Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w00 7/1 kur. 13-18
  • Kupanda Mbegu za Kweli ya Ufalme

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupanda Mbegu za Kweli ya Ufalme
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yesu—Mpanzi wa Kweli ya Ufalme
  • Malaika Watangaza Taarifa za Mteremo
  • Twatimiza Wajibu Wetu kwa Hamu
  • Kazi ya Mungu wa Kweli
  • Tumekabidhiwa Hazina
  • Malaika—“Roho kwa Ajili ya Utumishi wa Watu Wote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Jinsi Malaika Wanavyoweza Kukusaidia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
  • Malaika—Je! Wao Wanaathiri Maisha Yako Wewe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Malaika—Jinsi Wanavyohusika Katika Maisha Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
w00 7/1 kur. 13-18

Kupanda Mbegu za Kweli ya Ufalme

“Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako.”—MHUBIRI 11:6.

1. Wakristo wanapandaje mbegu leo?

KILIMO kilikuwa muhimu sana kwa Waebrania wa kale. Ndiyo sababu Yesu, ambaye aliishi maisha yake yote ya kibinadamu katika Bara Lililoahidiwa, alitumia habari za kilimo katika vielezi vyake. Kwa mfano, alifananisha kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu na kupanda mbegu. (Mathayo 13:1-9, 18-23; Luka 8:5-15) Hadi leo hii, haidhuru twaishi katika jamii ya kilimo au la, kupanda mbegu za kiroho kwa njia hiyo ndiyo kazi muhimu zaidi kwa Wakristo.

2. Kazi yetu ya kuhubiri ni muhimu kadiri gani, na ni nini baadhi ya mambo yanayofanywa leo ili kuitimiza?

2 Ni pendeleo kubwa sana kushiriki kazi ya kupanda kweli ya Biblia wakati huu wa mwisho. Andiko la Waroma 10:14, 15 laonyesha vema umuhimu wa kazi hii: “Nao watasikiaje bila mtu fulani kuhubiri? Nao watahubirije isipokuwa wawe wametumwa? Kama vile imeandikwa: ‘Jinsi ilivyo yenye kupendeza miguu ya wale watangazao habari njema ya mambo mema!’” Ni muhimu sana leo kusonga mbele kwa mtazamo mzuri katika kutimiza utume huu kutoka kwa Mungu. Ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova wanajishughulisha sana na uchapishaji na ugawaji wa Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia katika lugha 340. Kazi hiyo huhitaji wajitoleaji zaidi ya 18,000 kwenye makao yao makuu na kwenye ofisi za tawi katika nchi mbalimbali. Na Mashahidi karibu milioni sita wanashiriki kugawa vichapo hivyo vya Biblia ulimwenguni kote.

3. Kupanda kweli ya Ufalme kunatimiza mambo gani?

3 Kazi hii ngumu imekuwa na matokeo gani? Kama katika siku za mapema za Ukristo, watu wengi leo wanaikubali kweli. (Matendo 2:41, 46, 47) Hata hivyo, la muhimu zaidi kuliko idadi kubwa ya wahubiri waliobatizwa karibuni ni uhakika wa kwamba ushahidi huu mkubwa huchangia kutakaswa kwa jina la Yehova na kutetewa kwake kuwa Mungu pekee wa kweli. (Mathayo 6:9) Na zaidi, ujuzi wa Neno la Mungu unaboresha maisha ya wengi na unaweza kuwaletea wokovu.—Matendo 13:47.

4. Mitume waliwahangaikia kadiri gani watu waliowahubiria?

4 Mitume walifahamu kikamili umuhimu wa habari njema katika kutoa uhai, nao waliwapenda sana watu waliohubiria. Hayo yanaonyeshwa wazi kwa maneno ya mtume Paulo, alipoandika hivi: “Tukiwa na shauku nyororo kwa ajili yenu, tulipendezwa vema kuwapa nyinyi, si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zetu wenyewe, kwa sababu mlipata kuwa wapendwa kwetu.” (1 Wathesalonike 2:8) Kwa kuwahangaikia watu kikweli, Paulo na wale mitume wengine walikuwa wanamwiga Yesu na malaika wa mbinguni, wanaohusika sana katika kazi hii yenye kuokoa uhai. Na tuchunguze tena wajibu muhimu ambao watumishi hao wa mbinguni wa Mungu hutimiza katika kupanda kweli ya Ufalme, kisha tuone vile mfano wao unavyotutia moyo tutimize wajibu wetu.

