzake kwa vipindi virefu vya wakati isipokuwa kukiwa na sababu isiyoepukika. Wenzi wa ndoa waweza kuongezeana furaha kwa kuonea shangwe ushirika wa ukaribu walio nao ndani ya kifungo cha ndoa. Kwa jinsi wanavyotendeana kwa shauku na bado kwa heshima, iwe peupe au faraghani, wakionyesha adabu inayofaa katika mavazi na tabia, wao waweza kuwasilisha bila maneno uthamini wa kina kirefu kwa ajili ya mmoja na mwenzake. Mfalme Sulemani mwenye hekima alionyesha hilo kwa maneno haya: “Chemchemi yako ibarikiwe; nawe umfurahie mke wa ujana wako.”—Mithali 5:18.
5, 6. Kwa nini waume wapaswa kutambua umaana wa kuwasiliana na wake zao?
5 Uwasiliano unataka pia mazungumzo, maongezi—kusemezana pamoja, si kuambiana vijambo tu. Ingawa wanawake fulani huweza kueleza hisia zao vizuri kuliko wanaume, hiyo si sababu nzuri ya waume kuwa wenzi wa kimya. Waume Wakristo wapaswa kutambua kwamba ukosefu wa uwasiliano ni tatizo kuu katika ndoa nyingi, na kwa hiyo wanapaswa wajitahidi kuendeleza njia za uwasiliano zikiwa wazi. Kwa kweli, watafanya hivyo ikiwa wao, pamoja na wake zao, wanafuata shauri zuri ambalo mtume Paulo atoa kwenye Waefeso 5:25-33. Ili mume ampende mke wake kama mwili wake mwenyewe, ni lazima ahangaikie hali njema na furaha ya mke wake, si yake mwenyewe. Ili kutimiza hayo, uwasiliano ni wa lazima.
6 Mume hapaswi kuwa na mtazamo kwamba mke wake apaswa awaze au akisi kwamba mume anamthamini. Mke anahitaji kuhakikishiwa upendo wa mume wake kwake. Mume aweza kuonyesha uthamini wake katika njia nyingi—kwa maneno ya upenzi na zawadi zisizotazamiwa, na pia kwa kumjulisha kikamili juu ya mambo ambayo huenda yakamhusu. Pia kuna lile tatizo la kuonyesha uthamini kwa jitihada za mke wake, ziwe katika kujipamba kwake binafsi, ziwe katika kazi yake yenye bidii kwa ajili ya familia, au katika utegemezo wake wenye moyo mzima wa utendaji mbalimbali wa kiroho. Kwa kuongezea, ili mume atii shauri la mtume Petro kwenye 1 Petro 3:7, ‘kukaa na mke wake kulingana na maarifa,’ ni lazima awe na hisia-mwenzi, inayoonyeshwa kwa kuwasiliana na mke wake mambo yote yanayowahusu wote wawili, akimpa heshima kuwa chombo dhaifu.—Mithali 31:28, 29.
7. Mke ana wajibu gani wa kuwasiliana na mume wake?
7 Vilevile, ili mke atii shauri kwenye Waefeso 5:22-24 kuhusu ujitiisho, anahitaji kuhangaikia kuendeleza njia za uwasiliano pamoja na mume wake zikiwa wazi. Anahitaji “kumstahi mumewe,” kwa usemi wake na kwa mwenendo wake pia. Hapaswi kamwe kutenda kwa kujitegemea au kupuuza matakwa yake. (Waefeso 5:33) Nyakati zote, kwapasa kuwe na maongezi ya kisiri kati yake na mume wake.—Linganisha Mithali 15:22.
8. Ili kudumisha njia za uwasiliano zikiwa wazi, ni lazima wake wawe na nia ya kufanya nini?
8 Zaidi ya hayo, mke apaswa kuepuka kuvumilia hali ya kuteseka akiwa amejinyamazia tu ili kuonyesha kujisikitikia. Ikiwa kuna kutoelewana, acha atafute wakati unaofaa wa kuzungumzia jambo hilo. Naam, ajifunze kutokana na Malkia Esta. Yeye alikuwa na jambo lililohusu kufa au kupona, la kumjulisha mume wake. Kutenda kwake kwa haraka akiwa na hekima na busara kulimaanisha wokovu kwa Wayahudi. Tuna wajibu kwa wenzi wetu na kwa sisi wenyewe kuwasilisha habari ikiwa tumeudhiwa au tunaudhiwa. Busara na ufurahifu unaopatana na utakatifu wa Mungu vyaweza kusaidia kufanya uwasiliano uwe rahisi zaidi.—Esta 4:15–5:8.
