Uhusiano Mwema Unaongoza Kwenye Kupashana Habari Kwema
“Nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na [nafsi] zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.”—1 The. 2:8.
1. Ni ulizo gani linalokabili mume na mke, nasi twatafuta jibu la kutegemeka wapi?
KAMA MUME NA MKE, je! ninyi kama watu waliooana mwaweza kupashana habari kabisa na kwa hiari? Imewapasa mfanye hivyo. Au mnaona kuna makosa fulani, au vizuizi, vikileta hata ukatili nyakati nyingine? Hadithi ya kupashana habari, namna kulivyoanzishwa na kusimamishwa juu ya msingi mzuri, inapendeza sana sana. Hatuangalii hadithi za uongo au mapokeo tupate uongozi juu ya habari hii, bali twaliangalia Neno la Mungu, chanzo cha pekee chenye habari za kutegemeka.
2. Maana yake nini kupashana habari, ikiongoza kwenye mkataa gani?
2 Kwanza, huenda ukauliza, maana yake nini kupashana habari? Maana yake ni kutoleana habari. Matokeo ni kushiriki jambo fulani wote pamoja. Hii inaweza kuhusu akili tu, kutia maarifa na ufahamu, lakini kati ya mume na mke yaweza na imepaswa ihusu mioyo yenu, mawazo yenu ya ndani na tamaa, kupendezwa kwenu kwa mmoja na mwenzake. Njia iliyo nyepesi na ya moja kwa moja ya kufanya hivi ni kwa kuzungumza. Kuzungumza pamoja. Yaani, ushirika unawekwa kati yenu, kufahamiana au kukutana kwa akili. Zaidi ya yanayosemwa, iko njia ya kuyasema. Hata kutazamana kwaweza kutoa maana na wazo la ndani, kama mnavyokumbuka bila shaka kutokana na siku za kwanza mlipokuwa mkichumbiana. Je! sivyo ilivyo? Je! huoni kutokana na hili kuwa ni kweli kwamba jambo la kwanza la lazima kwa kupashana habari kwema ni uhusiano mwema kati yenu?
3. (a) Biblia ni njia ya kupashana habari namna gani? (b) Katika habari hii, twajifunza nini kutokana na Mathayo 15:1-9?
3 Walakini, njia nyingine ya kupashana habari ni kutumia yaliyoandikwa, kama, inavyoonyeshwa wazi na unayoyasoma sasa. Yaliyoandikwa yanakupasha habari fulani. Bila shaka, mfano ulio bora ni Biblia Takatifu. Ni kweli, wengi leo, katika Kristendomu, hawakubali Biblia ilibuniwa kwa njia ya kimungu, ijapokuwa ingali ikitumiwa katika ibada zao makanisani. Hiyo isikushangaze wala kukuvunja moyo. Hali hii inalingana na ilivyokuwa siku za Yesu. Mafarisayo na waandishi walidai kwa nguvu kuiunga mkono Torati, lakini wao hasa walikuwa ndio wenye kushikilia sana mapokeo ya baba zao kama Yesu alivyoonyesha, hiyo ikiwafanya ‘waihalifu amri ya Mungu.’ Je! kosa lilikuwa upande wa Neno lililoandikwa la Mungu, Maandiko ya Kiebrania? Sivyo. Bali, wao walishindwa katika jambo la kwanza lililo la lazima, uhusiano mwema wa uaminifu kwa Yehova. Ni kama vile Yesu alivyosema juu yao, akiutaja unabii wa Isaya: “Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.”—Mt. 15:1-9.
4. Twawezaje kuwa wenye mioyo myepesi na kusikia vema, na kwa matokeo gani?
4 Kama vile viongozi wa kidini wa leo wa Kristendomu walio na Biblia yote, watu hao walijua sana vile Neno lililoandikwa lilivyosema, lakini wao walikuwa vipofu na viziwi wasiweze kuona na kuusikia ujumbe na roho liliyokusudiwa litoe. Walakini, wengine walikuwa tofauti wakati huo, nawe waweza kuwa kati ya hao walio tofauti leo. Kama vile Yesu alivyosema kwa wanafunzi wake wakati fulani mapema: “Ninyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa. . . . Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vema, na macho yao wameyafumba; wasije wakaona kwa macho yao, wakasikia kwa masikio yao, wakaelewa kwa mioyo yao, wakaongoka, nikawaponya. Lakini, heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia.”—Mt. 13:11-16.
