Yehova Na Kristo Wawasilianaji Mashuhuri
“Bwana MUNGU [Yehova NW] hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.”—AMOSI 3:7.
1. Ni njia zipi za uwasiliano zinazotumiwa leo?
LEO uwasiliano ni biashara ya dola milioni nyingi. Vitabu vyote vinavyotangazwa, magazeti ya habari na magazeti yote yanayochapwa kwa kawaida, programu zote za redio na televisheni zinazosambazwa, pamoja na sinema na michezo yote ya kuigiza, ni jitihada za uwasiliano. Ni vilevile na barua zote zinazoandikwa na kupelekwa na pia simu zote zinazopigwa. Zote ni jitihada za uwasiliano.
2. Ni ipi baadhi ya mifano ya maendeleo ambayo wanadamu wamefanya katika njia za uwasiliano za kimashine?
2 Maendeleo ambayo wanadamu wamefanya katika mashine za uwasiliano ni ya kushangaza. Kwa mfano, nyugwe za simu zenye kufanyizwa kwa nyuzinyuzi za kioo, ambazo ni bora sana kuliko nyugwe za simu za shaba nyekundu, zaweza kuwasilisha maongezi ya simu makumi ya maelfu kwa wakati mmoja. Kisha kuna uwasiliano wa satelaiti (vyombo vya angani), zinazoizunguka dunia zikiwa angani na zenye vifaa vya kupokea na kupeleka ishara za simu, redio na televisheni. Satelaiti moja kama hiyo yaweza kushughulikia jumbe 30,000 za simu kwa wakati mmoja!
3. Ni nini kinachotukia wakati kuna mapengo ya uwasiliano?
3 Lakini zijapokuwa njia hizo zote za uwasiliano, kuna huzuni nyingi ulimwenguni kwa sababu ya ukosefu wa uwasiliano kati ya watu. Hivyo, tunaambiwa “kuna shimo kubwa lenye kukua—‘pengo la uwasiliano’ lenye kupanuka—kati ya watawala na wanaotawalwa.” Na ni nini kile kiitwacho kwa kawaida pengo la kizazi ikiwa si kule kushindwa kwa wazazi na wazao wao kuwasiliana kwa mafanikio? Washauri wa ndoa huripoti kwamba tatizo lililo kubwa zaidi katika ndoa ni ukosefu wa uwasiliano kati ya mume na mke. Ukosefu wa uwasiliano wenye kufaa waweza hata kusababisha kifo. Mapema katika 1990, watu 73 walipoteza uhai wao katika anguko la ndege, kisababishi kimoja kilichochangia kikiwa ni ukosefu wa uwasiliano kati ya rubani na wenye kuongoza ndege kutoka chini. Kichwa cha gazeti moja la habari kilitangaza rasmi hivi: “Kizuizi Katika Uwasiliano Kiliongoza Kwenye Msiba.”
4. (a) Ni nini kinachomaanishwa na “uwasiliano”? (b) Mradi wa uwasiliano wa Kikristo ni nini?
4 Uwasiliano ni nini kwa habari ya Wakristo? Kulingana na kamusi moja, “uwasiliano” humaanisha “kupasha habari, wazo, au hisia ili ipokewe au ieleweke vizuri.” Kamusi nyingine huieleza kuwa “njia ya kueleza mawazo kwa matokeo.” Angalia fasili hiyo, “njia ya kueleza mawazo kwa matokeo.” Uwasiliano wa Kikristo hasa huhitaji kuwa wenye matokeo kwa sababu mradi wao ni kufikia mioyo ya watu na kweli kutoka Neno la Mungu ikitarajiwa kwamba, watatenda kulingana na yale wamejifunza. Tofauti na mengine, uwasiliano huo huongozwa na kutokuwa na ubinafsi, na upendo.