9. Kusikiliza kuna daraka gani katika uwasiliano?
9 Jambo linalodokezwa katika kutumia usemi ili kuendeleza njia za uwasiliano zikiwa wazi ni ule wajibu wa kila mmoja wa kusikiliza yale ambayo yule mwingine anasema—na kufanya jitihada ya kutambua yale yaliyodokezwa bila kusemwa. Hilo linahitaji kumsikiliza yule anayesema kwa makini. Mtu hahitaji tu kutambua mawazo yanayoelezwa bali pia anahitaji kuwa mwangalifu kuhusu hisia za kikweli za maneno yanayosemwa, jinsi jambo linavyosemwa. Mara nyingi mume hupungukiwa katika jambo hilo. Huenda wake wakateseka kwa sababu waume hukosa kusikiliza. Na wake pia wanahitaji kusikiliza kwa uangalifu ili waepuke kukata maneno upesi. “Mwenye hekima asikie na kuongezewa elimu.”—Mithali 1:5.
Uwasiliano Kati ya Wazazi na Watoto
10. Ili wawasiliane kikamili na watoto wao, ni lazima wazazi wawe na nia ya kufanya nini?
10 Pia kuna hali ambapo wazazi na wazao wao wana tatizo la kuwasiliana. ‘Kumlea mtoto katika njia impasayo’ kunahitaji kuanzisha njia za uwasiliano. Kufanya hivyo kutasaidia kuhakikisha kwamba “hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Jambo la kwamba wazazi fulani hupoteza watoto wao kwenye ulimwengu nyakati nyingine lahusiana na pengo la uwasiliano lililositawika wakati wa ubalehe. Wajibu wa wazazi wa kuwasiliana na watoto wao daima unatokezwa kwenye Kumbukumbu la Torati 6:6, 7 hivi: “Maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” Naam, ni lazima wazazi wapishe wakati pamoja na watoto wao! Ni lazima wawe na nia ya kufanya dhabihu kwa ajili ya watoto wao.
11. Ni baadhi ya mambo gani ambayo wazazi wapaswa kuwasilisha kwa watoto wao?
11 Wazazi wasilisheni kwa watoto wenu habari ya kwamba Yehova awapenda wao na kwamba nyinyi pia mwawapenda. (Mithali 4:1-4) Acheni waone nia yenu ya kudhabihu raha na anasa kwa ajili ya ukuzi wao wa kiakili, kihisia, kimwili na kiroho. Yenye umaana katika jambo hilo ni hisia-mwenzi, yaani, uwezo wa wazazi kuona mambo kupitia macho ya watoto wao. Kwa kuonyesha upendo usio wa ubinafsi, nyinyi wazazi mwaweza kujenga kifungo cha mwungano chenye nguvu pamoja na watoto wenu na kuwatia moyo watumainishe siri zao kwenu badala ya kuzitumainisha kwa marika wao.—Wakolosai 3:14, HNWW.
12. Kwa nini vijana wapaswa kuwasiliana na wazazi wao kwa uhuru?
12 Kwa upande mwingine, vijana, mna wajibu wa kuwasiliana na wazazi wenu. Kuthamini yale ambayo wamewafanyia kutawasaidia nyinyi mwatumainie. Mnahitaji msaada na utegemezo wao, na itakuwa rahisi zaidi kwao kuwapa huo mkiwasiliana nao kwa uhuru. Kwa nini mfanye marika wenu wawe chanzo chenu kikuu cha kupata shauri? Yaelekea kwamba hao hawajawafanyia mengi kwa kulinganishwa na wazazi wenu. Hawajaona mengi maishani kupita nyinyi, na ikiwa wao si washiriki wa kundi, hawajali kweli kweli hali njema yenu ya milele.