5. Lilikuwa jambo gani la kutokeza juu ya kuumbwa kwa mwanadamu kukilinganishwa na matendo mengine ya kuumba kwa kidunia?
5 Tukikuhesabu wewe kati ya watu wenye furaha walio tofauti, ebu na tuichunguze tena hadithi ya kupashana habari na kuona namna ilivyoanzishwa, na tunayoweza kujifunza kwayo. Katika habari ya Mwanzo juu ya uumbaji, sura ya kwanza, twaona kwamba kila siku, kufikia siku ya sita, tendo linajulishwa kwa kiarifa cha Kiebrania kinachomaanisha kwamba jambo limepaswa litokee. Ndiyo, Mungu alikuwa akitoa habari juu ya maagizo yake, lakini hakuna anayetajwa kama akiitikia. Walakini, wakati unapofika wa kufanyiza viumbe vya kidunia, twaona badiliko kubwa tunaposoma: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu.” Ijapokuwa Muumba alikuwa na cheo cha kutoa amri kana kwamba kwa msaidizi, sasa alikuwa akiruhusu ushirikiano. Sauti ya kirafiki na upole yaonyeshwa; uhusiano mwema, urafiki wenye furaha. Ndivyo ipaswavyo kuwa kati ya wenzi waliooana. Ikiwa wewe u mume, je! hivyo ndivyo unavyosema na mkeo, ukisema hivi: “Haya, na tu-. . . ”?—Mwa. 1:3, 6, 9, 14, 20, 24, 26.
6. Katika habari hii, ni uongozi gani unaotolewa kwa wazee kundini?
6 Ingawa sasa twazungumza hasa juu ya uhusiano wa ndoa, kanuni ii hii yatumika kwa uhusiano mwingine, kutia na ule ulio kati yenu mlio wazee au waangalizi na wengine katika makundi ya mashahidi wa Yehova. Ijapokuwa ninyi kama wazee mna daraka la pekee, lenye mamlaka ya kadiri fulani, nia kuu na njia ya kupashana habari imepaswa iwe ya kuruhusu ushirikiano, kuliko kutoa maagizo. Mnaposaidia mtu mwenye tatizo, kama lile liwezalo kupatikana wakati wa kutoa ushuhuda katika maeneo fulani, badala ya kusema tu linalopaswa kufanywa, ni afadhali sana kusema hivi: “Acha twende tukalitatue tatizo hili pamoja.” Roho ya uchangamfu yenye uaminifu usio wa kichoyo wenye upendo imepaswa ionyeshwe, si katika tunayoyasema tu, bali pia kwa namna ya sauti yetu na tendo. Angalia hii inavyosemwa kwa wazi na kwa uzuri na mtume Paulo akiliandikia kundi la Thesalonike: “Nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na [nafsi] zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.” Lo! ni mfano mwema namna gani wa uhusiano mwema unaoongoza kwenye kupashana habari kwema kwa neno na tendo pia!—1 The. 2:8.
MFANO MWEMA SANA WA KUPASHANA HABARI KWEMA
7. Yohana anamjulishaje yeye ambaye Mungu alisema naye kama ilivyoandikwa katika Mwanzo 1:26?
7 Tukiirudia hadithi yetu, je! twamjua yeye ambaye Yehova alikuwa akipashana habari naye wakati wa kuumbwa kwa mwanadamu? Jibu litatusaidia tuuone uzito wa maana ya kuumbwa kwa mwanadamu kwa mfano na sura ya Mungu. Yohana anamjulisha kama “Neno” anapoianza habari yake ya Injili juu ya Yesu, aliyekuwako “mwanzoni pamoja na Mungu. Vitu vyote vilipata kuwako kupitia kwake,” kutia na mwanadamu. Halafu, Yohana anasema hivi: “Neno akawa mwili . . . nasi tuliuona utukufu wake . . . alijaa fadhili zisizostahili na kweli,” na kwamba yeye, akiwa “mahali pa kifua pamoja na Baba ndiye ambaye amemweleza.” Kwa kweli masimulizi haya yanayopendeza ya Yesu yanaonyesha roho ifaayo hasa ya uhusiano mwema na kupashana habari kwa hiari.—Yohana 1:1-3, 14, 18, NW; tazama pia Mithali 8:22, 30, 31.
