Kujifunza Njia Ipitayo Zote ya Upendo
Kosovo, Lebanoni, na Ireland. Hizo ni sehemu ambazo zimetajwa mara nyingi kwenye habari katika miaka ya karibuni. Zinawakumbusha watu umwagikaji wa damu, mashambulizi ya mabomu, na uuaji. Bila shaka, mapambano yenye jeuri yanayosababishwa na tofauti za kidini, za kijamii, za kikabila, au tofauti nyinginezo si mapya. Kwa kweli, historia imejaa mambo hayo, nayo yamewaletea wanadamu mateseko mengi sana.
KWA KUWA kumekuwa na vita katika historia yote, wengi wamefikia mkataa wa kwamba vita haviwezi kuepukika na kwamba ni kawaida kwa wanadamu kuchukiana. Lakini, maoni hayo ni tofauti kabisa na mafundisho ya Neno la Mungu, Biblia. Maandiko hutangaza waziwazi hivi: “Yeye ambaye hapendi hajaja kujua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Ni wazi kwamba Muumba hutaka wanadamu wapendane.
Biblia pia hufunua kwamba mwanadamu aliumbwa kwa mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:26, 27) Hilo lamaanisha kwamba mwanadamu alipewa uwezo wa kudhihirisha sifa za Mungu, upendo ukiwa ndio sifa kuu zaidi. Kwa kuwa hali iko hivyo, kwa nini wanadamu wameshindwa kabisa kupendana katika historia yote? Kwa mara nyingine, Biblia inatoa ufahamu wenye kina. Ni kwa sababu wenzi wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, walimwasi Mungu wakafanya dhambi. Tokeo likawa kwamba wazao wao wote walirithi dhambi na kutokamilika. Andiko la Waroma 3:23 lafafanua: “Wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” Uwezo tuliopewa na Mungu wa kupenda umeathiriwa na dhambi na kutokamilika tulikorithi. Je, hilo lamaanisha kwamba wanadamu hawawezi tena kupendana? Kuna tumaini gani kwamba tutapata kufurahia uhusiano wenye amani na upendo pamoja na wanadamu wenzetu?
Lazima Tujifunze Kumpenda Mungu
Yehova Mungu ajua kwamba licha ya kutokamilika kwetu, mwanadamu bado anaweza kuonyesha upendo. Hiyo ndiyo sababu yeye awataka wote wanaotaka kumpendeza waonyeshe upendo kadiri wawezavyo. Takwa hilo lilifafanuliwa wazi na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alipoulizwa ataje amri kubwa zaidi katika Sheria waliyopewa Waisraeli. Yeye alisema: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri kubwa zaidi sana na ya kwanza.” Kisha akaongezea: “Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Juu ya amri mbili hizi Sheria yote yaning’inia.”—Mathayo 22:37-40.
Hata hivyo, watu wengi huona ni vigumu sana kupenda mtu wasiyeweza kumwona, na kwa kuwa Yehova Mungu ni Roho sisi wanadamu hatuwezi kumwona. (Yohana 4:24) Lakini, sisi huathiriwa kila siku na mambo ambayo Mungu hufanya, kwa vile sote hutegemea vitu vingi vizuri alivyoumba kwa manufaa yetu. Mtume Paulo alionyesha uhakika huo aliposema: “[Mungu] hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa nyinyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.”—Matendo 14:17.
Hata ingawa kwa njia moja au nyingine kila mtu hunufaika na maandalizi ya Muumba, ni watu wachache kwa kulinganisha wanaosukumwa kumshukuru. Hivyo, twahitaji kupitia mambo yote mazuri ambayo Mungu ametufanyia na kutafakari juu ya sifa nzuri sana ambazo hudhihirika katika matendo yake yote. Kufanya hivyo kwapaswa kutusaidia tufahamu hekima yenye kutia kicho na pia nguvu za Muumba wetu Mtukufu. (Isaya 45:18) Zaidi ya yote, kwapaswa kutusaidia tufahamu jinsi yeye alivyo Mungu mwenye upendo, kwa kuwa alitupa sisi uhai na pia akatuwezesha kufurahia sana kuishi.
Kwa mfano, fikiria maua mazuri ya aina nyingi ambayo Mungu aliumba duniani. Inapendeza kama nini kwamba alituwezesha pia kuona na kufurahishwa sana na vitu hivyo maridadi! Vivyo hivyo, Mungu alituandalia vyakula vya aina zote vyenye lishe ili tuendelee kuishi. Ni ufikirio ulioje kwamba alituumba pia tukiwa na uwezo wa kuonja ili tuweze kufurahia kula! Je, huo si uthibitisho wa wazi kwamba Mungu anatupenda kikweli na anatutakia yaliyo bora?—Zaburi 145:16, 17; Isaya 42:5, 8.
