Mpango wa Funzo la Kitabu la Kundi
Sehemu ya 5: Ziara ya Mwangalizi wa Utumishi
1 Mwangalizi wa utumishi apasa awe mweneza evanjeli na mwalimu. Yeye huwa na sehemu ya maana katika kusaidia kundi litimize daraka lalo la kuhubiri na kufundisha habari njema katika eneo lalo lililogawiwa. (Mk. 13:10) Anapochukua daraka lake kwa uzito na kila mtu anashirikiana, wahubiri watakuza ustadi mwingi zaidi katika kutoa habari njema na eneo litaenezwa kwa ukamili zaidi.
2 Mwangalizi wa utumishi hukazia kuchochea utendaji mwingi zaidi katika utumishi wa shambani. Hilo hutimizwa kwa msingi kupitia Funzo la Kitabu la Kundi. Kwa kawaida, mwangalizi wa utumishi hupewa mgawo wa kuongoza funzo la kitabu, lakini mara moja kila mwezi msaidizi wake anaweza kuongoza wakati yeye azurupo kikundi kingine.—km-SW 11/81 kur. 4.
3 Matayarisho kwa Ajili ya Ziara: Kabla ya juma la ziara hii, mwangalizi wa utumishi apasa kuchunguza kadi za Rekodi ya Mhubiri ya Kundi za wale wanaoshirikiana na kikundi hicho. Yeye apasa pia kupanga kukutana na kiongozi na kupitia utendaji wa wahubiri waliogawiwa kuwa kwenye kikundi hicho. Kiongozi anaweza kumjulisha mwangalizi wa utumishi matatizo yoyote yanayohusiana na utumishi au kuhusu mahitaji ambayo huenda yasiwe wazi kwenye kadi za rekodi. Kiongozi wa funzo apasa akumbushwe kwamba funzo lapasa liwe na urefu wa dakika 45 ili kuruhusu wakati wa hotuba ya utumishi ya dakika 15 ikitolewa na mwangalizi wa utumishi.
4 Hotuba hiyo italenga kuendeleza uthamini mkubwa zaidi kwa huduma. Ikiwa wahubiri wahitaji msaada katika mambo fulani ya huduma, mwangalizi wa utumishi apasa atoe madokezo yenye kutumika ili wafanye maendeleo. Maelezo yake yapasa kuwa chanya na yenye kutia moyo ili kuepuka kuaibisha au kuvunja moyo yeyote kwa maneno hasi. Hiyo ingefanya tu ziara yake ikose kutimiza kusudi layo. Hotuba yake yapasa iwatie moyo wote kufanya maendeleo.
5 Mwangalizi wa utumishi hujitahidi kuelekeza fikira kwa mtu mmoja mmoja kwa ndugu na dada wengi iwezekanavyo kwa kadiri ratiba yake inavyoruhusu. Anaweza kufanya miadi kufanya kazi pamoja na watu mbalimbali katika utumishi. Anapofanya kazi ya nyumba kwa nyumba pamoja na wahubiri, huenda akatoa dokezo moja au mawili kuhusu njia za kufanyia maendeleo utoaji wao. Hilo lapasa kufanywa si kwa njia ya kuchambua bali kwa tamaa ya kusaidia kwa moyo. Yeye aweza pia kujitoa kuandamana na wahubiri katika ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia. Ikiwa wowote katika kikundi huenda wakahitaji msaada wa kibinafsi, huenda akafanya ziara ya uchungaji katika juma hilo ili kuwasaidia. Baada ya hapo, yeye aweza kumjulisha kiongozi kuhusu madokezo yaliyotolewa. Uelekezo huu mchangamfu wa fikira kwa mtu binafsi umekuwa kichocheo kwa wengine ambao wamepunguza mwendo katika utumishi wao wa shambani.
6 Kukutana kwa Ajili ya Utumishi: Mikutano ya utumishi wa shambani katika juma hilo yapasa iongozwe na mwangalizi wa utumishi. Hiyo yapasa kuanza kwa wakati hata ikiwa ni wachache tu wanaopatikana. Mkutano huo haupaswi kuzidi dakika 10 kufikia 15. Kuangalia Andiko la siku ni uchaguzi wa hiari. Kabla ya kikundi kutawanywa, kila mtu apasa kujua atafanya kazi wapi na pamoja na nani. (1 Kor. 14:33, 40) Mwangalizi wa utumishi apasa kutia moyo kila mtu aondoke bila kukawia kwenda kwenye utumishi wa shambani.
7 Ziara za kawaida za mwangalizi wa utumishi kwenye vikundi vya funzo la kitabu zaweza kuwa zenye baraka halisi kwa kundi. Kila mmoja wetu akishirikiana naye anapozuru, utumishi wetu utakuwa na utaratibu na wenye matokeo. Zaidi ya hilo, yeye atapata furaha kwa kazi yake. (Ebr. 13:17) Watu wenye mfano wa kondoo watakusanywa, na tutakuwa na furaha ya kujua tumetimiza utume wetu wa kuwahubiri wote watakaosikia.—Isa. 61:1, 2; Eze. 9:11; Yn. 17:26.