Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 11/09 kur. 3-9
  • Kuwahubiria Watu Wanaozungumza Lugha ya Kigeni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwahubiria Watu Wanaozungumza Lugha ya Kigeni
  • Huduma ya Ufalme—2009
  • Habari Zinazolingana
  • Mwenye Nyumba Anapozungumza Lugha ya Kigeni
    Huduma Yetu ya Ufalme—2008
  • Kuonyesha Hali ya Kutopendelea Katika Huduma Yetu
    Huduma Yetu ya Ufalme—1993
  • Namna Lugha Moja Itakavyoleta Umoja kwa Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kuboresha Ustadi Wetu Katika Huduma—Kumhubiria Mtu Anayezungumza Lugha Nyingine
    Huduma Yetu ya Ufalme—2015
Pata Habari Zaidi
Huduma ya Ufalme—2009
km 11/09 kur. 3-9

Kuwahubiria Watu Wanaozungumza Lugha ya Kigeni

1. Tuna fursa ya kufanya nini tunapohubiri katika maeneo tuliyogawiwa?

1 Yesu Kristo alitabiri kwamba habari njema ingehubiriwa duniani kote “ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” Kila mhudumu anayeshiriki kazi ya kuhubiri na kufundisha anaelewa vizuri maneno hayo. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Tunapohubiri na kufanya wanafunzi, huenda tukawapata watu wa mataifa mbalimbali ambao wanazungumza lugha tofauti na yetu. Watu hawa pia wanahitaji kusikia ujumbe wa Ufalme na kuchukua msimamo imara kwa ajili ya kweli kabla siku ya Yehova yenye kuogopesha haijafika. (Mal. 3:18) Tunaweza kufanikiwaje kuwahubiria watu wanaozungumza lugha ya kigeni katika eneo letu?

2. Tunamwiga Yehova kwa njia gani tunapoongea na watu wanaozungumza lugha ya kigeni?

2 Uwe na Maoni Kama ya Yehova Kuwahusu Watu Wanaozungumza Lugha ya Kigeni: Ili kuwaonyesha watu wote katika eneo kwamba tunawapenda jinsi Yehova anavyowapenda, ni lazima tuwe na tamaa kubwa ya kuwasaidia wapate ujuzi sahihi kumhusu Mungu wa kweli, hata wawe wanazungumza lugha gani. (Zab. 83:18; Mdo. 10:34, 35) Ingawa tunawahubiria hasa watu wanaozungumza lugha ya kutaniko letu, ni lazima pia tufikirie mahitaji ya wale wanaozungumza lugha ya kigeni na kutafuta njia za kuwahubiria kuhusu Ufalme wa Mungu. Kuwapuuza watu wanaozungumza lugha ya kigeni ni kinyume na kusudi la Yehova la kuwahubiria watu wa mataifa yote. Hivyo basi, tunawezaje kuwasaidia watu wanaozungumza lugha ya kigeni?

3. Tumeandaliwa kijitabu gani kizuri, na tunaweza kujitayarishaje kukitumia?

3 Tumia Good News for People of All Nations: Kijitabu hiki kimekusudiwa kutumiwa tunapokutana na watu wanaozungumza lugha ya kigeni. Beba kijitabu hiki nyakati zote, pata kukijua vizuri, na uwe tayari kukitumia. Ili uweze kupata haraka lugha unayotaka, tia alama lugha mbalimbali za kigeni zinazozungumzwa katika eneo lenu. Ikiwa kuna vitabu katika lugha hizo, ingefaa kuchukua kadhaa ili kumwachia mtu baada ya kusoma ujumbe katika kijitabu hiki.

4. Kijitabu Nations kinaweza kutumiwaje katika huduma?

4 Ukikutana na mtu katika huduma ya shambani anayezungumza lugha ya kigeni na hujui anazungumza lugha ipi, anza kwa kumwonyesha jalada la kijitabu hicho. Fungua upande wa ndani wa jalada ambapo kuna ramani ya ulimwengu. Kisha, mwonyeshe mwenye nyumba kwa ishara unaishi wapi, na kwamba ungependa kujua nchi yake na lugha anayozungumza. Ukishajua lugha anayozungumza, tazama sehemu ya yaliyomo na ufungue ukurasa ambapo lugha yake inapatikana, kisha umwonyeshe sentensi ambayo imechapwa kwa herufi nzito upande wa juu wa ukurasa. Mwonyeshe kwa ishara kwamba ungependa asome ujumbe ulio kwenye ukurasa huo. Anapomaliza kusoma, mpe trakti katika lugha yake au umwonyeshe sentensi yenye rangi ya kijivu, ambayo inasema uko tayari kurudi na kumletea kitabu cha lugha yake. Mwonyeshe maneno “jina langu” yaliyochapwa kwa herufi nzito, na utamke jina lako waziwazi. Halafu umwonyeshe maneno “jina lako” yaliyochapwa kwa herufi nzito, na ungoje jibu lake. Fanya mipango hususa ya kurudi.

5. Tunapaswa kuchukua hatua gani ili kuwashughulikia ifaavyo watu wenye kupendezwa wanaozungumza lugha ya kigeni?

5 Mipango ya Kurudi: Tunapaswa kujitahidi kuwatembelea wale wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme, hata wawe wanazungumza lugha gani. Tunapotambua kwamba mtu anapendezwa kumjua Mungu na Neno lake, Biblia, tunapaswa kujaza fomu Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43), kisha tumpe mwandishi wa kutaniko fomu hiyo bila kukawia. Mwandishi anapaswa kuituma kwenye ofisi ya tawi ili mtu huyo mwenye kupendezwa atembelewe na mhubiri anayezungumza lugha yake. Ofisi ya tawi itatuma fomu hiyo kwenye kutaniko au kikundi kinachozungumza lugha ya mtu huyo. Fomu hiyo inapofika, mtu huyo anapaswa kutembelewa mara moja. Mwandishi anayepokea fomu hiyo kutoka kwenye ofisi ya tawi anaweza kumpa mwangalizi wa utumishi nakala moja ya fomu hiyo ili apate kujua itikio la watu ambao wanazungumza lugha fulani ya kigeni. Fomu hiyo inapaswa kutumwa tu mtu anapoonyesha anapendezwa kikweli.

6. Tunapompata mtu mwenye kupendezwa anayezungumza lugha ya kigeni, tuna jukumu gani?

6 Kuanzia wakati fomu ya S-43 inapotumwa, hadi wakati mtu mwenye kupendezwa anapotembelewa na mhubiri anayezungumza lugha yake, huenda muda fulani ukapita. Kwa hiyo, ili kuendelea kumsaidia mtu anayependezwa, mhubiri ambaye alituma fomu ya S-43 anaweza kuendelea kuzungumza na mtu huyo hadi wakati atakapotembelewa na mhubiri anayezungumza lugha yake. Katika visa fulani, hata anaweza kuongoza funzo la Biblia na mtu huyo mwenye kupendezwa. Lakini, katika kipindi hicho, mhubiri huyu anaweza kupataje vitabu vya lugha ya mwenye kupendezwa?

7. Kuna maandalizi gani ya kupata vitabu katika lugha ya watu ambao tunakutana nao?

7 Vitabu vya Lugha za Kigeni: Makutaniko hayapaswi kuweka vitabu vingi vya lugha nyingine. Lakini, mwangalizi wa utumishi akitambua kwamba kuna watu wa lugha fulani ambao wameanza kupendezwa na kweli, anaweza kuweka kiasi kidogo cha vitabu vya lugha hiyo kwa ajili ya wahubiri. Ikiwa kutaniko halina vitabu hivyo, linaweza kuviagiza. Huenda ikachukua muda kabla havijafika, kwa hiyo, kutaniko linaweza kuchapa nakala za vitabu hivyo kutoka kwenye www.watchtower.org. Kuna vitabu vingi katika mamia ya lugha kwenye Intaneti, na wahubiri au wenye kupendezwa wanaweza kuvipata hapo. Hapana shaka kwamba maandalizi haya yanafaa tunapowasaidia watu wanaozungumza lugha ya kigeni waendelee kupendezwa na kweli.