Uwasiliano Ndani ya Kundi
13, 14. Ni kanuni zipi za Biblia zinazohusisha uwasiliano kati ya Wakristo?
13 Tatizo lingine ni kuendeleza njia za uwasiliano pamoja na ndugu zetu kundini zikiwa wazi. Tunahimizwa kwa uthabiti “tusiache kukusanyika pamoja.” Kusudi letu la kukusanyika ni nini? “Kuhimizana katika upendo na kazi nzuri.” Hilo lahitaji uwasiliano. (Waebrania 10:24, 25) Mtu akikuudhi, hiyo si sababu kabisa ya kutohudhuria mikutano. Endeleza njia za uwasiliano zikiwa wazi kwa kufuata kanuni ya msingi ya shauri ambalo Yesu alitupa kama lilivyorekodiwa kwenye Mathayo 18:15-17. Ongea na yule ambaye waona asababisha kutofurahi kwako.
14 Unapokuwa na matatizo pamoja na mmoja kati ya ndugu zako, fuata shauri la Kimaandiko kama lile lipatikanalo kwenye Wakolosai 3:13, NW: “Endeleeni kuchukuliana mmoja na mwenzake na kusameheana kabisa mmoja na mwenzake ikiwa ye yote ana sababu ya kulalamika juu ya mwenzake. Hata kama vile Yehova alivyowasamehe kabisa nyinyi.” Hilo ladokeza uwasiliano badala ya kukataa kusema na mtu. Na iwapo unaona kwamba mtu fulani anaonekana kutokuwa mwenye urafiki kuelekea wewe, fuata shauri lipatikanalo kwenye Mathayo 5:23, 24. Wasiliana, na kujaribu kufanya amani pamoja na ndugu yako. Hilo lahitaji upendo na unyenyekevu kwa upande wako, lakini una wajibu kwako mwenyewe na kwa ndugu yako kufuata shauri la Yesu.
Shauri na Kitia Moyo
15. Kwa nini Wakristo hawapaswi kukosa kuwasilisha shauri wakiwa na uwezo wa kufanya hivyo?
15 Wajibu wa kuwasilisha habari unahusika pia katika kufuata shauri la Paulo kwenye Wagalatia 6:1: “Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho [wenye sifa za kiroho, NW] mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe.” Kiasi chapasa kutufanya tukubali kwa utayari wakati mtu anapotuonyesha mahali tumefanya makosa katika usemi au mwenendo wetu. Kwa kweli, sisi sote twapaswa kuwa na mtazamo kama ule ambao mtunga zaburi Daudi alikuwa nao alipoandika hivi: “Mwenye haki na anipige, itakuwa fadhili; anikemee, itakuwa kama mafuta kichwani; kichwa changu kisikatae.” (Zaburi 141:5) Wazee hasa wapaswa kuwa mifano yenye kutokeza ya unyenyekevu, si kusisitiza juu ya maoni ya kibinafsi bali kuwa tayari kukubali kurekebishwa, wakikumbuka kwamba ‘jeraha zitiwazo na rafiki ni amini.’—Mithali 27:6.
16. Wasemaji wachanga wapaswa kupokea kwa furaha aina gani ya uwasiliano?
16 Ni mwendo wa hekima na kiasi kwa vijana kutafuta shauri na mwelekezo kutoka kwa Wakristo wakomavu, ambao yaelekea wana jambo lenye kujenga la kutoa. Hata wazee wa kundi waweza kunufaika katika njia hiyo. Kwa mfano, mzee mmoja alisema katika hotuba yake kwamba mibaraka inayotajwa kwenye Ufunuo 7:16, 17, juu ya kutokuwa na njaa na kiu tena, ni mambo ambayo kondoo wengine wangeweza kutazamia katika ulimwengu mpya. Hata hivyo, imeonyeshwa kwamba andiko hilo linatumika hasa kwa wakati wa sasa. (Ona Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kurasa 126-8.) Mzee aliyekuwa msikilizaji aliona kwamba apaswa kutaja jambo hilo kwa msemaji, lakini kabla ya kuwa na nafasi ya kufanya hivyo, msemaji mwenyewe alimpigia simu na kumwomba dokezo lolote la kufanyia maendeleo hotuba yake. Ndiyo, acheni tufanye iwe rahisi kwa wale ambao wangetaka kutusaidia kwa kuwasilisha tamaa yetu ya kupata shauri. Tusiwe wenye kuudhiwa na mambo madogo sana au wenye hasira inayogusika upesi mno.