Yesu—Mpanzi wa Kweli ya Ufalme

5. Yesu alijishughulisha na kazi gani hasa alipokuwa duniani?

5 Yesu, mwanadamu mkamilifu, alikuwa na uwezo wa kuwapa watu wa siku yake vitu vingi vizuri vya kimwili. Kwa mfano, angaliweza kufafanua dhana nyingi bandia za kitiba za siku yake, au angaliweza kuboresha uelewevu wa wanadamu katika nyanja nyinginezo za elimu. Ingawa hivyo, alisema waziwazi mapema sana katika huduma yake kwamba utume wake ni kuhubiri habari njema. (Luka 4:17-21) Na mwishoni mwa huduma yake, alieleza hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Basi alijishughulisha na upandaji wa mbegu za kweli ya Ufalme. Kuwafundisha watu wa siku yake kuhusu Mungu na makusudi Yake kulikuwa muhimu zaidi kuliko elimu nyingine yoyote ambayo Yesu angaliwapa.—Waroma 11:33-36.

6, 7. (a) Yesu alitoa ahadi gani ya ajabu kabla ya kupaa mbinguni, naye anaitimizaje? (b) Mtazamo wa Yesu kuelekea kazi ya kuhubiri unakuathirije kibinafsi?

6 Yesu alidokeza kwamba yeye ni Mpanzi wa kweli ya Ufalme. (Yohana 4:35-38) Alitumia kila fursa kusambaza mbegu za habari njema. Hata alipokuwa akifa mtini, alitangaza habari njema kuhusu paradiso ya wakati ujao duniani. (Luka 23:43) Isitoshe, hangaiko lake kubwa la kuhubiriwa kwa habari njema halikukoma wakati alipokufa kwenye mti wa mateso. Kabla ya kupaa mbinguni, aliwaamuru mitume waendelee kupanda mbegu za kweli ya Ufalme na kufanya wanafunzi. Kisha Yesu akatoa ahadi ya ajabu. Akasema: “Tazameni! mimi nipo pamoja nanyi siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 28:19, 20.

7 Kwa maneno hayo, Yesu alitoa ahadi ya kutegemeza, kuelekeza, na kuilinda kazi ya kuhubiri habari njema “siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.” Hadi leo hii, Yesu anaendelea kupendezwa kibinafsi na kazi ya kueneza evanjeli. Ndiye Kiongozi wetu, anayesimamia upandaji wa kweli ya Ufalme. (Mathayo 23:10) Akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, anawajibika mbele za Yehova kwa kazi hii ya ulimwenguni kote.—Waefeso 1:22, 23; Wakolosai 1:18.

Malaika Watangaza Taarifa za Mteremo

8, 9. (a) Malaika wameonyeshaje kwamba wanapendezwa kikweli na mambo ya wanadamu? (b) Ni kwa njia gani sisi ni kitu cha kutazamwa mahali pa michezo kwa malaika?

8 Yehova alipoiumba dunia, malaika ‘waliimba pamoja na kupiga kelele kwa furaha.’ (Ayubu 38:4-7) Tangu wakati huo, viumbe hao wa mbinguni wamependezwa sana na mambo ya wanadamu. Yehova amewatumia kuwapelekea wanadamu hukumu zake. (Zaburi 103:20) Hayo yametimia hasa kuhusiana na kusambazwa kwa habari njema leo. Katika ufunuo aliopewa, mtume Yohana aliona ‘malaika akiruka katika mbingu ya kati’ akiwa na “habari njema idumuyo milele ili aitangaze kuwa taarifa za mteremo kwa wale wakaao juu ya dunia, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu, akisema kwa sauti kubwa: ‘Hofuni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imewasili.’”—Ufunuo 14:6, 7.

9 Biblia husema malaika ni “roho kwa ajili ya utumishi wa watu wote, waliotumwa kuwahudumia wale watakaorithi wokovu.” (Waebrania 1:14) Malaika watekelezapo migawo yao kwa hamu, wanapata nafasi ya kututazama sisi na kazi yetu. Twafanya kazi yetu mbele ya watazamaji wa mbinguni, kana kwamba tupo kwenye jukwaa wazi la michezo. (1 Wakorintho 4:9) Inaamsha fikira na kusisimua kama nini kujua kwamba tukiwa wapandaji wa kweli ya Ufalme hatufanyi kazi peke yetu!

Twatimiza Wajibu Wetu kwa Hamu

10. Shauri la busara kwenye Mhubiri 11:6 laweza kutumiwaje katika kazi yetu ya kueneza evanjeli?

10 Kwa nini Yesu na malaika wanapendezwa sana na kazi yetu? Yesu alitoa sababu moja aliposema hivi: “Mimi nawaambia nyinyi, ndivyo shangwe hutokea miongoni mwa malaika za Mungu juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye.” (Luka 15:10) Sisi pia hupendezwa na watu kikweli. Basi, twafanya kadiri tuwezavyo kusambaza mbegu za kweli ya Ufalme kila mahali. Maneno ya Mhubiri 11:6 yaweza kuhusu kazi yetu. Hapo Biblia yatushauri hivi: “Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako. Kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa, kama ni hii au hii, au kama zote zitafaa sawasawa.” Naam, kwa kila mtu mmoja anayekubali ujumbe wetu, labda kuna mamia au hata maelfu wanaoukataa. Lakini sisi, kama vile malaika, hushangilia “mtenda-dhambi mmoja” anapokubali ujumbe wa wokovu.

