Kufasiriwa kwa Biblia Huathiriwa na Nani?
UFAFANUZI mmoja wa neno “fasiri” ni “kufahamu jambo kulingana na itikadi, maoni, au hali ya mtu binafsi.” (Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary) Hivyo, kwa kawaida malezi na elimu ya mtu huathiri jinsi anavyofasiri jambo lolote.
Namna gani kufasiriwa kwa Biblia? Je, tuko huru kueleza vifungu vya Biblia kulingana na “itikadi, maoni, au hali” zetu? Kwa kawaida, wasomi na watafsiri wengi wa Biblia hudai kuwa hawafanyi hivyo bali wao huongozwa na Mungu.
Mfano mmoja ni yale ambayo yamesemwa katika kielezi-chini cha Yohana 1:1 katika kichapo A New Version of the Four Gospels, kilichochapishwa na John Lingard mwaka wa 1836 na kupachikwa jina “Mkatoliki.” Chasema hivi: “Watu wa dini mbalimbali huamini kuwa maoni yao ya pekee huthibitishwa na Maandiko Matakatifu: kwa kuwa, bila shaka, si Maandiko ambayo huwajulisha, bali wao huyafasiri kulingana na maoni yao wenyewe.”
Ingawa hoja hiyo ni kweli, mwandishi huyo alikuwa na nia gani? Alitoa maelezo yake kuunga mkono fasiri yake ya mstari huo, ambao aliutafsiri hivi: “Hapo mwanzo kulikuwako ‘neno;’ naye ‘neno’ alikuwa pamoja na Mungu; naye ‘neno’ alikuwa Mungu,” mfano halisi wa tafsiri inayounga mkono Utatu.
Ni nini kilichomsukuma mwandishi huyo atafsiri Yohana 1:1 kwa kuunga mkono fundisho la Utatu? Je, ni ‘Maandiko ambayo humjulisha’ afanye hivyo? Hilo haliwezekani kwa kuwa fundisho la Utatu halipatikani popote katika Biblia. Ona yale kichapo The New Encyclopædia Britannica kinayosema kuhusu hilo: “Wala neno Utatu wala fundisho dhahiri kuuhusu halipatikani katika Agano Jipya.” Kwa kuongezea, profesa wa Chuo Kikuu cha Yale, E. Washburn Hopkins alisema: “Yaonekana Yesu na Paulo hawakujua fundisho hilo la utatu; . . . hawasemi lolote kuuhusu.”
Basi, twaweza kufikia mkataa gani kuhusu wale wanaounga mkono fasiri ya Utatu ya Yohana 1:1 au mstari mwingine wowote wa Biblia? Kulingana na kanuni ya Bw. Lingard mwenyewe, “siyo Maandiko ambayo huwajulisha, lakini wao huyafasiri kulingana na maoni yao wenyewe.”
Kwa uzuri, sisi tuna Neno la Mungu mwenyewe kutuongoza. “Mwajua hili kwanza,” akasema mtume Petro, “kwamba hakuna unabii wa Andiko uchipukao kutokana na fasiri yoyote ya faragha. Kwa maana unabii haukuletwa wakati wowote kamwe kwa mapenzi ya binadamu, bali wanadamu walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.”—2 Petro 1:20, 21.