Kuwalea Watoto Katika Ulimwengu Wenye Uendekevu
JE, UMEWAHI kumwona mtoto akimwomba mzazi amnunulie kifaa cha kuchezea ambacho mzazi hataki kununua? Au mtoto anayetaka kukimbia-kimbia na kucheza-cheza ingawa mzazi amemwambia atulie? Katika hali kama hizo, unaona kwamba mzazi anafanya jambo linalomfaa zaidi mtoto wake. Lakini, mara nyingi mwishowe mzazi anakubali ombi la mtoto wake. Kwa sababu ya kusumbuliwa sana mzazi huyo anabadili siyo yake kuwa ndiyo.
Inaonekana wazazi wengi wanaamini kwamba kuwa mzazi mzuri kunamaanisha kuwaruhusu watoto wafanye lolote wanalotaka. Kwa mfano, huko Marekani, watoto 750 wenye umri wa miaka 12 mpaka 17 walihojiwa. Walipoulizwa wanafanya nini wazazi wao wanapokataa maombi yao, karibu asilimia 60 ya watoto hao walisema kwamba wanaendelea kuomba. Asilimia 55 waligundua kwamba kwa kawaida mbinu hiyo inafanya kazi. Huenda wazazi wao wakahisi kwamba wanawaonyesha watoto upendo wanapowaruhusu wafanye wanachotaka. Lakini je, kweli huo ni upendo?
Fikiria methali hii ya zamani yenye hekima: “Mtu akimbembeleza mtumishi wake tangu ujanani, katika maisha yake ya baadaye hata atakuwa mtu asiye na shukrani.” (Methali 29:21) Ni kweli kwamba mtoto si mtumwa. Hata hivyo, je, hukubali kwamba kanuni hiyo inatumika katika kuwalea watoto? Kuwabembeleza watoto na kuwapa kitu chochote wanachotaka, kunaweza kuwafanya wawe watu wazima ‘wasio na shukrani,’ watundu, wenye kujitanguliza, na wasiothamini.
Kinyume chake, Biblia inawashauri wazazi hivi: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa.” (Methali 22:6) Wazazi wenye hekima wanafuata mwongozo huo. Wanaweka sheria zilizo wazi, zisizobadilika, na zenye usawaziko. Hawajidanganyi kwamba upendo unamaanisha kuendekeza; wala hawawapi watoto chochote wanachotaka eti kwa sababu wanalia, wanasumbua, au wanajitupa-tupa kwa hasira. Badala yake, wanakubaliana na maneno haya ya Yesu yenye hekima: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.” (Mathayo 5:37) Lakini kuwazoeza watoto kunatia ndani nini? Fikiria mfano mmoja.
“Kama Mishale Mkononi”
Kulingana na Biblia uhusiano wa mzazi na mtoto unazungumziwa kwa njia inayoonyesha kwamba mtoto anahitaji mwongozo wa mzazi. Zaburi 127:4, 5 inasema hivi: “Kama mishale mkononi mwa mwanamume mwenye nguvu, ndivyo walivyo wana wa ujanani. Mwenye furaha ni mwanamume ambaye amelijaza podo lake na hao.” Kwa hiyo, watoto wanafananishwa na mishale, na mzazi anafananishwa na shujaa mwenye nguvu. Kama vile mpiga-mishale anavyojua kwamba mishale yake haitapiga shabaha kimuujiza tu, ndivyo wazazi wenye upendo wanavyotambua kwamba daraka la kumlea mtoto halipaswi kufanywa ovyoovyo. Wanataka watoto wao wafikie “shabaha,” yaani, wawe na maisha yenye kuridhisha na yenye furaha wakiwa watu wazima wanaochukua wajibu wao kwa uzito. Wanataka watoto wao wafanye maamuzi mazuri, wawe na hekima, waepuke matatizo yasiyo ya lazima, na wafikie miradi inayofaa. Lakini jitihada zinahitajiwa.
Ni nini kinachohitajiwa ili mshale ufikie shabaha yake? Ni lazima utayarishwe kikamili, ulindwe, na kuelekezwa vizuri kwenye shabaha yake. Vivyo hivyo, watoto wanahitaji kutayarishwa, kulindwa, na kuelekezwa ili wawe watu wazima wenye mafanikio. Acheni tuchunguze mambo hayo matatu yanayohusu kuwalea watoto. Tutachunguza jambo moja baada ya lingine.
Kutayarisha Mshale Kikamili
Mishale iliyotumiwa na wapiga-mishale katika nyakati za Biblia ilitayarishwa kwa uangalifu sana. Mpini wake, ambao huenda ulitengenezwa kwa ubao mwepesi, ulichongwa kwa mkono na kunyooshwa kabisa. Ncha yake ilipaswa kuwa kali. Manyoya yalifungiliwa upande wa nyuma wa mpini ili mshale uwe na usawaziko unapokuwa hewani, na kuusaidia kuelekea upande unaofaa.
Wazazi wanataka watoto wao wawe kama mishale hiyo iliyonyooka, wawe wanyoofu na wasiokengeuka. Kwa hiyo, wazazi wenye hekima hawapuuzi makosa mazito ya watoto, badala yake wanawasaidia watoto wao kwa upendo kuyarekebisha. Jitihada nyingi kama hizo zinahitajika kwa kila mtoto kwa kuwa “ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.” (Methali 22:15) Hivyo, Biblia inawahimiza wazazi wawatie nidhamu watoto wao. (Waefeso 6:4) Kwa kweli, nidhamu ni ya maana sana katika kujenga na kunyoosha akili na utu wa mtoto.
Haishangazi kwamba Methali 13:24 inasema hivi: “Anayezuia fimbo yake anamchukia mwana wake, lakini anayempenda ni yule anayemwangalia kwa nidhamu.” Katika andiko hilo, fimbo ya nidhamu inawakilisha njia yoyote ile inayotumiwa kumrekebisha mtoto. Mzazi anapotoa nidhamu kwa upendo, lengo lake ni kurekebisha makosa ambayo, yakiachiliwa yatie mizizi, yanaweza kumletea mtoto huzuni kubwa atakapokuwa mtu mzima. Kwa kweli, mzazi anayekosa kumtia mtoto nidhamu anamchukia; kumtia nidhamu ni tendo la upendo.
Pia, mzazi mwenye upendo anamsaidia mtoto aelewe kwa nini sheria zinawekwa. Hivyo, nidhamu haitii ndani kutoa amri na adhabu tu, bali pia inatia ndani jambo muhimu zaidi, yaani, kumpa mtoto uelewaji. Biblia inasema hivi: “Mwana mwenye uelewaji anashika sheria.”—Methali 28:7.
Manyoya ambayo mpiga-mishale anashikamanisha na mishale yake yanaisaidia mishale inapopigwa kwa upinde iende kwa njia iliyonyooka. Kama manyoya hayo, mafundisho ya Biblia kutoka kwa Mwanzilishi wa familia yataendelea kukumbukwa na watoto hata wanapoondoka nyumbani, nayo yatawasaidia katika maisha yao yote. (Waefeso 3:14, 15) Lakini wazazi wanaweza kuhakikisha jinsi gani kwamba kwa kweli mafundisho hayo ‘yameshikamanishwa’ na watoto wao?
Ona shauri ambalo Mungu aliwapa wazazi Waisraeli katika siku za Musa: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Kwa hiyo, wazazi wanahitaji kufanya mambo mawili. Kwanza, wao wenyewe wanahitaji kujifunza na kufuata Neno la Mungu, na kuzipenda kikweli sheria za Mungu. (Zaburi 119:97) Kisha, wanaweza kutimiza sehemu ya pili ya andiko hilo, yaani, ‘kukazia’ sheria za Mungu kwa watoto wao. Hilo linamaanisha kukazia umuhimu wa sheria hizo ndani ya mioyo ya watoto wao kwa kufundisha vizuri na kwa kurudia-rudia.
Ni wazi kwamba kufundisha kanuni za Biblia au kutoa nidhamu kwa upendo ili kurekebisha makosa mazito ya watoto si mambo ya kizamani au yaliyopitwa na wakati. Hizo ni njia muhimu za kutayarisha “mishale” hiyo yenye thamani ili ifuate njia iliyonyooka bila kuyumbayumba kufikia utu uzima.
Kuulinda Mshale
Acheni turudi kwa mfano ulio katika Zaburi 127:4, 5. Kumbuka kwamba mpiga-mishale ‘alijaza podo lake’ na mishale yake. Mishale iliyotayarishwa ilihitaji kulindwa. Hivyo, mpiga-mishale aliiweka katika podo, ambamo haingeharibiwa kwa urahisi au kuvunjwa. Inapendeza kwamba unabii wa Biblia unasema Masihi alikuwa kama mshale ulionolewa ambao Baba yake ‘aliuficha katika podo lake.’ (Isaya 49:2) Kwa kweli, Yehova Mungu, Baba mwenye upendo usio na kifani, alimlinda Mwana wake mpendwa, Yesu, asipate madhara yoyote mpaka ulipofika wakati uliowekwa wa Masihi kuuawa kama ilivyotabiriwa. Mungu alimlinda Mwana wake hata wakati huo ili kifo kisimletee madhara ya kudumu. Alimwezesha kurudi mbinguni akiwa salama ili aishi milele.
Vivyo hivyo, wazazi wazuri wanajitahidi kuwalinda watoto wao kutokana na hatari za ulimwengu huu uliopotoka. Huenda wazazi wakawakataza watoto wao wasifanye mambo fulani ambayo yanaweza kuwahatarisha isivyo lazima. Kwa mfano, wazazi wenye hekima wanachukua kanuni hii kwa uzito: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Inaelekea kwamba kuwalinda watoto ili wasishirikiane na watu ambao hawaheshimu viwango vya maadili vya Biblia kutawazuia watoto wasifanye makosa mengi ambayo yanaweza kuwaletea matatizo maishani au hata kifo.
Huenda watoto wasithamini sikuzote ulinzi wa wazazi. Kwa kweli, huenda nyakati nyingine wakachukia ulinzi huo, kwa kuwa mara nyingi kuwalinda kunahusisha kuwakataza wasifanye mambo fulani. Mtungaji mwenye kuheshimika wa vitabu kuhusu kuwalea watoto anasema hivi: “Ingawa hawaonyeshi sikuzote kwamba wanathamini na huenda hawatakushukuru wakati huo, kwa kweli wanataka wazazi wawape ulinzi na mwongozo imara maishani. Sisi wazazi tunaweza kufanya hivyo kwa kuchukua mamlaka yetu kwa uzito na kuweka mipaka kuhusu tabia.”
Ndiyo, kuwalinda watoto kutokana na chochote kinachoweza kuharibu amani, maadili, au msimamo wao safi mbele za Mungu ni njia muhimu ya kuonyesha unawapenda. Inaelekea kwamba baadaye wataelewa kwa nini unawawekea sheria, nao watathamini ulinzi wako wenye upendo.
Kuelekeza Mshale
Ona kwamba Zaburi 127:4, 5 inamlinganisha mzazi na “mwanamume mwenye nguvu.” Je, hilo linamaanisha kwamba baba tu ndiye mzazi anayeweza kuwaelekeza watoto kwa mafanikio? Hapana. Kwa kweli, kanuni ya mfano huo inawahusu akina baba na mama, na vilevile wazazi wasio na wenzi. (Methali 1:8) Maneno “mwanamume mwenye nguvu” yanadokeza kwamba nguvu nyingi zilihitajiwa ili kupiga mshale kwa upinde. Katika nyakati za Biblia, upinde ungefunikwa kwa shaba, na ilisemekana kwamba askari-jeshi ‘aliukanyaga upinde.’ Labda aliukanyaga kwa mguu wake ili aufunge kamba. (Yeremia 50:14, 29) Ni wazi kwamba nguvu na jitihada nyingi sana zilihitajiwa ili kuvuta kamba hiyo iliyokazika na kupiga mishale hiyo ili ilenge shabaha!
Vivyo hivyo, kuwalea watoto kunahitaji jitihada nyingi sana. Mshale hauwezi kujilenga wenyewe tu na kupiga shabaha, vivyo hivyo, watoto hawawezi kujilea. Kwa kusikitisha, inaonekana wazazi wengi leo hawataki kujitahidi ili kuwalea watoto wao ifaavyo. Wanachagua njia rahisi. Wanaacha televisheni, shule, na marafiki wawafundishe watoto wao mambo yanayofaa na yasiyofaa, maadili, na ngono. Wanawapa watoto wao chochote wanachotaka. Na inapoonekana vigumu sana kusema hapana, wazazi wanasema tu ndiyo, mara nyingi wakijitetea kwa kusema kwamba wanafanya uamuzi huo ili wasiumize hisia za watoto wao. Ukweli ni kwamba kuwaacha watoto wafanye wanavyotaka kutawaletea madhara ya kudumu.
Kulea watoto ni kazi ngumu. Bila shaka, jitihada nyingi zinahitajiwa ili kufanya kazi hiyo kwa moyo wote na kwa kufuata mwongozo wa Neno la Mungu, lakini kazi hiyo inaleta thawabu nyingi sana. Gazeti fulani (Parents) linasema hivi: “Uchunguzi . . . umeonyesha kwamba watoto wanaolelewa na wazazi wenye upendo lakini wanaotumia mamlaka yao ifaavyo—wazazi wanaowategemeza watoto wao lakini wanaoweka mipaka imara—wanafanya vyema shuleni, wana uhusiano mzuri na watu wengine, wanajiheshimu, na kwa ujumla wana furaha zaidi kuliko watoto ambao wazazi wao wanawaendekeza au ni wakali kupita kiasi.”
Kuna thawabu nzuri hata zaidi. Mwanzoni, tulizungumzia sehemu ya kwanza ya Methali 22:6 inayosema: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa.” Mstari huo unaongezea maneno haya yenye kuchangamsha moyo: “Hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.” Je, methali hiyo iliyoongozwa na roho inawapa wazazi uhakikisho wa kufanikiwa? Si lazima. Mtoto wako ana uhuru wa kuchagua, na atautumia atakapokuwa mtu mzima. Lakini mstari huo unawapa wazazi uhakikisho wenye upendo. Uhakikisho gani?
Ukifuata mashauri ya Biblia kuwalea watoto wako, unaandaa mazingira bora yatakayoleta mafanikio mazuri sana—kuwaona watoto wako wakikua na kuwa watu wazima walio na furaha, maisha yenye kuridhisha, na wanaotegemeka. (Methali 23:24) Hivyo, fanya yote unayoweza ili kuitayarisha “mishale” hiyo yenye thamani, ilinde, na ujitahidi kuielekeza. Hutajuta kamwe.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Je, wazazi wanaonyesha upendo kwa kuwaacha watoto wao wafanye jambo lolote wanalotaka?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Mzazi mwenye upendo anaeleza sababu ya kuweka sheria za familia
[Picha katika ukurasa wa 15]
Wazazi wazuri wanawalinda watoto wao kutokana na hatari za ulimwengu huu uliopotoka
[Picha katika ukurasa wa 16]
Kulea watoto ni kazi ngumu, lakini inaleta thawabu nyingi sana