Mbali na kujifunua kwetu kupitia “kitabu cha asili,” Muumba pia, hutuonyesha yeye ni Mungu wa aina gani kupitia Neno lake, Biblia. Hii ni kwa sababu Biblia ina rekodi ya mambo mengi yenye upendo ambayo Yehova Mungu alifanya wakati uliopita na pia baraka nyingi ambazo anaahidi kuwapa wanadamu hivi karibuni. (Mwanzo 22:17, 18; Kutoka 3:17; Zaburi 72:6-16; Ufunuo 21:4, 5) Zaidi ya yote, Biblia hutufunulia udhihirisho mkubwa zaidi wa upendo wa Mungu kwa wanadamu—kumtoa Mwana mzaliwa-pekee wake kuwa Mkombozi wetu ili tukombolewe kutokana na utumwa wa dhambi na kifo. (Waroma 5:8) Kwa kweli, kadiri tujifunzavyo zaidi juu ya Muumba wetu mwenye upendo, ndivyo tusukumwavyo zaidi kumpenda kutoka moyoni.
Kujifunza Kuwapenda Wanadamu Wenzetu
Kama Yesu alivyoonyesha, mbali na kumpenda Mungu kwa moyo, nafsi, na akili yetu yote, yatupasa pia kuwapenda jirani zetu kama tujipendavyo. Kwa kweli, kumpenda Mungu hutuwajibisha kuwapenda wanadamu wenzetu. Mtume Yohana alifafanua hivi: “Wapendwa, ikiwa hivi ndivyo Mungu alivyotupenda, basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu kupendana.” Aliendelea kukazia hivi: “Ikiwa yeyote atoa taarifa: ‘Mimi nampenda Mungu,’ na bado anachukia ndugu yake, yeye ni mwongo. Kwa maana yeye ambaye hapendi ndugu yake, ambaye ameona, hawezi kuwa anapenda Mungu, ambaye hajaona. Na amri hii tunayo kutoka kwake, kwamba yeye ambaye hupenda Mungu apaswa kuwa anapenda ndugu yake pia.”—1 Yohana 4:11, 20, 21.
Leo tunaishi katika ulimwengu ambapo watu wengi wana mtazamo wa mimi kwanza, wakiwa “wenye kujipenda wenyewe,” kama vile Biblia ilivyotabiri. (2 Timotheo 3:2) Hivyo, tukitaka kujifunza njia ipitayo zote ya upendo, basi ni lazima tujitahidi sana kugeuza akili zetu na kumwiga Muumba wetu mwenye upendo, badala ya kufuata njia zenye ubinafsi za watu kwa ujumla. (Waroma 12:2; Waefeso 5:1) Mungu hata ni “mwenye fadhili kuelekea wasio na shukrani na waovu,” naye “hufanya jua lake lichomoze juu ya watu waovu na wema na kufanya mvua inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” Kwa kuwa Baba yetu wa kimbingu hutuwekea kielelezo kizuri sana, yatupasa kujitahidi kuwa wenye fadhili na wenye kusaidia wote. Kwa kufanya hivyo, twaweza kujithibitisha kuwa ‘wana wa Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo.’—Luka 6:35; Mathayo 5:45.
Nyakati nyingine matendo hayo yenye upendo husaidia watu wawe waabudu wa Mungu wa kweli. Miaka kadhaa iliyopita mke wa nyumbani ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova alijaribu kumweleza jirani yake ujumbe wa Biblia, lakini yule jirani akakataa katakata. Hata hivyo, itikio hilo halikumvunja moyo. Badala yake, aliendelea kumwonyesha fadhili na kujaribu kumsaidia jirani huyo. Wakati mmoja alimsaidia kuhamia nyumba nyingine. Wakati mwingine akapanga mtu fulani aandamane na jirani huyo kwenda kwenye uwanja wa ndege kulaki jamaa zake. Baadaye, jirani huyo alikubali funzo la Biblia na hatimaye akawa Mkristo mwenye bidii licha ya mnyanyaso mkali kutoka kwa mume wake. Naam, vitendo hivyo vya upendo viliweka msingi wa kupata baraka za milele.
Tukisema kwa unyofu, tutakubali kwamba Mungu anatupenda si kwa sababu tuna sifa nyingi zenye kupendeza. Badala yake, yeye anatupenda hata ingawa tuna makosa mengi na kasoro nyingi. Kwa hiyo, yatupasa sisi vilevile tujifunze kuwapenda wanadamu wenzetu licha ya kasoro zao. Tukijizoeza kufahamu na kuthamini sifa nzuri za wengine badala ya kutafuta kuona kasoro zao, itakuwa rahisi zaidi kwetu kuwapenda. Mbali na kuwaonyesha upendo wenye kuongozwa na kanuni, huenda pia tukawaonyeshe shauku nyororo na upendo ambao rafiki za karibu huonyeshana.
Kukuza Upendo Wako
Upendo na urafiki wahitaji kusitawishwa, na weupe wa moyo na unyofu ni baadhi ya mambo muhimu yanayohitajiwa ili kuukuza. Wengine hujaribu kuficha kasoro zao ili wawapendeze watu wanaotaka kuwafanya rafiki zao. Hata hivyo, mara nyingi mwenendo kama huo haufaulu, kwa kuwa hatimaye wengine hupata kujua ukweli wa mambo nao huchukizwa na ukosefu huo wa unyofu. Kwa hiyo, hatupaswi kuogopa kuwaacha wengine wajue jinsi tulivyo kikweli—hata ingawa tuna kasoro tunazojitahidi kuzishinda. Hilo laweza kusaidia kuanzisha urafiki pamoja nao.
Kwa mfano, dada mmoja Shahidi mwenye umri mkubwa katika kutaniko moja kule Mashariki ya Mbali ana elimu kidogo sana. Hata hivyo, yeye hajaribu kamwe kuwaficha wengine hali hiyo. Kwa mfano, yeye hukubali waziwazi kwamba hawezi kuwaonyesha wengine jinsi ya kuthibitisha akitumia unabii mbalimbali wa Biblia na historia kwamba Nyakati za Mataifa ziliisha mwaka wa 1914.a Hata hivyo, yeye huweka kielelezo kizuri sana kwa kuwa mwenye bidii katika huduma, na vilevile mwenye upendo na ukarimu kwa akina ndugu, hivi kwamba yeye hutajwa kwa upendo kuwa mtu mwenye thamani sana katika kutaniko.
Katika tamaduni fulani, watu huudhika shauku inapoonyeshwa hadharani; watu hufundishwa kuonyesha adabu wanaposhughulika na wengine. Ingawa ni vema sikuzote kuwa wenye adabu na wenye kufikiria wengine, adabu hiyo haipaswi kutufanya tuzuie au tufiche hisia zetu kwa wengine. Yehova hakuona haya kukiri waziwazi shauku yake kwa Waisraeli wa kale, watu wake wachaguliwa, akiwaambia: “Nimekupenda kwa upendo wa milele.” (Yeremia 31:3) Vivyo hivyo, mtume Paulo aliwaambia waamini wenzake huko Thesalonike hivi: “Tukiwa na shauku nyororo kwa ajili yenu, tulipendezwa vema kuwapa nyinyi, si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zetu wenyewe, kwa sababu mlipata kuwa wapendwa kwetu.” (1 Wathesalonike 2:8) Hivyo, tujitahidipo kusitawisha shauku ya kweli kwa wanadamu wenzetu, jambo hilo hupatana zaidi na mafundisho ya Biblia juu ya kuonyesha hisia hizo kiasili badala ya kuzizuia.
Jitihada Yenye Kuendelea Yahitajiwa
Kujifunza kuwa na hisia kwa wengine na kuwapenda ni jambo linaloendelea. Kufanya hivyo kwahitaji jitihada nyingi kwa sababu inatupasa tujikakamue kushinda hali yetu wenyewe ya kutokamilika na vilevile kukinza uvutano wenye nguvu wa ulimwengu huu usio na upendo. Hata hivyo, thawabu nyingi zitokanazo na kufanya hivyo hufanya jambo hilo lifae kabisa.—Mathayo 24:12.
Hata katika ulimwengu huu usiokamilika kabisa, tunaweza kufurahia mahusiano yaliyoboreka pamoja na wanadamu wenzetu, yakitokeza furaha, amani, na uradhi mwingi kwetu wenyewe na kwa wengine. Kwa kujitahidi hivyo, tunaweza kujithibitisha kuwa twastahili tumaini zuri ajabu la kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Zaidi ya yote, kwa kujifunza njia ipitayo zote ya upendo, tunaweza kupata kibali na baraka za Muumba wetu mwenye upendo, sasa na kwa umilele!
[Maelezo ya Chini]
a Ili kupata habari zaidi, ona Insight on the Scriptures, Buku la Kwanza, ukurasa wa 132-135.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Upendo wa Kikristo waweza kuonyeshwa kwa matendo ya fadhili
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]
UN PHOTO 186226/M. Grafman