Namna Lugha Moja Itakavyoleta Umoja kwa Wanadamu
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1, 2. Ni hali gani iliyopo kati ya mataifa yote juu ya umoja, na ni nini mojawapo la mambo yanayolaumiwa kama kizuizi kikubwa cha umoja?
SASA hivi kuna ushindani mwingi wa kitaifa na mashaka. Wasafiri wanajua sana sheria nyingi mno za fanya hivi na hivi zinazopasa upataji wa paspoti, hati za kusafiria na uchunguzi wa forodhani (customs). Ugawaji wa chakula na mambo mengine yanayotakiwa sana unazuiwa na ushuru unaotozwa juu ya bidhaa zinazotoka katika nchi za kigeni na vizuizi vya biashara, na uchumi na ufanisi wa kila nchi unapaswa vibaya sana.
2 Kizuizi cha lugha ndilo mojawapo la mambo yanayolaumiwa kwa kukosa ushirikiano wa kati ya mataifa. Wengine wameunga mkono wazo la kwamba kuwa na lugha moja ya mataifa yote ndiyo mojawapo ya njia za kuondolea magumu mengi. Ni kweli kwamba kuwasiliana zaidi kwa njia ya lugha moja yenye kutumiwa na watu wengi kungeleta faida fulani. Kungeelekea kuondoa kutofahamiana fulani, na kukawia na migogoro mingi ingeondolewa.
3-6. (a) Je! lugha moja peke yake ingekuwa ufumbuzi? (b) Ni kwa sababu gani Mungu aliwapa wanadamu lugha mbalimbali?
3 Lakini je! lugha moja peke yake ingekuwa ufumbuzi? Sivyo, kunahitajiwa zaidi. Kwa kweli, Mungu mwenyewe ndiye aliyefanyiza tofauti za lugha wakati watu wote walipokuwa wakisema lugha moja. Naye alifanya hivyo kwa faida ya jamii ya wanadamu. Hili likoje?
4 Hii ilikuwa kwa sababu, kufuata gharika ya dunia yote katika siku za Nuhu, watu waliasi. Mungu alikuwa amewaamuru watu waenee ili, wakati watu wangeongezeka duniani, waieneze ibada ya kweli katika dunia yote. Ile lugha moja ambayo walikuwa wakisema ingalikuwa faida kubwa, nguvu yenye kuunganisha.—Mwa. 9:1.
5 Lakini Nimrodi kilembwe (kijukuu) cha Nuhu hakuikubali enzi kuu ya Mungu kama Nuhu. Kwa kutaka kuwatawala watu wote duniani wakati huo, Nimrodi aliona kwamba ingefaa kusudi lake ikiwa angewakusanya watu katika eneo moja. Basi aliwatia moyo watu katika uasi wao wajenge mnara wa kidini, ili awatiishe pamoja chini ya utawala wake.—Mwa. 11:1-6.
6 Njia ya Mungu ya kuichafua lugha yao iliwalinda wanadamu na utawala wenye kuonea. Yehova akasema juu ya hili: “Tazama, watu hawa ni taifa moja, na lugha yao ni moja; na haya ndiyo wanayoanza kuyafanya, wala sasa hawatazuiliwa neno wanalokusudia kulifanya.” Hivyo kwa mwujiza Mungu aliwafanya waziseme lugha mpya.—Mwa. 11:5-8.
7. Tendo la Mungu katika kuichafua lugha yao lilitokeza nini kwa faida ya wanadamu?
7 Kizuizi cha lugha ambacho Mungu aliweka kimeendelea kwa muda wapata miaka 4,000. Kimezuia mwungano mkubwa—ndiyo, mwungano wa pote chini ya dini moja ya uongo, dini iliyoanza katika Babeli. Kuwa na lugha moja inayotumiwa na watu wengi kunawasaidia watu wabaya washirikiane kwa vyepesi zaidi katika jambo baya.
