Uwasiliano Katika Huduma Ya Kikristo
“Kwa hiyo nendeni, mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”—MATHAYO 28:19, NW.
1. Ni utume upi uliopewa na Kristo unaodokeza uhitaji wa kuwasilisha habari?
UTUME wa Yesu, ulionukuliwa juu, unatutolea mwito wa ushindani wa kuwasiliana na watu katika huduma yetu tuendapo nyumba kwa nyumba, kufanya ziara za kurudia, na kushiriki katika sehemu nyingine zote za kuhubiri Ufalme. Daraka la kujulisha kweli juu ya Yehova Mungu, Yesu Kristo, na Ufalme wa Kimesiya ambamo Yesu atawala sasa, linatiwa katika utume huo.—Mathayo 25:31-33.
2. Ili kuwasilisha habari kwa njia yenye matokeo, twapaswa kufanya nini?
2 Twaweza kuwasilishaje habari kwa njia yenye matokeo? Kwanza, ni lazima tuamini habari ile tunayowasilisha. Maana yake, ni lazima tuwe na imani yenye nguvu kwamba Yehova ndiye yule Mungu mmoja wa kweli, kwamba Biblia ni Neno la Mungu kweli kweli, na kwamba Ufalme wa Mungu ndilo tumaini la pekee kwa ainabinadamu. Kwa njia hiyo, yale tufundishayo yatatoka moyoni, nasi tutakuwa tukifuata shauri la Paulo kwa Timotheo: “Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.”—2 Timotheo 2:15.
Uwasiliano Bila Maneno
3-5. (a) Twaweza kuwasilishaje habari bila hata kusema lolote? (b) Ni mambo gani yaliyoonwa yanayoonyesha hilo?
3 Uwasiliano mara nyingi huhusisha maneno. Lakini, kwa uhakika, sisi huwasiliana na watu hata kabla hatujasema nao. Jinsi gani? Kwa mwenendo wetu na kwa njia tunayojivika na kujipamba. Miaka kadhaa iliyopita misionari mhitimu wa Watchtower Bible School of Gilead alikuwa akisafiri kwa meli kwenda kwenye mgawo wake wa kigeni. Baada ya siku chache baharini, mtu asiyemjua alimwuliza kwa nini yeye alikuwa tofauti sana na watu wengine wote melini. Misionari alikuwa akiwasilisha jambo linalostahili kuangaliwa—kwamba alikuwa na viwango tofauti na mwenye kufikilika—kwa sura yake na mwenendo wake tu. Hilo lilimtolea misionari huyo nafasi nzuri ya kutoa ushahidi.
4 Halafu tena, dada mmoja aliyekuwa akisimama barabarani akitolea wapitaji vichapo vya Biblia alimpa mwanamke aliyekuwa akitembea karibu naye tabasamu ya kirafiki. Mwanamke huyo akaanza kuteremka ngazi kwenda kituo cha gari-moshi inayopita chini ya ardhi. Kisha akabadili nia yake, akarudi penye dada, akaomba funzo la Biblia nyumbani. Ni nini kilichomvutia? Ingawa hakuwa ametolewa vichapo vya Biblia, alikuwa amepokea tabasamu ya kirafiki kutoka kwa Shahidi aliyekuwa akifanya kazi ya barabarani.
5 Mfano wa tatu: Kikundi cha Mashahidi vijana walikula katika mkahawa wakashangaa wakati mtu wasiyemjua alipokaribia meza yao na kuwalipia chakula chao. Mbona alifanya hivyo? Alikuwa amevutiwa na mwenendo wao. Bila kumwambia lolote mtu huyo wasiyemjua, Wakristo hao wachanga walikuwa wamewasilisha habari kwamba walikuwa watu wenye kumhofu Mungu. Kwa wazi, kwa mwenendo, sura, na urafiki wetu, sisi tunawasilisha habari hata kabla ya kusema neno lolote.—Linganisha 1 Petro 3:1, 2.
Kusababu Ni Muhimu
kwa Uwasiliano
6. Toa kielezi kuonyesha jinsi kusababu ni jambo muhimu katika uwasiliano?
6 Ili kuwasiliana na watu kwa maneno juu ya habari njema, ni lazima tuwe tayari, si kusema kwa ushupavu, bali kusababu nao. Tunasoma tena na tena kwamba Paulo alisababu pamoja na wale ambao alijaribu kutolea habari njema. (Matendo 17:2, 17; 18:19) Twaweza kufuataje mfano wake? Hali za ulimwengu zenye kuharibika hata zaidi huenda zikawaongoza wengine kushuku kuwako kwa Mungu mweza yote na mwenye upendo anayejali ainabinadamu. Ingawaje, tungeweza kusababu nao kwamba Mungu ana wakati kwa kila jambo. (Mhubiri 3:1-8) Hivyo, Wagalatia 4:4 husema kwamba wakati wa Mungu barabara ulipofika, alituma mwana wake duniani. Hiyo ilikuwa maelfu ya miaka baada ya mara yake ya kwanza kuahidi hilo. Vivyo hivyo, wakati wake barabara ufikapo, atakomesha kuteseka na uovu. Isitoshe, Neno la Mungu linaonyesha kwamba Mungu ana sababu za kushurutisha za kuruhusu kuteseka na uovu kuendelee kwa muda mrefu sana. (Linganisha Kutoka 9:16.) Kusababu kwa njia hiyo, na kutegemeza kusababu huko na vielezi na uthibitisho imara wa Kimaandiko, kutasaidia walio wanyofu kung’amua kwamba kuenea kwa uovu hakuwezi kutumiwa kuwa hoja kwamba Yehova hayuko au hajali.—Warumi 9:14-18.
7, 8. Kusababu kwaweza kutusaidiaje kuwasiliana na Myahudi Mworthodoksi?
7 Tuseme kwamba unapokuwa ukienda nyumba kwa nyumba, mwenye nyumba akuambia: “Mimi ni Myahudi. Mimi sipendezwi.” Ungeweza kuendeleaje? Ndugu mmoja aripoti kufanikiwa kwa kutumia njia hii: ‘Sina shaka utakubaliana nami kwamba Musa alikuwa mmoja wa manabii wakuu zaidi aliyepata kutumiwa na Mungu wakati wowote. Na je, ulijua kwamba alisema kama ilivyorekodiwa kwenye Kumbukumbu la Torati 31:29: “Najua baada ya kufa kwangu mtajiharibu . . . na kukengeuka katika njia niliyowaamuru; nayo mabaya yatawapata”? Musa alikuwa nabii wa kweli, kwa hiyo maneno yake yalipasa yatimie. Je, yawezekana kwamba yalitimia wakati Mungu alipotuma Mesiya kwa Wayahudi na hiyo ndiyo sababu Wayahudi hawakumkubali? Huenda ikawa hivyo. Kwa hiyo ikiwa ndivyo, nao walikosea, je, kuna sababu yoyote ya wewe na mimi kufanya kosa hilo hilo?’
8 Kumbuka, pia, kwamba Wayahudi wameteseka sana mikononi mwa Jumuiya ya Wakristo, hasa muda wa karne hii. Kwa hiyo ungeweza kumwambia mwenye nyumba kwamba sisi hatukushiriki katika hilo. Kwa mfano, waweza kusema hivi: ‘Je, ulijua kwamba wakati Hitla alipokuwa akitawala, Mashahidi wa Yehova walikataa kutii amri yake ya kutengea mbali Wayahudi? Wao walikataa pia kusema “Mwokozi ni Hitla” na kutumikia katika jeshi lake.a
9, 10. Kusababu kwaweza kutumiwaje kumsaidia mtu anayeamini moto wa helo?
9 Katika kujitahidi kuwasiliana na mtu anayeamini moto wa helo, waweza kusababu kwamba ikiwa mtu atateseka milele na milele katika helo, ni lazima awe ana nafsi isiyoweza kufa. Mwamini wa moto wa helo atakubali kwa utayari. Kisha waweza kutaja masimulizi ya uumbaji wa Adamu na Hawa na kumuuliza kwa fadhili ikiwa alipata wakati wowote kuona katika masimulizi hayo mtajo wowote wa nafsi isiyoweza kufa. Ukiendelea na kusababu kwako, waweza kuelekeza fikira zake kwenye Mwanzo 2:7, ambapo Biblia hutuambia kwamba Adamu akawa nafsi. Adamu alipotenda dhambi alihukumiwa kifo. Na angalia yale ambayo Mungu alisema yangekuwa tokeo la dhambi ya Adamu: “Kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Kwa hiyo, Adamu yule nafsi alirudi mavumbini.
10 Ungeweza pia kuelekeza fikira kwenye uhakika wa kwamba hakuna mahali popote katika masimulizi ya Mwanzo ambapo Mungu anataja kuteseka kwa milele katika moto wa helo. Mungu alipomwonya Adamu asile tunda lililokatazwa, alisema hivi: “Siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Hakuna mtajo wowote wa moto wa helo! Ikiwa tokeo la dhambi la Adamu lisingekuwa kifo, ‘kurudi mavumbini,’ bali kuteseka milele, je, kwa kuonyesha haki Mungu asingalipaswa kueleza jambo hilo wazi? Kwa hiyo, kusababu kwa uangalifu na fadhili huenda kukasaidia mtu mnyofu kuona kutokupatana kwa imani yake. Tusikose kuona kamwe umaana wa kutumia kusababu tunaposhiriki na wengine kweli ya Neno la Mungu.—Linganisha 2 Timotheo 2:24-26; 1 Yohana 4:8, 16.
Sifa Zinazohitajiwa kwa Ajili
ya Uwasiliano Wenye Matokeo
11-13. Ni sifa zipi za Kikristo zinazoweza kutusaidia kuwasilisha habari kwa njia yenye matokeo?
11 Sasa, ni sifa zipi tunazopaswa kusitawisha ili kuwasilisha kweli za Ufalme kwa njia yenye matokeo zaidi? Mfano wa Yesu watuambia nini? Kwenye Mathayo 11:28-30, tunasoma maneno yake: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo [hali ya kujishusha katika moyo, NW]; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” Hapo twaona sababu moja kwa nini Yesu alifanikiwa katika kuwasilisha habari. Alikuwa mpole na hali ya kujishusha katika moyo. Wenye mioyo minyofu walimwona kuwa mwenye kuburudisha. Mtume Paulo aliweka mfano mzuri pia, kwa kuwa, kama alivyowaambia wazee kutoka Efeso, tangu siku ya kwanza ya kuja kwao, alikuwa akimtumikia Bwana “kwa unyenyekevu wote.”—Matendo 20:19.
12 Kwa kuonyesha kwetu kiasi na hali ya kujishusha katika akili sikuzote, wengine wataona kwamba sisi pia ni wenye kuburudisha, na itakuwa rahisi zaidi kwetu kuwasiliana nao. Mtazamo mwingine wowote huenda ukaweka kizuizi kati yetu na wale ambao tunajaribu kuwasiliana nao. Kwa kweli, “hekima hukaa na wanyenyekevu [wenye kiasi, NW].”—Mithali 11:2.
13 Ili kutoa habari kwa njia yenye matokeo, tunahitaji pia kuwa wenye subira na busara. Mtume Paulo bila shaka alikuwa mwenye busara alipokuwa akitoa ushahidi kwa wanafalsafa waliokuwa wamekusanyika mbele yake kwenye Kilima cha Mars. Alitoa habari njema katika njia ambayo wangeweza kuelewa. (Matendo 17:18, 22-31) Ikiwa tunataka kuwasiliana na wasikilizaji wetu kwa kufanikiwa, ni lazima tufuate shauri ambalo mtume Paulo aliwapa Wakolosai aliposema hivi: “Acheni mazungumzo yenu yawe yenye neema sikuzote, na si yenye kukosa ladha kamwe; jifunzeni jinsi ya kuongea vizuri iwezekanavyo na kila mtu ambaye mwakuta.” (Wakolosai 4:6, The New English Bible) Usemi wetu wapasa sikuzote kuwa wenye ladha nzuri. Usemi kama huo utaelekea kufungua akili za wasikilizaji wetu, hali maneno yasiyofikiriwa vizuri yatawasababisha kutokuwa wasikivu.
14. Mfikio wenye utulivu, na wa kimaongezi waweza kutusaidiaje kuwasiliana na wengine?
14 Tunataka kuonekana kuwa watulivu nyakati zote. Hilo lasaidia kuwastarehesha wasikilizaji wetu. Kuwa na utulivu kunahusisha kutotaka mno kuwa msema yote. Badala ya hiyo, tukiwa na mwelekeo wa kutofanya haraka, na maswali ya kirafiki, tunawapa wasikilizaji wetu nafasi ya kujieleza. Ni jambo la hekima kumtia moyo mtu yule mwingine aongee hasa tutoapo ushahidi wa kivivi hivi. Kwa mfano, Shahidi mmoja alijipata ameketi karibu na padri wa Katoliki ya Kiroma ndegeni. Kwa zaidi ya muda wa saa moja, Shahidi huyo aliendelea kumuuliza-uliza padre huyo maswali yenye busara, na padre, katika kujibu, alikuwa akiongea sana. Lakini wakati walipoachana, padre alikuwa amechukua vichapo kadhaa vya Biblia. Mfikio kama huo wenye subira utatusaidia kuzoea sifa nyingine inayohitajiwa, yaani hisia-mwenzi.
15, 16. Hisia-mwenzi yaweza kutusaidiaje kuwasilisha habari?
15 Hisia-mwenzi humaanisha kujiweka katika hali ya wengine. Mtume Paulo alithamini sana uhitaji wa hisia-mwenzi, kama inavyoweza kuonwa kutokana na yale aliyoandikia Wakorintho: “Ingawa nimekuwa huru kwa watu wote, nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi. Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria,) ili niwapate walio chini ya sheria. Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si kwamba sina sheria mbele za Mungu, bali mwenye sheria mbele za Kristo), ili niwapate hao wasio na sheria. Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu.”—1 Wakorintho 9:19-22.
16 Ili kumwiga mtume Paulo katika njia hizo, tunahitaji kuwa wenye busara, utambuzi, na wenye kuangalia. Hisia-mwenzi itatusaidia kuwasilisha kweli kwa wasikilizaji wetu kulingana na njia yao ya kufikiri na ya kuhisi. Kichapo Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kinatoa msaada mwingi katika jambo hilo. Uwe nacho hudumani sikuzote.
Upendo—Msaada Katika Uwasiliano
17. Kati ya sifa zote za Kikristo, ni ipi iliyo yenye thamani zaidi katika kuwasilisha kweli kwa njia yenye matokeo, nayo yaonyeshwaje?
17 Kiasi, hali ya kujishusha katika akili, subira, na hisia-mwenzi husaidia katika uwasiliano wenye matokeo. Hata hivyo, zaidi ya yote, upendo usio wa ubinafsi utatusaidia kuwa wenye kufanikiwa katika kufikia mioyo ya wengine. Yesu alionea watu huruma kwa sababu walikuwa “wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” Upendo ndio uliomsukuma Yesu aseme hivi: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.” (Mathayo 9:36; 11:28) Sisi pia tunataka kuburudisha watu na kuwasaidia waje kwenye njia ielekeayo kwenye uhai, kwa sababu tunawapenda. Ujumbe wetu ni wa upendo, kwa hiyo acheni tuendelee kuusema kwa njia ya upendo. Upendo huo wajionyesha kwa tabasa-mu ya kirafiki, kwa fadhili na uanana, kwa furaha na uchangamfu.
18. Twaweza kumwigaje Paulo, kama alivyomwiga Bwana?
18 Katika jambo hilo mtume Paulo alikuwa mwigaji mzuri wa Bwana wake, Yesu Kristo. Ni kwa nini alikuwa mwenye kufanikiwa sana katika kuanzisha kundi moja baada ya jingine? Kwa sababu ya bidii yake? Ndiyo. Lakini pia kwa sababu ya upendo aliouonyesha. Angalia maneno yake yenye shauku kuhusu kundi jipya la Thesalonike: “Tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na roho zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.” Kumwiga Paulo kutatusaidia katika bidii zetu za kuwasilisha habari.—1 Wathesalonike 2:7, 8.
19. Kwa nini tusiache eneo lisilo na matokeo lituvunje moyo?
19 Ikiwa tumefanya vizuri iwezekanavyo katika kuwasilisha habari na twakosa kupata matokeo yanayotakiwa, je! twapaswa kuvunjika moyo? Sivyo hata kidogo. Wanafunzi wa Biblia (kama vile Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakiitwa zamani) walikuwa wakisema kwamba ili watu wakubali kweli, wanahitaji kuwa na sifa tatu. Wanahitaji kuwa wanyofu, wanyenyekevu, na wenye njaa ya kiroho. Hatuwezi kutazamia watu wasio na moyo mweupe, wasio wanyofu, waiitikie kweli vizuri; wala hatuwezi kutazamia watu wenye kiburi au wenye kujivuna kusikiliza habari njema. Zaidi ya hayo, hata kama mtu ni mnyofu na mnyenyekevu kwa kadiri fulani, haielekei kwamba atakubali kweli ikiwa hana njaa ya kiroho.
20. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba jitihada zetu hazijawa za bure?
20 Bila shaka wengi ambao unakuta kwenye eneo lenu watakuwa wakikosa sifa moja au zaidi kati ya zile tatu. Nabii Yeremia alipatwa na jambo hilo hilo. (Yeremia 1:17-19; linganisha Mathayo 5:3.) Bado, bidii zetu si za bure. Kwa nini sivyo? Kwa sababu tunatangaza jina na Ufalme wa Yehova. Kwa kuhubiri kwetu na kwa kuwapo kwetu kwenye eneo tunawaonya waovu. (Ezekieli 33:33) Na usisahau kamwe kwamba kwa jitihada zetu za kuwasilisha kweli kwa wengine, tunajinufaisha wenyewe. (1 Timotheo 4:16) Tunaendeleza imani yetu ikiwa imara na tumaini letu la Ufalme likiwa jangavu. Isitoshe, tunadumisha ukamilifu wetu na hivyo tunashiriki katika kutakasa jina la Yehova Mungu, tukifanya moyo wake utereme.—Mithali 27:11.
21. Twaweza kusema nini kwa muhtasari?
21 Kujumlisha yote: Uwasiliano ni kupasha habari kwa njia yenye matokeo. Ustadi katika uwasiliano ni muhimu, na madhara mengi hutokea wakati uwasiliano unapoharibika. Tumeona kwamba Yehova Mungu na Yesu Kristo ni wawasilianaji mashuhuri na kwamba Yesu Kristo alipanga njia ya uwasiliano kwa siku yetu. Tumeona pia kwamba kwa kujipamba kwetu na mwenendo wetu, tunawasiliana, tukipelekea wengine ujumbe mbalimbali. Tumejifunza kwamba kusababu kuna sehemu yenye umaana katika kujaribu kwetu kuwasiliana na watu na kwamba ili kuwasilisha habari kwa njia yenye matokeo, tunahitaji kuwa wenye kiasi na wanyenyekevu, wenye kuonyesha hisia-mwenzi, wenye kuzoea subira, na, zaidi ya yote, wenye kusukumwa na moyo uliojaa upendo. Tukisitawisha sifa hizo na kufuata mifano ya Biblia, tutakuwa wawasilianaji Wakristo wenye kufanikiwa.—Warumi 12:8-11.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa madokezo zaidi juu ya jinsi ya kuwasiliana na Wayahudi na wengine, ona Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, kurasa 21-24.
Ungejibuje?
◻ Uwasiliano huanzaje kabla neno lolote halijasemwa?
◻ Ni baadhi ya mifano gani ya kuwasiliana kwa kutumia kusababu kwenye matokeo?
◻ Ni sifa zipi zilizowezesha Yesu Kristo na Paulo kuwasilisha habari kwa njia yenye matokeo?
◻ Kwa nini tusivunjike moyo ikiwa matokeo yanakuja polepole?