Kutoa Habari Njema kwa Kutumia Vichapo kwa Hekima
1 Programu ya siku ya kusanyiko la Pekee kwa mwaka wa utumishi wa 1991 ilikuwa na mazungumzo juu ya “Huduma Yetu—Si Jambo la Kawaida Tu, Bali Ni Takatifu.” Ilikazia kwamba kazi yetu ni takatifu na haipasi kuonwa vivi hivi. Kwa kuwa utumizi wa fasihi iliyochapwa ni sehemu isiyotenganika ya huduma yetu, hiyo pia yapasa kushughulikiwa kwa staha. Kila mmoja wetu aweza kuonyesha heshima kubwa tunayohisi kwa kutumia vichapo vyetu kwa hekima.
2 Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1990, Sosaiti ilichapisha magazeti milioni 678 na Biblia na vitabu vilivyojalidiwa zaidi ya milioni 51 vitumiwe katika shamba la ulimwenguni pote. Hiyo huwakilisha gharama kubwa sana ya mali iliyowekwa wakfu, kutia ndani wakati, nishati, na pesa. Tokeo la jitihada za pamoja za wengi wenye kujitolea hutokeza fasihi bora kwa matumizi ya kibinafsi na pia kwa kugawanywa katika utumishi wa shambani. Ni baadhi ya njia zipi twaweza kuonyesha uthamini wenye kuhisiwa moyoni kwa fasihi tuwajulishapo watu wenye mioyo minyofu ujumbe wa Ufalme?
3 Funzo la Binafsi na la Familia: Kwenye Warumi 2:21 mtume Paulo asema hivi: “Basi wewe umfundishaye mwingine, je! hujifundishi mwenyewe?” Tutumiapo wakati kusoma, kujifunza, na kutafakari kwa njia ya sala juu ya fasihi yetu yenye msingi wa Biblia, twaonyesha kibinafsi kwa njia hiyo jinsi tuthaminivyo sana maandalizi ya Yehova ya wakati ufaao ya chakula cha kiroho kupitia jamii ya wakili. (Lk. 12:42) Iwe ni kwa funzo la kibinafsi au la familia, kwenda sambamba na kweli zilizofunuliwa hutuwezesha kusitawisha heshima ya hali ya juu kwa yote ambayo Yehova ametuaminisha tuyatunze. Watoto, vilevile, wapasa kufundishwa kuthamini na kutunza fasihi yao, bila kuchora-chora ovyoovyo au kuiharibu. Kwa kuongezea, fasihi yetu yapasa kuwekwa ifaavyo ili ikae ikiwa safi na nadhifu kwa matumizi ya shambani.
4 Epuka Kutapanya: Ili kunufaisha kikweli, fasihi yetu lazima itiwe mikononi mwa watafutaji wa ukweli, yaani, wale ambao wanapendezwa kikweli na ujumbe na kazi yetu. (Mt. 10:11) Kwa hiyo yatupasa tuepuke kuwapa vichapo bila utambuzi wale ambao hawaonyeshi kuthamini kikweli ujumbe wa Biblia. Kutapanya kwaweza kutokea pia tukiachilia magazeti, vitabu, au fashihi nyingine irundamane nyumbani.
5 Kwa kuwa magazeti yana tarehe, tuna wakati mfupi tu wa kuyatoa yakiwa ya karibuni. Kwa hiyo jitihada kubwa inatakwa kwa upande wetu tutoke twende nje katika huduma na kutoa magazeti hayo kwa watu wenye kupendezwa. Tukiona kwamba magazeti yetu bado yanaelekea kurundamana, labda ingekuwa vizuri kurekebisha ratiba tutumie wakati zaidi katika kazi ya magazeti. Au ikiwa hilo haliwezekani, twapaswa kurekebisha agizo letu. Kwa kufuata madokezo hayo, tutajionyesha wenyewe kuwa mawakili waaminifu wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu.—1 Kor. 4:2; 1 Pet. 4:10, 11; linganisha Luka 16:1, 10.
6 Yehova ‘ameweka amana’ kwa watu wake walio wakfu daraka zito sana na kazi, kutia na “vitu vingi” ambavyo “wakili” wake mwaminifu ana mamlaka juu yavyo. (2 Tim. 1:12; Lk. 12:42-44, 48b; 1 Tim. 6:20) Kwa uthamani wenye kina kwa mapendeleo yetu katika utumishi wa Mungu, na tuendelee kutumia kwa hekima vichapo vyetu katika kutoa habari njema kwa wengine.