Yehova Akiwa Mwasilianaji
5. Ni nini moja ya njia za kwanza ambazo Yehova aliwasiliana na binadamu?
5 Yehova Mungu bila shaka ndiye Mwasilianaji mkuu zaidi. Kwa sababu alituumba katika mfano wake, yeye aweza kuwasiliana na sisi, nasi twaweza kuwasiliana na wengine juu yake. Tangu kuumbwa kwa mwanadamu, Yehova amewasiliana na viumbe wake wa kidunia juu yake mwenyewe. Njia moja ambayo amefanya hivyo imekuwa kupitia uumbaji wake uonekanao. Hivyo, mtunga zaburi atuambia hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake. Mchana husemezana na mchana, usiku hutolea usiku maarifa.” (Zaburi 19:1, 2) Na Warumi 1:20 yatujulisha kwamba “sifa zake [Mungu] zisizoonekana zinaonekana wazi tangu kuumbwa ulimwengu na kuendelea.” “Zinaonekana wazi”—inaonyesha uthibitisho wa uwasiliano wenye matokeo!
6. Yehova aliwasilisha nini kwa viumbe wake wa kidunia walipokuwa katika bustani ya Edeni?
6 Wale wasio na imani katika Mungu na ufunuo wake wa kimungu wangependa kujaribu kutufanya tuamini kwamba binadamu apaswa kutegemea chanzo chake mwenyewe cha habari ili apate kujua kwa sababu gani yu hai. Lakini Neno la Mungu laonyesha wazi kwamba Mungu amewasiliana na binadamu tangu mwanzo. Hivyo, Mungu aliwapa mwanamume na mwanamke wa kwanza agizo hili la uzazi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale . . . kila kiumbe chenye uhai.” Mungu pia aliwaacha wale matunda ya bustani mpaka washibe—isipokuwa matunda ya mti mmoja. Halafu, Adamu na Hawa walipokosa kutii, Yehova aliwasilisha ahadi ya kwanza ya Kimesiya, akiipa ainabinadamu mwonzi wa tumaini: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako [mbegu yako, NW] na uzao wake [mbegu yake, NW]; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.”—Mwanzo 1:28; 2:16, 17; 3:15.
7. Kitabu cha Mwanzo kinafunua nini juu ya kuwasiliana kwa Yehova pamoja na watumishi wake?
7 Mwana wa Adamu Kaini alipojawa na kijicho chenye kutaka kuua, Yehova Mungu aliwasiliana naye, akisema, kama hivi: ‘Jihadhari! Wewe waelekea kwenye taabu!’ Lakini Kaini alikataa kutii onyo hilo akamwua ndugu yake. (Mwanzo 4:6-8) Halafu, dunia ilipojaa jeuri na uovu, Yehova aliwasilisha kwa mwanamume mwadilifu Noa kusudi Lake la kusafisha dunia kwa kufagilia mbali yote yaliyokuwa yakiichafua. (Mwanzo 6:13–7:5) Baada ya Gharika, Noa na familia yake walipotoka kwenye safina, Yehova aliwasilisha kwao kusudi lake kuhusu utakati-fu wa uhai na damu, na kupitia upinde akatoa uhakikisho kwamba yeye hangeharibu tena vitu vyote vyenye uhai kwa furiko. Karne nyinginezo baadaye, Yehova aliwasilisha kwa Abrahamu kusudi Lake kufanya familia zote za ainabinadamu zijibariki kupitia Mbegu ya Abrahamu. (Mwanzo 9:1-17; 12:1-3; 22:11, 12, 16-18) Na Mungu alipotoa amri kwamba angeharibu watu wa Sodoma na Gomora waliopotoka, aliwasilisha jambo hilo kwa Abrahamu, akisema hivi: “Je! ninaweka jambo ninalofanya likiwa limefunikwa kutoka kwa Abrahamu?”—Mwanzo 18:17, NW.
8. Yehova amewasiliana na watumishi wake duniani katika njia zipi nne?
8 Kuanzia na Musa, Yehova alitumia mfuatano mrefu wa manabii kuwasiliana na Israeli. (Waebrania 1:1) Nyakati nyingine alitumia imla simulizi kama alipomwambia Musa: “Andika maneno haya.” (Kutoka 34:27) Yehova aliwasiliana na wasemaji wake mara nyingi zaidi kwa njia ya njozi, kama alivyokuwa tayari amefanya na Abrahamu.a Yehova alitumia ndoto pia kuwasiliana na wanadamu, si na watumishi wake tu bali pia na wale waliokuwa na shughuli pamoja na watumishi wake. Kwa mfano, Yehova alisababisha wafungwa wawili wenzi wa Yusufu kuwa na ndoto, ambazo Yusufu aliwafafanulia. Yehova alisababisha Farao na Nebukadreza pia wawe na ndoto, ambazo watumishi wake Yusufu na Danieli waliwafafanulia. (Mwanzo 40:8–41:32; Danieli sura za 2 na 4) Kwa kuongezea, Yehova alitumia wajumbe wa kimalaika pindi nyingi kuwasiliana na watumishi wake.—Kutoka 3:2; Waamuzi 6:11; Mathayo 1:20; Luka 1:26.
9. Ni nini kilichomsukuma Yehova kuwasiliana na watu wake Israeli, kama inavyoonwa kwa maneno gani yake?
9 Uwasiliano wote kama huo wa Yehova kupitia manabii wake ulionyesha upendo wake kwa watu wake Israeli. Hivyo, alitaarifu kwa njia ya nabii wake Ezekieli hivi: “Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi. Ghairini, ghairini, mkaache njia zenu mbaya; mbona mnataka kufa, Enyi nyumba ya Israeli?” (Ezekieli 33:11) Yehova alikuwa Mwasilianaji mstahimilivu na mwenye subira na watu wake wa kale wenye kuasi, kama inavyoweza kuonwa kutokana na 2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16: “BWANA [Yehova, NW] Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake; lakini . . . [walidharau] maneno yake, na kuwacheka manabii wake hata . . . kusiwe na kuponya.”
10. Yehova huwasilianaje na watu wake leo, naye ni Mungu wa uwasiliano kwa kadiri gani?
10 Leo, tuna Neno la Mungu lililopuliziwa roho, Biblia Takatifu, ambalo kupitia hilo Yehova hutuwasilishia habari juu yake, makusudi yake, na penzi lake kwa ajili yetu. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa kweli, akiwa Mwasilianaji Mwenye Fahari, Yehova atangaza rasmi hivi: “Hakika Bwana MUNGU [Yehova, NW] hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.” (Amosi 3:7) Yeye huwajulisha watumishi wake yale anayokusudia kufanya.
Mwana wa Mungu Akiwa Mwasilianaji
11. Ni nani mwenye kutumiwa na Yehova kama chombo cha mbele zaidi cha kuwasiliana na mwanadamu, na ni kwa nini cheo chake “Neno” kinafaa?
11 Kati ya wajumbe wote waliotumiwa na Yehova kuwasilisha penzi Lake, aliye wa mbele zaidi ni yule Neno, Logosi, aliyekuwa Yesu Kristo. Ni nini maana ya kuitwa kwake Neno, au Logosi? Inaonyesha kwamba ndiye Msemeaji Mkuu wa Yehova. Na msemeaji ni nani? Mtu anayewasilisha yale ambayo mwingine anasema. Kwa hiyo Logosi akawa mwasilianaji wa neno la Yehova Mungu kwa uumbaji Wake wa kidunia wenye akili. Daraka hilo ni lenye maana sana hivi kwamba aitwa Neno.—Yohana 1:1, 2, 14.
12. (a) Yesu alikuja duniani kwa kusudi gani? (b) Ni nini kinachoshuhudia kutimiza kwake kusudi hilo kwa uaminifu?
