Mwenye Nyumba Anapozungumza Lugha ya Kigeni
1. Kwa nini kuna uhitaji unaoongezeka wa kushirikiana wakati eneo linapohubiriwa?
1 Wahubiri wa Ufalme ulimwenguni pote wanazidi kuwapata watu wenye kupendezwa ambao wanazungumza lugha nyingine tofauti na ile inayotumiwa na kutaniko. Ili kuwasaidia kiroho watu hao, ofisi nyingi za tawi zinaona ni muhimu kuunda vikundi na makutaniko ya lugha za kigeni. Kwa kuwa huenda watu wakawa wanazungumza lugha nyingi katika eneo moja, makutaniko kadhaa ya lugha tofauti yanaweza kuhubiri katika eneo moja. Makutaniko yanaweza kushirikianaje ili kuhakikisha kwamba kazi ya kuhubiri inatimizwa kwa utaratibu?—1 Kor. 14:33.
2. Tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunawezaje kushirikiana na kikundi au kutaniko la lugha nyingine katika eneo letu?
2 Ushirikiano Mzuri: Mhubiri anapohubiri barabarani au kwa njia isiyo rasmi, anapaswa kujihisi huru kumhubiria mtu yeyote, kutia ndani wale ambao huenda wanazungumza lugha nyingine, na anapaswa kumtolea mtu huyo vichapo katika lugha ambayo anapendelea kusoma. Hata hivyo, mhubiri anapohubiri nyumba kwa nyumba katika maeneo fulani ambayo yanahubiriwa pia na kikundi au kutaniko la lugha nyingine, kwa kawaida anapaswa kukazia fikira nyumba za wale ambao wanazungumza lugha inayotumiwa na kutaniko ambalo yeye anahudhuria. Makutaniko mbalimbali yanapohubiri katika eneo moja, ni muhimu sana kuwa na rekodi nzuri ya utumishi ya eneo hilo. Waangalizi wa utumishi wanapaswa kuwasiliana na kupanga mambo kwa njia ambayo itayafaidi makutaniko yote. (Met. 11:14) Hata hivyo, ikiwa mhubiri amempata mtu anayezungumza lugha nyingine katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba na hakuna makutaniko ya lugha hiyo karibu, mhubiri huyo anapaswa kujitahidi kumhubiria na kuendelea kumsaidia mtu huyo anayependezwa.
3. Tunapaswa kutendaje tunapokutana na wahubiri wa kikundi au kutaniko lingine ambao wanahubiri katika eneo moja pamoja nasi?
3 Tunatimiza Kazi Moja: Mambo yanapaswa kushughulikiwaje wahubiri kutoka makutaniko mbalimbali wanapohubiri katika eneo moja siku ileile? Bila shaka, upendo wa Kikristo unapaswa kushinda tofauti zozote za lugha na wote wanapaswa kwanza kuhangaikia mahitaji ya watu wa eneo hilo. (Yoh. 13:34, 35) Kwa hiyo, wale wanaoongoza wataonyesha usawaziko na upendo kwa kuamua ikiwa kikundi kimoja kinapaswa kwenda kuhubiri kwa muda katika eneo lingine.—Yak. 3:17, 18.
4. Ni unabii gani ambao unatimizwa leo?
4 Biblia ilitabiri kwamba watu wa lugha mbalimbali wangesikia habari njema. (Ufu. 14:6, 7) Wote wanaohusika wanaposhirikiana kwa ukaribu, wahubiri kutoka vikundi au makutaniko ya lugha mbalimbali wanaweza kuepuka kurudia nyumba zilizokuwa zimehubiriwa na wengine, na hivyo wapya wengi watafikiwa na habari njema, kutia ndani wale wanaozungumza lugha nyingine.—Efe. 4:16.