8. Ni nini maana ya cheo “Neno,” nalo hili latumikaje kwa Kristo Yesu?
8 Hii yaonekana zaidi katika maana ya cheo “Neno.” Kina maana ya mpelekaji wa ujumbe au mnenaji, kama vile yule afisa katika nyakati za zamani aliyesimama mbele ya dirisha lenye pazia na kuwaeleza wengine ujumbe wa mfalme asiyeonekana aliye ndani, kwa kupaza sauti. Afisa huyo alikuwa na cheo cha Kal Hatze yaani “sauti au neno la mfalme.” Kwa habari ya Mwana wa Mungu, yeye ndiye aliyekuwa Kinywa au Mnenaji wa Baba yake, Yehova. Yeye ndiye aliyeaminika kwa kuwapasha wengine habari zo zote ambazo Muumba alitaka kuzitoa. Alitumikia kwa uaminifu namna ile ile wakati wa huduma yake ya kidunia. Wakati mmoja alisema hivi: “Mimi sikunena kwa nafsi yangu tu; bali Baba aliyenipeleka, yeye mwenyewe ameniagiza nitakayonena na nitakayosema. . . . Basi hayo ninenayo mimi, kama Baba alivyoniambia, ndivyo ninenavyo.” Anasema na kutenda kwa njia ile ile anapoyaongoza majeshi ya kimbinguni kufikiliza hukumu za Mungu za haki katika pigano la Har–Magedoni, akiitwa “Neno la Mungu.”—Yohana 12:49, 50; 14:10; Ufu. 19:13.
9. Ni mfano gani mwema tuliowekewa katika Mwanzo 1:26, na je! ingali yawezekana kuufuata?
9 Tukiyakumbuka mambo haya, imetupasa tupendezwe namna gani kuwazia kwamba mwanadamu aliumbwa katika mfano na sura ya Muumba mkuu na Mwanawe mpendwa! Uhakika wa kwamba twaweza kulithamini hili na kuzungumza mmoja na mwenzake juu yake waonyesha kwamba hii ni kweli. Zaidi ya hayo, kwa fadhili Yehova ametupa mfano wa uhusiano mwema na kupashana habari katika Neno lake lililoandikwa, na hata baada ya miaka elfu sita ya kuwako kwa dhambi na kutokamilika, ingali yawezekana kuufuata mfano huo. Mamia ya maelfu ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanajaribu kufanya hivyo, kwa msaada wa kimungu. Je! ninyi mume na mke, mnajaribu kufanya hivyo?
10. Ni kwa njia gani na kwa sababu gani wale wanaotegemea hekima ya kibinadamu wanashindwa kushughulika na magumu ya ndoa inavyofaa?
10 Ebu na tuuchunguze mfano huu kwa makini zaidi na kuyaona mambo ya lazima yapaswayo kuigwa, pia mambo yapaswayo kuepukwa na, ikiwa lazima, kufutiliwa mbali. Kwa kweli, hii ndiyo njia ya pekee yenye matokeo mema ya kuyatatua na kuyashinda matatizo yanayokabiliwa, hasa katika uhusiano wa ndoa. Ni kweli, ziko shule mbalimbali za mawazo yanayotolewa na matengenezo ya kijamii zinazoshughulikia matatizo hayo na kuwa na nia ya kutoa mashauri juu ya namna ya kutenda. Bila ya kutua tutilie shaka sababu zake, lazima isemwe kwamba kwa vyo vyote jitihada zao zinaonyesha hekima ya kibinadamu kwa habari ya kushughulika na akili za wanadamu. Kwa sababu hiyo, wanasema kwamba ndoa ni uhusiano wa kibinadamu nayo yapaswa ionwe hivyo. Wao wanashindwa na kukataa kumpa Muumba cheo chake kifaacho kama Mwanzilishi wa uhusiano huu, au kama Mbuni mwenyewe wa Biblia Takatifu, pamoja na mashauri na maagizo yake juu ya kila uhusiano wa kibinadamu. Nani aliyepata kusikia daktari wa akili akimwelekeza mgonjwa au rafiki yake kwenye Maandiko Matakatifu kama njia ya pekee ya uongozi? Kwa habari hiyo, ni mapadre au viongozi wa kidini wangapi ambao wangeshauri kufuata mwendo huo kwa ye yote wa kundi lao katika kushughulika na matatizo hayo?
11. (a) Ni wazi namna gani kwamba mwanadamu hakutokea kwa mageuzi? (b) Ni nini linaloonyeshwa wazi na maneno ya kwanza ya Adamu yaliyoandikwa katika Mwanzo 2:23?
11 Hata hivyo, sisi tutajiepusha na hekima ya kilimwengu na kukiendea Kitabu kilichotolewa na Mganga Mkuu, tukiutafuta msaada wake kwa matumaini kabisa, “pasipo shaka yo yote.” (Yak. 1:6) Tunapoendelea kusoma kuanzia Mwanzo 1:26, ni wazi kama nini kwamba mwanadamu hakutokea kwa mageuzi, kama wanavyofundisha wenye hekima wa kilimwengu. Ni nini lililotukia wakati “ule ubavu alioutwaa katika Adamu [Yehova] Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa Adamu”? Mwanamume hakuduwaa. Hakumpokea vivi hivi tu bila kushangilia. Bali, alipaza sauti akitoa maoni yake kwa zawadi hii iliyo nzuri ajabu, msaidizi huyu aliye bora sana. Badala ya kusimama hapo tu, akimtazama, inaelekea sana kutokana na yale aliyoyasema kwamba alimshika karibu karibu alipokuwa akiyasema maneno hayo yenye maana nyingi sana na mawazo ya ndani:
“Mwishowe huu ni mfupa wa mifupa yangu
Na nyama ya nyama yangu.
Huyu ataitwa Mwanamke,
Kwa maana kwa mwanamume huyu alitwaliwa.”
Lo! hilo lilikuwa shairi hasa, la kweli katika namna na kiasi cha maneno kila neno likifuatana vizuri na jingine, mawazo yakiendelea kuonyeshwa na usawa kamili. Bila shaka hii ingeweza kuonekana zaidi katika lugha ya kwanza. Mwanadamu aliumbwa kweli kwa mfano wa Mungu, akiwa na uwezo mzuri wa kupashana habari.—Mwa. 2:22, 23, NW.
12. Neno la Mungu linamaliziaje kwa njia ya kuvuta?
12 Hivyo katika kurasa zake za kwanza Neno la Mungu linasimulia habari ya kupendeza na yenye kutia moyo ya maongezi kati ya watu, mbinguni na duniani pia. Kwa kupendeza, Neno la Mungu linamalizia pia, si kwa upeo wenye kujulikana pote, bali kwa mazungumzo ya kipekee na ya kirafiki kati ya watu wawili ambao kwa wazi walifurahia uhusiano wenye furaha. “Yeye [Kristo Yesu] mwenye kuyashuhudia haya asema, Naam; naja upesi.” Halafu twamsikia mzee mpendwa Yohana akiitikia kwa shauku, kwa macho yenye kung’aa: “Amina; na uje, Bwana Yesu.” Ndiyo, akija upesi iwezekanavyo ndiyo afadhali zaidi. Hiyo ndiyo maana yake.—Ufu. 22:20.