11. Vichapo vinavyotegemea Biblia vyaweza kuwa na matokeo kadiri gani?

11 Mengi yanahusika katika kuhubiri habari njema. Vichapo vinavyotegemea Biblia ambavyo Mashahidi wa Yehova hutumia ni msaada muhimu katika kazi hii. Kwa namna fulani, vichapo hivyo ni kama mbegu zinazosambazwa kila mahali. Hatujui vitafanikiwa wapi. Nyakati nyingine kichapo chaweza kupitia mikononi mwa watu kadhaa kabla ya mtu fulani kukisoma. Huenda hata Yesu na malaika wakaongoza mambo katika visa fulani ili kutokeza jambo hilo kwa faida ya watu wenye mioyo minyofu. Ona baadhi ya mambo yaliyoonwa yaelezayo jinsi ambavyo Yehova aweza kutokeza mambo mazuri yasiyotarajiwa akitumia kichapo ambacho watu wamepewa.

Kazi ya Mungu wa Kweli

12. Gazeti fulani kuukuu lilitimiza fungu gani muhimu la kuisaidia familia moja ipate kumjua Yehova?

12 Mwaka wa 1953, Robert, Lila, na watoto wao walihama jiji moja, wakaingia nyumba mbovu huko Pennsylvania mashambani, nchini Marekani. Muda mfupi baada ya kuingia humo, Robert aliamua kujenga bafu chini ya chumba cha ngazi. Baada ya kutoa mbao kadhaa, aligundua kwamba panya wameweka vipande vya karatasi, maganda ya njugu, na takataka nyingine nyuma ya ukuta. Na ndani ya takataka hiyo yote mlikuwemo gazeti la The Golden Age. Robert alivutiwa hasa na makala inayohusu kulea watoto. Alipendezwa sana na mwelekezo wa gazeti hilo, uliokuwa wazi na wenye kutegemea Biblia, hivi kwamba akamwambia Lila watajiunga na “dini ya The Golden Age.” Katika muda wa majuma machache tu, Mashahidi wa Yehova waliwatembelea, lakini Robert akawaambia kwamba familia inapendezwa na “dini ya The Golden Age” peke yake. Mashahidi walimweleza kwamba gazeti la The Golden Age sasa lina jina jipya, Amkeni! Robert na Lila wakaanza kujifunza Biblia kwa ukawaida na Mashahidi hao, kisha wakabatizwa. Hao nao wakapanda mbegu za ile kweli katika watoto wao na kuvuna kwa wingi. Leo, washiriki zaidi ya 20 wa familia hiyo, kutia ndani watoto saba wa Robert na Lila, ni watumishi waliobatizwa wa Yehova Mungu.

13. Ni nini kilichowachochea mume na mke nchini Puerto Riko kusitawisha upendezi katika Biblia?

13 Miaka ipatayo 40 iliyopita, William na Ada, mume na mke raia wa Puerto Riko, hawakupenda kujifunza Biblia. Kila mara Mashahidi wa Yehova walipobisha mlango wao, wenzi hao walijifanya hawamo nyumbani. Siku moja William akaenda kwenye duka la bidhaa kuukuu ili kununua kifaa cha kufanyia marekebisho fulani nyumbani. Alipokuwa anaondoka, aliona kitabu cha rangi ya manjano kwenye pipa la takataka. Kitabu hicho kinaitwa Religion, na kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1940. William alienda na kitabu hicho nyumbani naye akasisimka kusoma kuhusu tofauti kati ya dini isiyo ya kweli na dini ya kweli. Mashahidi wa Yehova walipowatembelea baadaye, William na Ada walisikiliza ujumbe wao kwa furaha na kuanza kujifunza nao Biblia. Wakabatizwa miezi kadhaa baadaye kwenye Kusanyiko la Kimataifa la Mapenzi ya Mungu mwaka wa 1958. Tangu wakati huo, wamesaidia watu zaidi ya 50 kujiunga na udugu wetu wa Kikristo.

14. Kama jambo lililoonwa lionyeshavyo, vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia vyaweza kuwa na matokeo gani?

