Kutoa Habari Njema—Kwa Magazeti Katika Maeneo Tofauti-tofauti
1 Kwenye Matendo 8:25, HNWW, twasoma kwamba Petro na Yohana walitoa ushuhuda kikamili katika Samaria na kisha wakajulisha wazi “Habari Njema katika vijiji vingi vya Samaria.” Leo, sisi pia twapaswa kuwa wenye bidii yenye kuendelea katika kueneza eneo lililogawiwa kundi letu ili ushuhuda kamili upate kutolewa.
2 Kukiwa na ukuzi wa haraka katika wahubiri, sasa makundi mengi yanaeneza eneo lao mara nyingi. Ingawa itikio letu la kwanza la kufanya kazi katika maeneo yanayoenezwa mara nyingi huenda lisiwe la mwelekeo ufaao, haipasi kuwa hivyo. Kwa kila toleo la Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, sikuzote kuna vichwa vipya na vyenye kupendeza ambavyo twaweza kushiriki na watu katika eneo letu.
3 Hata hivyo, katika Afrika Mashariki maeneo yaliyo mengi sana-sana huenezwa mara mbili kwa mwaka na katika visa vilivyo vingi labda mara moja tu kwa mwaka. Hivyo sisi twaendelea kutumia utoaji mfupi wa magazeti ili kueneza eneo letu lote na kutoa ugawanyaji mkubwa wa magazeti yetu.
4 Kama ilivyotajwa katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1991 kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba kwa magazeti katika siku ya magazeti kwa kawaida huhitaji eneo kubwa zaidi. Mwangalizi wa utumishi na kiongozi wa funzo la kitabu la kundi watataka kuwa na eneo la kutosha kwa kikundi. Tafadhali endeleeni kufuata dokezo la kueneza eneo kwa zamu kati ya ushuhuda wa magazeti na toleo la kila mwezi la fasihi ili kufanyia kazi kila eneo wakati mmoja kwa magazeti peke yake na wakati ufuatao kwa toleo la kawaida la fasihi.
5 Iwe ni katika eneo linalofanyiwa kazi mara chache au eneo linaloenezwa mara nyingi twapata watu wa malezi na mapendezi tofauti-tofauti. Kwa hiyo, lazima tuwe tayari kuzungumza na watu wa namna mbalimbali. Hivyo imependekezwa kufikiria makala zitakazowapendeza watu mahsusi katika eneo lenu. Jaribu kuwa na makala moja akilini itakayovutia kila mmoja wa aina hizi tatu: wanaume, wanawake, vijana. Hilo laweza kutimizwaje?
6 Ni jambo la muhimu ufahamiane na makala katika magazeti. Hilo lataka wakati na kufikiria mapema. Unaposoma magazeti, amua ni makala zipi zitavutia watu katika eneo lenu. Halafu, kabla ya kwenda kwenye utumishi, pitia magazeti na kuteua vichwa utakavyoonyesha. Fikiria ni makala zipi utaonyesha upatapo hali mbalimbali milangoni. Tumia mojawapo habari nzuri katika gazeti likiwa jambo kuu katika utangulizi wako. Halafu soma sentensi moja au mbili kutoka fungu hususa linaloshughulika na jambo hilo. Onyesha jinsi gazeti linavyomhusu mwenye nyumba na jinsi familia nzima itakavyolifurahia. Kisha toa gazeti unaloonyesha pamoja na gazeti jenzi.
KUMBUKA KUSUDI LETU
7 Kusudi letu katika kwenda mlango kwa mlango ni kusaidia wengine waje kwenye maarifa sahihi ya kweli. Petro na Yohana walinena neno la Yehova kwa Wasamaria kikamili, nasi vivyo hivyo twataka kutoa ushuhuda wenye matokeo tukitumia magazeti yetu mazuri ajabu. Twapaswa kusali kwa ajili yetu na wengine kwamba tupewe ‘uwezo wa kufumbua kinywa ili tuhubiri ile siri takatifu ya habari njema kwa ujasiri.’—Efe. 6:18-20, NW.