Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w06 3/15 kur. 17-20
  • Kutumika Katika Kutaniko la Lugha ya Kigeni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutumika Katika Kutaniko la Lugha ya Kigeni
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupambana na Lugha
  • Endelea Kufanya Maendeleo
  • Kutumika Katika Kutaniko
  • Kudumisha Nguvu za Kiroho
  • Kuhesabu Gharama
  • Unaweza kujifunza lugha nyingine!
    Amkeni!—2007
  • Je, Wataka Kujifunza Lugha ya Kigeni?
    Amkeni!—2000
  • Kwa Nini Ujifunze Lugha Nyingine?
    Vijana Huuliza
  • Kuwahubiria Watu Wanaozungumza Lugha ya Kigeni
    Huduma ya Ufalme—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
w06 3/15 kur. 17-20

Kutumika Katika Kutaniko la Lugha ya Kigeni

MTUME Yohana aliandika hivi: “Nikamwona malaika mwingine akiruka katikati ya mbingu, naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufunuo 14:6) Katika utimizo wa maono hayo ya kinabii, habari njema ya Ufalme wa Mungu inahubiriwa ulimwenguni pote katika ndimi, au lugha mbalimbali. Nyingi za lugha hizo zinazungumzwa na wahamiaji wanaoishi mbali na nchi zao za asili. Watu hao pia wanasikia habari njema kutoka kwa Mashahidi wa Yehova wenye bidii ambao wamejifunza lugha nyingine.

Je, wewe ni miongoni mwa Mashahidi hao wanaotumika katika kutaniko la lugha ya kigeni? Au je, huenda unafikiria kufanya hivyo? Ili kufaulu katika jitihada zako, unahitaji kuwa na nia isiyo na ubinafsi na mtazamo unaofaa. Kwa kuwa kusudi lako ni kuwasaidia wengine wajifunze kweli kutoka katika Neno la Mungu, una nia nzuri sana, yaani, upendo wako kwa Mungu na kwa jirani. (Mathayo 22:37-39; 1 Wakorintho 13:1) Tamaa ya kuwasaidia wengine wamjue Mungu ndiyo inayoweza kukuchochea hata zaidi kuliko kufurahia tu ushirika, chakula, na utamaduni wa watu wa taifa au kikundi kingine. Je, unaogopa kujifunza lugha nyingine? Ikiwa ndivyo, kuwa na mtazamo unaofaa kutakusaidia. James, aliyejifunza Kijapani, anasema hivi: “Usiogopeshwe na lugha.” Kujua kwamba wengine wengi ambao wamejifunza lugha hiyo kabla yako wamefaulu, kunaweza kukusaidia kuvumilia na kudumisha mtazamo mzuri. Basi, unaweza kujifunzaje lugha mpya? Ni nini kitakachokusaidia kubadilika kulingana na hali za kutaniko linalotumia lugha hiyo? Unapaswa kufanya nini ili kuwa na nguvu kiroho?

Kupambana na Lugha

Kuna njia nyingi za kujifunza lugha. Wanafunzi na walimu huwa na maoni tofauti-tofauti kuhusu kujifunza lugha. Hata hivyo, wanafunzi wengi huonelea kwamba kufundishwa kwa muda fulani na mwalimu mwenye ustadi humfanya mtu ajifunze haraka zaidi na kwa urahisi zaidi. Ukisoma Biblia na vitabu vinavyoizungumzia katika lugha ambayo unajifunza na kusikiliza kaseti utaongeza msamiati wako na ujuzi wako wa maneno yanayotumiwa kutanikoni. Vipindi vinavyofaa kwenye redio, televisheni, na video vinaweza pia kukusaidia kufahamiana na lugha na utamaduni wa watu wanaozungumza lugha hiyo. Kwa kawaida, kusoma kidogo kila siku huwa na matokeo zaidi kuliko kusoma mara mojamoja kwa muda mrefu sana.

Kujifunza lugha ni kama kujifunza kuogelea. Huwezi kujifunza kuogelea kwa kusoma vitabu tu. Unapaswa kuingia ndani ya maji. Ndivyo ilivyo na kujifunza lugha. Ni vigumu kujifunza lugha kwa kusoma vitabu tu. Unahitaji kuchangamana na watu wakati wowote iwezekanapo, kusikiliza jinsi wanavyozungumza, kushirikiana nao, na hasa kuzungumza nao! Utendaji wa Kikristo unatoa nafasi nzuri ya kutimiza yote hayo. Mara nyingi, unaweza kutumia moja kwa moja yale unayojifunza katika huduma ya shambani. Midori anayejifunza Kichina anasema hivi: “Huenda likaonekana kuwa jambo la kuogopesha. Hata hivyo, wenye nyumba wanaweza kuona kwamba sisi Mashahidi tunajitahidi sana. Hilo linaweza kuwachochea watusikilize. Tunahitaji tu kuwaambia hivi katika lugha yao, ‘Ninafurahi kukujua,’ na utaona nyuso zao zikionyesha kwamba wanafurahi kuzungumza nawe!”

Pia, mikutano ya Kikristo inasaidia sana. Katika kila mkutano, jaribu kutoa maelezo angalau mara moja. Usijali, hata ikiwa utaogopa mwanzoni. Kutaniko linataka ufaulu! Monifa, ambaye anajifunza Kikorea, anasema hivi: “Ninamshukuru sana dada ambaye huketi kando yangu wakati wa mikutano na kuniandikia maana ya maneno fulani. Yeye hunisaidia sana kwa kunitegemeza kwa shauku na subira.” Kadiri msamiati wako utakavyoongezeka, ndivyo utakavyoanza kufikiri katika lugha hiyo mpya kwa kuhusianisha moja kwa moja maneno na maana yake badala ya kutafsiri akilini kila neno.

Kusudi lako la kwanza la kujifunza lugha linapaswa kuwa ‘kusema maneno yenye kueleweka kwa urahisi.’ (1 Wakorintho 14:8-11) Hata ikiwa watu watakuvumilia, huenda makosa au matamshi yaliyo tofauti yakawakengeusha na kuwafanya wasisikilize ujumbe wako. Kukazia uangalifu matamshi mazuri na sarufi tangu mwanzo kutakusaidia usisitawishe mazoea mabaya ambayo itakuwa vigumu kuyaacha. Mark, aliyejifunza Kiswahili, anadokeza hivi: “Waombe wasemaji wazuri wakukosoe, kisha uwashukuru!” Onyesha kwamba unajali wakati na jitihada za wale wanaokusaidia. Ingawa huenda ukamwomba mtu mwingine achunguze kazi yako, jaribu kutayarisha hotuba na maelezo yako kwa kutumia maneno ambayo tayari unayajua au yale ambayo umeyafanyia utafiti. Kufanya hivyo kutaharakisha maendeleo yako ya kujifunza na kutakusaidia kusema kwa uhakika.

Endelea Kufanya Maendeleo

Monifa anasema hivi: “Kujifunza lugha nyingine ndiyo kazi ngumu zaidi ambayo nimewahi kufanya. Kuna nyakati nimetamani kuacha. Lakini mimi hukumbuka jinsi mwanafunzi wangu wa Biblia anavyopenda kusikiliza kweli za kiroho katika Kikorea changu kibaya na shangwe ambayo akina ndugu wanaonyesha ninapofanya hata maendeleo madogo.” Jambo kuu ni kwamba, usikate tamaa haraka. Mradi wako ni kuweza kuwafundisha wengine kweli za Kimaandiko zinazookoa uhai. (1 Wakorintho 2:10) Hivyo, kujifunza kufundisha Biblia katika lugha nyingine kunahitaji uwe makini na ujitahidi kwa muda mrefu. Unapoendelea kujifunza, epuka kulinganisha isivyofaa maendeleo yako na ya wengine. Wale wanaojifunza lugha mpya hawafanyi maendeleo kwa kadiri ileile wala kwa njia ileile. Hata hivyo, ni muhimu kutambua maendeleo yako mwenyewe. (Wagalatia 6:4) Joon ambaye ameanza kujifunza Kichina anasema hivi: “Kujifunza lugha ni kama kupanda ngazi. Unapohisi kwamba hufanyi maendeleo, ndipo unapotambua kwamba umefanya maendeleo makubwa.”

Kujifunza lugha mpya ni kazi inayoendelea muda wote wa maisha yako. Kwa hiyo, furahia kujifunza lugha mpya, na usitarajie ukamilifu. (Zaburi 100:2) Hatuwezi kuepuka kufanya makosa. Kukosea ni mojawapo ya njia za kujifunza. Alipoanza kuhubiri katika Kiitaliano, Mkristo mmoja alimwuliza mwenye nyumba, “Je, unajua ufagio wa maisha?” Alikuwa akimaanisha, “kusudi la maisha.” Shahidi mmoja aliyekuwa anajifunza Kipolishi alialika kutaniko kuimba mbwa badala ya wimbo. Mwingine aliyekuwa akijifunza Kichina alipobadili matamshi kidogo tu, aliwahimiza wasikilizaji wake wawe na imani katika mkoba wa vitabu wa Yesu badala ya kuwa na imani katika dhabihu ya Yesu. Kukosea humsaidia mtu kukumbuka kabisa maneno sahihi aliyojifunza.

Kutumika Katika Kutaniko

Zaidi ya tofauti za lugha, kuna mambo mengine yanayowagawanya watu. Mara nyingi, utamaduni, rangi, na tofauti za kitaifa huwagawanya wanadamu hata zaidi. Hata hivyo, tunaweza kushinda vizuizi hivyo. Msomi mmoja aliyefanya uchunguzi kuhusu vikundi vya kidini vinavyotumia Kichina huko Ulaya alisema kwamba Mashahidi wa Yehova “hawabagui watu wa taifa lolote.” Alitambua kwamba miongoni mwa Mashahidi “kabila la mtu si muhimu sana, na lugha ni njia tu ya kuwasaidia watu kuelewa neno la Mungu.” Kutumia kanuni za Biblia huwasaidia Wakristo wa kweli kushinda tofauti za kitaifa. Kwa wale wanaovaa ‘utu mpya, hakuna Mgiriki wala Myahudi wala mgeni.’—Wakolosai 3:10, 11.

Hivyo, wote kutanikoni wanapaswa kusaidia kuendeleza umoja. Hilo linahitaji mtu awe tayari kukubali njia mpya za kufikiri, za kuhisi, na za kufanya mambo. Unaweza kuzuia tofauti za kikabila zisisababishe migawanyiko kwa kuepuka kukazia fikira mapendezi yako. (1 Wakorintho 1:10; 9:19-23) Jifunze kufurahia mambo mazuri zaidi katika kila utamaduni. Kumbuka kwamba upendo usio na ubinafsi ndio siri ya kuwa na uhusiano mzuri na umoja wa kweli.

Makutaniko mengi ya lugha ya kigeni huanza yakiwa vikundi vidogo, na mara nyingi yanafanyizwa na wengi wanaojifunza lugha mpya pamoja na baadhi ya wale ambao wameanza kujifunza kanuni za Biblia hivi karibuni. Hivyo, kutoelewana kunaweza kutokea mara nyingi katika vikundi kama hivyo kuliko ilivyo katika kutaniko kubwa lililositawi. Wakristo wakomavu wanapaswa kujitahidi kuliimarisha kutaniko. Kuonyeshana upendo na fadhili kwa maneno na kwa matendo husaidia kufanyiza mazingira mazuri yanayowawezesha wapya kukua kiroho.

Wale wanaojitolea kusaidia katika kutaniko la lugha ya kigeni wanapaswa pia kuwa na usawaziko katika yale wanayotarajia wengine wawatendee. Rick, ambaye ni mzee katika kutaniko moja kama hilo, anaeleza: “Huenda wengine katika kutaniko kama hilo ni Mashahidi wapya ambao hawana ustadi wa kupanga mambo kama Mashahidi wengine wa makutaniko yaliyositawi. Hata hivyo, ingawa hawana ustadi, wana upendo na shauku. Isitoshe, watu wengi wanaopendezwa wanakubali kweli.” Ukihudhuria mikutano kwa ukawaida, kushiriki katika utendaji mwingine wa kutaniko, na kuwasaidia wengine kwa njia yoyote ile, utalisaidia kutaniko sana hata ikiwa bado unaendelea kujifunza lugha. Kwa kushirikiana, wote wanaweza kufanya hali ya kiroho ya kutaniko iwe nzuri.

Kudumisha Nguvu za Kiroho

Ndugu mmoja aliyekuwa mpya katika kutaniko moja la lugha ya kigeni alimsikia mama mmoja akimsaidia mtoto wake kutayarisha maelezo. “Lakini mama, mbona jibu hili ni ndefu sana?” mtoto huyo akauliza. Mama huyo akamjibu: “Hapana, mtoto wangu. Majibu mafupi tunawaachia wale wanaojifunza lugha.”