17. Uwasiliano waweza kutumikaje kujenga ndugu zetu?
17 Mfalme Sulemani alitaja kanuni inayoweza kutumika kwa kufaa katika mazungumzo yetu. Alisema hivi: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” (Mithali 3:27) Tuna deni la upendo kwa ndugu zetu. Paulo alisema hivi: “Msiwe na deni kwa mtu ye yote, isipokuwa tu deni la kupendana. Ampendaye jirani yake ameitekeleza Sheria.” (Warumi 13:8, HNWW) Kwa hiyo uwe mwenye ukarimu kwa maneno yako ya kutia moyo. Je, mtumishi wa huduma mchanga atoa hotuba ya watu wote iliyo yake ya kwanza? Msifu. Je, dada amejitahidi sana au amefanya vizuri sana katika mgawo wake wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Mwambie jinsi ulivyoonea shangwe jitihada zake. Kwa ujumla, ndugu na dada zetu wanajitahidi kufanya vizuri iwezekanavyo nao watatiwa moyo na maneno ya uthamini yenye upendo.
18. Kujiamini sana kunapoonyeshwa, lingekuwa jambo la fadhili kufanya nini?
18 Tofauti na hilo, huenda msemaji mchanga akawa na uwezo mwingi, lakini kwa sababu ya kuwa mchanga, huenda akaonyesha kujiamini sana isivyofaa. Ni aina gani ya uwasiliano inayohitajiwa hapa? Je, halingekuwa jambo la fadhili ikiwa mzee mkomavu angeweza kumsifu kwa mambo yoyote mazuri katika hotuba yake lakini, wakati ule ule, amtolee kwa upole madokezo juu ya njia ambazo katika hizo angeweza kusitawisha kiasi katika wakati ujao? Uwasiliano kama huo ungeonyesha upendo wa kidugu na kusaidia wachanga kuondolea mbali mielekeo mibaya mapema, kabla haijakwama sana.
19. Kwa nini wazee na vichwa vya familia wapaswa kuwa wawasilianaji?
19 Wazee huwasiliana wenyewe kwa wenyewe na pamoja na kundi juu ya mambo yenye manufaa—wakiepuka, bila shaka, kufunua mambo ya kisiri, kama yale yanayohusika na matatizo ya kihukumu. Hata hivyo, kuwa wenye kufichaficha mambo mno hutokeza shuku na kuvunjika moyo na kwaweza kudhuru hali ya urafiki katika kundi—au katika familia. Kwa mfano, kila mtu huonea shangwe kusikia ripoti yenye kujenga. Kama vile mtume Paulo alivyotamani kuwasilisha zawadi za kiroho, wazee vilevile wapaswa kutamani kuwapa wengine habari zenye kujenga.—Mithali 15:30; 25:25; Warumi 1:11, 12.
20. Makala ifuatayo itazungumzia sehemu gani ya uwasiliano?
20 Naam, uwasiliano ni wa muhimu katika kundi la Kikristo na katika familia ya Kikristo pia. Isitoshe, ni wa lazima katika sehemu nyingine zaidi. Gani? Katika huduma ya Kikristo. Katika makala ifuatayo, tutazungumzia njia za kufanyia maendeleo stadi zetu za uwasiliano katika utendaji huu wenye umaana sana.
Ungejibuje?
◻ Kizuizi cha mara nyingi cha uwasiliano wa familia chaweza kushindwaje?
◻ Waume na wake waweza kutatuaje tatizo la uwasiliano?
◻ Wazazi na watoto waweza kuepukaje pengo la uwasiliano?
◻ Uwasiliano katika makundi na katika familia waweza kuthibitikaje kuwa wenye kujenga?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Uwasiliano mzuri huongeza hali njema na furaha ya familia