Jinsi ya Kunufaika Kutokana na Kikundi Chako cha Utumishi wa Shambani
1. Ni faida zipi za mpango wa Funzo la Kitabu la Kutaniko ambazo bado zinapatikana katika kikundi chetu cha utumishi wa shambani?
1 Je, unakosa baadhi ya mambo fulani ya Funzo la Kitabu la Kutaniko? Vikundi vilikuwa vidogo na mazingira yalikuwa yenye kustarehesha zaidi. Jambo hilo lilifanya iwe rahisi kukuza urafiki uliotusaidia kubaki imara katika imani. (Met. 18:24) Mwangalizi wa funzo la kitabu alijua hali zetu naye angeweza kumtia moyo mtu mmoja mmoja. (Met. 27:23; 1 Pet. 5:2, 3) Bado tunapata faida hizo zote katika kikundi chetu cha utumishi wa shambani.
2. Tunawezaje kuchukua hatua ya kwanza kukuza urafiki na washiriki wa kikundi chetu cha utumishi wa shambani ambao watatusaidia kubaki imara katika imani?
2 Chukua Hatua ya Kwanza: Kwa ujumla vikundi vya utumishi wa shambani vina ukubwa sawa na ule wa vikundi vya funzo la kitabu. Kwa kufanya kazi katika huduma “pamoja” na wengine, tunaweza kuwa na urafiki wa karibu pamoja nao. (Flp. 1:27) Umehubiri pamoja na watu wangapi katika kikundi chenu? Je, unaweza ‘kupanuka’ kuhusiana na jambo hilo? (2 Kor. 6:13) Kwa kuongezea, mara kwa mara tunaweza kumkaribisha mtu fulani kutoka katika kikundi chetu kwa ajili ya chakula au ashirikiane nasi katika jioni ya Ibada yetu ya Familia. Katika makutaniko mengine, vikundi vya utumishi wa shambani huwa na zamu ya kuandaa chakula kwa ajili ya msemaji anayezuru. Katika juma hilo, kikundi hukusanyika kwa ajili ya chakula na kutiana moyo, iwe msemaji atakaa kwa ajili ya chakula au la.
3. Ni zipi baadhi ya fursa tunazoweza kufaidika na ziara ya uchungaji ya mwangalizi wetu wa kikundi cha utumishi wa shambani?
3 Ingawa sasa kutaniko hukutana mara mbili tu kwa juma, hilo halimaanishi kwamba kuwe na ziara chache za uchungaji. Katika kila kikundi kuna mwangalizi aliyewekwa rasmi ambaye huwatia moyo washiriki wa kikundi na kuwazoeza katika huduma. Ikiwa bado mwangalizi wa kikundi chako hajafanya mipango ya kuhubiri nawe, kwa nini usimwombe ushirikiane naye katika huduma? Isitoshe, kila mwezi mwangalizi wa utumishi hushiriki katika huduma na kikundi tofauti katika mwisho-juma mmoja. Katika makutaniko madogo yenye vikundi vichache vya utumishi wa shambani, anaweza kupanga kutembelea kila kikundi mara mbili kwa mwaka. Je, wewe huratibu wakati wako ili ushiriki katika huduma wakati anapotembelea kikundi chako?
4. (a) Mikutano ya utumishi wa shambani hupangwa jinsi gani? (b) Kwa nini tunapaswa kufikiria kujitolea ili nyumba zetu zitumiwe kwa ajili ya mikutano ya utumishi wa shambani?
4 Mara nyingi kuna faida zaidi kwa kila kikundi kufanya mkutano wake wa utumishi wa shambani katika mwisho-juma kwa ajili ya huduma. Kuwa na sehemu kadhaa za kukutana kwa ajili ya utumishi karibu wakati uleule huenda kukawasaidia wahubiri kufika kwa urahisi mahali pa kukutana kwa ajili ya utumishi na labda hata kwenye eneo. Wahubiri wanaweza kupangwa haraka na kuelekea kwenye eneo bila kukawia. Pia ni rahisi kwa mwangalizi wa kikundi kumpa uangalifu kila mtu aliye katika kikundi chake. Hata hivyo, kulingana na hali, inaweza kuwa jambo la busara kuviunganisha vikundi viwili au zaidi. Ikiwa kutaniko zima hukutana pamoja kwa ajili ya mkutano wa utumishi wa shambani katika Jumamosi ya kwanza ya mwezi au baada ya Funzo la Mnara wa Mlinzi, mara nyingi kuna faida kwa kila kikundi kukaa pamoja na kila mwangalizi wa kikundi kupewa dakika chache ili apange kikundi chake kabla ya mkutano huo kumalizwa kwa sala.—Ona sanduku “Je, Unaweza Kujitolea Ili Nyumba Yako Itumiwe?”
5. Ingawa mpango wa Funzo la Kitabu la Kutaniko umeisha, tunaweza kuwa na uhakika gani?
5 Ingawa mpango wa Funzo la Kitabu la Kutaniko umeisha, Yehova anaendelea kutupa kila kitu tunachohitaji ili kufanya mapenzi yake. (Ebr. 13:20, 21) Chini ya utunzaji wa Yehova, hatukosi chochote. (Zab. 23:1) Tunapata baraka nyingi kutokana na kikundi chetu cha utumishi wa shambani. Tukichukua hatua ya kwanza ya ‘kupanda kwa wingi, tutavuna kwa wingi.’—2 Kor. 9:6.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Je, Unaweza Kujitolea Ili Nyumba Yako Itumiwe?
Kwa sababu ya ukosefu wa nyumba za kutosha kwa ajili ya mikutano ya utumishi, makutaniko mengine huunganisha vikundi kadhaa vya utumishi wa shambani katika mwisho-juma. Mikutano ya utumishi wa shambani ni sehemu ya mpango wa kutaniko, hivyo kuruhusu ifanywe katika nyumba zetu ni pendeleo kwelikweli. Je, utaweza kujitolea ili nyumba yako itumiwe? Usisite kujitolea ili nyumba yako itumiwe eti kwa sababu ni ya hali ya chini. Wazee watazingatia eneo unaloishi na mambo mengine kama hayo waliyozingatia walipokuwa wakichagua mahali pa kukutana kwa ajili ya funzo la kitabu. Ikiwa ungependa kujitolea ili nyumba yako itumiwe, mjulishe mwangalizi wa kikundi chako.