Mpango wa Funzo la Kitabu la Kundi
Sehemu ya 4: Endeleeni Kujengana Mmoja na Mwenzake
1 Kila mmoja katika kikundi cha Funzo la Kitabu la Kundi anaweza kutimiza sehemu muhimu katika ukuzi wa kiroho wa wengine katika kikundi. Sisi sote twataka kutii ile amri ya Kimaandiko ‘tukahimazane katika upendo na kazi nzuri, hasa kwa kadiri twanavyo kuwa mwisho ule unakaribia.’—Ebr. 10:24, 25.
2 Kusaidiana Mmoja na Mwenzake: Wote waweza kusaidia katika kusitawisha hali yenye uchangamfu na urafiki kwenye funzo la kitabu. Kila mmoja wetu aonyeshapo kupendezwa kibinafsi na washiriki wengine, jambo hilo huchangia kukaribiana katika kikundi. Kwenye Wagalatia 6:10 tunaagizwa “tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” Kwa mfano, je! unatambua wakati baadhi ya washiriki wa kikundi ni wagonjwa na hawakuja kwenye mikutano? Labda waweza kuwasiliana nao kwa simu au kuwatembelea kibinafsi. Roho kama hiyo katika kikundi cha kitabu huwavuta ndugu karibu zaidi.
3 Je! baadhi yao wanahitaji kitia-moyo kwa sababu ya mikazo ya kila siku, madaraka ya kifamilia, au matatizo mengine? Unaweza kufanya nini ili kusaidia? Fanya jitihada ya pekee kushirikisha wengine katika mazungumzo mikutanoni, si kuwasalimu tu. Huenda baadhi yao wakaelekea kuwa wenye haya lakini wanatafuta mtu wa kuongea naye, nao wangeongea wakiendewa. (uw-SW kur. 137-8) Mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo ‘wawatie moyo walio dhaifu, wawatie nguvu wanyonge; wawavumilie watu wote.’ (1 The. 5:14) Ikiwa mtu fulani ni mgonjwa au amevunjika moyo, ni jambo lenye kufariji kama nini wakati marafiki wanapompitia na kumtembelea au kumtolea usaidizi! Mara nyingi, kujua tu kwamba mtu mwingine anajali ndilo jambo linalohitajiwa tu.
4 Twataka pia kushirikiana na mipango ya utumishi wa shambani. Yatupasa tujaribu kufanya kazi na watu tofauti-tofauti katika kikundi. (2 Kor. 6:11-13; 12:15) Nyakati nyingine huenda tukaombwa na kiongozi wa funzo la kitabu tusaidie mtu fulani. Sisi huitikiaje? Kikundi cha funzo la kitabu kinatiwa nguvu sana wakati wahubiri na mapainia wanapofanya kazi mmoja na mwenzake katika pande mbalimbali za kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi.
5 Kielelezo cha Kibinafsi: Kuna njia nyingine ambazo unaweza kuchangia mpango wa funzo la kitabu. Kielelezo chako chema ni cha maana. Kwa mfano, unapovalia kama vile ungevalia unapohudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme, unaonyesha heshima. Unaweka kielelezo kinachofaa kwa wale ambao huenda wakawa wamesitawisha zoea la kuvalia kwa uzembe. Je! unazoea kufika kwa wakati ili usivuruge mkutano?
6 Mpango wa Funzo la Kitabu la Kundi ni uandalizi wa upendo kutoka kwa Yehova tunaohitaji kuunga mkono kikamili. (Isa. 40:11) Ni mahali ambapo twaweza kupata usaidizi wa kibinafsi na pia kuchangia burudisho la kiroho la wengine. Acheni sisi sote ‘tufarijiane na kujengana kila mtu na mwenzake’ kwa kuunga mkono kikamili mpango huo.—1 The. 5:11.