Mtu mzima anaweza kudhoofika kiakili, kihisia, na kiroho asipoweza kuwasiliana vizuri kwa miezi mingi au hata kwa miaka mingi. Janet, ambaye sasa anazungumza vizuri Kihispania, anakumbuka: “Nilifadhaika sana kwa sababu ya kupungukiwa kwangu.” Hiroko, ambaye alijifunza Kiingereza, anakumbuka akiwaza hivi: ‘Hata mbwa na paka wa eneo hili wanaelewa Kiingereza vizuri zaidi kuliko mimi.’ Halafu Kathie anasema hivi: “Kabla ya kuhamia kutaniko la Kihispania, nilikuwa na mafunzo mengi ya Biblia na ziara za kurudia, lakini baada ya kuhamia kutaniko hilo sikuwa na funzo la Biblia wala ziara ya kurudia. Nilihisi kwamba sikuwa nikifanya chochote.”

Katika hali kama hiyo, ni muhimu kuwa na mtazamo unaofaa. Alipovunjika moyo, Hiroko alifikiri hivi: “Ikiwa wengine wanaweza kujifunza lugha nyingine, mimi pia ninaweza.” Kathie anasema: “Nilifikiri kuhusu mume wangu, ambaye anafanya maendeleo mazuri na kutimiza mengi kutanikoni. Hilo lilinisaidia kushinda matatizo mwanzoni, na hivyo nikaanza kufanya maendeleo makubwa zaidi. Bado nina mengi ya kujifunza, lakini hatua kwa hatua ninaweza sasa kuhubiri na kufundisha, na hilo hunifurahisha.” Mume wake Jeff, anaongeza hivi: “Inaweza kuvunja moyo kutoelewa kila jambo linalosemwa wakati wa matangazo na kwenye mikutano ya wazee. Ninahitaji kuwa mnyoofu na mnyenyekevu ili kuuliza yale yaliyosemwa. Hata hivyo akina ndugu wanafurahi kunisaidia.”

Ili kuepuka uchovu wa kiroho unaposhirikiana na kutaniko linalotumia lugha ya kigeni, unapaswa kutilia maanani hali yako ya kiroho. (Mathayo 5:3) Kazuyuki, ambaye kwa miaka mingi ametumika katika eneo la Kireno, anasema hivi: “Ni muhimu tule chakula cha kutosha cha kiroho. Kwa sababu hiyo, tukiwa familia, tunajifunza na kutayarisha mikutano katika lugha yetu ya asili na pia katika Kireno.” Mara kwa mara wengine huhudhuria mikutano inayofanywa katika lugha yao ya asili. Isitoshe, ni muhimu kupumzika vya kutosha.—Marko 6:31.

Kuhesabu Gharama

Ikiwa unafikiria kuhamia kutaniko ambalo linatumia lugha tofauti na yako, unapaswa kwanza kuhesabu gharama. (Luka 14:28) Kuhusiana na hilo, jambo muhimu la kufikiria ni hali yako ya kiroho na uhusiano wako pamoja na Yehova. Sali kuhusu hali yako. Fikiria mwenzi wako wa ndoa na watoto wako. Jiulize hivi, ‘Je, hali yangu na nguvu zangu za kiroho na za kihisia zinaniruhusu kuanza mradi wa muda mrefu kama huo?’ Ni jambo la hekima kufanya mambo ambayo yatakufaidi wewe na familia yako kiroho. Popote unapotumikia ukiwa mhubiri wa Ufalme, utakuwa na mengi ya kufanya na utapata shangwe nyingi.

Kuna thawabu kubwa kwa wale wanaoweza kutumika katika kutaniko la lugha ya kigeni. Barbara, ambaye alihamia kutaniko la Kihispania pamoja na mume wake, anasema hivi: “Hilo ni mojawapo ya mambo ambayo yameniletea furaha zaidi maishani. Ni kama ninajifunza tena kweli ya Biblia. Ninathamini sana nafasi hiyo, hasa kwa kuwa hatuwezi kuwa wamishonari katika nchi nyingine.”

Ulimwenguni pote, maelfu ya watu wa kawaida wa kila umri wanajitahidi kujifunza lugha nyingine ili kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema. Ikiwa wewe ni miongoni mwao, endelea kuonyesha nia hiyo nzuri na mtazamo unaofaa. Zaidi ya yote, mtumaini Yehova ili abariki jitihada zako.—2 Wakorintho 4:7.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kufundishwa lugha na mwalimu mwenye ustadi humfanya mtu ajifunze haraka zaidi na kwa urahisi zaidi

[Picha katika ukurasa wa 20]

Haifai kuhatarisha afya yako ya kiroho unapojifunza lugha ya kigeni

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki