Mkaribie Mungu
Anakumbuka Kwamba “Sisi Ni Mavumbi”
“SIKUAMINI kwamba Yehova anaweza kunisamehe kabisa, na nilifikiri kuwa ningesumbuliwa na dhamiri yangu katika maisha yangu yote.” Hivyo ndivyo alivyoandika mwanamke mmoja Mkristo kuhusu makosa aliyofanya zamani. Kwa kweli, kusumbuliwa na dhamiri ni mzigo mzito kubeba. Hata hivyo, Biblia inatoa faraja inayoweza kuwasaidia wakosaji waliotubu wasilemewe na mzigo wa kusumbuliwa na dhamiri. Fikiria maneno ya mtunga-zaburi Daudi kwenye Zaburi 103:8-14.
Daudi alijua kwamba “Yehova ni mwenye rehema” na “hataendelea kutafuta makosa.” (Mstari wa 8-10) Mungu anapopata sababu ya kutuonyesha rehema, anafanya hivyo kikamili na kwa moyo wote. Daudi, mtungaji stadi wa mashairi, anatumia mifano mitatu ya ulinganisho ili kuonyesha kwamba rehema za Mungu kutuelekea hazina kifani.
“Kama mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo fadhili zake zenye upendo zilivyo kuu kuwaelekea wale wanaomwogopa.” (Mstari wa 11) Tunapotazama anga wakati wa usiku, hatuwezi kuelewa kihalisi umbali uliopo kati ya dunia na mbingu zenye nyota. Hivyo, Daudi anatusaidia kuona wingi wa rehema za Yehova, ambazo ni sehemu ya upendo wake mshikamanifu. Mungu anawaonyesha rehema hizo “wale wanaomwogopa,” yaani, wale “walio wapole na wanaoheshimu mamlaka yake,” anasema msomi mmoja.
“Kama vile mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo ameweka makosa yetu mbali sana na sisi.” (Mstari wa 12) Je, unaweza kuwazia umbali uliopo kati ya mashariki na magharibi? Kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinasema: “Kadiri unavyoendelea kusafiri kuelekea mashariki, ndivyo unavyozidi kwenda mbali kutoka magharibi.” Hapa Daudi anatueleza kwamba Mungu anapotusamehe dhambi zetu, anaziweka mbali nasi kwa kadiri tusiyoweza kuwazia.
“Kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa.” (Mstari wa 13) Kwa kuwa Daudi mwenyewe alikuwa baba, alijua vizuri jinsi baba mwenye upendo anavyohisi moyoni. Baba kama huyo anasukumwa kuwaonyesha watoto wake huruma, hasa wanapoteseka. Daudi anatuhakikishia kuwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anawaonyesha watoto wake walio duniani rehema, hasa wakati mioyo yao iliyotubu ‘inapovunjika na kupondwa,’ kwa sababu ya dhambi zao.—Zaburi 51:17.
Baada ya kutaja mifano hiyo mitatu ya ulinganisho, Daudi anafunua jambo linalofanya Yehova awaonyeshe rehema wanadamu wasio wakamilifu: “Yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Mstari wa 14) Yehova anajua kuwa tumeumbwa kutokana na mavumbi na tuna udhaifu mbalimbali. Kwa kuwa anajua kwamba sisi ni wenye dhambi, Yehova yuko ‘tayari kutusamehe’—bora tu tuonyeshe kwamba tumetubu kutoka moyoni.—Zaburi 86:5.
Je, umeguswa moyo na maneno ya Daudi kuhusu rehema za Yehova? Mwanamke aliyetajwa mwanzoni alijifunza yale Biblia inayosema kuhusu utayari wa Mungu wa kusamehe, naye akachochewa kusema: “Nimeanza kuhisi kwamba ninaweza kumkaribia Yehova, na ninahisi kuwa mzigo mzito niliokuwa nao umeondolewa.”a Tunakutia moyo ujifunze mengi zaidi kuhusu rehema za Mungu na jinsi unavyoweza kuzipata. Huenda hata wewe utahisi kuwa mzigo mzito ulio nao umeondolewa.
Usomaji wa Biblia Unaopendekezwa kwa Mwezi wa Agosti (Mwezi wa 8):
[Maelezo ya Chini]
a Ona sura ya 26, yenye kichwa “Mungu Aliye ‘Tayari Kusamehe,’” ya kitabu Mkaribie Yehova, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Blabu katika ukurasa wa 13]
“Nimeanza kuhisi kwamba ninaweza kumkaribia Yehova, na ninahisi kuwa mzigo mzito niliokuwa nao umeondolewa”