8. Kutaniko lina jukumu gani kuhusiana na kuwasaidia watu wanaopendezwa na kweli ambao wanazungumza lugha ya kigeni?

8 Jukumu la Kutaniko: Huenda katika maeneo fulani kuna watu kadhaa wenye kupendezwa wanaozungumza lugha ya kigeni, lakini hakuna kutaniko la lugha hiyo lililo karibu. Kwa hiyo, watu hao wanapaswa kualikwa wahudhurie mikutano katika kutaniko lenu. Ndugu wanapowakaribisha kwa uchangamfu na kuwaonyesha kwamba wanawajali, watu hao wanaweza kutiwa moyo waendelee kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Mwanzoni, huenda ikawa vigumu kuchangamana nao kwa sababu ya lugha na utamaduni wao; lakini upendo wa Kikristo kati ya Mashahidi wa Yehova duniani kote hauwezi kuzuiwa na chochote. (Sef. 3:9; Yoh. 13:35) Je, unazungumza lugha fulani ya kigeni kwa ufasaha? Ikiwa ndivyo na uko tayari kuwatembelea watu wanaozungumza lugha hiyo, tafadhali mjulishe mwandishi wa kutaniko lenu ili awasiliane na ofisi ya tawi. Jambo hilo litasaidia ofisi ya tawi inapotafuta mhubiri wa kumsaidia mtu mwenye kupendezwa.

9. Ni wakati gani huenda darasa la lugha ya kigeni likaanzishwa, na ni utaratibu gani unaofuatwa?

9 Kujifunza Lugha: Unapowasaidia watu wanaozungumza lugha nyingine, ni vema kuwatia moyo waanze kuhudhuria mikutano katika kutaniko la lugha yao ikiwa inawezekana kufanya hivyo. Hata hivyo, ikiwa haiwezekani, wahubiri fulani wanaweza kuamua kujifunza lugha hiyo, na hivyo kuwasaidia wenye kupendezwa. Ikiwa hakuna kutaniko karibu, na ikiwa idadi ya wenyeji au wahamiaji wanaozungumza lugha hiyo ni kubwa vya kutosha, ofisi ya tawi inaweza kuamua kwamba kuna uhitaji wa darasa la kufundisha lugha hiyo. Ikiamuliwa kwamba darasa la lugha hiyo litaanzishwa, ofisi ya tawi inaweza kuyaeleza makutaniko yaliyo karibu kuhusu uhitaji wa kuwa na darasa hilo, na kufanya mpango ili tangazo litolewe kulihusu. Wale wanaotuma ombi la kujiunga na darasa hilo, wanapaswa kuwa na lengo la kujiunga na kikundi au kutaniko la lugha hiyo ili kuwasaidia watu wanaoizungumza katika eneo lao.

10. Kikundi cha lugha ya kigeni kinaweza kuanzishwa lini, na jambo hilo linaamuliwaje?

10 Kuanzisha Kikundi: Ili kikundi cha lugha fulani kianzishwe, kuna matakwa manne yanayopaswa kutimizwa. (1) Lazima kuwe na watu wengi vya kutosha wenye kupendezwa ambao wanazungumza lugha hiyo. (2) Lazima kuwe na wahubiri kadhaa wanaojua au wanaojifunza lugha hiyo. (3) Lazima kuwe na mzee au mtumishi wa huduma anayestahili, ambaye anaweza kuongoza angalau mkutano mmoja kila juma katika lugha hiyo. (4) Baraza fulani la wazee linapaswa kuwa tayari kutegemeza kikundi hicho. Matakwa hayo yanapotimizwa kwa kadiri inayofaa, lile baraza la wazee la kutaniko linalotegemeza kikundi cha lugha ya kigeni, litaiandikia ofisi ya tawi barua kukihusu na kuomba kitambuliwe rasmi. (Ona kitabu Tengenezo, uku. 106-107.) Mzee anayeongoza kikundi hicho anaweza kuitwa “mwangalizi wa kikundi,” naye mtumishi wa huduma anaweza kuitwa “mtumishi wa kikundi.” Ndugu hao wana jukumu la kusimamia kikundi hicho.

11. Kwa nini ni pendeleo kubwa kuwahubiria watu wanaozungumza lugha ya kigeni katika eneo letu?

11 Kuwahubiria watu wanaozungumza lugha ya kigeni katika eneo letu ni sehemu muhimu ya kampeni ya kuhubiri duniani kote, iliyoanzishwa na Yesu Kristo, aliye Kielelezo chetu. Na tufanye sehemu yetu kwa bidii na kuona jinsi Yehova anavyoendelea kuyatikisa mataifa na kuwaleta watu wenye kutamanika. (Hag. 2:7) Inaridhisha kama nini kushirikiana kikamili na wengine katika kazi hii! Yehova na abariki jitihada zetu za pamoja za kuwahubiria watu wanaozungumza lugha ya kigeni katika maeneo yetu, huku sikuzote tukikumbuka kwamba licha ya vizuizi vya lugha, Mungu anaweza kufanikisha kazi hii!—1 Kor. 3:6-9.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki