Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wp19 Na. 2 kur. 6-7
  • Unapofiwa na Mtu Unayempenda

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unapofiwa na Mtu Unayempenda
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu Wote)—2019
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAMBO AMBAYO YAMEWASAIDIA WENGINE
  • Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
  • Kukabiliana na Huzuni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Msaada kwa Wale Wanaoomboleza
    Amkeni!—2011
  • Kwa Nini Baba Alikufa?
    Amkeni!—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu Wote)—2019
wp19 Na. 2 kur. 6-7
Wenzi wa ndoa ambao wamefiwa wakiwa kwenye ufuo wa bahari wakitazama mbali

Unapofiwa na Mtu Unayempenda

“Kaka yangu alipokufa ghafla, nilihisi sina nguvu. Hata baada ya miezi kupita, bado kuna siku ambazo ghafla tu nilimkumbuka na kuhisi maumivu makali kana kwamba ninachomwa kisu. Nyakati nyingine nilikasirika na kujiuliza kwa nini ndugu yangu alikufa. Na nilijuta kwa kuwa sikutenga muda mwingi wa kushirikiana naye alipokuwa hai.”—Vanessa, Australia.

IKIWA umefiwa na mtu unayempenda, huenda umekuwa na hisia tofauti-tofauti kama vile huzuni, upweke, na kuhisi huna nguvu. Labda pia unahisi hasira, hatia, na woga. Huenda hata ukajiuliza ikiwa kweli kuna haja ya kuendelea kuishi.

Kumbuka kwamba kuhuzunika baada ya kufiwa si udhaifu. Ni ishara ya kwamba ulimpenda sana yule aliyekufa. Hata hivyo, je, inawezekana kupunguza maumivu makali unayohisi?

MAMBO AMBAYO YAMEWASAIDIA WENGINE

Mapendekezo yafuatayo yanaweza kukusaidia licha ya kwamba huenda ukahisi uchungu ulio nao hauwezi kuisha:

KUJIPATIA NAFASI YA KUOMBOLEZA

Watu huomboleza kwa njia tofauti-tofauti. Vilevile, huzuni ya wengine hudumu kwa muda mrefu na ya wengine muda mfupi. Vyovyote vile, kulia kunaweza kuondoa hisia za uchungu moyoni. Vanessa, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, alisema: “Nililia mara nyingi; nilihitaji kutoa uchungu niliokuwa nao.” Sofía, ambaye alifiwa ghafla na mdogo wake, alisema: “Ninahisi uchungu mwingi ninapofikiria kile kilichotokea. Ni kama kufungua na kusafisha kidonda. Maumivu ni makali sana, lakini ni muhimu kufanya hivyo ili kidonda kipone.”

KUELEZA MAWAZO NA HISIA

Nyakati nyingine, huenda ukahisi unataka kuwa peke yako. Lakini huzuni ya kufiwa ni mzigo mzito ambao huwezi kuubeba mwenyewe. Jared, mwenye umri wa miaka 17, ambaye alifiwa na baba yake, anasema hivi: “Niliwaeleza wengine jinsi nilivyohisi. Sidhani kama walinielewa, lakini nilihisi vizuri nilipojieleza.” Janice, aliyetajwa kwenye makala ya kwanza, anataja faida nyingine: “Kuzungumza na wengine kulinifariji sana. Nilihisi wengine wanaelewa hali yangu, na kwamba sikuwa peke yangu.”

KUKUBALI KUSAIDIWA NA WENGINE

Daktari mmoja anasema: “Watu waliofiwa ambao hukubali msaada wa marafiki na washiriki wa familia mara tu baada ya kufiwa, hukabiliana na huzuni yao kwa urahisi zaidi.” Waeleze rafiki zako jinsi wanavyoweza kukusaidia; huenda wanataka kukusaidia lakini hawajui waanzie wapi.—Methali 17:17.

KUMKARIBIA ZAIDI MUNGU

Tina anasema: “Mume wangu alipokufa ghafla kutokana na kansa, sikuwa tena na mtu wa kumweleza hisia zangu, hivyo nilimweleza Mungu kila kitu! Kila siku asubuhi nilimwomba Mungu anipe nguvu za kuvumilia siku hiyo. Mungu alinisaidia katika njia nyingi ambazo hata siwezi kutaja.” Tarsha, ambaye alikuwa na umri wa miaka 22 alipofiwa na mama yake, anasema: “Kusoma Biblia kila siku kulinifariji sana. Nilipata jambo zuri la kufikiria kila siku.”

KUWAZIA UKIMPOKEA MPENDWA WAKO ATAKAPOFUFULIWA

Tina anaongezea kusema: “Mwanzoni, tumaini la ufufuo halikunifariji kwa sababu nilihisi kwa wakati huo, nilimhitaji mume wangu, na wanangu walimhitaji baba yao. Hata hivyo, sasa miaka minne imepita, na tumaini hilo ndilo linaloniimarisha. Ni kama nanga ya maisha yangu. Huwa ninawazia nikimwona tena, na jambo hilo hunipa amani na shangwe isiyoelezeka!”

Inaelekea huzuni yako haitaisha mara moja. Lakini unaweza kupata faraja kwa kufikiria maneno ya Vanessa. Anasema, “Mtu hufikiri kwamba huzuni haitawahi kuisha, lakini hali hubadilika hatua kwa hatua.”

Kumbuka, ingawa huenda pengo unalohisi moyoni halitazibwa, bado una sababu nzuri za kuendelea kuishi. Kwa msaada wa Mungu, bado unaweza kufurahia urafiki pamoja na wengine, na kuwa na kusudi maishani. Na hivi karibuni Mungu atawafufua wale waliokufa. Anataka umkumbatie tena mpendwa wako atakapofufuliwa. Na maumivu uliyo nayo moyoni, yataisha kabisa!

Maandiko Yanayoweza Kukusaidia

Mungu anaona kilio na huzuni uliyo nayo.

Mwandikaji mmoja wa Biblia alimwambia Mungu hivi: “Yakusanye machozi yangu katika kiriba chako cha ngozi. Je, hayajaandikwa katika kitabu chako?”​—Zaburi 56:8.

Mmiminie Mungu moyo wako wote.

“Ninamwaga mahangaiko yangu mbele [zako Mungu] . . . Ninakulilia unisaidie, Ee Yehova.”a​—Zaburi 142:2, 5.

Kuna tumaini.

“Kutakuwa na ufufuo.”​—Matendo 24:15.

Mungu anaahidi kuwafufua mamilioni ya watu waliokufa, na ana hamu kubwa ya kufanya hivyo.b​—Ayubu 14:14, 15, maelezo ya chini.

a Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.

b Kwa habari zaidi kuhusu ufufuo, soma somo la 30 la kitabu Furahia Maisha Milele! kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova na unachoweza kupakua bila malipo kwenye tovuti ya www.jw.org/sw.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki