Kutangaza Habari Njema—Kwa Shangwe
1 Yesu Kristo alipata shangwe nyingi katika huduma yake. Kwake, kufanya mapenzi ya Baba yake kulikuwa kama chakula. (Yn. 4:34) Vivyo hivyo, Paulo alipata shangwe kubwa kutokana na kazi yake katika huduma. Ni nini iliyokuwa siri ya kupata kwao shangwe katika huduma yajapokuwa magumu na minyanyaso ambayo walikuwa wamevumilia? Utumishi wao kwa Yehova ulikuwa wa moyo wote. Wao walifanya kazi kwa bidii katika migawo yao waliyopewa na Mungu, na matokeo yalikuwa shangwe kwa sababu ya kazi zao. (Yn. 13:17; Ufu. 14:13) Unawezaje kuongezea shangwe yako katika huduma unapotumikia Yehova?
FIKIRIA KWA NJIA YA KUWASAIDIA WATU
2 Yesu Kristo na Paulo walikuwa walimu wazuri sana. Wao walilenga shabaha ya kufikia moyo wa wale waliokuwa wakisikiliza. Wengi hawakuitikia, lakini wale ambao waliitikia walikuwa kisababisho cha shangwe kweli kweli. (Flp. 4:1; linganisha Luka 15:7.) Ndiyo, kuwasaidia watu wajifunze juu ya Yehova na kuona wakichukua msimamo kwa kweli kunatufanya tuwe na furaha. Katika karne ya kwanza, “kule kuongoka kwa watu wa mataifa” kulikuwa sababu ya “shangwe kubwa kwa wale ndugu wote.”—Mdo. 15:3, NW.
3 Wewe pia unaweza kupata shangwe hii kwa kushiriki na wengine kwa ustadi yale ambayo unajua. Tengenezo la Yehova limeandaa vifaa bora vya kutusaidia tunapowafundisha wengine ukweli. Mathalani, tuna Kichwa cha Mazungumzo kinachopatikana Huduma ya Ufalme Yetu. Pia kuna kitabu Reasoning, ambacho kina matangulizi mengi yenye kuvutia na majibu kwa maswali ya maana ambayo watu wanauliza. Unapojitayarisha kwa ajili ya huduma fikiria jinsi unavyoweza kutumia madokezo kutoka Huduma ya Ufalme Yetu na kitabu Reasoning ili kuwasaidia wale wanaoishi katika eneo lenu. Fanya kazi kwa nguvu ili uwasaidie watu wawe katika njia ya wokovu kwa kujitayarisha vizuri kuanzisha mazungumzo mazuri pamoja nao. Hilo linaweza kuongoza kwenye mafunzo ya Biblia yenye kuzaa matunda na shangwe kubwa katika utumishi wetu.—Yak. 1:25.
MWELEKEO CHANYA
4 Uwe unatumika ukiwa mhubiri au painia, kumbuka kusudi la huduma. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kuhubiriwa kwa habari njema kwa ajili ya ushuhuda ni mgawo kutoka kwa Mungu. Ni pendeleo, nasi tunapaswa kuthamini kwamba kile ambacho Yehova anaomba kutoka kwa watumishi wake si mzigo. (1 Yn. 5:3) Anataka watu wake wafurahie utumishi wake. Basi, ingawa huenda wengine wasiitikie kazi ya kuhubiri, bado unaweza kupata shangwe kubwa katika huduma. Kwa sababu gani hivyo?
5 Wanafunzi wa Yesu walipata shangwe kubwa katika huduma yao, naye aliwaeleza sababu kubwa ya shangwe yao inapasa kuwa nini. (Luka 10:17-20) wale wa “mkutano mkubwa,” ambao wana matumaini ya kuishi duniani, pia wana kila sababu ya kushangilia. (Ufu. 7:9, 10) Tumaini lako liwe la kimbingu au la kidunia, uhakika wa kwamba unafanya mapenzi ya Mungu unapasa kukupa shangwe kubwa kwa sababu ‘taabu yako siyo ya bure katika Bwana.’ (1 Kor. 15:58) Yehova “si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake.” (Ebr. 6:10) Kutumikia Yehova kwa moyo wote ni chanzo cha shangwe kwa wale wanaopenda yeye.—Zab. 40:8.
6 Mkristo anapaswa kufurahia utumishi wake kwa Mungu. Endelea kupata shangwe katika huduma, ukiwa na uhakika wa kwamba Yehova anathamini hata tendo dogo la kujitolea kwa kweli. (Linganisha Marko 12:41-44.) Sisi sote na tuendelee ‘kutukuza huduma yetu’ na kupata shangwe ambayo huduma inaleta.—Rum. 11:13.