12 Yesu mwenyewe alimwambia Pontio Pilato kwamba kusudi lake kuu la kuja duniani lilikuwa kuwasilisha kweli kwa ainabinadamu: “Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli.” (Yohana 18:37) Na rekodi katika Gospeli husimulia jinsi alivyoutekeleza mgawo huo vema. Mahubiri yake juu ya Mlima yanatambuliwa kuwa ndiyo mahubiri makuu yaliyopata kuhubiriwa na binadamu wakati wowote. Jinsi alivyowasiliana vema kupitia hotuba hiyo! “Ikawa . . . makutano [waliosikia mahubiri hayo] walishangaa mno kwa mafundisho yake.” (Mathayo 7:28) Kuhusu pindi nyingine, tunasoma hivi: “Mkutano mkubwa walikuwa wakimsikiliza kwa furaha.” (Marko 12:37) Maofisa fulani walipotumwa wakamkamate Yesu, walirudi bila yeye. Kwa nini? Waliwajibu Mafarisayo hivi: “Hajanena kamwe mtu ye yote kama huyu anavyonena.”—Yohana 7:46.
Wanafunzi wa Kristo Wapewa Utume wa Kuwa Wawasilianaji
13. Ni nini kinachoonyesha kwamba Kristo hakuridhika na kuwa mwasilianaji wa pekee?
13 Kwa kutoridhika na kuwa mwasilianaji wa pekee, Yesu kwanza aliwapa mitume 12 na kisha waevanjeli 70 utume wa kuenenda wakiwa wawasilianaji wa habari njema za Ufalme. (Luka 9:1; 10:1) Halafu muda mfupi kabla ya kupaa kwake mbinguni, aliwapa wanafunzi wake utume wa kufanya kazi ya kipekee. Kazi gani? Kama tusomavyo kwenye Mathayo 28:19, 20, aliwaagiza kuwa wawasilianaji; nao walitakiwa wafundishe wengine zaidi wawe wawasilianaji pia.
14. Wawasilianaji Wakristo wa mapema walikuwa wenye matokeo kwa kadiri gani?
14 Je, wanafunzi walikuwa wawasilianaji wenye matokeo? Bila shaka walikuwa! Likiwa tokeo la kuhubiri kwao siku ya Pentekoste 33 W.K., nafsi 3,000 ziliongezwa kwenye kundi la Kikristo lililoanzishwa karibuni. Upesi idadi ikaongezeka kuwa watu 5,000. (Matendo 2:41; 4:4) Si ajabu kwamba adui zao Wayahudi waliwashtaki kuwa walikuwa wameijaza Yerusalemu yote na mafundisho yao na baadaye wakalalamika kwamba kwa kuhubiri kwao walikuwa wameipindua dunia yenye kukaliwa!—Matendo 5:28; 17:6.
15. Yehova ametumia nini katika nyakati za kisasa kama chombo cha kuwasiliana na watu?
15 Ni vipi nyakati za kisasa? Kama ilivyotabiriwa kwenye Mathayo 24:3, 45-47, Bwana, Yesu Kristo, ameweka “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” aliye Wakristo wapakwa mafuta, atunze mali zake zote duniani muda wa siku hii ya kuwapo kwake. Huyo mtumwa mwaminifu mwenye akili anawakilishwa leo na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, lililo na Watch Tower Bible and Tract Society ikiwa shirika layo la utangazaji. Kwa kufaa sana, mtu-mwa mwaminifu na mwenye akili huyo amekuwa pia akiitwa mfereji wa Mungu wa uwasiliano. Mtumwa huyo kisha atutia moyo kuwa wawasilianaji wazuri. Kwa hakika, toleo la kwanza kabisa la Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence liliwashauri wasomaji walo hivi: “Ikiwa una jirani au rafiki ambaye unafikiri angependezwa au kunufaika na maagizo [ya gazeti hili], waweza kuyajulisha kwao; hivyo uhubiri Neno na kufanya mema kwa watu wote kama ulivyo na nafasi.”
16. Ni nini kinachoonyesha kwamba mengi zaidi yanahitajiwa kuliko Biblia tu ili Mungu awasiliane na watumishi wake wa kidunia kwa njia yenye matokeo?
16 Hata hivyo, kuwa na Neno la Mungu tu na kulisoma kibinafsi hakutoshi ili kupata maarifa sahihi yatakayomfanya mtu atembee kwenye barabara ielekeayo kwenye uhai. Kumbuka yule ofisa wa kifalme Mwethiopia aliyekuwa akisoma unabii wa Isaya lakini asielewe aliyokuwa akisoma. Filipo mwevanjeli alimweleza unabii huo, na baada ya hapo akawa tayari kubatizwa akiwa mwanafunzi wa Kristo. (Matendo 8:27-38) Ukweli wa kwamba mengi zaidi yanahitajiwa kuliko tu kusoma Biblia mwenyewe waweza kuonwa kutokana na Waefeso 4:11-13, NW, ambapo Paulo aonyesha kwamba Kristo hakutoa wengine kuwa watume wenye kupuliziwa roho na manabii tu bali pia alitoa wengine “kuwa waevanjeli, wengine kuwa wachungaji na walimu, kwa kusudi la kurekebisha upya watakatifu, kwa ajili ya kazi ya huduma, kwa ajili ya kujengwa kwa mwili wa Kristo, mpaka sisi sote tuufikie umoja katika imani na katika maarifa sahihi ya Mwana wa Mungu, kufikia mtu mzima, kwenye kipimo cha kimo ambacho ni cha ujazi wa Kristo.”
17. Tunaweza kutambua shirika ambalo Yehova anatumia leo kuwasilisha makusudi yake kwa ainabinadamu kwa alama zipi za utambulisho?
17 Twaweza kutambuaje wale wanaotumiwa na Yehova Mungu na Yesu Kristo kusaidia watu ambao wangekuwa Wakristo kufikia hatua ya kuwa mtu mzima? Kulingana na Yesu, alama moja ya kuwatambulisha ingekuwa kwamba hao hupendana kama Yesu alivyowapenda wafuasi wake. (Yohana 13:34, 35) Alama nyingine ya utambulisho: Wao hawangekuwa sehemu ya ulimwengu, hata kama vile Yesu hakuwa sehemu ya ulimwengu. (Yohana 15:19; 17:16) Alama nyingine bado ingekuwa kwamba wanakubali Neno la Mungu kuwa kweli, kama Yesu alivyokubali, wakitumia mamlaka yalo daima. (Mathayo 22:29; Yohana 17:17) Kutanguliza jina la Mungu, kama alivyofanya Yesu, kungekuwa alama nyingine. (Mathayo 6:9; Yohana 17:6) Na alama nyingine moja ingekuwa kufuata mfano wa Yesu katika kuhubiri Ufalme wa Mungu. (Mathayo 4:17; 24:14) Kuna kikundi kimoja tu kinachotimiza matakwa hayo, yaani, wawasilianaji wa kimataifa wajulikanao kuwa Mashahidi wa Yehova wa Kikristo.
18. Ni sehemu zipi tatu za uwasiliano zitakazozungumziwa na makala zifuatazo?
18 Hata hivyo, uwasiliano hudokeza daraka kuelekea wengine. Wakristo wana daraka la kuwasiliana na nani? Kwa msingi, kuna sehemu tatu ambazo katika hizo Wakristo wapaswa kuhangaikia kudumisha uwasiliano: familia, kundi la Kikristo, na huduma ya shambani ya Kikristo. Makala zifuatazo zitazungumzia sehemu hizo nyingine za habari yetu.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Mwanzo 15:1; 46:2; Hesabu 8:4; 2 Samweli 7:17; 2 Mambo ya Nyakati 9:29; Isaya 1:1; Ezekieli 11:24; Danieli 2:19; Obadia 1; Nahumu 1:1; Matendo 16:9; Ufunuo 9:17.
Ungejibuje?
◻ Madhara gani yaweza kutokea kutokana na ukosefu wa uwasiliano?
◻ Ni nani walio wawasilianaji wawili wa mbele zaidi?
◻ Yehova ametumia njia zipi mbalimbali kuwasiliana na binadamu?
◻ Yesu alikuwaje mwasilianaji bora sana?
◻ Wakristo wa mapema walifanikiwa kwa kadiri gani katika uwasiliano?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kama Baba yake wa kimbingu, Yesu alikuwa mwasilianaji mwenye huruma