14 Karl alikuwa na miaka 11 tu naye alikuwa mtundu-mtundu. Alijikuta matatani kila mara. Baba yake, mhubiri wa Methodist huko Ujerumani, alimfundisha kwamba watu wabaya huchomeka kwenye helo baada ya kifo. Basi Karl akaogopa sana helo. Siku moja mwaka wa 1917, Karl aliona karatasi fulani yenye maandishi barabarani na kuiokota. Alipokuwa anaisoma, mara moja akaona swali hili: “Helo ni nini?” Karatasi hiyo iliwaalika watu kwenye hotuba ya watu wote juu ya helo, ambayo iliandaliwa na Wanafunzi wa Biblia, ambao sasa huitwa Mashahidi wa Yehova. Mwaka mmoja hivi baadaye, baada ya kujifunza Biblia mara kadhaa, Karl alibatizwa na kuwa mmoja wa Wanafunzi wa Biblia. Mwaka wa 1925, alialikwa akafanye kazi kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova—naye bado anatumikia huko. Kazi-maisha ya Kikristo ambayo ameifanya kwa zaidi ya miaka 80 ilitokana na karatasi barabarani.

15. Yehova aweza kufanya nini kama apendavyo?

15 Ni kweli, mwanadamu hana uwezo wa kujua iwapo malaika walihusika, na ni kwa kadiri gani walihusika moja kwa moja katika mambo hayo yaliyoonwa. Ijapokuwa hivyo, hatupaswi kamwe kutilia shaka kwamba Yesu na malaika wanahusika sana katika kazi ya kuhubiri na kwamba Yehova aweza kuongoza mambo apendavyo. Mambo hayo na mengine mengi yaliyoonwa yaonyesha kwamba vichapo vyetu vyaweza kuwa na matokeo mazuri baada ya kuwapa watu.

Tumekabidhiwa Hazina

16. Twaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya 2 Wakorintho 4:7?

16 Mtume Paulo alitaja “hazina hii katika vyombo vya udongo.” Hazina hiyo ni utume wa kuhubiri kutoka kwa Mungu, na vyombo vya udongo ni wanadamu ambao Yehova amekabidhi hazina hiyo. Kwa kuwa wanadamu hao si wakamilifu na wana udhaifu, Paulo aendelea kusema kwamba sababu ya kupewa hazina hiyo ni ili “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe.” (2 Wakorintho 4:7) Naam, twaweza kumtumaini Yehova atupe nguvu tunazohitaji ili tutimize kazi iliyopo.

17. Tutakabili nini tupandapo mbegu za kweli ya Ufalme, na licha ya hayo, kwa nini tudumishe mtazamo mzuri?

17 Mara nyingi inakuwa lazima tujidhabihu. Huenda ikawa vigumu au isifae kuhubiri maeneo fulani. Maeneo fulani yana watu wengi wanaoonekana kuwa na ubaridi mkali na hata uhasama. Huenda jitihada nyingi zikatumiwa kuhubiri maeneo hayo bila kuona mafanikio. Lakini jitihada hizo zafaa kwa maana masuala mengi yanahusika. Kumbuka kwamba mbegu unazopanda zaweza kuwapa watu furaha sasa na vilevile uhai udumuo milele wakati ujao. Mara nyingi maneno ya Zaburi 126:6, Biblia Habari Njema, yametimia: “Wanaokwenda kupanda mbegu wakilia, watarudi kwa furaha wakichukua mavuno.”

18. Twaweza kukazaje uangalifu daima kwa huduma yetu, na kwa nini tufanye hivyo?

18 Na tutumie kila nafasi inayofaa ili kupanda kwa wingi mbegu za kweli ya Ufalme. Tusisahau kamwe kwamba, tujapopanda mbegu na kuzitilia maji, Yehova ndiye huzikuza. (1 Wakorintho 3:6, 7) Ingawa hivyo, kama vile Yesu na malaika wanavyotimiza fungu lao la kazi, ndivyo Yehova anavyotutarajia tutimize huduma yetu kikamili. (2 Timotheo 4:5) Na tukaze uangalifu daima kwa mafundisho yetu, mitazamo yetu, na hamu yetu katika huduma. Kwa nini? Paulo ajibu hivi: “Kwa kufanya hivi utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.”—1 Timotheo 4:16.

Tulijifunz Nini?

• Ni katika njia zipi kazi yetu ya kupanda inakuwa na matokeo mazuri?

• Yesu Kristo na malaika wanahusikaje katika kazi ya kueneza evanjeli leo?

• Kwa nini twapaswa kupanda kweli ya Ufalme kwa wingi?

• Tunapokabili ubaridi au uhasama katika huduma yetu, ni nini kinachopasa kutuchochea tuvumilie?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kama wakulima katika Israeli ya kale, Wakristo leo husambaza kwa wingi mbegu za kweli ya Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Mashahidi wa Yehova huchapisha na kugawa vichapo vingi mbalimbali vinavyotegemea Biblia katika lugha 340

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki