MAISHA YA MKRISTO
Kushirikiana Kuhubiri Katika Eneo Lenye Lugha Mbalimbali
Mara nyingi watu huitikia kwa utayari zaidi wanaposikia ujumbe wa Ufalme katika lugha yao ya asili. Huenda hiyo ndiyo sababu katika Pentekoste ya 33 W.K., Yehova alipanga mambo ili “Wayahudi waliomwogopa Mungu kutoka kila taifa lililo chini ya mbingu” wasikie habari njema katika “lugha [yao] ya asili,” ingawa inaelekea walizungumza lugha nyingine kama vile Kiebrania au Kigiriki. (Mdo 2:5, 8) Katika maeneo yenye lugha mbalimbali leo, makutaniko yanayoongoza mikutano katika lugha mbalimbali yanaweza kuwa yakihubiri kwenye eneo lilelile. Wahubiri katika makutaniko hayo wanawezaje kushirikiana ili kumtolea kila mtu ushahidi huku wakiepuka kuwaudhi wenye nyumba kwa kuhubiri mara nyingi katika eneo moja au kurudia kuhubiri katika eneo lililohubiriwa siku chache zilizopita?
Zungumzeni (Met 15:22): Waangalizi wa utumishi wanapaswa kuzungumza na kukubaliana kuhusu mfumo utakaowaridhisha wote wa kueneza habari njema. Ikiwa eneo lao ni dogo, makutaniko yanayohubiri katika lugha nyingine huenda wakataka msihubiri kwenye nyumba zilizo katika eneo la lugha yao. Lakini ikiwa hawawezi kumaliza eneo lao kwa ukawaida kwa sababu ya ukubwa, huenda wakawaomba mhubiri nyumba zote, kisha muwaeleze mnapopata mtu anayependezwa. (od 93 ¶37) Au huenda wakaomba kutaniko lenu liwasaidie kuwapata watu wanaozungumza lugha ya kutaniko lao ili anwani zao ziongezwe kwenye eneo lao. (km 7/12 5, sanduku) Kumbuka kwamba katika visa fulani, watu katika nyumba moja wanaweza kuwa wanazungumza lugha zaidi ya moja. Mipango ya kushughulikia eneo inapaswa kufuata sheria za kulinda taarifa zinazotumiwa.
Mshirikiane (Efe 4:16): Fuata kwa uangalifu mwongozo wowote unaopata kutoka kwa mwangalizi wako wa utumishi. Je, unaongoza funzo la Biblia na mtu anayependelea lugha tofauti na ile ya kutaniko lenu? Huenda anaweza kufanya maendeleo haraka zaidi ukimpa mtu wa kutaniko au kikundi jirani kinachozungumza lugha yake.
Jitayarishe (Met 15:28; 16:1): Ikiwa mwenye nyumba katika eneo lenu anazungumza lugha nyingine, jitahidi kumtangazia habari njema. Unaweza kujitayarisha kwa kufikiria lugha ambazo huenda ukakutana nazo na kupakua mapema Biblia na video za lugha hizo kwenye kifaa chako. Unaweza pia kutumia programu ya JW Lugha kujifunza salamu katika baadhi ya lugha.