Je! Unaweza Kufanya Upainia Msaidizi Aprili?
1Yesu alianzisha kazi yenye umaana sana hivi kwamba wakati ujao wa aina ya binadamu yote unategemea matokeo yayo. (Mt. 4:17) Ni kazi ya kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. Kazi hii itafikia mwisho wayo kabla tu ya “mwisho” wakati ujumbe wa Ufalme utakapokuwa ‘umehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ushuhuda kwa mataifa yote.’—Mt. 24:14.
2Kwa kuwa sasa tumefikia umalizio wa mfumo wa mambo, kazi hii ni ya haraka kuliko wakati mwinginewo wote. Maisha zikiwa hatarini, kukawia-kawia kusikohitajiwa kunaweza kuwa na matokeo makubwa sana. Mpango wa upainia msaidizi umetia moyo wengi wawe watendaji zaidi katika kufanya kazi hii yenye uharaka. Je! unaweza kufanya upainia msaidizi Aprili?
APRILI WAANDAA FURSA NZURI
3Ukiwa na miisho-juma mitano, Aprili utakuwa mwezi mzuri sana kwa wengi kujiandikisha kama mapainia wasaidizi. Hata wengine wanaofanya kazi ya kimwili ya wakati wote huenda wakafanya hivyo. Wengine waliopainia mwaka uliopita walibarikiwa sana nao wameonyesha tamaa yao ya kutaka kutumikia tena mwaka huu. Kwa kufanya mipango sasa, je! unaweza kufanya upainia msaidizi Aprili? Mbona usizungumzie uwezekano huu pamoja na wale ambao tayari wamewekwa rasmi ili upate madokezo fulani yenye mafaa kutoka kwao?
4Kupanua utumishi wetu kunaweza kuleta furaha iliyoongezeka. Ijapokuwa huenda hii ikahitaji kudhabihu mapendezi mengine ya kibinafsi, kwa kupanda kwa wingi, tutavuna baraka zilizoongezeka za kiroho. (2 Kor. 9:6b) Wale wanaomfanyia Yehova kazi kwa nafsi yote nzima ‘wanajaa furaha’ katika mavuno ya wingi wa wanafunzi wapya.—Mdo. 13:48, 52.
JIWE LA KUKANYAGIA LA KITHEOKRASI
5Baada ya kuonja kwanza shangwe za utumishi wa painia msaidizi, wengi wamekuwa mapainia wa kawaida. Katika njia hii, utumishi wa painia msaidizi unaweza kuwa jiwe la kukanyagia kuelekea furaha kubwa zaidi. Ikiwa unaweza kufanya upainia msaidizi Aprili na miezi inayofuata, huenda ukasitawisha ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia ambayo yatakusaidia uingie katika utumishi wa painia wa kawaida kwa urahisi mwanzoni mwa mwaka mpya wa utumishi Septemba.
6Kwa nini wengi wa Mashahidi wa Yehova wanapanua huduma yao wakati huu badala ya kutafuta faida zaidi za kimwili katika mfumo huu? Ni kwa sababu wanataka kusifu Yehova na kuwaambia wengine juu ya makusudi yake. Wanajua kwamba “dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.” (1 Yoh. 2:17) Wanatenda kwa moyo mweupe kulingana na sala yao kwamba Bwana-mkubwa wa mavuno “apeleke watenda kazi katika mavuno yake.”—Mt. 9:37, 38.
7Upendo wa kweli kwa Mungu na jirani unatusukuma tushiriki kazi ya kufanya wanafunzi kulingana na uwezo wetu. (Mt. 22:37-39; 28:19) Ijapokuwa hali za kibinafsi zinawazuia wengi wasiwe wahubiri mapainia, kufanya yoteyote tuwezayo katika utumishi wa Yehova kulingana na hali zetu kunatupendekeza kuwa wale ‘wanaojitaabisha na kujitahidi kwa kusudi la kuwasaidia watu wote waokoke.’—1 Tim. 4:10.