Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w13 8/1 kur. 3-7
  • Ponografia—Je, Ina Madhara?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ponografia—Je, Ina Madhara?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ponografia inawaathirije watu wanaoitazama?
  • Ponografia huathirije familia?
  • Biblia inasema nini kuhusu ponografia?
  • Ninaweza kuepukaje Ponografia?
    Amkeni!—2007
  • Madhara Yanayosababishwa na Ponografia
    Amkeni!—2003
  • Kwa Nini Niepuke Ponografia?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Kwa Nini Ujiepushe na Ponografia?
    Vijana Huuliza
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
w13 8/1 kur. 3-7
[Picha katika ukurasa wa 2, 3]

HABARI KUU

Ponografia​—Je, Ina Madhara?

Ponografia imesambaa ulimwenguni pote.a Inapatikana kwenye matangazo ya biashara, mitindo, sinema, muziki, na magazeti, vilevile kwenye televisheni, michezo ya video, simu, vifaa vya kielektroniki vinavyobebwa, na pia kwenye Intaneti. Inaonekana ponografia inapendwa na watu wengi sana. Watu wengi zaidi katika maeneo mbalimbali wanatazama ponografia kuliko wakati mwingine wowote katika historia.—Ona sanduku “Ukweli Kuhusu Ponografia.”

Ponografia inazidi kubadilika. Profesa Gail Dines anaandika hivi: “Leo, picha zinazidi kuwa mbaya hivi kwamba ponografia iliyoonwa kuwa chafu sana imekuwa ya kawaida.”

Wewe una maoni gani? Je, ni sawa kutazama ponografia, ni hatari, au huna msimamo wowote? Yesu alisema: “Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa.” (Mathayo 7:17) Ponografia hutokeza matunda ya aina gani? Ili tupate jibu, acheni tuchunguze maswali fulani ya msingi kuhusu ponografia.

Ponografia inawaathirije watu wanaoitazama?

WATAALAMU HUSEMA: Watu wanaotazama ponografia huwa na mazoea sugu ya kuitazama, na watafiti fulani huilinganisha na kutumia kokeini kali.

Brian,b ambaye alikuwa na mazoea ya kutazama ponografia kwenye Intaneti anasimulia: “Hakuna kitu ambacho kingenizuia. Ni kana kwamba nilikuwa katika ulimwengu mwingine. Nilitetemeka na kuhisi maumivu kichwani. Nilijitahidi kuacha, lakini niliendelea kutazama kwa miaka mingi.”

Mara nyingi, watu wanaotazama ponografia huficha zoea hilo. Ni wasiri na pia wadanganyifu. Si ajabu kwamba wengi wao huhisi upweke, huona aibu, hushuka moyo, huwa na wasiwasi, na kukasirika. Hata wengine wao hutamani kujiua. “Nilijitenga na watu na kukata tamaa,” anasema Serge ambaye alitazama ponografia kwenye simu yake ya mkononi karibu kila siku. “Nilijihisi mwenye hatia, asiyefaa, mpweke, na aliyenaswa. Niliaibika sana na nikaogopa kutafuta msaada.”

Hata kutazama ponografia kifupi bila kukusudia kunaweza kuwa na madhara. Akitoa ushahidi mbele ya kamati ya Seneti ya Marekani, mtafiti wa mambo ya ponografia Dkt. Judith Reisman alisema: “Picha za ponografia hubaki akilini, na kuhifadhiwa kwa njia ya kudumu ambayo hutokeza kumbukumbu ambazo ni vigumu au haziwezi kufutwa.” Susan mwenye umri wa miaka 19 ambaye alitazama Tovuti za ponografia anasema: “Bado picha hizo ziko akilini. Mimi huzikumbuka bila kutaka. Ninahisi kwamba sitafaulu kamwe kuzifuta kabisa.”

JAMBO HAKIKA: Ponografia hutokeza mazoea sugu na huwaathiri watu wanaoitazama.​—2 Petro 2:19.

Ponografia huathirije familia?

WATAALAMU HUSEMA: “Ponografia huvunja ndoa na familia.”​—Kitabu The Porn Trap, cha Wendy na Larry Maltz.

Ponografia huharibu ndoa na familia kwa:

  • Kusababisha kutoaminiana, kuvuruga upendo na mapenzi.​—Methali 2:12-17.

  • Kusababisha ubinafsi, mtengano wa kihisia, na kutoridhika na mwenzi wa ndoa.​—Waefeso 5:28, 29.

  • Kuchochea mawazo na hamu ya ngono haramu.​—2 Petro 2:14.

  • Kumshawishi mtazamaji amlazimishe mwenzi wake kufanya ngono kwa njia isiyo ya kawaida.​—Waefeso 5:3, 4.

  • Kuendeleza ukosefu wa uaminifu wa kihisia na kimwili.​—Mathayo 5:28.

Biblia huwashauri wenzi wa ndoa ‘wasitendeane kwa hila.’ (Malaki 2:16) Ukosefu wa uaminifu ni hila ambayo inaweza kuvuruga ndoa na kusababisha kutengana na talaka. Ndoa inapovunjika, watoto huteseka sana.

[Picha katika ukuras wa 4, 5]

Ponografia inaweza pia kuwaathiri watoto moja kwa moja. Brian aliyetajwa mapema, anasema: “Nilipokuwa na umri wa miaka kumi hivi, nilipata magazeti ya baba yenye picha za ponografia tulipokuwa tukicheza. Nilianza kuyatazama kisiri, bila kuelewa hasa kwa nini nilivutiwa na picha hizo. Nikawa na zoea baya lililoendelea kwa miaka mingi.” Uchunguzi unaonyesha kwamba ponografia inaweza kuwashawishi vijana waanze kufanya ngono wakiwa na umri mdogo na pia kuwa na maadili mapotovu, kuwa wajeuri kingono, na kuvurugika kihisia na kisaikolojia.

JAMBO HAKIKA: Ponografia huharibu uhusiano katika familia na kusababisha maumivu na uchungu mwingi.​—Methali 6:27.

Biblia inasema nini kuhusu ponografia?

NENO LA MUNGU LINASEMA: “Viueni viungo vya mwili wenu . . . kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.”​—Wakolosai 3:5.

Kwa ufupi, Yehovac Mungu anachukia ponografia. Hilo halimaanishi kwamba anachukia mambo ya ngono. Ndiye aliyeumba uwezo wetu wa kingono na kukusudia mume na mke wautumie kufurahishana, kukaribiana kihisia, na kushirikiana kuzaa watoto.​—Yakobo 1:17.

Kwa nini basi Yehova anachukia sana ponografia? Acheni tuchunguze sababu chache.

  • Anajua ponografia inaweza kuharibu maisha ya watu.​—Waefeso 4:17-19.

  • Anatupenda na anataka kutulinda tusipate madhara.​—Isaya 48:17, 18.

  • Yehova anataka kulinda ndoa na familia.​—Mathayo 19:4-6.

  • Anataka tuwe na maadili safi na tuheshimu haki za wengine.​—1 Wathesalonike 4:3-6.

  • Anataka tuheshimu uwezo wetu wa ngono na kuutumia kwa njia yenye kuheshimika.​—Waebrania 13:4.

  • Yehova anajua ponografia huendeleza mawazo ya kibinafsi, ya kishetani, na yaliyopotoka kuhusu ngono.​—Mwanzo 6:2; Yuda 6, 7.

JAMBO HAKIKA: Ponografia huharibu uhusiano wa mtu pamoja na Mungu.​—Waroma 1:24.

Hata hivyo, Yehova anawahurumia wale ambao wangependa kuacha kutazama ponografia. Biblia inasema: “Yehova ni mwenye rehema na mwenye neema, si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa fadhili zenye upendo. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:8, 14) Anawasihi watu wanyenyekevu wamwendee ili ‘wapokee rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa kuwa msaada kwa wakati unaofaa.’​—Waebrania 4:16; ona sanduku “Kushinda Zoea la Kutazama Ponografia.”

Watu wengi wamekubali msaada wa Mungu. Je, wamefaidika? Ona kile ambacho Biblia inasema kuhusu watu walioshinda mazoea mabaya: “Mmeoshwa mkawa safi, . . . mmetakaswa, . . . mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.” (1 Wakorintho 6:11) Kama mtume Paulo, watu kama hao wanaweza kusema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”​—Wafilipi 4:13.

Susan, aliyeshinda zoea la kutazama ponografia, anasema: “Yehova tu ndiye anayeweza kukuweka huru. Ukimwomba msaada na mwongozo, unaweza kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye. Hatakuacha kamwe.”

Kushinda Zoea la Kutazama Ponografia

Je, unamfahamu mtu yeyote anayejitahidi kuacha zoea la kutazama ponografia? Hebu ona hatua ambazo watu fulani wamechukua ili kushinda zoea hilo.

1. Sali kwa Mungu.

[Picha]

“Hatua muhimu zaidi ya kushinda mtego wa ponografia ni kusali kwa Yehova ili akusaidie.”​—Franz.

Yehova anaweza kumpa mtu roho takatifu ili imsaidie awe na “nia na kutenda pia.” (Wafilipi 2:13) Mtu huyo akikubali kuongozwa na roho takatifu, atafaulu kushinda ‘mawazo na tamaa mbaya.’​—Wagalatia 5:16, 24.

2. Tafuta msaada kutoka kwa wengine.

[Picha]

“Zoea la kutazama ponografia ni la kisiri na linaaibisha sana hivi kwamba unahisi vigumu kuomba msaada. Unadhani unaweza kulishinda ukiwa peke yako. Lakini hilo si kweli. Lazima usaidiwe ili kufaulu. Hivyo nilijinyenyekeza nikamwambia mke wangu. Pia, niliomba msaada kutoka kwa rafiki niliyemwamini. Hilo ndilo jambo gumu zaidi ambalo nimewahi kufanya, lakini nilipata msaada niliohitaji.”​—Yoshi.

Unahitaji ujasiri mwingi ili uwaeleze wengine. Lakini ni hatua muhimu ya kushinda zoea hilo na kurekebisha uhusiano kati yako na watu unaowapenda. Susan aliyetajwa mapema, anasema: “Baadaye nilihisi utulivu mwingi. Kipindi hicho kilikuwa kigumu, lakini hatimaye nilipata amani na kibali.”​—Yakobo 5:16.

3. Tambua na uepuke mambo yanayochochea.

[Picha]

Ni hali, mawazo, au hisia gani zinazochochea tamaa mbaya? Je, ni kutumia Intaneti? Kutazama televisheni usiku? Kusoma magazeti? Kutembelea ufuo wa bahari? Anapohisi njaa, hasira, upweke, au uchovu? “Tambua udhaifu wako, na uepuke mambo hayo kabisa,” anasema Sven. Yesu alisema: “Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe ulitupilie mbali nawe.”​—Mathayo 5:29.

“Ninaposhawishiwa kumtazama mwanamke na kumtamani, mara moja ninasali kwa Yehova na kuyalazimisha macho yangu yatazame kwingine,” anasema Franz. Ayubu, mwanamume mwaminifu anayetajwa katika Biblia alisema: “Nimejifunga rasmi mimi mwenyewe, macho yangu yasimtazame msichana kwa tamaa.”​—Ayubu 31:1, Biblia Habari Njema.

4. Imarisha uhusiano wako pamoja na Mungu.

[Picha]

“Jaza akili yako mawazo yanayofaa, na uwe na shughuli nyingi za kiroho,” anaongezea Franz.

Biblia husema: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo . . . , na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.”​—Wafilipi 4:8, 9.

a Neno “ponografia” linamaanisha habari za ngono ambazo zimekusudiwa kuamsha nyege za mtazamaji, msomaji, au msikilizaji. Inatia ndani picha, maandishi, na pia sauti.

b Majina katika makala hii yamebadilishwa.

c Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.

UKWELI KUHUSU PONOGRAFIA

KILA SEKUNDE: Karibu watu 30,000 hutazama ponografia kwenye Intaneti.

KILA DAKIKA: Watumiaji wa Intaneti hutuma zaidi ya barua-pepe MILIONI 1.7 za ponografia.

KILA SAA: Angalau sinema MBILI za ponografia mbaya sana hutengenezwa nchini Marekani.

KILA SIKU: Kwa wastani sinema MILIONI MBILI za ponografia hukodishwa nchini Marekani.

KILA MWEZI: Nchini Marekani, karibu vijana wa kiume 9 kati ya 10 na wa kike 3 kati ya 10 hutazama ponografia.

KILA MWAKA: Ulimwenguni pote, biashara ya ponografia hupata faida ya dola za Marekani BILIONI 100.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki