Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w03 6/1 kur. 28-30
  • Kufukiza Uvumba—Je, Kunahitajiwa Katika Ibada ya Kweli?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kufukiza Uvumba—Je, Kunahitajiwa Katika Ibada ya Kweli?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mtakatifu kwa Ajili ya BWANA”
  • Wakristo wa Awali na Uvumba
  • Kufukiza Uvumba Leo
  • Sala ‘Zilizotayarishwa Kama Uvumba’
  • Siku ya Kufunika Dhambi Inakuhusuje?
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2020
  • Jinsi ya Kumkaribia “Msikiaji wa Sala”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Je, Sala Zako ‘Hutayarishwa Kama Uvumba’?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Mambo Tunayojifunza Katika Kitabu cha Mambo ya Walawi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
w03 6/1 kur. 28-30

Kufukiza Uvumba—Je, Kunahitajiwa Katika Ibada ya Kweli?

“MIUNGU hupenda harufu nzuri.” Wamisri wa kale walizoea kusema hivyo. Kufukiza uvumba kulikuwa jambo la kawaida katika ibada yao. Wamisri walifukiza uvumba kila siku katika mahekalu yao na katika madhabahu nyumbani mwao na hata katika biashara zao kwa kuwa waliamini kwamba miungu ilikuwa karibu nao. Mataifa mengine yalikuwa na desturi kama hizo.

Uvumba ni nini? Neno hilo linaweza kumaanisha moshi au ubani unaochomwa. Hutengenezwa na manemane yenye harufu nzuri na gundi, kama vile ubani na zeri. Vitu hivyo hupondwapondwa na mara nyingi huchanganywa na vitu kama vile viungo, magamba ya miti, na maua ili kutengeneza aina mbalimbali ya manukato kwa makusudi hususa.

Uvumba ulipendwa sana na hivyo ukawa bidhaa yenye thamani sana nyakati za kale na viungo vyake vikawa muhimu katika biashara. Misafara ya wafanyabiashara ilileta ubani kutoka nchi za mbali. Huenda ukakumbuka kwamba Yosefu, mwana mdogo wa Yakobo aliuzwa kwa wafanyabiashara Waishmaeli waliokuwa ‘wakija kutoka Gileadi na ngamia zao, wakichukua ubani na zeri na manemane, wakisafiri kuvichukua mpaka Misri.’ (Mwanzo 37:25) Watu walitaka sana ubani hivi kwamba njia iliyoanzishwa na wafanyabiashara wa ubani ilitumiwa kusafiri kati ya Asia na Ulaya.

Dini nyingi leo zingali zinafukiza uvumba katika sherehe na desturi zao. Zaidi ya hayo, watu wengi hupenda kufukiza ubani nyumbani mwao ili kufurahia tu harufu yake nzuri. Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani kuelekea kufukiza uvumba? Je, Mungu anakubali utumiwe katika ibada? Hebu tuchunguze maoni ya Biblia kuhusu jambo hilo.

“Mtakatifu kwa Ajili ya BWANA”

Katika Israeli ya kale, sehemu muhimu ya kazi ya makuhani katika tabenakulo ilikuwa kufukiza uvumba. Cyclopedia ya McClintock na Strong inasema: “Kwa kweli, yaelekea kwamba Waebrania waliona kufukiza uvumba kuwa tendo la ibada au utoaji mtakatifu na ndiyo sababu hatuoni wakitumia uvumba kwa njia nyingine yoyote isipokuwa hiyo.”

Yehova Mungu aliagiza viungo vinne vichanganywe na kuchomwa kwenye tabenakulo: “Jitwalie manukato mazuri, yaani, natafi, na shekelethi, na kelbena; viungo vya manukato vizuri pamoja na ubani safi; vitu hivyo vyote na viwe vya kipimo kimoja; nawe utafanya uvumba wa vitu hivyo, manukato ya kazi ya ustadi wa mtengenezaji manukato, yatakuwa yamekolea, safi, matakatifu; nawe baadhi yake utayaponda sana, na kuyaweka mbele ya ushuhuda ndani ya hema ya kukutania.” (Kutoka 30:34-36) Wasomi wanadai kwamba viungo vingine viliongezwa baadaye na marabi Wayahudi kwa matumizi ya hekaluni.

