Sura 21
Yesu Akiwa Katika Sinagogi la Mji wa Kwao
BILA shaka kuna msisimuko katika Nazareti Yesu anaporudi nyumbani. Kabla hajaondoka kwenda kubatizwa na Yohana muda unaozidi kidogo mwaka mmoja, Yesu alijulikana kuwa seremala. Lakini sasa amejulikana sana kuwa mfanya miujiza. Wakaaji wenyeji wataka sana kumwona akifanya baadhi ya kazi hizo za ajabu miongoni mwao.
Matazamio yao yanaongezeka wakati Yesu anapoenda kwenye sinagogi la kwao kulingana na desturi yake. Wakati ibada zinapoendelea humo, yeye asimama asome, naye apewa hati-kunjo ya nabii Isaya. Akunjua mahali pamaposema juu ya Yule aliyepakwa mafuta kwa roho ya Yehova, ambapo katika Biblia zetu leo ni sura ya 61.
Akiisha kusoma juu ya jinsi Huyu angehubiria mateka kufunguliwa kwao, vipofu kufumbuliwa macho, na juu ya mwaka uliokubalika wa Yehova, Yesu amrudishia mtumishi hati-kunjo kisha aketi. Wote wamkazia macho. Halafu asema nao, labda kwa muda mrefu kidogo, akieleza hivi: “Leo andiko hili ambalo mmesikia sasa hivi limetimizwa.”
Watu wastaajabia ‘maneno yake ya kuvutia sana’ na kusemezana hivi: “Huyu ni mmoja wa wana wa Yusufu, sivyo?” Lakini yeye akijua kwamba wataka kumwona akifanya miujiza, Yesu aendelea kusema: “Hakuna shaka mtautumia mfano huu kunihusu mimi, ‘Tabibu, jiponye mwenyewe; mambo tuliyosikia kuwa yalitukia katika Kapernaumu yafanye hapa pia katika eneo la nyumbani kwenu.’” Kwa wazi, watu hawa waliokuwa jirani za Yesu hapo kwanza, wanaona kwamba mtu apaswa kuanzia nyumbani maponyo anayofanya, kwa faida ya watu wake mwenyewe kwanza. Kwa hiyo wanaona wamepuuzwa na Yesu.
Kwa kutambua kuwaza kwao, Yesu asimulia historia fulani yenye matumizi yanayofaa. Asema kwamba walikuwako wajane wengi katika Israeli katika siku za Eliya lakini Eliya hakutumwa kwa yeyote kati yao. Bali, alienda kwa mjane asiye Mwisraeli katika Sidoni, ambako alifanya muujiza wenye kuokoa uhai. Na katika siku za Elisha, walikuwako wenye ukoma wengi, lakini Elisha alisafisha Naamani wa Shamu (Siria) peke yake.
Kwa kukasirishwa na ulinganisho huo wa kihistoria wenye sifa mbaya unaofunua uchoyo wao na ukosefu wa imani, wale walio katika sinagogi wainuka na kumsukumiza Yesu nje ya mji. Huko, kwenye ukingo wa mlima ambao mji wa Nazareti umejengwa juu yao, wajaribu kumtupa akaanguke chini. Lakini Yesu awaponyoka na kwenda zake akiwa salama. Luka 4:16-30, NW; 1 Wafalme 17:8-16; 2 Wafalme 5:8-14.
▪ Kwa nini kuna msisimuko mwingi Nazareti?
▪ Watu wafikiri nini juu ya hotuba ya Yesu, lakini ni jambo gani linalowakasirisha sana?
▪ Watu wajaribu kumtendaje Yesu?