Wasomaji Wetu Wanauliza
Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawaendi Vitani?
Hata wawe wanaishi wapi, Mashahidi wa Yehova wana historia ndefu ya kutojihusisha na vita kati ya mataifa au kati ya watu wanaopigana katika nchi ileile. “Mashahidi wa Yehova wanadumisha msimamo imara wa kutounga mkono upande wowote wakati wa vita,” kilisema kitabu kimoja (Australian Encyclopædia) miaka 50 hivi iliyopita.
Sababu moja kuu inayowafanya Mashahidi wasijihusishe na vita ni kwamba kufanya hivyo kutachafua dhamiri yao ya Kikristo. Dhamiri yao imefundishwa kufuata sheria na mfano wa Bwana wao Yesu Kristo. Aliwaagiza wafuasi wake wawapende majirani wao. Pia alitoa agizo hili: “Endeleeni kuwapenda adui zenu, kuwafanyia mema wale wanaowachukia.” (Luka 6:27; Mathayo 22:39) Mmoja wa wafuasi wake alipojaribu kumlinda kwa kutumia upanga, Yesu alimwambia: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Hivyo, kwa maneno na kwa matendo, alionyesha waziwazi kwamba wafuasi wake hawatatumia silaha za vita.
Sababu nyingine inayowafanya Mashahidi wa Yehova wasiende vitani ni kwamba wao ni washiriki wa jamii ya waamini wa ulimwenguni pote. Kwenda vitani kungemaanisha ndugu angekuwa dhidi ya ndugu, na hicho kingekuwa kinyume cha sheria ya Yesu ya kuwa na ‘upendo kati yao wenyewe.’—Yohana 13:35.
Kanuni zilizotajwa hapo juu kuhusu upendo si maneno yasiyo na maana kwa Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, chunguza mwenendo wao katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, 1939-1945. Nchini Marekani, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 4,300 walifungwa katika magereza kwa kukataa kwenda jeshini. Huko Uingereza, zaidi ya watu 1,500, kutia ndani wanawake zaidi ya 300, walifungwa kwa sababu ya kukataa kufanya kazi zilizohusiana na vita. Katika Ujerumani ya Nazi, Mashahidi zaidi ya 270 waliuawa kufuatia agizo la Serikali kwa kukataa kutumia silaha. Katika utawala wa Nazi, Mashahidi zaidi ya 10,000 walifungwa katika magereza au kambi za mateso. Vilevile, Mashahidi huko Japani waliteswa sana. Mtu yeyote aliyempoteza mpendwa wake katika Vita vya Pili vya Ulimwengu au katika vita vingine baada ya hapo, anaweza kuwa na hakika kwamba hakuna Shahidi wa Yehova hata mmoja aliyesababisha vifo kama hivyo.
Maoni ya Mashahidi wa Yehova kuhusu vita yameelezwa vizuri katika maneno ya mwisho ya Wolfgang Kusserow. Mnamo 1942, Wanazi walimkata kichwa Mjerumani huyo mwenye umri wa miaka 20 kwa sababu alikataa kwenda vitani. (Isaya 2:4) Alisema hivi mbele ya mahakama ya kijeshi: “Nililelewa na Mashahidi wa Yehova, kulingana na neno la Mungu lililoandikwa katika Maandiko Matakatifu. Sheria kuu na takatifu zaidi aliyowapa wanadamu ni: ‘Mpende Mungu wako kuliko kitu kingine chochote na jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Sheria nyingine inasema hivi: ‘Usiue.’ Je, Muumba wetu aliiandikia miti maneno hayo yote?”—Marko 12:29-31; Kutoka 20:13.
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba ni Yehova pekee, Mungu mweza-yote, atakayeleta amani ya kudumu duniani. Wanatarajia kwamba atatimiza ahadi yake ya ‘kukomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’—Zaburi 46:9.