Uvumba uliochomwa kwenye tabenakulo ulikuwa mtakatifu, ulitumiwa katika ibada ya Mungu peke yake. Yehova aliamuru: “Na uvumba utakaofanya, hamtajifanyia uvumba wenye viungo sawasawa na uvumba huo; utakuwa kwenu mtakatifu kwa ajili ya BWANA. Mtu yeyote atakayefanya mfano wa huo, ili kuunusa mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake.” (Kutoka 30:37, 38) Makuhani walifukiza uvumba mara mbili kwa siku juu ya madhabahu maalumu. (2 Mambo ya Nyakati 13:11) Na katika Siku ya Kufunika, kuhani mkuu alifukiza uvumba katika Patakatifu Zaidi.—Mambo ya Walawi 16:12, 13.

Mungu hakukubali kila aina ya uvumba. Aliwaadhibu watu ambao walifukiza uvumba kwa kimbelembele kana kwamba walikuwa makuhani. (Hesabu 16:16-18, 35-40; 2 Mambo ya Nyakati 26:16-20) Yehova alichukizwa na uvumba uliofukizwa na taifa la Israeli walipokuwa wakishiriki katika ibada ya uwongo na kumwaga damu. Yehova alitangaza hivi kwa sababu ya unafiki wao: “Uvumba ni chukizo kwangu.” (Isaya 1:13, 15) Waisraeli waliipuuza ibada ya Yehova wakafunga hekalu na kufukiza uvumba kwenye madhabahu mengine. (2 Mambo ya Nyakati 28:24, 25) Miaka kadhaa baadaye, uvumba mtakatifu hata ulitumiwa katika ibada iliyopotoka ya miungu ya uwongo. Matendo hayo yalimchukiza Yehova.—Ezekieli 16:2, 17, 18.

Wakristo wa Awali na Uvumba

Agano la Sheria, kutia ndani agizo la makuhani kufukiza uvumba mtakatifu, lilikoma Kristo alipoanzisha agano jipya mwaka wa 33 W.K. (Wakolosai 2:14) Hakuna maandishi yoyote yanayoonyesha kwamba Wakristo wa awali walifukiza uvumba kwa makusudi ya kidini. Kuhusiana na hilo, Cyclopedia ya McClintock na Strong yasema hivi: “Ni kweli kwamba [Wakristo wa awali] hawakutumia uvumba. Ama kweli matumizi yake yalikuwa ishara ya upagani . . . Kunyunyiza chembechembe za uvumba juu ya madhabahu ya kipagani kulikuwa tendo la ibada.”

Wakristo wa awali walikataa pia kufukiza uvumba ili kukiri “uungu” wa maliki Mroma, hata kama wangeuawa. (Luka 4:8; 1 Wakorintho 10:14, 20) Hata hawangefanya biashara ya uvumba kwa sababu uvumba ulitumiwa katika ibada ya sanamu wakati huo.

Kufukiza Uvumba Leo

Uvumba hutumiwaje leo? Katika makanisa mengi ya Jumuiya ya Wakristo, uvumba hufukizwa wakati wa sherehe na ibada. Familia nyingi za Asia hufukiza uvumba katika mahekalu au mbele ya madhabahu nyumbani ili kuheshimu miungu yao na kuwalinda wafu. Katika ibada za kidini, uvumba umekuwa ukitumiwa kwa njia mbalimbali kuleta harufu nzuri, kuponya, kutakasa, na kulinda.

Hivi karibuni uvumba umeanza kutumiwa tena hata na watu wasio na dini. Wengine hufukiza uvumba wanapotafakari. Kitabu kimoja cha mwongozo kinapendekeza kutumia uvumba ili “kufahamu mambo yasiyo ya kawaida” na “kuwa na uwezo wa pekee” usio wa kawaida. Ili kupata suluhisho kwa matatizo ya maisha, kitabu hicho kinapendekeza pia desturi za kufukiza uvumba ambazo hutia ndani kuwasiliana na “viumbe wa roho.” Je, Wakristo wafuate mazoea hayo?

Yehova hushutumu kabisa wale wanaochanganya mazoea ya dini isiyo ya kweli na ibada safi. Mtume Paulo alinukuu unabii wa Isaya na kuwasihi Wakristo wajiepushe na mazoea machafu ya dini isiyo ya kweli. Aliandika hivi: “‘Tokeni miongoni mwao, na jitengeni wenyewe,’ asema Yehova, ‘na komeni kugusa kitu kisicho safi’; ‘na hakika mimi nitawakaribisha ndani.’” (2 Wakorintho 6:17; Isaya 52:11) Wakristo wa kweli huhakikisha kwamba wanajiepusha na chochote kinachohusiana na ibada isiyo ya kweli au mambo ya uchawi.—Yohana 4:24.

Je, kufukiza uvumba ni kosa eti kwa sababu unatumiwa katika sherehe za kidini na uwasiliani-roho? Si lazima. Huenda mtu akataka kufukiza uvumba nyumbani mwake ili afurahie harufu yake nzuri. (Mithali 27:9) Hata hivyo, Mkristo anapaswa kufikiria mambo fulani anapoamua kufukiza uvumba. Je, majirani watafikiri kwamba unashiriki desturi fulani ya kidini wakikuona ukifukiza uvumba? Je, kufukiza uvumba huhusianishwa na desturi za uwasiliani-roho katika eneo lenu? Au kwa kawaida hutumiwa kwa makusudi yasiyo ya kidini?

Mtu anapoamua kufukiza uvumba, anapaswa kufikiria dhamiri yake na hisia za wengine. (1 Wakorintho 10:29) Maneno ya Mtume Paulo kwa Waroma yanafaa. Aliandika hivi: “Acheni tufuatie mambo yafanyayo kuwe na amani na mambo yaliyo ya kujengana. Komeni kuibomoa kazi ya Mungu kwa ajili ya chakula tu. Ni kweli, vitu vyote ni safi, lakini ni jambo baya kwa mtu ambaye ala kukiwa na sababu ya kukwaza. Ni vema kutokula nyama au kunywa divai au kufanya jambo lolote ambalo juu yalo ndugu yako akwazika.”—Waroma 14:19-21.

Sala ‘Zilizotayarishwa Kama Uvumba’

Kufukiza uvumba wakati wa Waisraeli ni mfano unaofaa wa sala zinazosikiwa na Mungu. Kwa hiyo mtunga-zaburi Daudi alimwimbia Yehova hivi: “Sala yangu na itayarishwe kama uvumba mbele zako.”—Zaburi 141:2, NW.

Waisraeli waaminifu hawakufukiza uvumba kidesturi tu. Walitayarisha na kufukiza uvumba kwa makini sana kama walivyoagizwa na Yehova. Badala ya kufukiza uvumba halisi, Wakristo leo hutoa sala zinazoonyesha shukrani nyingi na heshima kwa Baba yao wa mbinguni. Kama uvumba wenye harufu nzuri uliofukizwa hekaluni na makuhani, Neno la Mungu latuhakikishia hivi: ‘Sala ya mtu mnyofu ni furaha yake.’—Mithali 15:8.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Uvumba uliofukizwa kwenye tabenakulo na hekaluni ulikuwa mtakatifu

[Picha katika ukurasa wa 30]

Je, inafaa Wakristo wafukize uvumba wanapotafakari?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki