Kutangaza Habari Njema-Kwa Magazeti
1 Mhubiri 12:12 yaonelea hivi: “Hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi.” Maneno hayo yamethibitika kuwa kweli katika siku yetu kwa maana mashine za kuchapa zenye mwendo wa kasi zimetokeza mabilioni ya kurasa za habari zilizochapishwa, zote zikishindania kuelekezewa fikira na wasomaji. Kupatikana kwa habari nyingi zilizochapishwa kunawatokezea wahubiri wa habari njema za Ufalme wito wa ushindani. Tunaweza kuwasadikishaje watu mmoja mmoja kwamba Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ndiyo magazeti yenye thamani kubwa zaidi yanayochapishwa leo?
MAGAZETI YENYE THAMANI
2 Ni vizuri kuchunguza mtazamo wetu wa kibinafsi kuelekea Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Je! unayaona magazeti kuwa yenye thamani, ukitazamia kila toleo kwa hamu nyingi? Je! wewe unaratibu wakati wa kusoma makala zote? Ikiwa sisi tunayathamini magazeti kibinafsi, idili yetu ya kweli na usadikisho wa kutoka moyoni yatatusaidia tuwe wenye mafanikio katika kuwatolea wengine.
3 Watu walio katika eneo letu wanahitaji habari zenye thamani zilizomo katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kama vile sisi tunavyozihitaji. Tulinufaika kutokana na makala zilizofunua kikamili uovu wa makasisi wa dini bandia na kueleza maonyo ya kiunabii kuhusu uharibifu unaokuja wa Babuloni Mkubwa. Katika Mnara wa Mlinzi wa Septemba 15, 1989, habari “Ni Lazima Mimi Nifanye Nini Nipate Kuokoka?” ilitoa kitia-moyo chenye mafaa kuhusu mwenendo na mwendo wetu wa maisha. Makala za karibuni za Amkeni! zimekaza fikira kwenye kutosimamia vizuri kwa mwanadamu mazingira ya dunia na ahadi za Mungu za kurudisha dunia iwe paradiso. Lo! ni akiba tele kama nini ya chakula cha kiroho ambayo magazeti haya yanaandaa ili kuamsha katika watu uhitaji wao wa kiroho!
YAJUE MAGAZETI YAKO
4 Tunaweza kumsadikishaje mtu kwamba atanufaika kwa kusoma magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!? Njia bora zaidi ni kumwonyesha jambo hususa ambalo huenda likampendeza na kumhusu. Kufanya hivyo kwa matokeo kunataka tufahamiane kikamili na magazeti na kujitayarisha mapema. Kujitayarisha huko kunaanza kwa kusoma magazeti kibinafsi kabla hatujayatumia kwenye huduma. Mbona usitie alama kwenye mambo haya katika nakala zako za kibinafsi za magazeti kisha upitie habari ulizoandika unapojitayarisha kwenda kwenye utumishi wa shambani ukiwa na toleo hilo?
5 Unaposoma Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kibinafsi ni jambo zuri pia kufikiria ni makala zipi zitakuwa zenye upendezi wa kipekee kwa watu fulani katika eneo lenu. Je! ni makala ambazo zitavutia hasa madaktari, wanasheria, au walimu? Kwa habari hii, usisahau kuangalia taarifa zinazohusu makala za matoleo yajayo ili uweze kupanga kimbele na kuagiza nakala zozote za ziada ambazo huenda ukahitaji. Kutengeneza orodha ya majina ya watu mmoja mmoja ambao ungependa kutolea magazeti hayo kunaweza kuwa msaada sana.
6 Baada ya kuzungumza juu ya kutunga vitabu vingi, Mhubiri 12:12 inasema kwamba “na kusoma sana [kujitoa, NW] huuchosha mwili.” Kusoma vichapo vya kilimwengu kunaweza kuchosha kwa sababu haviandai burudisho la kiroho. Tofauti na hilo, sisi ni wenye shukrani kama nini kushiriki katika kueneza magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, ambayo yanamheshimu Yehova na kupiga mbiu ya jina na Ufalme wake!—Mit. 3:9.