Je, Wajua?
Kwa nini Yesu alimponya kipofu hatua kwa hatua?
Katika Marko 8:22-26, tunasoma kwamba Yesu alimponya mtu aliyekuwa kipofu huko Bethsaida. Simulizi hilo linasema kwamba Yesu alimpaka mate machoni kisha akamwuliza alichoona. Jibu la mtu huyo lilionyesha kwamba alikuwa amechanganyikiwa kidogo: “Ninaona watu, kwa sababu ninaona vitu vinavyoonekana kama miti, lakini vinatembea huku na huku.” Kisha Yesu akagusa macho ya mtu huyo tena na mambo yakawa hivi: “Mtu huyo akaona waziwazi, naye akapona, naye alikuwa akiona kila kitu waziwazi.” Ni wazi kwamba Yesu alimponya mtu huyo hatua kwa hatua. Kwa nini alifanya hivyo?
Biblia haitoi jibu kamili, lakini tunaweza kufikiria kisa hicho kwa njia hii. Kuanza kuona baada ya kuwa kipofu kwa miaka mingi au maisha yako yote, ni badiliko kubwa sana. Kwa mfano: Wakati fulani farasi waliwekwa katika migodi ili wafanye kazi. Walizoea sana giza hivi kwamba walipoletwa juu ya ardhi, walihitaji muda mrefu kufikia hata siku nzima ili wazoee mwangaza. Inapohusu upofu, badiliko lingekuwa kubwa hata zaidi. Katika nyakati za kisasa, madaktari wa upasuaji wamefaulu katika visa kadhaa kurekebisha matatizo ya macho ya vipofu na kuwawezesha kuona tena. Hata hivyo, wagonjwa hao wamelemewa sana na habari nyingi inayoingia katika ubongo kupitia macho yao. Wakistaajabia kuona rangi, maumbo, na pande mbalimbali za vitu, wanachanganyikiwa na kushindwa kutambua hata vitu walivyofahamu hapo awali. Baada ya muda, ubongo unajifunza kutambua kile ambacho macho yanaona.
Huenda Yesu alikuwa akimhangaikia kwa upendo mtu huyo aliyekuwa kipofu kwa kumponya hatua kwa hatua. Mwishowe, mtu huyo “alikuwa akiona kila kitu waziwazi,” yaani, alitambua kila kitu alichokuwa akiona.
Katika siku za Yesu, kwa nini ilikuwa vigumu kusoma kitabu cha kukunjwa?
Kurasa za kawaida zilizotumiwa kutengeneza vitabu vya kukunjwa zilikuwa na urefu wa kuanzia sentimita 23 mpaka 28 na upana wa kuanzia sentimita 15 mpaka 23. Kurasa kadhaa ziliunganishwa kwa gundi au kushonwa kwa uzi wa kitani. Nyakati nyingine kurasa ndefu zaidi zilitumiwa. Kitabu cha Kukunjwa cha Bahari ya Chumvi cha Isaya kilikuwa na kurasa 17 zilizounganishwa, na sehemu iliyohifadhiwa ina urefu wa mita 7 hivi. Huenda kitabu cha kukunjwa cha Isaya ambacho Yesu alitumia katika sinagogi huko Nazareti kilikuwa na urefu kama huo.—Luka 4:16, 17.
Kuhusu simulizi hilo, Alan Millard anasema hivi katika kitabu chake (Discoveries From the Time of Jesus): “Msomaji alishika kitabu hicho [kitabu cha kukunjwa] na kukikunjua kwa mkono wake wa kushoto, akishika sehemu ya nje kwa mkono wa kulia na kukikunja alipokuwa akisoma, safu baada ya safu. Ili afike Isaya 61, sura ambayo alisoma katika sinagogi, Yesu alihitaji kukunjua sehemu kubwa ya kitabu cha kukunjwa kisha akikunje tena.”
Wakati huo, kitabu cha Isaya hakikuwa kimegawanywa katika sura na mistari kama ilivyo leo. Yesu alipopewa kitabu cha kukunjwa cha Isaya katika sinagogi huko Nazareti, alihitaji kutafuta simulizi ambalo sasa ni Isaya 61:1, 2 katika Biblia zetu. Kwa urahisi Yesu ‘alipata mahali palipokuwa pameandikwa,’ na hilo linaonyesha jinsi alivyofahamu sana Neno la Mungu.