Jinsi Ambavyo Mpango wa Funzo la Kitabu la Kutaniko Hutusaidia
1 Kila moja ya mikutano yetu mitano huongozwa kwa njia tofauti na ina kusudi lake. Hata hivyo, yote ni muhimu ili kutusaidia “tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.” (Ebr. 10:24, 25) Mpango wa Funzo la Kitabu la Kutaniko una mambo gani ya pekee na yenye kufaidi?
2 Hutusaidia Kufanya Maendeleo ya Kiroho: Kwa kawaida, idadi ya watu wanaohudhuria funzo la kitabu ni ndogo kuliko ile ya wale wanaohudhuria mikutano mingine ya kutaniko. Hilo hufanya iwe rahisi kupata marafiki watakaotusaidia kiroho. (Met. 18:24) Je, umejaribu kufahamiana na kila mtu katika funzo lenu la kitabu, pengine kwa kumwomba kila mhubiri ahubiri pamoja nawe? Mpango wa funzo la kitabu pia humwezesha mwangalizi wa funzo la kitabu kujua hali za kila mmoja katika kikundi na kumtia moyo mtu mmoja-mmoja.—Met. 27:23.
3 Je, umewaalika wanafunzi wako wa Biblia wahudhurie funzo la kitabu pamoja nawe? Huenda watu wanaopendezwa ambao husita kuhudhuria mikutano yetu mikubwa wasiogope kuhudhuria mkutano mdogo, hasa ikiwa unafanywa kwenye nyumba ya mtu. Kikundi hicho chenye urafiki hufanya iwe rahisi kwa wachanga na wale ambao wameanza tu kushirikiana na watu wa Yehova kutoa maelezo. Na kwa kuwa kikundi hicho ni kidogo, tuna fursa nyingi zaidi za kutoa maelezo na hivyo kumsifu Yehova.—Zab. 111:1.
4 Mafunzo ya kitabu hufanyiwa mahali panapowafaa wahubiri katika eneo. Ingawa haiwezekani kwa funzo la kitabu kuwa karibu na kila mhubiri, huenda tusisafiri mbali sana ili kufika kwenye funzo letu la kitabu kama inavyokuwa tunapokwenda kwenye mikutano mingine ya kutaniko. Mahali ambapo funzo la kitabu linafanyiwa panaweza pia kuwa mahali panapofaa kwa ajili ya mikutano ya utumishi wa shambani.
5 Msaada Katika Huduma: Mwangalizi wa funzo la kitabu anapendezwa kumsaidia kila mtu ashiriki kwa ukawaida, awe na shangwe katika huduma, na pia apate matokeo mazuri. Hivyo, yeye hujitahidi kuhubiri na kila mtu katika kikundi chake, akiwasaidia katika sehemu mbalimbali za huduma. Ikiwa una matatizo katika sehemu fulani ya huduma kama vile kufanya ziara za kurudia, mjulishe mwangalizi wako wa funzo la kitabu. Anaweza kupanga uhubiri na mhubiri mwenye uzoefu katika kikundi chenu. Utaboresha uwezo wako wa kufundisha wanafunzi wako wa Biblia ukisikiliza kwa makini jinsi ambavyo mwangalizi wa funzo la kitabu anafundisha anapoongoza funzo la kitabu.—1 Kor. 4:17.
6 Funzo la Kitabu la Kutaniko ni mpango mzuri kama nini! Mpango huo wenye upendo kutoka kwa Yehova hutusaidia tusimame imara kiroho katika siku hizi ngumu tunamoishi.—Zab. 26:12.
[Maswali ya Funzo]
1. Mikutano yetu mitano hutusaidiaje?
2. Kuna faida gani za kukutana katika kikundi kidogo cha funzo la kitabu?
3. Mpango wa funzo la kitabu huwatiaje moyo wanafunzi wa Biblia wahudhurie na kutoa maelezo?
4. Mpango wa funzo la kitabu unaweza kuwa na faida zipi?
5. Mwangalizi wa funzo la kitabu anaweza kutusaidiaje katika huduma?
6. Kwa nini tujitahidi kufaidika kikamili na mpango wa funzo la kitabu?