8. Ni nini kilicho cha lazima zaidi kwa umoja kuliko lugha moja?
8 Lakini jambo jingine lenye maana lapaswa liangaliwe hapa. Kutokana na yaliyotukia, ni wazi kwamba wakati watu wote waliposema lugha moja hii haikuleta amani. Leo watu wanaosema lugha moja hawapatani sikuzote. Hasha, ijapokuwa inafaa kwa umoja wa tendo lugha moja kwa lazima haileti umoja wa moyo na akili, wenye furaha. Wakati lugha moja haijaweza kutumiwa katika njia yenye kufaidi sana, ingewapasa watu wote waungane katika dini moja, ibada safi ya Mungu mmoja wa kweli, kulingana na njia iliyowekwa na Mungu katika Neno lake. Je! hili laweza kutokea? Je! litatokea?
IBADA MOJA YA MWUNGANO YATOKEA KWANZA
9-11. “Lugha iliyo safi” inayosemwa katika Sefania 3:8, 9 ni nini, na kwa sababu gani si lugha ile ile inayomaanishwa?
9 Ibada moja safi chini ya Mungu mmoja wa kweli yaweza kuwako, na itakuwako. Akisema kwa habari ya wakati wa sasa, Mungu anasema hivi mbele ya kuonyesha ghadhabu yake juu ya falme za ulimwengu: “Maana hapo ndipo nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la [Yehova], wamtumikie kwa nia moja.”—Sef. 3:8, 9.
10 “Lugha iliyo safi” inayosemwa hapa isingeweza kuwa lugha ile ile, kama vile Kiingereza, Kispania, Kirusi, Kifaransa, na vivyo hivyo. Hatuwezi kusema kwamba ni lazima yo yote ya lugha hizi iondolewe kwa sababu si safi. Lugha ya kwanza aliyopewa Adamu ilikuwa njema. (Mwa. 1:31) Na wakati uliofuata, wakati Mungu alipowapa watu lugha mpya kwa mwujiza katika Babeli, hizi hazikuwa lugha chafu, hazikuwa mbaya. Zilitoka kwa Mungu, ambaye zawadi zake ni njema sikuzote, nazo zimetumikia kusudi jema.—Yak. 1:17.
11 Hivyo namna mpya ya usemi wa kibinadamu isingeweza kuwa “lugha iliyo safi” ambayo nabii alisema. “Lugha iliyo safi” ni kweli ya Mungu kutoka katika Biblia. Yaweza kusemwa sasa na kutumiwa kwa maisha ya mtu bila kujali yeye anasema lugha gani. Inafanyiza mageuzi, si katika maneno peke yake, bali vile vile na katika mambo ambayo mtu anafikiria na kuyazungumza. Usemi wake unasafishwa na unakuwa wenye kujenga, wenye kuendeleza hali bora pamoja na wengine.
SERIKALI INAYOENDELEZA KWELI
12. Ufalme utahakikishaje kwamba “lugha iliyo safi” ya kweli itasemwa duniani?
12 Wakati wa utawala wa miaka elfu wa ufalme wa Mungu ulimwengu mzima—ndiyo, ulimwengu wote—utaisema hii “lugha iliyo safi.” Watakaokuwa watawala katika serikali hii ni Yesu Kristo, Mfalme Mkuu wa serikali hiyo na ambaye ni Kuhani Mkuu, na 144,000 wafalme washirika na makuhani wadogo, watakaotawala kutoka mbinguni. Hawa wote walisema hii “lugha iliyo safi” ya kweli wakati walipokuwa duniani. Kristo mwenyewe alikuja duniani ili ‘aishuhudie kweli.’ (Yohana 18:37) Na kwa habari ya 144,000 wafalme washirika wake, imeandikwa hivi: “Katika vinywa vyao haukuonekana uongo.” (Ufu. 14:5; Efe. 4:25) Katika kutawala kwa miaka elfu watahakikisha kwamba ile “lugha iliyo safi” imeendelezwa na wakaaji wa dunia. Kama vile mtunga zaburi alivyotabiri: “Ukweli wenyewe utachipuka katika dunia, na haki yenyewe itachungulia kutoka mbingu zenyewe.”—Zab. 85:11, NW; 2 Pet. 3:13.
13, 14. (a) Je! wafalme wa kimbinguni wataendelea kuzisema lugha zao za zamani walizozaliwa nazo? (b) Je! watasahau lugha walizokuwa wakisema walipokuwa duniani?
13 Wafalme hawa wa kimbinguni “wamenunuliwa katika wanadamu,” kutoka mataifa yote. (Ufu. 14:4; Mt. 28:19) Je! huko mbinguni, watazisema lugha zao za zamani walizozaliwa nazo? Lisingekuwa jambo la busara kufikiri hivyo. Hakuna shaka kwamba wote wale waliomo mbinguni watasema lugha moja, zawadi ya lugha hii ikipewa kwao katika miili yao mipya ya kiroho wakati wa kufufuka kwao kutoka kwa wafu. Mtume Paulo aliandika juu ya “lugha za wanadamu na za malaika,” nasi twasoma juu ya mazungumzo kati ya Mungu na malaika.—1 Kor. 13:1; 1 Fal. 22:19-22; Ayubu 1:6-12; 2:1-6.
14 Hii haina maana ya kwamba lugha yao ya zamani ya kidunia itafutika katika akili zao. Sivyo, kwa maana kwa lugha yao ya zamani wataweza kujijua wenyewe kama wakiwa watu wale wale. Lakini katika ufufuo wao wa kimbinguni hawatahitaji watafsiri ili wasemezane wao kwa wao. Watasema lugha ya Bwana Yesu Kristo, naye atasema lugha ya Baba yake wa kimbinguni, Yehova Mungu.
15, 16. Je! ni jambo la akili kufikiri kwamba watu duniani wataendelea kusema kulingana na jamii tofauti za lugha zilizopo wakati huu?
15 Basi, ni lugha gani itakayosemwa na wakaaji wa dunia wakati wa utawala huo wa ufalme wa mbinguni? Je! wale watakaokuwamo duniani ambao lugha yao ya kuzaliwa ni Kigiriki watatawaliwa na mmoja wa wafalme wa kimbinguni ambaye, alipokuwa duniani, alisema Kigiriki, na katika eneo jingine la wasemao Kirusi watawaliwe na mrithi wa Ufalme asemaye Kirusi, na katika eneo jingine Mchina, na vivyo hivyo, kulingana na jamii mbalimbali za lugha? Kwa kuwa lugha zinafanyiza kizuizi cha kusikilizana na vile vile cha umoja ulio kamili zaidi, je! hivi ndivyo itakavyokuwa?
16 Katika hili, ni lazima isemwe kwamba Biblia haionyeshi migawo ya madaraka ya kifalme ambayo Yesu Kristo atawagawia wafalme wake wadogo, 144,000, lakini lingekuwa jambo lisilopatana kabisa na kufikiri kwa akili kudhani kwamba Ufalme ungeacha kizuizi cha kusikilizana katika taratibu mpya ya Mungu yenye haki—kizuizi alichofanyizia watu wenye kuasi, ili awalinde na kuwazuia wasiwe na umoja kamili katika utendaji mbaya.
TAIFA MOJA, LUGHA MOJA
17. Ni kwa sababu gani Mungu alimpa Adamu zawadi ya lugha?
17 Tunapolichunguza kusudi la kwanza la Mungu juu ya lugha ya wanadamu, inakuwa wazi kwamba yeye atafanya mpango ili lugha moja tu iwe ikisemwa wakati wa utawala wa Kristo wa miaka elfu. Mungu alitaka wanadamu waongee. Yeye mwenyewe alisema kwa Adamu, na akamfanyia Adamu mpango aseme kwake. (Mwa. 2:15-23) Tena, yeye alimpa mwanadamu lugha kama chombo cha maana cha mawazo. Adamu angeweza kuongeza lugha wakati angejifunza mambo mapya au wakati ambapo angehitaji kuongeza maneno ya lugha (vocabulary). Adamu angeweza kuijazia nafasi ya kiroho ambayo Mungu alimpa, akijifunza juu ya Mungu na kujisemea mwenyewe sana.
18, 19. Ilikuwa lugha gani ya kwanza aliyopewa mtu wa kwanza? Kwa sababu gani wajibu hivyo?
18 Ilikuwa lugha gani moja ya kwanza? Bila shaka ilikuwa ile ambayo baadaye (nyuma) ikaja kuitwa Kiebrania. Sababu gani twaweza kusema hivi? Basi, wakati mchafuko wa lugha ulipotukia katika Mnara wa Babeli, si wote waliopatwa. Nuhu hakuwa ameasi. Yeye aliikubali enzi kuu ya Mungu, asijifanye mfalme, kama alivyojifanya Nimrodi. Shemu, mwana wa Nuhu alikuwa amebarikiwa kwa unabii, inaonekana aliendelea kuwa na Nuhu na ibada ya kweli. (Mwa. 9:26, 27) Maandishi ya Biblia yanaonyesha kwamba ibada ya kweli iliendeshwa na watu wa Shemu, zaidi kupitia kwa mtu mwenye imani mwenye kujulikana sana, Ibrahimu. Ibrahimu (Abramu) aliitwa Mwebrania.—Mwa. 14:13.
19 Baadaye (nyumaye), Musa, mzao wa Ibrahimu, aliandika habari yake (Mwanzo mpaka Kumbukumbu la Torati) katika lugha iitwayo Kiebrania. Labda kulikuwako mageuzi machache katika lugha ya Musa kutoka kwa lugha ile ya kwanza aliyosema Adamu. Kwa sababu gani? Kwa sababu wakati huo wanadamu walijifurahisha maisha marefu sana, maisha zao mara nyingi zikiendelea mpaka katika vizazi vya tano au vya sita. Kwa hiyo, lugha ingaliweza kupitishwa katika mistari ya kibinadamu mitano tu kati ya Adamu na Musa, yaani, Methusela, Shemu, Isaka, Lawi, Amramu. (Mwa. 5:3-32; 11:10-32; 21:5; 25:26; 29:34; Kut. 6:16, 18, 20) Bila shaka, baada ya uhamisho wa Israeli Babeli katika mwaka wa 607 B.C.E., na mpaka nyakati zetu za kisasa, lugha ya Kiebrania imevutwa na lugha nyingine. Vile vile, namna jina la Mungu lilivyokuwa likitamkwa katika siku za Musa haijulikani sasa. Lakini kwa vyepesi Mungu aweza kuirudisha lugha iliyo safi ili wale watakaoishi katika Taratibu Mpya waiseme sawasawa na kwa ufasaha.
20. Matokeo yatakuwa nini kwa wakaaji wa dunia kwa kusema lugha moja?
20 Kusema huku kwa lugha yenyewe kutakuwa ndicho kitimizo cha umoja unaofanyizwa na “lugha iliyo safi” ya kweli—kwa uzuri sana! Vizuizi vyote vya kidini, vya kitaifa, vya kijamii na vya kikabila havitakuwapo, na, isitoshe, kwa kuwa na namna moja ya maneno ya lugha wote wataweza kueleza sana mawazo yao na kufahamiwa vizuri. Ebu fikiri tena utakavyoweza kujisomea mwenyewe maana ya yale ambayo manabii wa Kiebrania waliandika—katika lugha yao wenyewe! Wengi watakaofufuliwa ambao zamani hawakumjua Mungu wataona kwamba Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanatoa masimulizi ya kweli juu ya historia ya kibinadamu mpaka siku za nabii Malaki. Ndipo wenye mioyo minyofu watakapoweza kusema, kama alivyosema mtume Paulo: “Mwacheni Mungu aonekane kuwa wa kweli, ijapokuwa kila mwanadamu aonekane mwongo.”—Rum. 3:4, NW.
JIFUNZE “LUGHA ILIYO SAFI” YA KWELI SASA
21, 22. Onyesha kwamba ye yote anayetaka aweza kujifunza “lugha iliyo safi” ya kweli sasa.
21 Kuishi katika ulimwengu huo kutakuwa furaha kweli kweli. Unaweza kuwa na mwonjo wake sasa hivi. Kwa maana takwa kubwa laweza kutimizwa sasa. Takwa hilo ni kujifunza ile “lugha iliyo safi” ya kweli kutoka katika Biblia. Hii “lugha iliyo safi” inaondoa vizuizi vyote vya kijamii, kikabila na kitaifa. “Lugha” hii ndiyo ambayo mamia ya maelfu ya watu wanajifunza na kuisema leo, nao wako katika umoja, kama nabii Isaya alivyoongozwa na roho ya Mungu kutabiri:
22 “Na itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya [Yehova ya ibada yake] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; . . . nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isa. 2:2-4.
23-28. Ni mpango gani ambao Mungu amewafanyia watu ili wajifunze “lugha iliyo safi,” na je! umekuwa wenye matokeo?
23 Serikali ya Ufalme itafanyiza usemi wa lugha moja duniani pote wakati wa utawala wa Kristo wa miaka elfu, lakini sasa hivi “lugha iliyo safi” yapatikana kwako. Mashahidi wa Yehova wanakufikia wewe, si kuja kuendeleza mawazo yao wenyewe, bali wanakuja kama mabalozi na wajumbe wa serikali hiyo ya Ufalme. Kwamba kweli Mungu anaitegemeza kazi yao, na kwamba “lugha iliyo safi” ya Biblia ina nguvu kubwa ndiyo mambo ya hakika yanayoonekana. Namna gani?
24 Katika maisha zilizogeuzwa, zilizosafishwa na umoja wa zaidi ya watu 1,600,000 kutoka katika lugha zote. Umoja wao, utulivu na kupendana wao kwa wao vimewastaajabisha watazamaji. Tunda la kuzifuata kwao njia za Biblia linaonyeshwa katika maelezo yaliyomo katika gazeti Detroit News la Juni 21, 1973, kwa habari ya kusanyiko la mashahidi wa Yehova lililofanywa katika Tiger Stadium ya Detroit:
25 “Ndiyo . . . namna ya kusanyiko ambalo utawaona mapolisi wakitanga-tanga tu, wakijua hawana jambo jingine la kufanya, na kutoka kwenda kufanya mambo yaliyo ya maana zaidi.”
26 Na katika kusanyiko la Düsseldorf, Ujeremani, ambapo wajumbe wengi kutoka mataifa mengi walipokusanyika, gazeti Süddeutsche Zeitung la Julai 28, 1973, lilieleza hivi:
27 “Tangu Jumatano karibu watu 60,000 wamekusanyika—ndilo kusanyiko kubwa kuliko yote ambayo yamepata kufanywa katika Düsseldorf, mji wa maonyesho. Nao ni mkutano wa watu wengi unaofuata sheria zake wenyewe. Hatujapata kuona watu wengi mno wakikutana pamoja ambao ni wenye utaratibu sana, wenye adili sana, wenye adabu sana kama hawa walivyo.”
28 Mashahidi wa Yehova hawautumii upendo wao kwa wenyewe kwa wenyewe tu. Wanataka sana kuwasaidia wote wanaotaka kuishi chini ya utawala wenye haki wa ufalme wa Mungu wa Kimasihi, ambao chini yake kila kizuizi cha umoja kitaondolewa kabisa. Ikiwa wataka ujifunze “lugha iliyo safi” waweza kufanya hivyo, kwa msaada wao.—Ufu. 22:17.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.