KUSHINDA KIZUIZI
13. Njia na hali ya kupashana habari iligeuzwaje na kosa la mwanadamu?
13 Wakati uhusiano mwema ulipoendelezwa na Adamu na mkewe kwa Muumba wao na kati yao wenyewe, hakukuwa na tatizo lo lote. Lakini mara tu uhusiano huo ulipozuiwa na kosa la makusudi, kizuizi kilitokezwa mara hiyo cha kupashana habari. “Adamu na mkewe wakajificha kati ya miti ya bustani, [Yehova] Mungu asiwaone” walipoisikia sauti yake bustanini, kwa maana, kama vile Adamu alivyosema, “nikaogopa.” Wao hawakuweza kumtazama Mungu wao nao waliogopa mambo ambayo angewaambia. Hali ya kupashana habari kati ya mwanamume na mkewe isingaliweza kuwa ya uchangamfu sana. Ijapokuwa maelezo mengi hayatolewi, hii yaonyeshwa na kutoa udhuru kwa Adamu mwenyewe akimwambia Yehova: “Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala.” Halafu, Hawa aliambiwa hivi: “Tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala.” Kama tutakavyozungumza baadaye, neno ‘kutawala’ kwa kweli laonyesha mojawapo ya sababu kubwa za matatizo yanayohusu kupashana habari, hasa ikiwa ni kwa upande wa mke.—Mwa. 3:8-16.
14. (a) Maana yake nini kutembea pamoja na Mungu? (b) Usemi “kwa imani,” katika Waebrania, sura ya 11, unaonyesha nini?
14 Je! maana yake ni kwamba hali hiyo ilikuwa isiyo na tumaini kwetu, tumaini la kulishinda tatizo? Kuna usemi unaotumiwa katika Mwanzo juu ya watu fulani unaoonyesha vingine. Yasemekana kwamba Henoko na Nuhu waliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli, si mara moja tu, bali maisha yao yote. Bila shaka ndivyo ilivyokuwa na kwa Habili. (Mwa. 5:22-24; 6:9) Watu wawili wakiendelea kutembea pamoja, lazima uwepo uhusiano ulioimarishwa sana na hiari ya kupashana habari. Hii yaonyeshwa pia na usemi mwingine unaotumiwa juu ya watu watatu hawa, pia juu ya wengine wengi. Akianza na Habili, Paulo asema juu ya wale wanaotajwa katika Waebrania, sura ya 11, kwamba “kwa imani” waliuonyesha uaminifu wao kwa Mungu, wakiamini kwamba yeye “huwapa thawabu wale wamtafutao.” Sifa hizi ni sehemu ya lazima ya mfano wa kuigwa.—Ebr. 11:4-6.
15. Kwa sababu gani Yehova alikiondoa kizuizi kilichosababishwa na dhambi, nasi tuitikieje?
15 Kwa rehema na fadhili zake za upendo Yehova ndiye aliyewezesha kizuizi hicho kishindwe, “kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” Walakini, kwa upande wetu yapaswa iwepo nia ifaayo ya moyoni, au walau nia ya kufundishwa maoni yafaayo, kwa maana “fadhili za [Yehova] zina wamchao . . . na kuyakumbuka maagizo yake ili wayafanye.” (Zab. 103:10-14, 17, 18) Ukaidi au kupiga ubwana hakupaswi kuwapo. Kwa upande ufaao, tukiendelea kuwatazama wale wanaotajwa na Paulo, twaona wawili, Ibrahimu na Musa, ambao kwao twaweza kujifunza mengi kwa kuuchunguza mfano tunaotaka kuufuata.
16. (a) Ni jambo gani linalostahili kuangaliwa juu ya uhusiano? (b) Ibrahimu aliionyeshaje imani yake na uaminifu, ikitokeza nini?
16 Ni vigumu kwa uhusiano kusimama mahali pamoja tu. Ama unasitawi au unapungua. Tena, ukuzi wake ama ni wenye afya au si wenye afya. Hili ni jambo la kuangaliwa, hasa wakati watu wanapoishi karibu karibu pamoja kama mume na mke. Huenda kwanza kuaminiana na kutumainiana kukawapo, lakini haiwezi kusemwa kwamba mambo yataendelea kuwa hivyo tu. Iweni tayari, hata katika mambo madogo, kuzionyesha sifa njema hizo. Ibrahimu alifanya hivi maisha yake yote, kama maandishi yaonyeshavyo, kuanzia Mwanzo, sura ya 12. Paulo anataja matukio matatu makuu ambapo Ibrahimu aliionyesha imani yake yenye nguvu na uaminifu kwa Yehova, kwa kuwa tayari kutii: (1) Kuondoka kwake katika mji na nchi yake alipoitwa, na (2) kuishi kwake miaka mingi “ugenini,” na hasa (3) ‘kutoa kwake Isaka awe dhabihu? (Ebr. 11:8-10, 17-19) Angalia yaliyotangulia yanavyoungwa mkono na Yakobo anaposema hivi akilitaja tukio hili la kwanza: “Waona kwamba imani ilitenda kazi pamoja na matendo yake, na ya kwamba imani ile ilikamilishwa kwa njia ya matendo yale. Maandiko yale yakatimizwa yaliyonena, Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa ni haki; naye aliitwa rafiki wa Mungu.” Lo! ni ukuzi wenye afya namna gani kuelekea kwenye uhusiano mwema! Ni mwisho wenye kusisimua namna gani! Ibrahimu alikuwa na imani kuu katika Yehova, naye Yehova alikuwa na matumaini yenye nguvu katika, rafiki yake.—Yak. 2:21-23; Mwa. 18:19; Rum. 4:16-22; Gal. 3:7-9.
17. (a) Ni kielelezo gani Yesu alichowawekea wafuasi wake? (b) Urafiki unafuatana na nini, nayo hii ilionekanaje katika habari ya Ibrahimu?
17 Yesu alizungumza juu ya kielelezo cha urafiki wa kweli kuhusiana na kupashana habari kwema. Unyenyekevu pamoja na hiari ya kutumikia, ni sehemu ya maana ya kielelezo hicho. Baada ya kuiosha miguu ya wanafunzi wake ule usiku wa mwisho akiwa pamoja nao, alisema hivi: “Ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi. Kwa kuwa nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo.” Baadaye usiku uo huo, aliwaambia hivi: “Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo. Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.” (Yohana 13:14, 15; 15:14, 15; Flp. 2:3) Yeye aliwatumaini wala hakuwaficha lo lote. Vivyo hivyo, kama vile kwa rafiki, Yehova alizungumza na Ibrahimu mara nyingi, na wakati mmoja kwa muda mrefu kwa njia ya usiri, alipokuwa akimruhusu Ibrahimu asihiane naye kwa habari ya Sodoma na Gomora, kama ilivyoandikwa katika Mwanzo, sura ya 18. Mkewe Ibrahimu, Sara, anaingizwa katika habari sasa. Yeye alikuwa tayari kutumikia. Alionyesha imani. Alionyesha heshima kuu. Naye Petro asema ninyi wake mwaweza kuwa “watoto wake, mfanyapo mema, wala hamkutishwa kwa hofu yo yote.”—1 Pet. 3:5, 6; Mwa. 18:6; Ebr. 11:11.
18. Ni jambo gani lililokuwa la kutokeza katika habari ya Musa, likiongoza kwenye kupashana gani kwa habari kwa pekee?
18 Ibrahimu alikuwa na uhusiano wa karibu kama “rafiki wa Mungu,” lakini Musa alikuwa na njia ya pekee ya kupashana habari. Alipokuwa akikaripia Miriamu na Haruni kwa kumlaumu Musa, Yehova alisema hivi: “Akiwapo nabii kati yenu, mimi, [Yehova], nitajifunua kwake katika maono, nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote; kwake nitanena mdomo kwa mdomo, maana, waziwazi wala si kwa mafumbo; na umbo la [Yehova] yeye ataliona.” (Yak. 2:23; Hes. 12:6-8) Miaka mingi mapema, wakati yanaposimulia namna Yehova alivyoitumia hema ya Musa, ‘iliyokitwa mbali na marago,’ kama “Hema ya kukutania,” maandishi yanasema kwamba “watu wote wakaiona nguvu ya wingu ikisimama penye mlango wa hema . . . Naye [Yehova] akasema na Musa uso kwa uso, kama vile mtu asemavyo na rafiki yake.” Hii iliongoza kwenye kupashana huko kwa habari kuliko kuzuri sana wakati, katika kumjibu Musa ombi lake, ‘Yehova alipopita mbele’ yake, akatangaza, Yehova, Yehova, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.’—Kut. 33:7-11, 17-20; 34:6, 7.
19. Ni sababu gani ziwezazo kutolewa za hali ya pekee ya Musa?
19 Kwa kweli Musa alikuwa wa pekee kufurahia njia hiyo ya karibu karibu ya kupashana habari na Yehova. Sababu yake? Kwanza kwa sababu ya kuhitajiwa sana kama kiongozi wa watu wenye shingo ngumu sana na wenye ‘kujielekeza kwa mabaya,’ na pia kwa sababu yeye kwa upande wake mwenyewe aliendeleza uaminifu usiogeuka-geuka kwa Yehova. (Kut. 32:9, 22, 25-29) Sifa nyingine yatajwa. “Basi huyo mtu, huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” Katika hili pia alikuwa wa pekee, kama vile neno hili la mwisho linavyosema juu yake: “Wala hajainuka tena katika Israeli nabii kama Musa, ambaye [Yehova] alimjua uso kwa uso.”—Hes. 12:3; Kum. 34:10.
MUHTASARI
20, 21. (a) Twajifunza nini kutokana na kielelezo cha kimbinguni cha uhusiano na kupashana habari? (b) Twajifunza nini pia kutokana na kielelezo cha kidunia?
20 Kwa hiyo twaweza kuwa na muhtasari gani? Ni nini linalofanyiza uhusiano mwema, ukiongoza kwenye kupashana habari kwema? Tukiyachunguza Maandiko yaliyoongozwa kwa roho, kwanza uko mfano wa Yehova na Mwanawe. Tangu mwanzo, walipendezwa kwa kweli na mtu na mwenzake. “[Yehova] alikuwa nami katika mwanzo wa njia yake . . . nikawa furaha yake kila siku; nikifurahi daima mbele zake.” Ajapokuwa mkuu zaidi, Yehova alimruhusu Mwanawe ashirikiane naye. Kwa upande wake, Mwana alikuwa mwenye heshima nyingi na mtiifu sikuzote. Ulikuwako umoja mwingi sana na matumaini kati yao. Walikuwa na urafiki kamili kati ya mmoja na mwenzake.—Mit. 8:22, 30; Mwa. 1:26; Yohana 11:42; 14:10, 11.
21 Tunapokitazama kielelezo cha kidunia katika Neno la Mungu, twaona nini? Ijapokuwa mwenzi wako ni asiyekamilika kama wewe, jifunze namna ya kuthaminiana kwa njia ya busara, si siku za kwanza tu, bali hata miaka ya uzeeni. Epuka nia ya kupiga ubwana kwa sababu ya kiburi na choyo, si kutaka kufuata yako mwenyewe wala kumtazamia mwenzi wako afuate njia zako hata katika mambo madogo madogo yasiyo na maana sana. Bali, jifunze namna ya kutembea pamoja na kuzungumza pamoja, mkiwa tayari kupatanisha hatua zenu na nia. Sitawisheni na kuendeleza kuaminiana na kutumainiana. Kuoneana shuku ndiye adui aliye mbaya zaidi wa kupashana habari kwa hiari. Iweni macho msitawishe na kukitia nguvu kifungo cha urafiki wa kweli. Jizoezeni na kuonyeshana “shauku” pamoja na rehema na upole.—Flp. 1:8; 1 The. 2:8; Yak. 5:11.
22. Ni ulizo gani zaidi linalostahili kuangaliwa nasi?
22 Ijapokuwa wenzi wanajitahidi wayafanye mambo haya kwa unyofu wote, matatizo yaweza kutokea kwa vyepesi, wenzi wote wawili wawe ni Wakristo wa kweli au sivyo. Mwendo wa uaminifu wawezaje kuendelezwa, hasa katika jamaa iliyogawanyika? Katika makala ifuatayo tutaliona jibu la ulizo hili.
[Picha katika ukurasa wa 512]
Mnenaji au “Kal Hatze” wa mfalme wa Ethiopia